Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uumbaji Hutangaza Utukufu wa Mungu!

Uumbaji Hutangaza Utukufu wa Mungu!

Uumbaji Hutangaza Utukufu wa Mungu!

“Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.”—ZABURI 19:1.

1, 2. (a) Kwa nini wanadamu hawawezi kuuona utukufu wa Mungu moja kwa moja? (b) Wale wazee 24 humtukuzaje Mungu?

“HUWEZI kuuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na bado aishi.” (Kutoka 33:20) Ndivyo Yehova alivyomwonya Musa. Kwa kuwa wanadamu wana mwili dhaifu, hawawezi kuutazama utukufu wa Mungu moja kwa moja na waendelee kuishi. Hata hivyo, katika maono fulani yenye kuvutia, mtume Yohana alionyeshwa Yehova akiwa kwenye kiti Chake cha enzi chenye utukufu.—Ufunuo 4:1-3.

2 Tofauti na wanadamu, viumbe wa roho washikamanifu wanaweza kuuona uso wa Yehova. Kati yao kuna wale “wazee ishirini na wanne” wanaowakilisha wale 144,000, ambao Yohana aliona katika maono yake ya kimbingu. (Ufunuo 4:4; 14:1-3) Wao hutendaje wanapoona utukufu wa Mungu? Kulingana na Ufunuo 4:11, wao hutangaza: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”

Kwa Nini “Hawana Sababu ya Kujitetea”?

3, 4. (a) Kwa nini kumwamini Mungu kunapatana na sayansi? (b) Katika visa fulani, ni nini iliyo sababu ya kutomwamini Mungu?

3 Je, unachochewa kumtukuza Mungu? Wanadamu walio wengi hawamtukuzi, wengine hata hukana kuna Mungu. Kwa mfano, mtaalamu mmoja wa anga aliandika: “Je, Mungu ndiye aliyeingilia kati na kuumba ulimwengu kwa manufaa yetu? . . . Hayo ni maoni yenye kupendeza. Lakini nasikitika kusema kwamba siamini kuwa jambo hilo ni la kweli. . . . Haitoshi tu kusema kwamba Mungu aliuumba ulimwengu.”

4 Utafiti wa kisayansi una mipaka, kwa kuwa unategemea tu yale wanadamu wanayoweza kuona au kujifunza. Vinginevyo utafiti huo unakuwa nadharia au mambo ya kukisia tu. Kwa kuwa “Mungu ni Roho,” hawezi kuchunguzwa kupitia utafiti wa kisayansi. (Yohana 4:24) Kwa hiyo, ingekuwa kiburi kusema kwamba kumwamini Mungu hakupatani na sayansi. Mwanasayansi Vincent Wigglesworth wa Chuo Kikuu cha Cambridge alisema kwamba utafiti wa kisayansi wenyewe “hutegemea imani.” Jinsi gani? “Hutegemea imani thabiti kwamba mambo ya asili yanaweza kuelezwa tu kwa msingi wa ‘sheria za asili.’” Hivyo, hata kama mtu atakataa kumwamini Mungu, atahitaji kuwa na imani hiyohiyo ili kuamini mambo ya kisayansi. Katika visa fulani, yaonekana kutomwamini Mungu ni hatua ya kimakusudi tu ya kuukataa ukweli. Mtunga-zaburi aliandika: “Kwa sababu ya kujigamba kwake, mwovu hatafuti; mawazo yake yote ni: ‘Hakuna Mungu.’”—Zaburi 10:4.

5. Kwa nini hakuna sababu ya kujitetea kwa kutomwamini Mungu?

5 Hata hivyo, kumwamini Mungu si jambo lisilo la msingi, kwa kuwa kuna uthibitisho mwingi sana kwamba kuna Mungu. (Waebrania 11:1) Mtaalamu wa anga Allan Sandage alisema: “Naona ni jambo lisilowezekana kwamba utaratibu [katika ulimwengu] ulitokana tu na machafuko. Lazima utaratibu huo uwe na chanzo fulani. Mimi humwona Mungu kuwa fumbo, lakini yeye ndiye anayeweza kueleza muujiza wa kuwapo kwa vitu, kueleza vilikotoka.” Mtume Paulo aliwaambia Wakristo wa Roma kwamba ‘sifa za Mungu ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba wasioamini hawana sababu ya kujitetea.’ (Waroma 1:20) Tangu “kuumbwa kwa ulimwengu”—hasa tangu kuumbwa kwa wanadamu wenye akili, wanaoweza kuelewa kwamba kuna Mungu—imekuwa wazi kwamba kuna Muumba mwenye nguvu nyingi sana, Mungu tunayepaswa kujitoa kwake. Hivyo, wale wanaokataa kutambua utukufu wa Mungu hawana sababu ya kujitetea. Hata hivyo, uumbaji unatoa uthibitisho gani?

