Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anakujali Kwelikweli

Mungu Anakujali Kwelikweli

Mungu Anakujali Kwelikweli

NI JAMBO la kawaida kumlilia Mungu atusaidie tunapokuwa katika shida. Hiyo ni kwa sababu yeye “ni mkuu na mwenye nguvu nyingi; uelewaji wake hauwezi kusimuliwa.” (Zaburi 147:5) Yeye hasa ndiye anayeweza kutusaidia kukabiliana na matatizo yetu. Pia, Biblia hutualika ‘tumimine moyo wetu’ mbele zake. (Zaburi 62:8) Hivyo, kwa nini watu wengi sana hufikiri kwamba Mungu hajibu sala zao? Je, hiyo inamaanisha kwamba yeye hajali?

Badala ya kumlaumu Mungu haraka-haraka kwa kuonekana kama hajali, kumbuka wakati ulipokuwa mtoto. Wazazi wako walipokataa kukutimizia kila jambo ulilotaka, je, uliwahi kuwashutumu kwamba hawakupendi? Watoto wengi hufanya hivyo. Hata hivyo, ulipokua ukawa mtu mzima, ulitambua kwamba upendo huonyeshwa katika njia nyingi, na kwamba kumwonyesha mtoto upendo hakumaanishi kumtimizia kila jambo analotaka.

Vivyo hivyo, haimaanishi kwamba Yehova anatupuuza ikiwa sikuzote hatajibu sala zetu kupatana na matarajio yetu. Ukweli ni kwamba Mungu huonyesha kwa njia nyingi kwamba anatujali sisi sote.

“Kwake Tuna Uhai”

Kwanza kabisa, sisi “tuna uhai na tunaenda na kuwako” kwa sababu ya Mungu. (Matendo 17:28) Bila shaka, kwa kutupa uhai, Mungu ameonyesha kwamba anatujali!

Pia, Yehova hutuandalia mahitaji yetu ili tuendelee kuwa hai. Tunasoma: “Anafanya majani mabichi yachipuke kwa ajili ya wanyama, na mimea ili itumikie wanadamu, ili chakula kitokezwe duniani.” (Zaburi 104:14) Kwa kweli, Muumba wetu hatuandalii tu mahitaji ya msingi ya maisha. Kwa ukarimu, yeye hutupa “mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo [yetu] kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.

Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza, ‘Ikiwa Mungu anatupenda sana hivyo, kwa nini yeye huruhusu tuteseke?’ Je, unajua jibu la swali hilo?

Je, Mungu Ndiye Husababisha Matatizo Yetu?

Mwanadamu ndiye husababisha mengi ya matatizo yanayompata. Kwa mfano, tunajua vizuri sana hatari zinazotokana na vitendo fulani. Na bado, watu hufanya uasherati, hutumia vibaya pombe na dawa nyingine, hutumia tumbaku, hushiriki katika michezo hatari, kuendesha gari kwa kasi, na kadhalika. Tumlaumu nani ikiwa mtu atateseka kwa sababu ya mazoea hayo hatari? Mungu au yule anayetenda kipumbavu? Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linasema: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.

Pia, mara nyingi wanadamu huumizana. Taifa linapotangaza vita, bila shaka, Mungu hawezi kulaumiwa kwa mateso yanayotokea. Mhalifu anapomshambulia raia mwenzake, je, tumlaumu Mungu kwa majeraha yoyote yanayotokea au kifo? La! Je, tumlaumu Mungu wakati mtawala wa kimabavu anapokandamiza, kutesa, na kuwaua watu anaotawala? Hilo halingekuwa jambo la akili.—Mhubiri 8:9.

Lakini namna gani mamilioni ya wale wanaoishi maisha ya ufukara au wana njaa? Je, tumlaumu Mungu? La, kwa kuwa dunia yetu huzalisha chakula cha kutosha kulisha kila mtu. (Zaburi 10:2, 3; 145:16) Kuna njaa na umaskini mwingi kwa sababu vitu ambavyo Mungu ametupatia havigawanywi kwa usawa. Na tatizo hilo haliwezi kutatuliwa kwa sababu ya ubinafsi wa mwanadamu.

