Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye Hai

Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye Hai

Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye Hai

“Mgeuke . . . mpate kumjia Mungu aliye hai, aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.”—MATENDO 14:15.

1, 2. Kwa nini inafaa kumtambua Yehova kuwa “Mungu aliye hai”?

BAADA ya mitume Paulo na Barnaba kumponya mtu fulani, Paulo aliwahakikishia hivi watazamaji huko Listra: “Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu uleule kama ninyi, nasi tunawatangazia ninyi habari njema, ili mgeuke kutoka kwa mambo haya ya bure mpate kumjia Mungu aliye hai, aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.”—Matendo 14:15.

2 Kwa kweli, Yehova ni “Mungu aliye hai” wala si sanamu isiyo hai! (Yeremia 10:10; 1 Wathesalonike 1:9, 10) Zaidi ya kuwa hai, Yehova ndiye Chanzo cha uhai wetu. “Yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Anataka tufurahie uhai sasa na wakati ujao. Paulo aliongeza kusema kwamba Mungu “hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.

3. Kwa nini tunaweza kutumaini mwongozo wa Mungu?

3 Kwa kuwa Mungu anapendezwa na uhai wetu hiyo hutupa sababu ya kutumaini mwongozo wake. (Zaburi 147:8; Mathayo 5:45) Huenda wengine wasikubali mwongozo wake wakipata amri ya Biblia wasiyoielewa au inayoonekana kuwa inawazuia kufanya jambo fulani. Lakini limekuwa jambo la hekima kutumaini mwongozo wa Yehova. Kwa mfano: Hata kama Mwisraeli hakuelewa sheria kuhusu kutogusa maiti, alinufaika kwa kuitii. Kwanza, utii wake ungemfanya amkaribie Mungu aliye hai; pili, ungemsaidia kuepuka magonjwa.—Mambo ya Walawi 5:2; 11:24.

4, 5. (a) Kabla ya enzi ya Ukristo, Yehova alitoa mwongozo gani kuhusu damu? (b) Tunajuaje kwamba mwongozo wa Mungu kuhusu damu unawahusu Wakristo?

4 Ndivyo ilivyo na mwongozo wa Mungu kuhusu damu. Alimwambia Noa kwamba wanadamu hawapaswi kula damu. Kisha katika Sheria, Mungu akafunua kwamba damu ilipaswa kutumiwa tu kwenye madhabahu—kwa ajili ya msamaha wa dhambi. Kupitia miongozo hiyo Mungu alikuwa akiweka msingi kwa ajili ya matumizi yaliyo bora zaidi ya damu, yaani, kuokoa uhai kupitia fidia ya Yesu. (Waebrania 9:14) Naam, Mungu alitoa mwongozo huo kwa kufikiria uhai na hali yetu njema. Akizungumzia andiko la Mwanzo 9:4, msomi wa Biblia wa karne ya 19, Adam Clarke, aliandika hivi: “Amri hii [kwa Noa] ingali inafuatwa kwa makini na Wakristo wa Kanisa la Othodoksi . . . Chini ya sheria, damu haikuliwa, kwa sababu iliwakilisha ile damu ambayo ingemwagwa kwa ajili ya dhambi za ulimwengu; na chini ya mpango wa Kikristo damu hiyo haipaswi kuliwa, kwa sababu sikuzote inapaswa kuonwa kuwa inawakilisha damu ambayo imemwagwa kwa ajili ya msamaha wa dhambi.”

5 Huenda msomi huyo alikuwa akirejelea habari njema za msingi kumhusu Yesu. Habari hizo zinatia ndani Mungu kumtuma Mwanaye kufa kwa ajili yetu, amwage damu yake ili tuweze kupata uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; Waroma 5:8, 9) Maelezo ya msomi huyo yalitia ndani pia amri ya baadaye kwamba wafuasi wa Kristo wajiepushe na damu.

