Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Ifaavyo Zawadi Yako ya Uhai

Thamini Ifaavyo Zawadi Yako ya Uhai

Thamini Ifaavyo Zawadi Yako ya Uhai

“Damu ya Kristo . . . itazisafisha dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai.”—WAEBRANIA 9:14.

1. Kuna uthibitisho gani kwamba tunathamini sana uhai?

KAMA ungeombwa ukadirie thamani ya uhai wako, ungejibuje? Tunathamini sana uhai—wetu wenyewe na ule wa wengine. Na hiyo ni kweli, kwa kuwa huenda tukaenda kumwona daktari tunapokuwa wagonjwa au tunapotaka kufanyiwa uchunguzi wa kawaida wa kitiba. Tunataka kuendelea kuwa hai na wenye afya. Hata wengi walio wazee au walemavu, hawataki kufa; wanataka kuendelea kuwa hai.

2, 3. (a) Andiko la Methali 23:22 linakazia wajibu gani? (b) Mungu anahusikaje katika wajibu unaotajwa kwenye Methali 23:22?

2 Uhusiano wako pamoja na wengine huathiriwa na jinsi unavyothamini uhai. Kwa mfano, Neno la Mungu hutuagiza hivi: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako kwa sababu tu amezeeka.” (Methali 23:22) “Kusikiliza” humaanisha mengi zaidi ya kusikia maneno tu; methali hiyo inamaanisha kusikia kisha kutii. (Kutoka 15:26; Kumbukumbu la Torati 7:12; 13:18; 15:5; Yoshua 22:2; Zaburi 81:13) Kwa nini Neno la Mungu linasema usikilize baba na mama yako? Si kwa sababu tu baba na mama yako wana umri mkubwa kuliko wewe au wana ujuzi zaidi. Sababu ni kwamba ‘walikuzaa.’ Biblia fulani hutafsiri hivi mstari huo: “Msikilize baba yako aliyekupa uhai.” Inaeleweka kwamba, kama unathamini uhai wako, unahisi ukiwa na wajibu kwa chanzo cha uhai huo.

3 Bila shaka, ikiwa wewe ni Mkristo wa kweli unamtambua Yehova kuwa Chanzo hasa cha uhai wako. Kwake yeye ‘una uhai;’ unaweza ‘kwenda,’ kuhisi; na sasa ‘uko,’ na unaweza kufikiri au kupangia wakati ujao, kutia ndani uzima wa milele. (Matendo 17:28; Zaburi 36:9; Mhubiri 3:11) Kupatana na andiko la Methali 23:22, inafaa ‘kumsikiliza’ Mungu kwa utii, ukiwa na tamaa ya kuelewa na kutenda kupatana na maoni yake kuhusu uhai badala ya kuwa na maoni tofauti na yake.

Heshimu Uhai

4. Mapema katika historia ya mwanadamu, heshima kwa uhai ilipataje kuwa suala muhimu?

4 Mapema katika historia ya mwanadamu, Yehova alionyesha wazi kwamba hakuwaruhusu wanadamu watumie (au watumie vibaya) uhai kwa njia yoyote ile. Akiwa mwenye hasira nyingi yenye wivu, Kaini alimuua ndugu yake Abeli asiyekuwa na hatia. Je, unafikiri kwamba Kaini alikuwa na haki ya kufanya uamuzi kama huo kuhusu uhai? Mungu hakufikiri hivyo. Alimtaka Kaini atoe hesabu: “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.” (Mwanzo 4:10) Ona kwamba damu ya Abeli kwenye udongo iliwakilisha uhai wake, uliokuwa umekatishwa kikatili, nayo ilimlilia Mungu alipize kisasi.—Waebrania 12:24.

5. (a) Mungu aliweka kizuizi gani katika siku za Noa, nacho kiliwahusu nani? (b) Kizuizi hicho kilikuwa hatua muhimu katika maana gani?

5 Baada ya Gharika, jamii ya kibinadamu ilianza upya ikiwa na watu wanane tu. Katika tangazo kwa wanadamu wote, Mungu alitoa habari zaidi kuhusu jinsi anavyothamini uhai na damu. Alisema kwamba wanadamu wanaweza kula nyama, lakini akaweka kizuizi hiki: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote. Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake—damu yake—msile.” (Mwanzo 9:3, 4) Wayahudi fulani hufasiri mstari wa 4 kuwa unamaanisha kwamba wanadamu hawakupaswa kula nyama au damu ya mnyama aliye hai. Lakini baadaye ilionyeshwa wazi kwamba hapa Mungu alikataza kula damu ili kutegemeza uhai. Isitoshe, amri ya Mungu kupitia Noa ilikuwa hatua muhimu katika kutimizwa kwa kusudi Lake kuu kuhusu damu—kusudi ambalo lingewawezesha wanadamu kupata uzima wa milele.

