Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wahitimu wa Gileadi Waondoka Wakiwa Wavunaji Wenye Bidii!

Wahitimu wa Gileadi Waondoka Wakiwa Wavunaji Wenye Bidii!

Wahitimu wa Gileadi Waondoka Wakiwa Wavunaji Wenye Bidii!

“MAVUNO ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Maneno hayo yalikuwa na maana ya kipekee kwa wanafunzi waliokuwa wakihitimu wa darasa la 116 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) ambao walikuwa wakijitayarisha kwenda kwenye migawo yao ya umishonari.

Siku ya Jumamosi, Machi 13, 2004, watu 6,684 walikusanyika kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, na kwenye sehemu nyingine ambapo programu hiyo ya kuhitimu ilionyeshwa katika televisheni, nao wanafunzi wakapokea shauri na kitia-moyo cha kuwaaga. Sote tunaweza kunufaika na shauri hilo lililotolewa tunapofanya kazi ya uvunaji wa kiroho kwa bidii.

Utangulizi uliotolewa na Ndugu Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza na mhitimu wa darasa la saba la Gileadi ulikazia maneno haya ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, 20) Maneno hayo yalifaa sana kwa kuwa wahitimu wanatumwa katika nchi 20. Aliwakumbusha wanafunzi kwamba maagizo kutoka katika Neno la Mungu yamewapa vifaa kamili vya kuwa wafanyakazi wenye bidii katika mavuno ya pekee ya kiroho.—Mathayo 5:16.

Jinsi ya Kuwa Wavunaji Wenye Matokeo

Msemaji wa kwanza kwenye programu alikuwa Robert Wallen, ambaye amefanya kazi katika Shule ya Gileadi kwa miaka mingi. Akizungumzia hotuba yenye kichwa “Sifa Bora ya Huruma,” aliwaambia wanafunzi hivi: “Huruma ni lugha ambayo hata viziwi wanaweza kusikia na vipofu kuona.” Yesu alifahamu vizuri shida za wengine naye alijitahidi kuzipunguza. (Mathayo 9:36) Wanafunzi watakuwa na nafasi nyingi za kufanya hivyo—katika kazi ya kuhubiri, kutanikoni, kwenye makao ya mishonari, na katika ndoa zao. Msemaji aliwahimiza hivi: “Onyesheni sifa bora ya huruma katika maisha yenu mnapowatumikia wengine. Tabia nzuri ndiyo tu itakayowasaidia katika makao ya mishonari. Kwa hiyo, azimieni kujivika wenyewe huruma.”—Wakolosai 3:12.

Baadaye, Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza na mhitimu wa darasa la 41 la Gileadi, alizungumzia hotuba yenye kichwa “Wahubiri wa Wokovu.” (Isaya 52:7) Ili watu waokoke mwisho unaokaribia wa mfumo huu wa mambo, lazima watwae ujuzi sahihi kutoka katika Neno la Mungu, wafanye tangazo la hadharani la imani yao, na kubatizwa. (Waroma 10:10; 2 Timotheo 3:15; 1 Petro 3:21) Hata hivyo, sababu kuu ya kuhubiri si kuwaletea wanadamu wokovu, bali ni kumletea Mungu sifa. Kwa hiyo, Ndugu Lösch aliwashauri hivi mishonari hao wa wakati ujao: “Pelekeni ujumbe wa Ufalme mpaka miisho ya dunia, na mwe wahubiri wa wokovu wenye bidii, na hivyo kumletea Yehova sifa.”—Waroma 10:18.

Mwalimu wa Gileadi Lawrence Bowen aliuliza swali hili, “Unaangazaje Nuru ya Kiroho?” Alirejelea maneno ya Yesu katika Mathayo 6:22 na kuwatia moyo wanafunzi waliokuwa wakihitimu wadumishe jicho “rahisi” ili “waangaze nuru ya kiroho inayomtukuza Yehova na kuwanufaisha wanadamu wenzetu.” Tangu mwanzo wa huduma yake, Yesu aliweka kielelezo bora kuhusiana na habari hiyo kwa kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu. Yesu aliweza kuvumilia majaribu ya Shetani huko nyikani kwa kutafakari mambo mazuri ambayo Baba yake alimfundisha walipokuwa pamoja mbinguni. (Mathayo 3:16; 4:1-11) Yesu alionyesha kwamba alimtegemea Yehova kabisa kwa kutimiza mgawo aliompa. Vivyo hivyo, ili kukabiliana na magumu yaliyo mbele, lazima mishonari wadumishe mazoea mazuri ya kujifunza Biblia na kumtegemea Yehova kabisa.

Mark Noumair, mwalimu wa Gileadi na mhitimu wa darasa la 77 la Gileadi, alimalizia mfululizo huo wa hotuba, kwa kutoa hotuba yenye kichwa, “Tupo Hapa Mkononi Mwako.” (Yoshua 9:25) Aliwatia moyo wanafunzi wawe na mtazamo kama wa Wagibeoni. Ingawa Gibeoni lilikuwa “jiji kubwa . . . na wanaume wake wote walikuwa wenye nguvu,” Wagibeoni hawakutafuta umashuhuri wala kutarajia mambo yafanywe kulingana na matakwa yao. (Yoshua 10:2) Walikubali kuwa “wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji” chini ya Walawi katika kutegemeza ibada ya Yehova. (Yoshua 9:27) Kwa kweli, wanafunzi waliokuwa wakihitimu wamemwambia Yoshua Mkuu, Yesu Kristo hivi: “Tupo hapa mkononi mwako.” Sasa wanapoanza migawo yao katika nchi za kigeni, wanapaswa kukubali kazi yoyote wanayopewa na Yoshua Mkuu.