6. Wakristo walipewa mwongozo gani kuhusu damu, na kwa nini?

6 Unajua kwamba Mungu aliwapa Waisraeli masharti mengi sana. Yesu alipokufa, haikuwa lazima kwa wanafunzi wake kufuata sheria hizo zote. (Waroma 7:4, 6; Wakolosai 2:13, 14, 17; Waebrania 8:6, 13) Hata hivyo, baada ya muda kulitokea swali kuhusu sharti moja la msingi—kutahiriwa kwa wanaume. Je, ingekuwa lazima kwa watu wasio Wayahudi waliotaka kunufaika na damu ya Kristo watahiriwe ili kuonyesha kwamba bado walikuwa chini ya Sheria? Mnamo mwaka wa 49 W.K., baraza linaloongoza la Kikristo lilishughulikia suala hilo. (Matendo, sura ya 15) Wakisaidiwa na roho ya Mungu, mitume na wanaume wazee walifikia mkataa kwamba lile takwa la kutahiriwa lilikoma pamoja na Sheria. Lakini, kuna baadhi ya matakwa ya Mungu ambayo Wakristo walihitaji kuendelea kuyafuata. Baraza linaloongoza liliandikia makutaniko barua hii: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi, ila mambo haya ya lazima, kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu na damu na vitu vilivyonyongwa na uasherati. Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa.”—Matendo 15:28, 29.

7. Ni jambo muhimu kadiri gani kwa Wakristo ‘kujiepusha na damu’?

7 Ni wazi kwamba baraza linaloongoza liliona kwamba ‘kujiepusha na damu’ ni muhimu kiadili kama vile kujiepusha na uasherati au ibada ya sanamu. Hiyo inathibitisha kwamba katazo la damu ni jambo zito. Wakristo wanaofanya uasherati au kuabudu sanamu bila kutubu hawawezi ‘kuurithi ufalme wa Mungu’; “fungu lao litakuwa . . . kifo cha pili.” (1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8; 22:15) Ona tofauti: Kupuuza mwongozo wa Mungu kuhusu utakatifu wa damu kunaweza kutokeza kifo cha milele. Kuheshimu dhabihu ya Yesu kunaweza kuongoza kwenye uzima wa milele.

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walichukua kwa uzito mwongozo wa Mungu kuhusu damu?

8 Wakristo wa mapema walielewa na kufuataje mwongozo wa Mungu kuhusu damu? Kumbuka maelezo ya Clarke: “Chini ya mpango wa Kikristo haipaswi kuliwa, kwa sababu sikuzote inapaswa kuonwa kuwa inawakilisha damu ambayo imemwagwa kwa ajili ya msamaha wa dhambi.” Historia inathibitisha kwamba Wakristo wa mapema waliona jambo hilo kuwa zito sana. Tertullian aliandika: “Fikiria jinsi ambavyo wale wenye kiu yenye pupa kwenye maonyesho katika uwanja, hunywa damu mbichi ya wahalifu waovu . . . na kuichukua ili wakaponye ugonjwa wao wa kifafa.” Ingawa wapagani walikula damu, Tertullian alisema kwamba Wakristo “hata hawana damu ya wanyama kwenye chakula [chao] . . . Kwenye kesi za Wakristo, nyinyi huwapa soseji zilizojazwa damu. Bila shaka, tayari mnajua kwamba [hiyo] ni kinyume cha sheria yao.” Naam, licha ya kutishwa kuuawa, Wakristo walikataa kabisa kula damu. Mwongozo wa Mungu ulikuwa muhimu sana kwao.

9. Kujiepusha na damu kulitia ndani nini mbali na kuila moja kwa moja?

9 Huenda wengine wakafikiri kwamba baraza linaloongoza lilimaanisha tu kwamba Wakristo hawakupaswa kula au kunywa damu moja kwa moja, kula nyama iliyo na damu, au kuchanganya damu na chakula. Ni kweli kwamba Mungu alimaanisha hivyo mwanzoni alipompa Noa amri hiyo. Nalo agizo la mitume liliwaeleza Wakristo ‘wajiepushe na vitu vilivyonyongwa,’ yaani, nyama iliyo na damu. (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 21:25) Hata hivyo, Wakristo wa mapema walijua kwamba kuna mengi yaliyohusika. Wakati mwingine, damu ililiwa kwa sababu za kitiba. Tertullian alisema kwamba wapagani fulani walikunywa damu mbichi ili kuponya ugonjwa wao wa kifafa. Na huenda kulikuwa na matumizi mengine ya damu ya kutibu magonjwa au kuboresha afya. Hivyo, msimamo wa Wakristo wa kuepuka damu ulitia ndani kutoitumia kwa sababu za “kitiba.” Walidumisha msimamo huo hata kama kufanya hivyo kungehatarisha uhai wao.