6. Kupitia Noa, Mungu alikaziaje maoni Yake kuhusu thamani ya uhai?

6 Mungu aliendelea kusema: “Damu ya nafsi zenu nitaitaka. Kwa mkono wa kila kiumbe kilicho hai nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa kila mmoja ambaye ni ndugu yake, nitaitaka nafsi ya mwanadamu. Yeyote anayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake nayo itamwagwa na mwanadamu, kwa maana kwa mfano wa Mungu alimfanya mwanadamu.” (Mwanzo 9:5, 6) Unaweza kuona kutokana na tangazo hilo lililotolewa kwa wanadamu wote kwamba Mungu huiona damu ya mwanadamu kuwa inawakilisha uhai. Muumba humpa mtu uhai, na hakuna mtu anayepaswa kukomesha uhai huo unaowakilishwa na damu. Ikiwa kama Kaini, mtu anamuua mwenzake, Muumba ana haki ya ‘kutaka’ uhai wa muuaji huyo.

7. Kwa nini tupendezwe na tangazo ambalo Mungu alimtolea Noa kuhusu damu?

7 Kupitia tangazo lake, Mungu alikuwa akiwaamuru wanadamu wasiitumie damu vibaya. Je, umewahi kujiuliza ni kwa nini? Naam, kwa nini Mungu alikuwa na maoni hayo kuhusu damu? Kwa kweli, jibu linahusu mojawapo ya mafundisho muhimu zaidi ya Biblia. Hilo ni fundisho la msingi katika ujumbe wa Kikristo, ingawa dini nyingi hulipuuza. Fundisho hilo ni gani, nalo linahusuje maisha, maamuzi, na matendo yako?

Damu Ingeweza Kutumiwaje?

8. Yehova aliweka kizuizi gani kuhusu matumizi ya damu katika Sheria?

8 Yehova alitoa habari zaidi kuhusu uhai na damu alipowapa Waisraeli Sheria. Alipowapa Sheria, Mungu alichukua hatua nyingine katika kutimiza kusudi lake. Labda unajua kwamba kulingana na Sheria, Waisraeli walitakiwa kumtolea Mungu matoleo kama vile nafaka, mafuta, na divai. (Mambo ya Walawi 2:1-4; 23:13; Hesabu 15:1-5) Pia walitakiwa kutoa dhabibu za wanyama. Mungu alisema hivi kuhusu dhabihu hizo: “Nafsi ya mwili iko katika damu, nami mwenyewe nimeiweka juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu, kwa sababu damu ndiyo hufanya upatanisho kupitia nafsi iliyo ndani yake. Ndiyo sababu nimewaambia wana wa Israeli: ‘Nafsi yoyote kati yenu isile damu.’” Yehova aliongeza kusema kwamba ikiwa mtu kama vile mwindaji au mkulima aliua mnyama kwa ajili ya chakula, alipaswa kutoa damu na kuifunika kwa mavumbi. Kwa kuimwaga damu hiyo kwenye dunia ambayo ni kiti cha miguu cha Mungu, mtu huyo alitambua kwamba uhai huo ulikuwa ukirudishwa kwa Mpaji-Uhai.—Mambo ya Walawi 17:11-13; Isaya 66:1.

9. Kulingana na Sheria damu ingetumiwa kwa jambo gani pekee, na kusudi lilikuwa nini?

9 Sheria hiyo haikuwa desturi tu ya kidini isiyo na maana kwetu. Je, uliona ni kwa nini Waisraeli hawakupaswa kula damu? Mungu alisema: “Ndiyo sababu nimewaambia wana wa Israeli: ‘Nafsi yoyote kati yenu isile damu.’” Kwa nini alisema hivyo? “Nami mwenyewe nimeiweka juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Je, unaona kwamba andiko hilo linafafanua ni kwa nini Mungu alimwambia Noa kwamba wanadamu hawapaswi kula damu? Muumba aliamua kuiona damu kuwa na umuhimu mkubwa sana, na kukubali itumiwe tu kwa njia moja ya pekee ambayo ingeweza kuokoa uhai wa watu wengi. Damu ingetimiza fungu kubwa katika kufunika dhambi (upatanisho). Kwa hiyo, chini ya Sheria, Yehova alikubali damu itumiwe tu kwenye madhabahu ili kufanya upatanisho kwa ajili ya uhai wa Waisraeli, waliotaka kupata msamaha wake.

