Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Alitufundisha Kuheshimu Dini Yake’

‘Alitufundisha Kuheshimu Dini Yake’

‘Alitufundisha Kuheshimu Dini Yake’

SHAHIDI mmoja wa Yehova kutoka jimbo la Rovigo, Italia, alijua kwamba ana uvimbe na kwamba uhai wake ulikuwa hatarini. Baada ya kulazwa hospitali mara nyingi, aliomba atibiwe bila kutiwa damu mishipani, naye alisaidiwa akiwa nyumbani, na wauguzi kutoka kituo cha kuhudumia wagonjwa wa kansa.

Mgonjwa huyo ambaye ana umri wa miaka 36 mwenye imani yenye nguvu na aliye tayari kushirikiana aliwashangaza sana madaktari na wauguzi waliomtibu. Muda mfupi kabla mgonjwa huyo hajafa kwa kansa, mmoja wa wauguzi aliyemsaidia aliandika katika gazeti la wauguzi kuhusu mambo aliyoona kwa mgonjwa ambaye alimwita Angela.

“Angela ni mchangamfu na ameazimia kuishi. Anatambua hali yake na kwamba ugonjwa wake ni hatari, na kama ilivyo tamaa ya kila mmoja wetu, anatafuta suluhisho, au dawa. . . . Sisi wauguzi tulianza kumjua pole kwa pole. Hakukataa msaada wetu. Badala yake, hali ya Angela ya kuwa wazi ilifanya kila kitu kiwe rahisi. Tulifurahi kumsaidia, kwa kuwa tulijua kila mara kwamba tungekutana na mtu mnyoofu na kwamba sote tungefaidika. . . . Papo hapo, tulitambua kwamba dini yake ingekuwa kizuizi kwetu kutibu ugonjwa wake.” Hayo yalikuwa maoni ya muuguzi huyo kwa kuwa alihisi kwamba Angela angetiwa damu mishipani, jambo ambalo Angela alikataa.—Matendo 15:28, 29.

“Kwa kuwa tumezoezwa kutunza wagonjwa, tulimwambia Angela kwamba hatukubaliani na uamuzi aliochukua, lakini kwa msaada wake, tulielewa jinsi alivyoona umuhimu wa uhai. Pia, tulielewa jinsi yeye na familia yake wanavyoona umuhimu wa dini yao. Angela hajakata tamaa. Hajashindwa na ugonjwa. Ni mwenye nguvu. Anataka kuishi, ameazimia kupambana ili kuendelea kuishi. Amejulisha azimio lake, na imani yake. Ana azimio ambalo kwa kawaida hatuna, na imani yenye nguvu kuliko yetu. Angela ametufundisha umuhimu wa kuheshimu dini yake, ingawa kanuni zetu za kazi zinaenda kinyume cha imani yake. . . . Tunaamini kwamba yale ambayo Angela ametufundisha ni muhimu sana, kwa sababu tunashughulika na watu wa aina zote, hali zote, na dini zote, nasi tunaweza kujifunza kutoka kwao na hivyo kumfaidi mtu yeyote tunayeshughulika naye.”

Kisha makala ya gazeti hilo ilikazia Kanuni za Maadili Mazuri ya Kazi kwa ajili ya Wauguzi wa Kiitaliano, zilizoidhinishwa mwaka wa 1999, ambayo inasema: “Muuguzi hufanya kazi yake kwa kufikiria dini ya mtu mmoja-mmoja, maadili, na utamaduni, rangi na pia jinsia.” Wakati mwingine, inaweza kuwa vigumu kwa madaktari na wauguzi kuheshimu imani ya kidini ya mgonjwa, lakini bila shaka mgonjwa huthamini na kushukuru wale walio tayari kuheshimu imani yake.

Maamuzi ambayo Mashahidi wa Yehova hufanya kuhusiana na afya yao na utafiti wa kitiba hufikiriwa kwa makini. Wao hufikiria kwa uzito yale ambayo Maandiko husema, na kama ilivyoonyeshwa na kisa cha Angela, wao si wenye imani kali za kidini. (Wafilipi 4:5) Duniani pote, hesabu ya madaktari walio tayari kuheshimu dhamiri ya wagonjwa ambao ni Mashahidi inazidi kuongezeka.