Kutumia Damu Kama Dawa

10. Damu inatumiwa katika njia zipi kitiba, na hiyo inatokeza swali gani?

10 Leo ni jambo la kawaida kutumia damu kama dawa. Mwanzoni, watu walitiwa damu mishipani ikiwa na sehemu zake zote. Damu hiyo ilitolewa kwa mtu, ikahifadhiwa, na kutiwa mgonjwa, labda majeruhi wa vita. Baadaye, wachunguzi walijua jinsi ya kutenganisha damu katika sehemu kuu mbalimbali. Kwa kutumia sehemu kuu za damu, madaktari wangeweza kugawanya damu iliyotolewa kuwatibu wagonjwa wengi zaidi, labda mtu aliyejeruhiwa angetiwa plazima (umajimaji wa damu) naye mwingine atiwe chembe nyekundu. Baada ya uchunguzi zaidi ilionekana kwamba sehemu fulani ya damu, kama vile plazima, inaweza kugawanywa kuwa visehemu mbalimbali, na hivyo kutumiwa kuwatibu wagonjwa wengi zaidi. Jitihada za kugawanya damu katika visehemu zaidi bado zinaendelea, na matumizi mapya ya visehemu hivyo yanaendelea kuripotiwa. Mkristo afanyeje kuhusiana na matumizi ya visehemu hivyo? Tuseme Mkristo ameamua kabisa kutotiwa damu mishipani, lakini daktari wake anamhimiza akubali kutiwa mojawapo ya zile sehemu kuu za damu, labda chembe nyekundu zilizotengenishwa. Au huenda matibabu hayo yakahusisha matumizi ya kisehemu kimoja tu kilichotokana na sehemu moja kuu. Mtumishi wa Mungu anawezaje kuamua kuhusu maswali hayo, kwa kukumbuka kwamba damu ni takatifu na kwamba damu ya Kristo inaokoa uhai katika maana iliyo kubwa zaidi?

11. Kwa miaka mingi, Mashahidi wamechukua msimamo gani sahihi wa kitiba kuhusu damu?

11 Mashahidi wa Yehova walijulisha waziwazi msimamo wao miaka mingi iliyopita. Kwa mfano, waliandika makala iliyochapishwa katika The Journal of the American Medical Association (Novemba 27, 1981; ilichapishwa tena katika broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? ukurasa wa 27-29). * Makala hiyo ilinukuu kitabu cha Mwanzo, Mambo ya Walawi, na Matendo. Ilisema: ‘Ingawa mistari hii haikusemwa kwa semi za kitiba, Mashahidi huiona kuwa hairuhusu kutiwa mishipani damu nzima, RBCs, na plazima, pamoja na WBC na vigandisha-damu.’ Kitabu Emergency Care, cha mwaka wa 2001, chini ya kichwa, “Composition of the Blood” (Sehemu za Damu), kilisema: “Damu imefanyizwa kwa sehemu mbalimbali: plazima, chembe nyekundu na nyeupe, na vigandisha-damu.” Hivyo, kupatana na habari za kitiba, Mashahidi hukataa kutiwa damu ikiwa na sehemu zake zote au yoyote kati ya sehemu zake kuu nne.

12. (a) Ni msimamo gani ambao umetolewa kuhusu visehemu vya damu vilivyotolewa katika zile sehemu kuu za damu? (b) Unaweza kupata wapi habari za ziada kuhusu matumizi ya damu?