10. Kwa nini damu ya mnyama haingeweza kutokeza msamaha kamili, lakini dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria ziliwakumbusha Waisraeli nini?

10 Wazo hilo linajulikana katika Ukristo. Akirejelea sehemu hiyo ya Sheria iliyopangwa na Mungu, mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na damu isipomwagwa hakuna msamaha unaotokea.” (Waebrania 9:22) Paulo alionyesha wazi kwamba dhabihu zilizotolewa hazikuwafanya Waisraeli wawe wanadamu wakamilifu, wasio na dhambi. Aliandika hivi: “Kwa dhabihu hizo kuna kukumbusha juu ya dhambi mwaka baada ya mwaka, kwa maana haiwezekani damu ya ng’ombe na ya mbuzi kuondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Hata hivyo, dhabihu hizo zilitimiza kusudi fulani. Ziliwakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa wenye dhambi na walihitaji kitu fulani zaidi ili kupata msamaha kamili. Lakini ikiwa damu ambayo iliwakilisha uhai wa wanyama haingeweza kufunika kabisa dhambi za wanadamu, je, kuna damu nyingine ambayo ingeweza kufanya hivyo?

Suluhisho la Mpaji-Uhai

11. Tunajuaje kwamba dhabihu za damu ya wanyama zilielekeza kwenye kitu fulani?

11 Kwa kweli, Sheria ilikuwa ikielekeza kwenye kitu fulani chenye matokeo zaidi katika kutimiza mapenzi ya Mungu. Paulo aliuliza: “Basi, kwa nini Sheria?” Akajibu: “Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi, mpaka ufike uzao ambao ulikuwa umepewa ahadi; na ilipitishwa kupitia malaika kwa mkono wa mpatanishi [Musa].” (Wagalatia 3:19) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Sheria ina kivuli cha mambo mema yatakayokuja, lakini si umbo halisi la mambo hayo.”—Waebrania 10:1.

12. Tunaweza kuelewaje ufunuo wa kusudi la Mungu kuhusu damu?

12 Kwa ufupi, kumbuka kwamba katika siku za Noa, Mungu aliagiza kwamba wanadamu wangeweza kula nyama ili wategemeze uhai, lakini hawakupaswa kula damu. Baadaye, Mungu alisema kwamba “nafsi ya mwili iko katika damu.” Kwa kweli, aliamua kuiona damu kuwa inawakilisha uhai na kusema: “Nami mwenyewe nimeiweka [damu] juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Hata hivyo, kungekuwa na ufunuo mkuu zaidi wa kusudi la Mungu. Sheria ilikuwa kivuli cha mambo mema ambayo yangekuja. Ni mambo gani hayo?

13. Kwa nini kifo cha Yesu kilikuwa muhimu?

13 Umbo hilo halisi lilihusu hasa kifo cha Yesu Kristo. Unajua kwamba Yesu aliteswa na kutundikwa mtini. Alikufa kama mhalifu. Paulo aliandika hivi: “Tulipokuwa tungali bado dhaifu, Kristo alikufa wakati uliowekwa. . . . Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Waroma 5:6, 8) Kwa kufa kwa ajili yetu, Kristo aliandaa fidia ili kufunika dhambi zetu. Fidia hiyo ni fundisho la msingi katika ujumbe wa Kikristo. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; 1 Wakorintho 15:3; 1 Timotheo 2:6) Fidia inahusianaje na damu na uhai, nao uhai wako unahusikaje?

14, 15. (a) Tafsiri fulani hukaziaje kifo cha Yesu kwenye Waefeso 1:7? (b) Ni jambo gani ambalo huenda ukakosa kuona kwenye Waefeso 1:7?

14 Makanisa fulani hukazia kifo cha Yesu, huku wafuasi wake wakisema mambo kama vile “Yesu alikufa kwa ajili yangu.” Ona jinsi Biblia fulani zinavyotafsiri andiko la Waefeso 1:7: “Ni katika yeye na kupitia kifo chake tunakombolewa, yaani, kuondolewa kwa makosa yetu.” (The American Bible, ya Frank Scheil Ballentine, 1902) “Kupitia kifo cha Kristo tunawekwa huru, na kusamehewa dhambi.” (Today’s English Version, 1966) “Ni katika Kristo na kupitia dhabihu ya uhai wake tumekombolewa, ukombozi unaomaanisha kusamehewa dhambi.” (The New Testament, ya William Barclay, 1969) “Tunasamehewa dhambi na kuwekwa huru kupitia kifo cha Kristo.” (The Translator’s New Testament, 1973) Unaweza kuona kwamba tafsiri hizo zinakazia kifo cha Yesu. Huenda wengine wakasema, ‘Lakini kifo cha Yesu ni muhimu kwelikweli. Hivyo, tafsiri hizo zinakosa kutaja nini?’