Mahojiano na Mambo Yaliyoonwa

Ndugu Wallace Liverance, mwalimu wa Gileadi na mhitimu wa darasa la 61 alizungumzia kichwa, “Fungua Maandiko” akiwa pamoja na kikundi cha wanafunzi fulani. Walisimulia na kuigiza mambo waliyoona shambani muda ambao walikuwa shuleni. Ilikuwa wazi kwamba bidii yao ya kujifunza Biblia katika muda wa miezi mitano ya mazoezi iligusa mioyo yao na kuwachochea wawaeleze wengine mambo waliyojifunza. (Luka 24:32) Wakati wa masomo hayo ya miezi mitano, mwanafunzi mmoja alimweleza ndugu yake wa kimwili mambo aliyokuwa akijifunza. Jambo hilo lilimtia moyo ndugu yake atafute kutaniko la eneo hilo na kuanza kujifunza Biblia. Sasa amestahili kuwa mhubiri asiyebatizwa.

Baada ya mambo hayo yaliyoonwa, Richard Ashe na John Gibbard waliwahoji watumishi kadhaa ambao wamemtumikia Yehova kwa uaminifu na kwa miaka mingi, kutia ndani waangalizi wasafirio waliokuwa wakipewa mazoezi ya pekee kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower. Walikuwa wahitimu wa madarasa ya awali ya Shule ya Gileadi. Mmoja wao alikumbuka kwamba pindi moja Ndugu Knorr alisema hivi darasa likiendelea: “Ukiwa Gileadi utajifunza sana. Lakini ukitoka huko ukiwa mwenye kiburi, tutakuwa tumefanya kazi bure. Tunataka utoke ukiwa na moyo wenye upendo.” Ndugu wasafirio waliwashauri wanafunzi hao wawe wanawajali watu, wawatendee kama Kristo alivyowatendea, na kukubali kwa unyenyekevu mgawo wowote wanaopewa. Bila shaka, kufuata shauri hilo kutawasaidia mishonari wapya wawe wenye matokeo katika migawo yao.

Nendeni Mkiwa Wavunaji Wenye Bidii!

Wahudhuriaji walipata nafasi ya kumsikiliza Ndugu Stephen Lett, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza. Alitoa hotuba kuu katika programu hiyo, ambayo ilikuwa na kichwa, “Nendeni Mkiwa Wavunaji Wenye Bidii!” (Mathayo 9:38) Katika mavuno halisi, muda wa kuvuna mazao huwa mfupi. Wavunaji wanahitaji kufanya kazi kwa bidii. Bidii inahitajiwa hata zaidi wakati huu wa umalizio wa mfumo wa mambo! Katika uvunaji mkubwa wa kiroho, maisha yako hatarini. (Mathayo 13:39) Ndugu Lett aliwatia moyo wahitimu wasiwe ‘wavivu katika kazi zao,’ bali ‘wawake roho’ na ‘kumtumikia Yehova’ katika kazi hii ya mavuno ambayo haitarudiwa kamwe. (Waroma 12:11) Msemaji alinukuu maneno haya ya Yesu: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yohana 4:35) Kisha aliwahimiza wahitimu wawe wenye bidii katika kazi ya kuvuna kwa kujitahidi kikweli kuwafikia watu mahali na wakati ambao wanapatikana, kwa kutumia nafasi zote wanazopata kutoa ushahidi usio rasmi. Kuwa chonjo ili kupata nafasi kunaweza kusaidia kutoa ushahidi wenye matokeo. Yehova ni Mungu mwenye bidii, naye anatazamia sote tumwige na kufanya kazi kwa bidii katika mavuno ya kiroho.—2 Wafalme 19:31; Yohana 5:17.

Ndugu Jaracz, aliyekuwa mwenyekiti, alimalizia programu kwa kusoma salamu kutoka ofisi za tawi mbalimbali na kuwapa wanafunzi diploma zao. Mmoja wa wahitimu alisoma barua iliyoandikwa na darasa hilo ambayo ilieleza jinsi walivyothamini sana mazoezi waliyopata. Bila shaka, programu ya kuhitimu ya darasa la 116 ilifanya wote waliohudhuria waazimie hata zaidi kwenda wakiwa wavunaji wenye bidii.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 6

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 20

Idadi ya wanafunzi: 46

Wastani wa umri: 34.2

Wastani wa miaka katika kweli: 17.2

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.9

[Picha katika ukurasa wa 26]

Darasa la 116 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Ceansu, R.; Sparks, T.; Piña, C.; Turner, P.; Cheney, L. (2) Suardy, M.; Sjöqvist, Å.; Amadori, L.; Smith, N.; Jordan, A.; Boissonneault, L. (3) Matlock, J.; Ruiz, C.; Dular, L.; Vigneron, M.; Henry, K. (4) Sjöqvist, H.; Laux, J.; Ruzzo, J.; Gustafsson, K.; Boissonneault, R.; Jordan, M. (5) Henry, D.; Turner, D.; Kirwin, S.; Florit, K.; Ceansu, S. (6) Amadori, S.; Cheney, J.; Ross, R.; Nelson, J.; Ruiz, J.; Vigneron, M. (7) Florit, J.; Matlock, D.; Ross, B.; Laux, C.; Ruzzo, T.; Dular, D.; Kirwin, N. (8) Gustafsson, A.; Nelson, D.; Suardy, W.; Piña, M.; Smith, C.; Sparks, T.