Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tutende Mema Au Tujizuie Tu Kutenda Mabaya?

Je, Tutende Mema Au Tujizuie Tu Kutenda Mabaya?

Je, Tutende Mema Au Tujizuie Tu Kutenda Mabaya?

“USIWATENDEE wengine yale usiyotaka wakutendee.” Kanuni hiyo ya maadili ilitolewa na Confucius, mwalimu na mwanafalsafa maarufu Mchina. Leo, miaka 2,500 baadaye, wengi bado wanaamini kwamba mtu anakuwa mnyoofu kwa kujizuia tu kuwadhuru wengine.

Kwa kweli, kanuni hiyo ya maadili ya Confucius ina manufaa yake. Kwa upande mwingine, Biblia inataja jambo lingine kuhusiana na tabia na mahusiano ya kibinadamu. Mbali na dhambi unazowatendea wengine, Biblia pia hutaja dhambi ya kutofanya unayopaswa kufanya. Mwanafunzi Mkristo Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa mtu anajua jinsi ya kufanya yaliyo sawa na bado hayafanyi, hiyo ni dhambi kwake.” (Yakobo 4:17) Badala ya kuwaagiza tu Wakristo wasiwatendee wengine mabaya, Yesu Kristo alitoa shauri hili: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

Kusudi la awali la Mungu lilikuwa kwamba wanadamu wote watendee wengine jinsi ambavyo wao wenyewe wangetaka watendewe. Aliweka kielelezo kizuri sana cha kuonyesha anajali masilahi ya wengine kwa jinsi alivyowaumba wanadamu: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwanzo 1:27) Hiyo inamaanisha kwamba kwa upendo Mungu aliwapa wanadamu dhamiri, ambayo inapozoezwa vizuri, ingewasaidia kuwatendea wengine jinsi ambavyo wao wenyewe wangetaka watendewe.

Leo watu wengi huteseka bila tumaini na bila msaada mikononi mwa watu wasiojali na wenye ubinafsi. Hivyo, ni wazi kwamba kinachohitajiwa si kujizuia tu kuwatendea wengine mambo mabaya na yenye kuwadhuru, bali ni kuwatendea mambo mazuri yenye kuwanufaisha. Kwa sababu hiyo Mashahidi wa Yehova hujitolea kuwasaidia wengine wajifunze tumaini zuri linalopatikana katika Neno la Mungu. Wanapowatembelea jirani zao kuwahubiria habari njema za Biblia, wao hufanya hivyo kwa roho ya upendo, wakiwatendea wengine jinsi ambavyo wao wenyewe wangetaka watendewe.