Ulimwengu Hutangaza Utukufu wa Mungu

6, 7. (a) Mbingu hutangazaje utukufu wa Mungu? (b) ‘Kamba za kupimia’ kutoka mbinguni zimefika kwa kusudi gani?

6 Zaburi 19:1 inajibu kwa kusema: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” Daudi alitambua kwamba nyota na sayari ambazo ziliangaza kupitia “anga,” zilithibitisha pasipo shaka kwamba kuna Mungu mtukufu. Anaendelea kusema: “Siku moja baada ya siku nyingine hufanya maneno yabubujike, na usiku mmoja baada ya usiku mwingine huonyesha ujuzi.” (Zaburi 19:2) Siku baada ya siku na usiku baada ya usiku, mbingu huonyesha hekima na nguvu za uumbaji za Mungu. Ni kana kwamba sauti za kumsifu Mungu ‘zinabubujika’ kutoka mbinguni.

7 Hata hivyo, inahitaji utambuzi ili kusikia ushahidi huo. “Hakuna usemi, wala hakuna maneno; sauti yao haisikiki.” Hata hivyo, ushuhuda wa kimya-kimya wa mbingu una nguvu sana. “Kamba yake ya kupimia imefika duniani pote, na maneno yake yamefika kwenye miisho ya nchi yenye kuzaa.” (Zaburi 19:3, 4) Ni kana kwamba ‘kamba za kupimia’ kutoka mbinguni zimefika ili kuhakikisha kwamba ushahidi wao wa kimya-kimya umeenea kila mahali duniani.

8, 9. Ni mambo gani yenye kutokeza kuhusu jua?

8 Kisha, Daudi anaeleza jambo lingine lenye kustaajabisha kuhusu uumbaji wa Yehova: “Katika hizo [mbingu zinazoonekana] amewekea jua hema, nalo ni kama bwana-arusi anapotoka katika chumba chake cha ndoa; linashangilia kama mwanamume mwenye nguvu anapokimbia njiani. Linaenda kutoka mwisho mmoja wa mbingu, nao mzunguko wake humalizikia katika ile miisho yake mingine; wala hakuna chochote kilichofichwa kisiweze kupatwa na joto lake.”—Zaburi 19:4-6.

9 Jua linapolinganishwa na nyota nyingine, lina ukubwa wa kadiri tu. Hata hivyo, jua ni nyota yenye kutokeza, ambayo hufanya sayari zinazolizunguka zionekane ndogo sana. Kichapo kimoja kinasema kwamba jua lina uzito wa “tani bilioni mbili mara bilioni moja mara bilioni moja,” yaani, asilimia 99.9 ya uzito wa mfumo wetu wote wa jua na sayari zake! Nguvu za uvutano za jua huiwezesha dunia kulizunguka ikiwa umbali wa kilometa milioni 150 bila kupeperuka au kulikaribia. Ni sehemu ndogo sana ya nishati za jua ambayo huifikia dunia yetu, lakini hiyo inatosha kutegemeza uhai.

10. (a) Jua huingiaje na kutoka katika “hema” lake? (b) Hukimbiaje kama “mwanamume mwenye nguvu”?

10 Mtunga-zaburi anazungumza kuhusu jua kwa njia ya mfano, akilitaja kuwa “mwanamume mwenye nguvu” ambaye mchana hukimbia kutoka mwisho mmoja wa mbingu hadi mwisho ule mwingine na kupumzika usiku katika “hema.” Inapotazamwa kutoka duniani wakati wa kutua, nyota hiyo yenye nguvu huonekana kama inaingia katika “hema” kupumzika. Asubuhi huonekana kama linachomoka ghafula, likiangaza “kama bwana-arusi anapotoka katika chumba chake cha ndoa.” Akiwa mchungaji, Daudi alihisi baridi kali ya usiku. (Mwanzo 31:40) Alikumbuka jinsi yeye na eneo alimokuwa lilivyopashwa joto kwa haraka na miali ya jua. Ni wazi kwamba jua halikuwa limechoshwa na “safari” yake kutoka mashariki hadi magharibi lakini lilikuwa kama “mwanamume mwenye nguvu,” aliye tayari kuirudia safari yake.

