Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kulea Watoto Wako?

Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kulea Watoto Wako?

Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kulea Watoto Wako?

UA LA okidi ni zuri sana, lakini ni vigumu sana kuliotesha. Ili ufanikiwe, unahitaji kurekebisha joto, mwangaza, na ukubwa wa kichungu. Ua hilo huathiriwa kwa urahisi na udongo na mbolea mbaya, na pia magonjwa na wadudu. Hivyo ni jambo la kawaida kushindwa kuliotesha mara ya kwanza.

Kulea watoto ni kazi ngumu hata zaidi kuliko kuotesha okidi, nayo huhitaji uangalifu pia. Hivyo, ni jambo la kawaida kwa wazazi kutojua la kufanya kuhusiana na kulea watoto. Wengi huhisi kwamba wanahitaji msaada, kama vile mtu anayepanda okidi anavyohitaji shauri kutoka kwa mtaalamu. Ni wazi kwamba, kila mzazi hutaka kupata mwongozo ulio bora. Anaweza kuupata wapi?

Ingawa Biblia si kitabu cha maagizo kuhusu kulea watoto, Muumba aliwaongoza waandikaji wa Biblia kwa roho yake ili waandike mashauri yafaayo kuhusu jambo hilo. Biblia hutilia mkazo kusitawisha sifa nzuri, ambazo mara nyingi wengi huhisi zinapuuzwa. (Waefeso 4:22-24) Kwa habari hiyo, shauri la Biblia ni muhimu sana ili kuelimisha watoto kwa njia iliyosawazika. Shauri hilo tayari limewanufaisha watu wengi ambao wamelitumia, bila kujali kipindi walichoishi au utamaduni wao. Hivyo, kufuata shauri la Biblia kunaweza kukusaidia ufanikiwe kulea watoto wako.

Wazazi Hufundisha Vizuri Zaidi kwa Kielelezo Chao

“Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi?”—Waroma 2:21, 22.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu la Seoul alisema: “Mtoto hufunzwa vizuri zaidi kwa kuwekewa kielelezo kizuri cha maneno na matendo” Wazazi wasipoweka kielelezo kizuri katika maneno na mwenendo na kumpa mtoto wao maagizo hususa, baada ya muda mfupi mtoto huyo atafikiri wao ni wanafiki. Maneno ya wazazi hayatakuwa na matokeo yoyote. Kwa mfano, ikiwa wazazi wanataka kumfundisha mtoto wao kusema kweli, wao wenyewe wanapaswa kusema kweli. Ni kawaida kwa wazazi fulani ambao hawataki kupokea simu kuwaambia watoto wao waseme, “Samahani, baba (au mama) hayuko.” Mtoto anayepewa agizo hilo ataona aibu na kuchanganyikiwa. Mwishowe, huenda akaanza kudanganya bila kuona aibu anapokuwa katika hali ngumu. Kwa hiyo, ikiwa kwa kweli wazazi wanataka mtoto wao asiseme uwongo, wao wenyewe wanapaswa kusema kweli na kutenda kupatana na maneno yao.

Je, unataka kumzoeza mtoto wako kuzungumza kwa adabu? Basi, lazima umwekee kielelezo kizuri. Mtoto wako atakuiga mara moja. Sung-sik, baba ya watoto wanne, anasema: “Mimi na mke wangu tuliamua tusitumie lugha chafu. Tuliheshimiana na hatukuinua sauti zetu hata tulipoudhika au kukasirika. Kielelezo kizuri kilikuwa na matokeo mazuri zaidi kuliko maneno matupu. Tunafurahi kwamba watoto wetu huzungumza na wengine kwa heshima na upole.” Biblia inasema hivi kwenye Wagalatia 6:7: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” Wazazi wanaotaka watoto wao wawe na maadili bora wanapaswa kwanza waonyeshe kwamba wao wenyewe wanafuata maadili hayo.

Dumisha Mawasiliano Mazuri

‘Kazia amri za Mungu kwa mwana wako na kuzisema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.’—Kumbukumbu la Torati 6:7.

