Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapaswa Kuchagua Dini Gani?

Unapaswa Kuchagua Dini Gani?

Unapaswa Kuchagua Dini Gani?

‘DINI mbalimbali ni barabara tofauti-tofauti tu zinazoelekea mahali pamoja. Ukweli ni kwamba kuna Mungu mmoja tu, sivyo?’ Wengi walio na maoni hayo huhisi kwamba ingawa ni muhimu kuwa mfuasi wa dini fulani, haidhuru mtu anachagua kuwa wa dini gani.

Kwa kuchunguza hoja hiyo kijuu-juu tu huenda ikaonekana kuwa inapatana na akili, kwa kuwa ni kweli kwamba kuna Mungu mmoja tu, aliye Mweza-Yote. (Isaya 44:6; Yohana 17:3; 1 Wakorintho 8:5, 6) Hata hivyo, hatuwezi kupuuza tofauti zilizo wazi au hata mambo yenye kupingana kati ya dini nyingi zinazodai kumtumikia Mungu wa kweli. Zinatofautiana sana katika desturi, imani, mafundisho, na matakwa yao. Tofauti hizo ni kubwa sana hivi kwamba watu wa dini au kikundi kimoja huona ni vigumu kuelewa au kukubali mafundisho au imani ya wengine.

Kwa upande mwingine, Yesu alisema: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Je, inawezekana kumwabudu Mungu katika kweli na wakati huohuo kuwe na maoni yenye kupingana kuhusu yeye ni nani, makusudi yake ni yapi, na jinsi anavyotaka kuabudiwa? Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba Mungu Mweza-Yote hajali jinsi tunavyomwabudu?

Wakristo wa Kweli Katika Karne ya Kwanza na Sasa

Nyakati nyingine, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na maoni tofauti-tofauti kuhusu mambo fulani. Kwa mfano, akizungumza kuhusu wale waliokuwa Korintho, mtume Paulo alisema hivi: “Ndugu zangu, wale wa nyumba ya Kloe walinifunulia juu yenu kwamba kuna magombano kati yenu. Ninalomaanisha ni hili, kwamba kila mmoja wenu anasema: ‘Mimi ni wa Paulo,’ ‘Lakini mimi ni wa Apolo,’ ‘Lakini mimi ni wa Kefa,’ ‘Lakini mimi ni wa Kristo.’”—1 Wakorintho 1:11, 12.

Je, Paulo aliona kwamba tofauti hizo hazikuwa muhimu sana? Je, kila mtu alikuwa akifuata njia yake mwenyewe ya wokovu? Sivyo! Paulo aliwashauri hivi: “Nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.”—1 Wakorintho 1:10.

Bila shaka, watu hawawezi kulazimishwa kuwa na umoja katika imani. Umoja huo unapatikana watu wanapochunguza mambo kwa makini na kufikia mikataa ileile. Hivyo, kujifunza Neno la Mungu kibinafsi na tamaa ya kweli ya kufuata mambo tunayojifunza ni hatua muhimu za kupata umoja ambao Paulo alizungumza juu yake. Je, umoja huo unaweza kupatikana? Kama tulivyoona, kwa muda mrefu Mungu amekuwa akishughulika na watu wake wakiwa kikundi. Je, tunaweza kutambua kikundi hicho leo?

Manufaa ya Kushirikiana na Watu Wanaofaa

Wakati fulani mtunga-zaburi Daudi aliuliza hivi: “Ee Yehova, ni nani atakayekuwa mgeni katika hema lako? Ni nani atakayekaa katika mlima wako mtakatifu?” Bila shaka, hilo ni swali lenye kuchochea fikira. Daudi alitoa jibu: “Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake.” (Zaburi 15:1, 2) Kuielewa Biblia kwa usahihi kutamwezesha mtu aitambue dini ambayo inatimiza matakwa hayo ya kimungu. Kisha atajengwa kwa kushirikiana na kikundi hicho cha watu wanaomwabudu Mungu kwa umoja, na pia “kwa roho na kweli.”

Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwamba inawezekana kuwa na imani moja na kutenda kwa upatano hata katika ulimwengu huu usio na umoja. Kati yao kuna watu ambao wametoka katika dini nyingi na makabila mbalimbali. Hapo zamani, Mashahidi wengine walikuwa wakana-Mungu au waliamini kwamba ya Mungu hayawezi kujulikana. Bado wengine walipuuza dini. Watu fulani wameacha dini hizo tofauti-tofauti, utamaduni, na falsafa na sasa wanafurahia umoja wa kidini ambao haupatikani katika ulimwengu wa leo.