Nyota na Magalaksi Yenye Kutia Woga

11, 12. (a) Ni nini chenye kutokeza kuhusu ulinganisho wa Biblia kati ya nyota na chembe za mchanga? (b) Ulimwengu unaweza kuwa na ukubwa gani?

11 Kwa kuwa Daudi hakuwa na darubini, angeweza kuona nyota elfu chache tu. Hata hivyo, kulingana na uchunguzi mmoja wa hivi karibuni, hesabu ya nyota ulimwenguni zinazoonekana kwa darubini za kisasa ni kubwa mno (namba 7 ikifuatwa na sufuri 22)! Yehova alionyesha kwamba nyota hizo ni nyingi sana alipofananisha hesabu yake na “chembe za mchanga zilizo kando ya bahari.”—Mwanzo 22:17.

12 Kwa miaka mingi, wataalamu wa anga waliona vile ambavyo vimetajwa kuwa “vitu vidogo vyenye mwangaza ambavyo havionekani vizuri.” Wanasayansi walikisia kwamba “vikundi hivyo vya nyota vilivyo kama mawingu yenye kujiviringa” ni sehemu ya galaksi ya Kilimia. Mnamo 1924, ilivumbuliwa kwamba kimojawapo cha vikundi hivyo vya nyota kinachoitwa Andromeda, ambacho ndicho kiko karibu zaidi na dunia, ni galaksi ambayo iko umbali wa kilometa trilioni 9.46 hivi! Wanasayansi sasa wanakadiria kwamba kuna mabilioni ya magalaksi, kila moja ikiwa na maelfu, au hata mabilioni ya nyota. Hata hivyo, Yehova “anahesabu idadi ya nyota; zote anaziita kwa majina yake.”—Zaburi 147:4.

13. (a) Ni nini chenye kutokeza kuhusu makundi-nyota? (b) Inaonekanaje wazi kwamba wanasayansi hawajui “sheria za mbingu”?

13 Yehova alimwuliza Ayubu hivi: “Je, unaweza kufunga vifungo vya kundi-nyota la Kima, au, je, unaweza kufungua kamba za kundi-nyota la Kesili?” (Ayubu 38:31) Kundi-nyota ni hesabu fulani ya nyota inayofanyiza muundo fulani wenye kuonekana. Ingawa huenda kukawa na umbali mkubwa kutoka nyota moja hadi nyingine, nyota hizo huonekana kuwa mahali palepale zinapotazamwa kutoka duniani. Kwa kuwa makundi hayo hubaki mahali pake hasa, nyota hizo “husaidia kuongoza meli baharini, wanaanga kuongoza vyombo vyao, na kutambulisha nyota.” (The Encyclopedia Americana) Hata hivyo, hakuna anayeweza kuelewa kabisa “vifungo” vinavyounganisha makundi ya nyota. Wanasayansi bado hawawezi kujibu swali ambalo Ayubu aliulizwa kwenye Ayubu 38:33: “Je, umepata kujua sheria za mbingu?”

14. Ni katika njia gani kugawanywa kwa nuru ni fumbo?

14 Wanasayansi hawawezi kujibu swali hili lingine ambalo Ayubu aliulizwa: “Basi sasa, iko wapi njia ambayo katika hiyo nuru hujigawanya?” (Ayubu 38:24) Mwandishi mmoja alilitaja swali hilo kuhusu nuru kuwa “swali gumu sana katika sayansi ya kisasa.” Kinyume cha hilo, wanafalsafa fulani Wagiriki walifikiri kwamba nuru ilitoka katika jicho la mwanadamu. Hivi karibuni, wanasayansi wamefikiri kwamba nuru hufanyizwa na chembechembe ndogo sana. Wengine wamefikiri kwamba nuru husafiri kama mawimbi. Leo, wanasayansi wanaamini kwamba nuru ni kama wimbi na pia ni kama chembechembe. Hata hivyo, hakuna ajuaye kikamili jinsi nuru ilivyo hasa na jinsi ambavyo “hujigawanya.”