Watu wengi wana mwelekeo wa kufanya kazi saa za ziada. Mume na mke wanapofanya kazi, hilo huathiri sana watoto. Wakati ambao wazazi wengi hutumia pamoja na watoto wao unapungua. Wanapokuwa nyumbani, wazazi wana kazi za nyumbani na kazi nyingine, hivyo huenda wakawa wamechoka sana. Katika hali hizo, mnawezaje kudumisha mawasiliano mazuri na watoto wenu? Mnaweza kupata nafasi za kuzungumza ikiwa ninyi na watoto wenu mnafanya kazi za nyumbani pamoja. Baba mmoja hata aliondoa televisheni, ili hasa awe na wakati mwingi zaidi wa kuzungumza na watoto wake. Alisema: “Mwanzoni, watoto walionekana kuchoka, lakini nilipocheza nao michezo ya mafumbo na kuzungumzia vitabu vyenye kupendeza, walianza kuzoea kukaa bila televisheni.”

Ni muhimu kwamba watoto wazoee kuzungumza na wazazi wao wakiwa wadogo. La sivyo, wanapokuwa matineja na labda wapatwe na matatizo, hawatawaona wazazi wao kuwa marafiki wanaoweza kuzungumza nao. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto waeleze yaliyo moyoni mwao? Methali 20:5 inasema: “Shauri moyoni mwa mtu ni kama kilindi cha maji, lakini mtu mwenye utambuzi ataliteka.” Kwa kutumia maswali ya maoni, kama vile, “Unaonaje?” wazazi wanaweza kuwatia moyo watoto wao waeleze maoni na hisia zao.

Utafanya nini mtoto wako akifanya kosa zito? Huo ndio wakati anaohitaji kuonyeshwa fadhili. Dhibiti hisia zako unapomsikiliza mtoto wako. Baba mmoja anasema hivi kuhusu jinsi anavyoshughulika na hali kama hiyo: “Watoto wanapofanya makosa, mimi hujitahidi nisichukue hatua inayopita kiasi. Mimi hukaa chini na kusikiliza wanayotaka kusema. Hujitahidi kuelewa hali. Ninapoona ni vigumu kudhibiti hasira, mimi hungoja kidogo na kujituliza.” Ukidhibiti hisia zako na usikilize, rekebisho utakalotoa litakubaliwa kwa rahisi.

Nidhamu Inayotegemea Upendo Ni Muhimu

“Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Ili kuwa na matokeo mazuri, njia unayotumia kutoa nidhamu yenye upendo ni muhimu. Wazazi wanawezaje ‘kuwakasirisha watoto wao’? Watoto watapinga nidhamu hiyo ikiwa haipatani na uzito wa kosa au inatolewa kwa shutuma kali. Sikuzote nidhamu yapaswa kutolewa kwa upendo. (Methali 13:24) Ukizungumza na watoto wako kwa akili, watatambua kwamba unawatia nidhamu kwa kuwa unawapenda.—Methali 22:15; 29:19.

Kwa upande mwingine, ni vizuri watoto wajue matokeo yasiyofaa ya mwenendo mbaya. Kwa mfano, mtoto akimkosea mtu mwingine, unaweza kusisitiza kwamba aombe msamaha. Anapovunja sheria za familia, unaweza kumnyima mapendeleo fulani ili kukazia umuhimu wa kufuata sheria.

Ni vizuri kutoa nidhamu wakati ufaao. Andiko la Mhubiri 8:11 linasema: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.” Vivyo hivyo, watoto wengi watajaribu kuona kama wanaweza kukwepa adhabu wanapokosa adabu. Hivyo, ukimwambia mtoto kwamba utamwadhibu akifanya kosa fulani, hakikisha kwamba unafanya hivyo.

Tafrija Ifaayo Ina Thamani

“Kuna . . . wakati wa kucheka . . . na wakati wa kurukaruka.”—Mhubiri 3:1, 4.

Tafrija ifaayo na yenye usawaziko ni muhimu ili mtoto akue akili na mwili. Wazazi wanapofurahia tafrija pamoja na watoto wao, uhusiano wao huimarika zaidi, nao watoto huhisi wakiwa salama. Familia inaweza kufurahia pamoja tafrija za aina gani? Mkifikiria jambo hilo, mnaweza kupata mambo mengi yenye kufurahisha mnayoweza kufanya pamoja. Kuna michezo ya nje, kama kuendesha baiskeli, na michezo ya mpira kama tenisi, mpira wa vinyoya, na voliboli. Wazia jinsi familia inavyoweza kufurahia kucheza ala za muziki pamoja. Familia inaweza kuwa na kumbukumbu nzuri baada ya kutembelea sehemu za karibu ili kufurahia uumbaji.

