Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Urithi Wenye Thamani Zaidi

Urithi Wenye Thamani Zaidi

Urithi Wenye Thamani Zaidi

ALIPOKUWA karibu kufa, mtume Yohana aliyezeeka aliandika: “Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 Yohana 4.

Mtume huyo mwaminifu alikuwa anarejelea watoto wake katika maana ya kiroho. Hata hivyo, wazazi wengi wangekuwa na hisia hizohizo kuhusu watoto wao. Wamejitahidi sana kulea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” na sasa wanafurahi kuona watoto wao walio watu wazima “wakitembea katika kweli.” (Waefeso 6:4) Kwa kweli, unapowafundisha watoto wako njia inayoongoza kwenye uzima wa milele, unawapa urithi wenye thamani zaidi. Hiyo ni kwa sababu ujitoaji-kimungu, ambao hutia ndani kuishi jinsi Yehova anavyotaka Wakristo waishi, “una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Timotheo 4:8.

Yehova, Baba aliye mkamilifu, anawathamini sana wazazi wanaomwogopa, ambao hujitahidi sana kuwaelimisha watoto wao kiroho. Watoto wakiitikia vizuri, watafurahia sana kuendelea na ibada ya kweli pamoja na wazazi wao. Watoto hao wanapokua, watakuwa na kumbukumbu nzuri za mambo hayo. Wengine hukumbuka kwa furaha mara yao ya kwanza kushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. * Au labda hukumbuka wakati waliposoma andiko la Biblia kwa mara ya kwanza katika huduma ya nyumba kwa nyumba wakiwa na mmoja wa wazazi wao. Hawawezi kusahau wakati wazazi wao walipowasomea Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia * au Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Gabriel anakumbuka sehemu alizopenda sana: “Nilipokuwa na umri wa miaka minne tu, mama aliniimbia kila siku alipokuwa akipika. Bado ninakumbuka kwa hisia nyingi sana wimbo fulani wa Ufalme ambao baadaye ulinisaidia kuona umuhimu wa kumtumikia Yehova.” Labda wewe pia unakumbuka wimbo huo mzuri ambao Gabriel anataja. Huo ni wimbo namba 157 katika kitabu cha nyimbo Mwimbieni Yehova Sifa, na una kichwa “Mwabudu Yehova Wakati wa Ujana.”

Wimbo huo unaanza: “Watoto kasifu Mungu kale;/Wakapa Yesu vigelegele.” Naam, kulikuwa na watoto waliokuwa na pendeleo la kushirikiana na Yesu, na yaelekea walimfurahisha na kumburudisha kwa unyoofu wao. Hata Yesu alitumia utayari wa watoto wa kufundishwa kama kielelezo cha kuigwa na wafuasi wake. (Mathayo 18:3, 4) Hivyo, watoto wana fungu lifaalo katika ibada ya Yehova. Maneno ya wimbo huo yanaendelea kusema: “Wanaweza kutukuza Mungu.”

Watoto wengi wamemheshimu Mungu na familia zao kupitia mwenendo wao mzuri nyumbani, shuleni, na kwingineko. Imekuwa baraka iliyoje kwao kuwa na ‘Wazazi wanaopenda kweli.’ (Kumbukumbu la Torati 6:7) Wazazi wanaomwogopa Mungu hufanya yale Mungu husema, na kwa kuwa ni Baba mwenye upendo, yeye hufundisha viumbe wake waende katika njia wanayopaswa kutembea ndani yake. Nao hupata baraka zilizoje! Wanapowafundisha watoto wao, wazazi hufurahi kama nini kuwa na watoto ‘wanaotii’! (Isaya 48:17, 18) Angelica, ambaye sasa anatumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico, anasema: “Sikuzote wazazi wangu walijitahidi kutumia kanuni za Biblia. Hiyo ilifanya maisha yangu ya utotoni yawe mazuri sana. Nilikuwa mwenye furaha sana.”

Wakristo hao hukubali kwamba ni muhimu kwa vijana kutunza vizuri urithi wao wa kiroho. Labda wewe ni kijana anayelelewa katika familia inayofuata kanuni za kweli za Kikristo. Ikiwa ndivyo, wimbo huo unakuhimiza: “Vijana, muwe safi mwendoni.” Wakati utafika utakapofanya maamuzi yako mwenyewe, hivyo, sasa ‘jifunze kumtegemea Mungu./Usitafute sifa ya watu.’

Ukifanya kosa la kutafuta kwanza sifa ya watu, huenda mazoezi yote uliyopata yasikusaidie, na huenda ukaharibu matarajio yako ya wakati ujao. Tamaa ya kusifiwa inaweza kufanya usiwe mwangalifu. Wengine wameishia kushirikiana na wale ambao hawapendezwi hata kidogo na viwango vya Kikristo, ingawa wanaonekana kuwa watu wazuri na hata wenye kupendeza. Jambo hilo lilionyeshwa kupitia Tara, mwigizaji mkuu katika ile video Young People Ask—How Can I Make Real Friends? Kama Tara, Mkristo yeyote kijana anayeshirikiana na watu wasiothamini ibada ya kweli, mwishowe atatambua kwamba “rafiki wabaya huharibu,” kama vile wimbo unavyosema. Inachukua miaka mingi ya jitihada ili kusitawisha tabia nzuri, lakini hiyo inaweza kuharibiwa upesi.

Kwa kweli, si rahisi kuishi maisha yenye kumheshimu Mungu. Hata hivyo, kama wimbo huo unavyoendelea kusema, ‘ukimkumbuka Mungu ujanani,/Na kumtumikia kwa roho na kweli,’ utajenga msingi mzuri wa kupata mafanikio ya kweli. Na ‘utakuja kufurahi sana.’ Utakuja kutambua hata zaidi kwamba chini ya utunzaji wenye upendo wa Yehova, hakuna kitu kinachoweza kukuzuia usifanye yaliyo sawa machoni pake. Hivyo ndivyo unavyoweza kuwa mtu mzima aliyekomaa na anayemwogopa Mungu. Pia, kutumia kwa hekima mazoezi ya Kikristo unayopata hukuwezesha ‘kuufurahisha moyo wa Mungu.’ Jambo hilo humletea mwanadamu heshima kubwa sana.—Methali 27:11.

Kwa hiyo, sikuzote vijana kumbukeni kwamba mazoezi mnayopata kutoka kwa Yehova na wazazi wenu Wakristo yana thamani kubwa. Upendo wao mwingi kwenu na uwachochee kufanya mambo yanayompendeza Yehova. Kama Yesu Kristo na kijana Timotheo aliyekuwa mwaminifu, ninyi pia mtamfurahisha Baba yenu wa mbinguni na wazazi wenu. Na kama utapata kuwa mzazi, labda utakubaliana na Angelica, aliyetangulia kutajwa, ambaye anasema: “Kama nitapata kuwa na mtoto, nitajitahidi sana kukazia upendo kwa Yehova moyoni mwake tangu utotoni, na kuufanya kuwa kanuni muhimu ya kumwongoza maishani.” Bila shaka, njia iliyonyooka iongozayo kwenye uzima wa milele ndiyo urithi wenye thamani zaidi!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Vijana kwa wazee wanaweza kujiunga na sehemu hii ya programu ya kujifunza Biblia inayofanywa katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 4 Vichapo ambavyo vimetajwa huchapishwa na Mashahidi wa Yehova.