15. Kama Daudi, tunapaswa kuhisije tunapotafakari kuhusu mbingu?

15 Unapotafakari hayo yote, unachochewa kuhisi kama mtunga-zaburi Daudi aliyesema: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?”—Zaburi 8:3, 4.

Dunia na Viumbe Wake Humtukuza Yehova

16, 17. Viumbe katika “vilindi vya maji” humsifuje Yehova?

16 Zaburi ya 148 inataja njia nyingine ambazo uumbaji hutangaza utukufu wa Mungu. Mstari wa 7 unasema: “Msifuni Yehova kutoka duniani, enyi wanyama wakubwa wa baharini, nanyi vilindi vyote vya maji.” Naam, “vilindi vya maji” vina maajabu mengi ambayo hukazia hekima na nguvu za Mungu. Nyangumi-samawi ana uzito wa tani 120 hivi—uzito wa tembo 30! Moyo wake tu una uzito wa kilogramu zaidi ya 450, nao unaweza kusukuma kilogramu 6,400 hivi za damu kuuzunguka mwili wake! Je, viumbe hao wakubwa wa baharini husafiri polepole na kwa shida baharini? La. Wao “husafiri baharini” kwa kasi sana, yasema ripoti moja ya harakati ya European Cetacean Bycatch Campaign. Nyangumi-samawi mmoja alifuatwa kwa kutumia setilaiti, naye “alisafiri umbali wa kilometa zaidi ya 16,000 kwa muda wa miezi 10.”

17 Pomboo mmoja mwenye pua pana hupiga mbizi zenye kina cha meta 45, lakini mbizi ndefu zaidi ambayo pomboo amewahi kupiga ni ya kina cha meta 547! Samaki huyo huwezaje kubaki hai anapopiga mbizi hizo zenye kina kirefu? Anapopiga mbizi, moyo hupiga polepole, nayo damu huelekezwa kwenye moyo, mapafu, na ubongo. Pia, misuli yake ina kemikali fulani ambayo huhifadhi oksijeni. Nyangumi mwenye nundu na yule ambaye hutoa nta kichwani wanaweza kupiga mbizi yenye kina kirefu hata zaidi. Gazeti Discover linasema, “Badala ya kupambana na uzito wa maji chini ya bahari, wao huuacha uyafinye mapafu yao kabisa.” Wao huhifadhi nyingi ya oksijeni wanayohitaji katika misuli yao. Hakika, viumbe hao ni ushuhuda ulio wazi kwamba kuna Mungu mwenye hekima na mwenye nguvu zote!

18. Maji ya baharini huonyeshaje hekima ya Yehova?

18 Hata maji ya bahari huonyesha hekima ya Yehova. Gazeti Scientific American linasema: “Kila tone la maji juu ya meta 100 za bahari lina mimea mingi midogo sana inayoelea.” ‘Msitu huo usioonekana’ husafisha hewa yetu kwa kuondoa mabilioni ya tani za kaboni dioksidi. Mimea hiyo hutoa zaidi ya nusu ya oksijeni tunayopumua.

19. Moto na theluji hutimizaje mapenzi ya Yehova?

19 Zaburi 148:8 inasema: “Enyi moto na mvua ya mawe, theluji na moshi mzito, enyi pepo zenye tufani, zinazotimiza neno lake.” Naam, Yehova pia hutumia nguvu za asili zisizo na uhai ili kutimiza mapenzi yake. Fikiria moto. Miaka mingi iliyopita, mioto ya misitu ilionwa kuwa yenye kuharibu tu. Sasa wachunguzi wanaamini kwamba moto hutimiza fungu muhimu katika mazingira, kwa kuondoa miti ya zamani au inayokufa, na kusaidia mbegu nyingi zichipuke, hurejeleza rutuba, na hata kupunguza hatari ya kutokea kwa ule moto wenye kuenea haraka. Theluji pia ni muhimu kwa kuwa hunywesha na kurutubisha udongo, huongeza maji mitoni, na hukinga miti na wanyama kutokana na baridi kali.