Katika hali hizo, wazazi wanaweza kukazia watoto wao wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu tafrija. Mwanamume mmoja Mkristo aliye na wana wanne alisema: “Mimi hujiunga na watoto wangu katika tafrija inapowezekana. Kwa mfano, wanapocheza michezo ya kompyuta, mimi huwauliza jinsi wanavyoicheza. Wanaponieleza kwa shauku jinsi ya kuicheza, mimi hutumia nafasi hiyo kuwaeleza hatari ya tafrija isiyofaa. Nimeona kwamba wao hukataa tafrija isiyofaa.” Naam, watoto wanaofurahia tafrija pamoja na familia nzima, hawatapendezwa sana na vipindi vya televisheni, video, sinema, na michezo ya Intaneti inayoonyesha mambo ya jeuri, uasherati, na matumizi ya dawa za kulevya.

Wasaidie Watoto Wako Wachague Marafiki Wazuri

“Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Baba mmoja Mkristo aliyefanikiwa kulea watoto wanne alisema: “Uchaguzi wao wa marafiki ni jambo muhimu sana. Rafiki mmoja mbaya anaweza kuharibu kazi yote ambayo umefanya.” Ili kuwasaidia watoto wake wachague marafiki wazuri, kwa hekima, aliwauliza maswali kama: Ni nani rafiki yako wa karibu? Kwa nini unampenda? Ana sifa gani unazotaka kuiga? Mzazi mwingine hupanga ili watoto wake waalike nyumbani marafiki wao wa karibu. Hivyo anaweza kuwachunguza na kuwasaidia watoto wake ifaavyo.

Ni muhimu pia kuwafundisha watoto kwamba wanaweza kufanya urafiki na watu wenye umri mkubwa na pia marika wao. Bum-sun, baba ya wana watatu, anasema: “Mimi huwasaidia watoto wangu waelewe kwamba marafiki wao wanaweza kuwa na umri mkubwa kuwashinda, kama ilivyokuwa katika kisa cha Daudi na Yonathani katika Biblia. Kwa kweli, mimi hualika Wakristo wenye umri mbalimbali ili wafurahie ushirika pamoja na watoto wangu. Hivyo, watoto wangu hushirikiana na watu wengi wenye umri tofauti na wao.” Kushirikiana na watu wazima ambao ni vielelezo vizuri huwasaidia watoto wajifunze mambo mengi.

Unaweza Kufanikiwa Kuwazoeza Watoto Wako

Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanywa Marekani, wazazi wengi waliojaribu kuwakazia watoto wao sifa kama kujizuia, kujitia nidhamu, na kusema kweli, walifanikiwa kidogo tu. Kwa nini ni vigumu sana kufanya hivyo? Mama mmoja aliyehojiwa alisema: ‘Jambo la kusikitisha ni kwamba njia pekee ya kuwalinda watoto wetu ni kuwafungia katika chumba fulani na kutowaruhusu kamwe watoke nje katika ulimwengu.’ Alikuwa anamaanisha kwamba mazingira ambayo watoto wanakulia ni mabaya sana sasa kuliko wakati mwingine wowote. Katika hali hiyo, je, kweli inawezekana kulea watoto kwa mafanikio?

Unaweza kuvunjika moyo ikiwa unataka kuotesha ua la okidi na una wasiwasi kwamba litakauka. Ungefurahi kama nini ikiwa mtaalamu wa kuotesha okidi angekuja na kukupa mashauri mazuri na kukuambia hivi kwa uhakika: “Utafanikiwa ukifanya hivi”! Yehova, ambaye ndiye anayejua vizuri zaidi maumbile ya mwanadamu, hutoa mashauri mazuri zaidi kuhusu kulea watoto. Anasema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” (Methali 22:6) Unapowazoeza watoto wako kupatana na shauri la Biblia, yaelekea utafurahia kuwaona wakikua na kuwa watu wazima wenye kutegemeka, kuwajali wengine, na kuzingatia maadili. Kisha, watapendwa na watu, na zaidi ya yote, watapendwa na Yehova, Baba yetu wa mbinguni.