15 Kwa kweli, kama ungetegemea tafsiri hizo, ungekosa kuona jambo fulani muhimu sana, na hilo lingekuzuia usielewe vizuri ujumbe wa Biblia. Tafsiri hizo hazionyeshi ukweli wa kwamba katika maandishi ya awali andiko la Waefeso 1:7 lina neno la Kigiriki linalomaanisha “damu.” Hivyo, Biblia nyingi kama vile Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hutafsiri maandishi ya awali kwa usahihi zaidi: “Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.”

16. Tafsiri “damu ya huyo” inapaswa kutukumbusha nini?

16 Tafsiri “damu ya huyo” ina maana muhimu sana na inapaswa kutufanya tufikirie mambo mengi kuhusu damu. Mengi yalihitajiwa kuliko tu kifo cha mtu fulani, hata kifo cha mwanadamu mkamilifu Yesu. Alitimiza mambo yaliyoonyeshwa kimbele katika Sheria, hasa kuhusu Siku ya Upatanisho. Katika siku hiyo ya pekee, wanyama ambao walitajwa na Sheria walitolewa wakiwa dhabihu. Kisha kuhani mkuu alipeleka kiasi fulani cha damu yao katika chumba cha Patakatifu Zaidi cha maskani au hekalu, na huko akaitoa, kana kwamba alikuwa mbele za Mungu.—Kutoka 25:22; Mambo ya Walawi 16:2-19.

17. Yesu alitimizaje mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho?

17 Yesu alitimiza mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho, kama alivyoeleza Paulo. Kwanza, Paulo alitaja kwamba kuhani mkuu katika Israeli aliingia Patakatifu Zaidi mara moja kwa mwaka akiwa na damu iliyotolewa “kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya dhambi za hali ya watu ya kutojua.” (Waebrania 9:6, 7) Kupatana na yaliyotokea siku hiyo, Yesu alienda mbinguni kwenyewe baada ya kufufuliwa akiwa kiumbe wa roho. Kwa kuwa alikuwa kiumbe wa roho, asiye na mwili wa nyama na damu, Yesu angeweza kuonekana “mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu.” Alimtolea Mungu nini? Hakutoa kitu halisi bali kitu muhimu sana. Paulo aliendelea kusema: “Kristo alipokuja akiwa kuhani mkuu . . . aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe-dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu. Kwa maana ikiwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe-dume . . . hutakasa kufikia usafi wa mwili, je, si zaidi damu ya Kristo, ambaye kupitia roho inayodumu milele alijitoa mwenyewe bila dosari kwa Mungu, itazisafisha dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai?” Naam, Yesu alimtolea Mungu thamani ya damu yake.—Waebrania 9:11-14, 24, 28; 10:11-14; 1 Petro 3:18.

18. Kwa nini maandiko ya Biblia kuhusu damu ni muhimu kwa Wakristo leo?

18 Ukweli huo kutoka kwa Mungu hutuwezesha kuelewa mambo yenye kustaajabisha ambayo Biblia husema kuhusu damu—kwa nini Mungu ana maoni hayo kuihusu, jinsi tunavyopaswa kuiona, na kwa nini tunapaswa kuheshimu vizuizi ambavyo Mungu ameweka kuhusu matumizi ya damu. Unaposoma vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, utaona kwamba vinataja damu ya Kristo mara nyingi. (Ona sanduku.) Hivyo vinaonyesha wazi kwamba kila Mkristo anapaswa kuwa na imani ‘katika damu ya Yesu.’ (Waroma 3:25) Tunaweza tu kupata msamaha na kuwa na amani pamoja na Mungu ‘kupitia damu ambayo Yesu alimwaga.’ (Wakolosai 1:20) Bila shaka, hiyo ni kweli kuhusu wale ambao Yesu alifanya nao agano la pekee la kutawala pamoja naye mbinguni. (Luka 22:20, 28-30; 1 Wakorintho 11:25; Waebrania 13:20) Pia, hilo ni kweli kuhusu “umati mkubwa” leo, ambao utaokoka “dhiki kuu” inayokuja na kuishi milele katika paradiso duniani. Kwa njia ya mfano, ‘wanafua kanzu zao katika damu ya Mwana-Kondoo.’—Ufunuo 7:9, 14.