Umoja huo unategemea Neno la Mungu, Biblia. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba hawawezi kuwalazimisha wengine watende kwa njia fulani. Lakini wanathamini pendeleo la kuwatia wengine moyo wajifunze Biblia ili waamue masuala yanayohusu ibada kwa kutegemea msingi huo thabiti. Kwa njia hiyo, wengi zaidi wanaweza kupata manufaa yanayotokana na kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.”

Leo kuna hatari kubwa sana ya kuathiriwa na uvutano mbaya na pia vishawishi. Ni muhimu kushirikiana na watu wanaofaa. Biblia inasema kwamba, “anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima” na kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Ni ulinzi kushirikiana na waabudu wa kweli wa Mungu. Kwa hiyo, Biblia inatukumbusha hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Tunapata baraka iliyoje wakati marafiki wa kweli, ndugu na dada za kiroho wanaposaidiana kwa upendo kutimiza madaraka yao mbele za Mungu!

Ottmar anaunga mkono maoni hayo. Ottmar aliyelelewa katika familia ya Wakatoliki huko Ujerumani aliacha kwenda kanisani. Anaeleza hivi: “Kila mara nilipoenda kanisani, nilitoka huko bila kuhisi nimefaidika na chochote.” Hata hivyo, aliendelea kumwamini Mungu. Kisha akakutana na Mashahidi wa Yehova na akapata kusadiki kwamba wao ni watumishi wa kweli wa Mungu. Alitambua umuhimu wa kushirikiana nao. Sasa anasema: “Ninafanya kazi kwa bidii pamoja na tengenezo la ulimwenguni pote, na sasa nina amani ya akili na moyo. Ninasaidiwa hatua kwa hatua kupata ujuzi zaidi ulio sahihi kuhusu Biblia. Hilo ni jambo lenye thamani kubwa sana kwangu.”

Mwaliko kwa Wale Wanaotafuta

Watu walio na upatano wanaweza kutimiza kazi fulani vizuri zaidi kuliko watu mmoja-mmoja wanaofanya kazi kwa kujitegemea. Kwa mfano, Yesu alipokuwa karibu kuwaacha wanafunzi wake, alitoa maagizo haya: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kazi hiyo ingeweza kutimizwaje vizuri bila mwongozo au tengenezo? Mtu angewezaje kutii amri hiyo ya Biblia ikiwa angejaribu kumtumikia Mungu kwa kujitegemea?

Mwaka jana, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waliwaachia watu vitabu vinavyozungumzia Biblia, vijitabu, na broshua 91,933,280, na magazeti 697,603,247, na hivyo kuwafikishia mamia ya mamilioni ya watu katika nchi 235 ujumbe wa Neno la Mungu. Bila shaka, hilo linathibitisha kwamba watu wanapoungana wanaweza kutimiza mengi zaidi kuliko yale yanayoweza kutimizwa na watu mmoja-mmoja.

Zaidi ya kugawanya vichapo vinavyozungumzia Biblia, Mashahidi wa Yehova huongoza mafunzo ya Biblia bila malipo ili kusaidia watu wapate ufahamu wenye kina kuhusu matakwa ya Mungu. Mwaka jana, wastani wa mafunzo ya Biblia 5,726,509 yaliongozwa kila juma pamoja na watu mmoja-mmoja au vikundi vya watu. Mafundisho hayo ya Biblia yamesaidia mamilioni ya watu kupata msingi thabiti wa kufanya uamuzi kuhusu mambo yanayohusu ibada. Unaalikwa kujifunza matakwa ya Mungu kama yanavyoonyeshwa katika Biblia. Kisha unaweza kuamua.—Waefeso 4:13; Wafilipi 1:9; 1 Timotheo 6:20; 2 Petro 3:18.

Ikiwa unataka kumpendeza Mungu, ni muhimu kushirikiana na dini fulani—lakini si madhehebu yoyote au kikundi chochote tu. Uamuzi wako kuhusu dini unapaswa kutegemea ujuzi sahihi wa Biblia, bali si imani ya kulazimishwa au mambo ya kuambiwa. (Methali 16:25) Jifunze matakwa ya dini ya kweli. Yalinganishe na imani yako. Kisha amua kulingana na matakwa hayo.—Kumbukumbu la Torati 30:19.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova wana umoja katika ulimwengu usio na umoja