12 Makala hiyo ya kitiba iliendelea kusema: “Uelewevu wa kidini wa Mashahidi haukatazi kabisa kabisa utumizi wa sehemu kama vile albyumini, globyulini za kinga, na matayarisho ya hemofiliaki; kila Shahidi lazima aamue kama aweza kupokea hivi.” Tangu 1981, visehemu vingi (ambavyo hutolewa katika mojawapo ya sehemu kuu nne za damu) vimetenganishwa kwa ajili ya matumizi ya kitiba. Hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2000, lilitoa habari zenye manufaa kuhusu matumizi ya damu katika makala, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji.” Ili kunufaisha wasomaji wengi leo, jibu hilo limechapishwa tena katika ukurasa wa 29-31 wa gazeti hili. Inaeleza mambo kindani na kutoa hoja kwa njia ya akili, lakini utaona kwamba yale ambayo makala hiyo inasema yanakubaliana na mambo ya msingi yaliyochapishwa mnamo 1981.

Daraka la Dhamiri Yako

13, 14. (a) Dhamiri ni nini, nayo inahusikaje katika mambo yanayohusu damu? (b) Mungu aliwapa Waisraeli mwongozo gani kuhusu kula nyama, lakini ni maswali gani ambayo huenda yalitokea?

13 Habari hizo humtaka mtu atumie dhamiri yake. Kwa nini? Wakristo wanakubali kwamba wanahitaji kufuata mwongozo wa Mungu, lakini katika hali fulani lazima wafanye maamuzi ya kibinafsi nayo huhusisha dhamiri. Dhamiri ni uwezo wa asili wa kuchanganua na kuamua mambo, mara nyingi mambo yanayohusiana na maadili. (Waroma 2:14, 15) Hata hivyo, unajua kwamba dhamiri hutofautiana. * Biblia hutaja kwamba watu wengine wana ‘dhamiri zilizo dhaifu,’ ikimaanisha kwamba kuna wengine walio na dhamiri zenye nguvu. (1 Wakorintho 8:12) Wakristo hutofautiana katika kiwango cha kufanya maendeleo kuhusiana na kujifunza mapenzi ya Mungu, kujua maoni yake, na kutumia maoni hayo wanapofanya maamuzi. Tunaweza kuonyesha jambo hilo kwa kufikiria Wayahudi na ulaji wa nyama.

14 Biblia inaonyesha wazi kwamba mtu anayemtii Mungu hapaswi kula nyama isiyotolewa damu. Hiyo ilikuwa muhimu sana hivi kwamba hata wakati wa dharura ambapo askari wa Israeli walikula nyama isiyotolewa damu, walikuwa na hatia ya kosa au dhambi nzito. (Kumbukumbu la Torati 12:15, 16; 1 Samweli 14:31-35) Hata hivyo, huenda kulitokea maswali. Mwisraeli alipomuua kondoo, alipaswa kutoa damu yake haraka kadiri gani? Je, alipaswa kukata koo la mnyama ili aitoe? Je, ilikuwa lazima kumning’iniza kondoo huyo kwa miguu yake ya nyuma? Kwa muda gani? Angeitoaje damu ya ng’ombe mkubwa? Hata baada ya kuitoa, kiasi fulani cha damu kingeweza kubaki katika nyama. Je, angekula nyama hiyo? Ni nani angeamua?

15. Wayahudi fulani walitendaje kuhusiana na kula nyama, lakini Mungu alitoa agizo gani?

15 Wazia Myahudi mwenye bidii aliyekabili masuala hayo. Huenda angefikiri kwamba ni salama zaidi kuepuka nyama zilizouzwa sokoni, huku Myahudi mwingine akikataa kula nyama ambayo huenda kwanza ilikuwa imetolewa kwa sanamu. Huenda Wayahudi wengine walikula nyama tu baada ya kufuata desturi fulani za kutoa damu. * (Mathayo 23:23, 24) Unaonaje kuhusu hatua hizo tofauti? Isitoshe, kwa kuwa Mungu hakuwataka watende hivyo, je, ingefaa Wayahudi walipelekee baraza la marabi maswali mengi ili watoe uamuzi kuhusu kila mojawapo ya maswali hayo? Ingawa Dini ya Kiyahudi ilikuwa na desturi hiyo, tunaweza kufurahi kwamba Yehova hakuwaagiza waabudu wa kweli waamue mambo yanayohusiana na damu kwa njia hiyo. Mungu alitoa mwongozo wa msingi juu ya kuchinja wanyama safi na kutoa damu yao, lakini hakusema zaidi ya hayo.—Yohana 8:32.