20. Milima na miti humnufaishaje mwanadamu?

20 “Enyi milima, nanyi vilima vyote, enyi miti ya matunda, nanyi mierezi yote,” yasema Zaburi 148:9. Milima yenye fahari ni ushuhuda wa kwamba Yehova ana nguvu kuu. (Zaburi 65:6) Milima pia hunufaisha kwa njia fulani. Ripoti moja kutoka Taasisi ya Jiografia huko Bern, Uswisi, inasema: “Milima ndiyo vyanzo vya mito yote mikubwa duniani. Zaidi ya nusu ya watu duniani hutegemea maji safi ambayo hukusanyika milimani. . . . ‘Minara hiyo ya maji’ ni muhimu sana kwa mwanadamu.” Hata mti wa kawaida humtukuza Mfanyi wake. Ripoti moja ya Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa inasema kwamba miti “ni muhimu kwa watu wa nchi zote. . . . Aina fulani ya miti ni muhimu sana kiuchumi kwa kuwa inatokeza mbao, matunda, njugu, utomvu, na gundi. Watu bilioni 2 duniani kote hupika kwa kuni.”

21. Eleza jinsi ambavyo jani la kawaida huthibitisha kwamba lilibuniwa.

21 Jinsi ambavyo kila mti umeumbwa hutoa ushuhuda kwamba kuna muumba mwenye hekima. Fikiria jani la kawaida. Upande wa nje wa jani umefunikwa kwa nta ambayo hulisaidia lisikauke. Chini ya nta hiyo upande wa juu kuna chembe zenye kiwiti. Chembe hizo huwa na rangi ya kijani kibichi ambayo hufyonza nishati ya nuru. Majani hufanyiza chakula kupitia mfumo uitwao usanidimwanga. Mti hufyonza maji kupitia mizizi na kuyapeleka juu kwenye majani. Maelfu ya matundu (yaitwayo stomata) yaliyo upande wa chini wa jani hufunguka na kufungika ili kufyonza kaboni dioksidi. Nuru hutoa nishati ili maji na kaboni dioksidi ziungane na kutokeza wanga. Sasa mti unaweza kutumia chakula ambacho umefanyiza. Hata hivyo, mfumo huo wa kutengeneza chakula unavutia na hufanya kazi kimya-kimya. Badala ya kuchafua hewa mfumo huo hutoa oksijeni.

22, 23. (a) Ndege na wanyama fulani wa nchi kavu wana uwezo gani mbalimbali? (b) Tutazungumzia maswali gani mengine?

22 “Enyi wanyama wa mwitu, nanyi wanyama wote wa kufugwa, enyi vitu vinavyotambaa na ndege wenye mabawa,” yasema Zaburi 148:10. Wanyama wengi wa nchi kavu na ndege wana uwezo mbalimbali wenye kustaajabisha. Ndege aitwaye Laysan albatross anaweza kuruka kwa masafa marefu sana (katika kisa kimoja aliruka kilometa 40,000 kwa muda wa siku 90 tu). Naye ndege aitwaye blackpoll warbler huruka kutoka Amerika Kaskazini hadi Amerika Kusini kwa muda wa saa 80 bila kutua. Ngamia huhifadhi maji katika mfumo wake wa kumeng’enya chakula, wala si katika nundu yake kama inavyofikiriwa na wengi. Hiyo humwezesha kukaa muda mrefu bila kuishiwa na maji mwilini. Basi, haishangazi kwamba mainjinia hutazama wanyama kwa makini wanapotengeneza mashini na vitu vipya. Mwandishi Gail Cleere anasema, “Ukitaka kutengeneza kitu kitakachofanya kazi vizuri . . . na kisichodhuru mazingira, yaelekea utaigiza uumbaji fulani.”

23 Naam, bila shaka uumbaji hutangaza utukufu wa Mungu! Mbingu yenye nyota, miti, na wanyama, vyote hivyo humtukuza Muumba, kila kimoja kwa njia yake. Lakini namna gani sisi wanadamu? Tunawezaje kumtukuza Mungu kama vitu hivyo vya asili?

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini wale wanaokana kwamba kuna Mungu hawana sababu ya kujitetea?

• Nyota na sayari humtukuzaje Mungu?

• Wanyama wa baharini na wa nchi kavu huthibitishaje kwamba kuna Muumba mwenye upendo?

• Nguvu za asili zisizo na uhai hutimizaje mapenzi ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wanasayansi hukadiria kwamba nyota zinazoweza kuonekana ni nyingi mno (saba ikifuatwa na sufuri 22)!

[Hisani]

Frank Zullo

[Picha katika ukurasa wa 12]

Pomboo mwenye pua pana

[Picha katika ukurasa wa 13]

Chembe ya theluji

[Hisani]

snowcrystals.net

[Picha katika ukurasa wa 13]

“Laysan albatross” mdogo