19, 20. (a) Kwa nini Mungu aliamua kuweka vizuizi kuhusu matumizi ya damu, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo? (b) Tunapaswa kupendezwa kujua nini?

19 Ni wazi kwamba damu ina maana ya kipekee machoni pa Mungu. Sisi pia tunapaswa kuiona hivyo. Muumba, ambaye anajali uhai, ana haki ya kuweka vizuizi kuhusu jinsi wanadamu wanavyotumia damu. Kwa kuwa anajali sana uhai wetu, aliazimia damu itumiwe tu kwa njia moja muhimu sana, ambayo hutuwezesha kupata uzima wa milele. Njia hiyo inahusisha damu ya Yesu yenye thamani. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova Mungu alitunufaisha kwa kutumia damu—damu ya Yesu—katika njia hii yenye kuokoa uhai! Na tunamshukuru Yesu kama nini kwa kumwaga damu yake kuwa dhabihu kwa ajili yetu! Kwa kweli, tunaweza kuelewa maneno haya ya mtume Yohana: “Kwake yeye anayetupenda na aliyetufungua kutoka katika dhambi zetu kupitia damu yake mwenyewe—naye alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake—ndiyo, kwake yeye na kuwe utukufu na nguvu milele. Amina.”—Ufunuo 1:5, 6.

20 Mungu wetu mwenye hekima yote na Mpaji-Uhai alifikiria kwa muda mrefu fungu hilo ambalo damu ingetimiza katika kuokoa uhai. Basi, huenda tukajiuliza, ‘Hilo linapaswa kuathirije maamuzi na matendo yetu?’ Swali hilo litajibiwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Tunaweza kujifunza nini kuhusu maoni ya Mungu kuelekea damu kutokana na masimulizi juu ya Abeli na Noa?

• Katika Sheria, Mungu aliweka vizuizi gani kuhusu matumizi ya damu, na kwa nini?

• Yesu alitimizaje mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho?

• Damu ya Yesu inawezaje kuokoa uhai wetu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

NI DAMU GANI HUOKOA UHAI?

“Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.”—Matendo 20:28.

“Kwa hiyo, kwa kuwa tumetangazwa kuwa waadilifu sasa kwa damu yake, tutaokolewa kutokana na ghadhabu kupitia yeye hata zaidi.”—Waroma 5:9.

“Hamkuwa na tumaini na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu. Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati mmoja mlikuwa mbali sana mmekuja kuwa karibu kupitia damu ya Kristo.”—Waefeso 2:12, 13.

“Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika yeye, na kupitia yeye apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyomwaga juu ya mti wa mateso.”—Wakolosai 1:19, 20.

“Kwa hiyo, akina ndugu, . . . tuna ujasiri wa njia ya kuingia katika mahali patakatifu kwa damu ya Yesu.”—Waebrania 10:19.

“Si kwa vitu vyenye kuharibika . . . kwamba mlikombolewa kutoka kwenye namna ya mwenendo wenu usiozaa matunda ambao ulipokewa kwa njia ya mapokeo kutoka kwa mababu zenu. Bali ilikuwa kwa damu yenye thamani, kama ile ya mwana-kondoo asiye na dosari na asiye na doa, ile ya Kristo.”—1 Petro 1:18, 19.

“Hata hivyo, ikiwa tunatembea katika nuru kama yeye mwenyewe alivyo katika nuru, tuna ushirika sisi kwa sisi, na damu ya Yesu Mwana wake hutusafisha kutoka katika dhambi yote.”—1 Yohana 1:7.

“Wewe unastahili kukichukua kile kitabu cha kukunjwa na kufungua mihuri yake, kwa sababu ulichinjwa na kwa damu yako ukamnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.”—Ufunuo 5:9.

“Mshtaki wa ndugu zetu ametupwa chini . . . Nao wakamshinda kwa sababu ya damu ya Mwana-Kondoo na kwa sababu ya neno la kutoa kwao ushahidi.”—Ufunuo 12:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kupitia Sheria, Mungu alionyesha wazi kwamba damu ingeweza kutimiza fungu fulani katika kusamehewa dhambi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kupitia damu ya Yesu, uhai wa wengi ungeweza kuokolewa