16. Kwa nini huenda Wakristo wakawa na maoni yaliyotofautiana kuhusu kukubali kudungwa sindano yenye kisehemu fulani kidogo kilichotokana na sehemu fulani ya damu?

16 Kama ilivyotajwa katika mafungu ya 11 na 12, Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu ikiwa na sehemu zake zote au zile sehemu zake kuu nne, yaani, plazima, chembe nyekundu, chembe nyeupe, na vigandisha-damu. Namna gani visehemu vidogo vinavyotolewa katika mojawapo ya zile sehemu kubwa, kama vile umajimaji wenye kinga za mwili za kupambana na ugonjwa au sumu ya nyoka? (Ona ukurasa wa 30, fungu la 4.) Wengine wamefikia mkataa kwamba visehemu vidogo fulani si damu na hivyo havihusishwi katika amri ya ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:29; 21:25; ukurasa wa 31, fungu la 1) Watatoa hesabu kwa maamuzi yao. Dhamiri za wengine huwachochea wakatae chochote kinachotokana na damu (ya wanyama au ya binadamu), hata kama ni kisehemu kidogo tu cha mojawapo ya zile sehemu kuu. * Huenda wengine wakakubali kudungwa sindano za plazima yenye protini ili kupambana na ugonjwa au sumu ya nyoka, lakini huenda wakatae visehemu vingine vidogo. Isitoshe, huenda kazi inayotimizwa na visehemu fulani vinavyotolewa katika mojawapo ya zile sehemu kuu nne ikafanana sana na kazi ya sehemu hiyo kuu ya damu ya kutegemeza uhai mwilini hivi kwamba Wakristo wengi wangeviona kuwa visivyokubalika.

17. (a) Dhamiri yetu inaweza kutusaidiaje tunapokabili masuala yanayohusu visehemu vya damu? (b) Kwa nini ni jambo zito sana kufanya maamuzi kuhusu suala hilo?

17 Yale ambayo Biblia husema kuhusu dhamiri hutusaidia tunapofanya maamuzi kama hayo. Hatua ya kwanza ni kujifunza yale yanayosemwa na Neno la Mungu na kujitahidi kuzoeza dhamiri yako kuyafuata. Hilo litakusaidia kuamua mambo kupatana na mwongozo wa Mungu, badala ya kumwomba mtu mwingine akuamulie. (Zaburi 25:4, 5) Kuhusu kukubali visehemu fulani vya damu, wengine wamewaza, ‘Hili ni jambo linalotegemea dhamiri, hivyo si la maana.’ Huko si kufikiri kuzuri. Kwa kuwa tu jambo fulani linategemea dhamiri, hiyo haimaanishi kwamba halina maana. Linaweza kuwa jambo zito sana. Sababu moja ni kwamba linaweza kuathiri watu ambao dhamiri zao si sawa na zetu. Tunaona jambo hilo kutokana na shauri la Paulo kuhusu nyama ambazo huenda zilikuwa kwanza zimetolewa kwa sanamu na baadaye kuuzwa sokoni. Mkristo anapaswa kuhangaika kuhusu ‘kuumiza dhamiri zilizo dhaifu.’ Akiwakwaza wengine, anaweza ‘kumharibu ndugu yake ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake’ na hivyo kutenda dhambi dhidi ya Kristo. Kwa hiyo, ingawa mtu binafsi ndiye anayepaswa kuamua kuhusu matumizi ya visehemu vidogo vya damu, maamuzi hayo yanapaswa kuchukuliwa kwa uzito sana.—1 Wakorintho 8:8, 11-13; 10:25-31.

18. Mkristo anawezaje kuepuka kuruhusu dhamiri yake ife ganzi anapofanya maamuzi kuhusu damu?

18 Jambo lingine la kufikiria linakazia uzito wa maamuzi unayofanya kuhusu damu. Jambo hilo linahusu jinsi unavyoweza kuathiriwa na maamuzi yako. Ikiwa kukubali kisehemu kidogo cha damu kungesumbua dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia, basi hupaswi kuipuuza. Wala hupaswi kupuuza mwelekezo wa dhamiri yako kwa kuwa tu mtu fulani anakuambia, “Ni sawa tu kukubali kisehemu hiki; wengi wamekikubali.” Kumbuka, leo watu wengi sana hupuuza dhamiri yao, nayo hufa ganzi, na kuwaruhusu wadanganye au kufanya makosa mengine bila kuhisi majuto. Bila shaka, Wakristo wanataka kuepuka mtazamo huo.—2 Samweli 24:10; 1 Timotheo 4:1, 2.

19. Tunapoamua masuala ya kitiba yanayohusu damu, tunapaswa kukumbuka hasa jambo gani?

19 Sehemu ya mwisho ya makala iliyochapwa tena ya jibu hilo kwenye ukurasa wa 29-31 inasema: “Je, jambo la kwamba maoni na maamuzi yanayotegemea dhamiri yaweza kutofautiana laonyesha kwamba hilo ni jambo dogo tu? La. Jambo hilo ni zito.” Ni zito sana kwa sababu uhusiano wako na “Mungu aliye hai” unahusika. Uhusiano huo ndio tu unaoweza kukuongoza kwenye uzima wa milele, unaotegemea nguvu za kuokoa za damu ya Yesu iliyomwagwa. Sitawisha heshima kubwa kuelekea damu kwa sababu ya yale Mungu anayotimiza kupitia damu, yaani, kuokoa uhai. Kwa kufaa, Paulo aliandika hivi: “Hamkuwa na tumaini na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu. Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati mmoja mlikuwa mbali sana mmekuja kuwa karibu kupitia damu ya Kristo.”Waefeso 2:12, 13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Wakati mmoja, Paulo na Wakristo wengine wanne walienda hekaluni ili kujitakasa kisherehe. Ingawa Sheria haikuwa halali tena, Paulo alifuata shauri la wanaume wazee huko Yerusalemu. (Matendo 21:23-25) Hata hivyo, huenda Wakristo fulani walihisi kwamba hawangeenda hekaluni wala kujitakasa kisherehe. Dhamiri zilitofautiana wakati huo, na bado hutofautiana leo.

^ fu. 15 Kichapo Encyclopaedia Judaica kinataja sheria “tata na ndogo-ndogo” kuhusu nyama “inayofaa.” Kinataja wakati ambao nyama inapaswa kukaa ndani ya maji, jinsi ya kuitoa umajimaji ikiwa kwenye ubao, aina ya chumvi inayopaswa kupakwa nyama hiyo, kisha mara ambazo ingepaswa kuoshwa katika maji baridi.

^ fu. 16 Sanasana watu hudungwa sindano ya umajimaji usiotokana na damu. Lakini katika visa vingine, umajimaji huo unaweza kuchanganywa na kisehemu fulani cha damu kama albyumini.—Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 1994.

Je, Unaweza Kukumbuka?

• Mungu alitoa mwongozo gani kuhusu damu kwa Noa, Waisraeli, na kwa Wakristo?

• Mashahidi wa Yehova hukataa nini katakata kuhusu damu?

• Ni katika maana gani kukubali visehemu vidogo vinavyotokana na sehemu kuu za damu kunategemea dhamiri ya mtu, lakini hiyo haimaanishi nini?

• Tunapofanya maamuzi, kwa nini tunapaswa kufikiria hasa uhusiano wetu na Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 22]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MSIMAMO WA MSINGI KUHUSU DAMU

DAMU NZIMA

HAIKUBALIKI

Chembe nyekundu

Chembe nyeupe

vigandisha-damu

Plazima

UAMUZI WA MKRISTO

Visehemu vilivyotolewa kwenye chembe nyekundu

Visehemu vilivyotolewa kwenye chembe nyeupe

Visehemu vilivyotolewa kwenye vigandisha-damu

Visehemu vilivyotolewa kwenye plazima

[Picha katika ukurasa wa 20]

Baraza linaloongoza lilifikia mkataa kwamba Wakristo wanapaswa ‘kujiepusha na damu’

[Picha katika ukurasa wa 23]

Usipuuze dhamiri yako ikiwa unafanya uamuzi kuhusu kisehemu fulani cha damu