Sababu ya Msingi

Lakini je, tumlaumu nani mtu anaposhikwa na ugonjwa au anapokufa kwa sababu ya uzee? Je, ungeshangaa kujua kwamba hatupaswi kumlaumu Mungu kwa mambo hayo? Mungu hakumuumba mwanadamu awe akizeeka na kufa.

Wakati wenzi wa kwanza, Adamu na Hawa, walipowekwa katika bustani ya Edeni, Yehova aliwapa taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, ni wazi kwamba alitaka dunia ikaliwe na watu ambao wangethamini urithi wao. Hivyo, matarajio ya uhai wao wa wakati ujao yangetegemea sharti fulani. Adamu na Hawa wangeishi katika Paradiso ikiwa tu wangeendelea kumtii Muumba wao mwenye upendo.—Mwanzo 2:17; 3:2, 3, 17-23.

Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa waliasi. Hawa aliamua kumsikiliza Shetani Ibilisi. Shetani alimdanganya na hivyo akaonyesha kwamba Mungu alikuwa akimnyima Hawa kitu fulani kizuri. Hivyo, akaanza kujitegemea na kujaribu ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ Adamu aliungana naye katika uasi huo.—Mwanzo 3:5, 6.

Kwa kutenda dhambi hiyo, Adamu na Hawa walionyesha kwamba hawastahili kuishi milele. Walipatwa na matokeo mabaya ya dhambi. Nguvu zao zilipungua, na mwishowe wakafa. (Mwanzo 5:5) Hata hivyo, uasi wao ulikuwa na matokeo mabaya zaidi. Tungali tunateseka kutokana na dhambi ya Adamu na Hawa. Mtume Paulo aliandika: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Naam, kwa sababu ya uasi wa Adamu na Hawa, dhambi na kifo vilienea kati ya wanadamu wote kama ugonjwa wenye kuua.

Uthibitisho Wenye Nguvu Zaidi Kwamba Mungu Anajali

Je, hiyo inamaanisha kwamba wanadamu walipatwa na madhara ya kudumu? La, na sasa tunaona uthibitisho wenye nguvu zaidi kwamba Mungu anatujali. Kwa bei kubwa, Mungu aliandaa njia ya kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Bei hiyo ya ukombozi ni uhai mkamilifu wa Yesu, alioutoa kwa hiari kwa ajili yetu. (Waroma 3:24) Hivyo, mtume Yohana aliandika: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa sababu ya tendo hilo kuu la upendo, kwa mara nyingine tena tuna tarajio la kuishi milele. Paulo aliwaandikia Waroma hivi: “Kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.”—Waroma 5:18.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika wakati wa Mungu unaofaa, kuteseka na kifo vitatoweka Duniani. Badala yake, hali zinazotabiriwa katika kitabu cha Ufunuo zitatimia: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Huenda ukasema, ‘Sitakuwa hai mambo hayo yanapotimia.’ Hata hivyo, ukweli ni kwamba huenda ukawa hai. Na hata ukifa, Mungu anaweza kukufufua. (Yohana 5:28, 29) Hilo ndilo kusudi la Mungu kwetu, nalo litatimia. Ni uwongo mtupu kusema kwamba Mungu hajali wanadamu.

“Mkaribieni Mungu”

Inafariji kujua kwamba Mungu ameanzisha suluhisho la kudumu kwa tatizo la kuteseka kwa wanadamu. Lakini namna gani leo? Tunaweza kufanya nini tukifiwa na mpendwa au mtoto wetu akishikwa na ugonjwa? Huu si wakati wa Mungu wa kuondoa magonjwa na kifo. Biblia inaonyesha kwamba itatubidi tungojee muda kidogo zaidi ndipo mambo hayo yaondolewe. Lakini hakutuacha bila msaada. Mwanafunzi Yakobo alisema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Naam, Muumba wetu hutukaribisha kuwa na uhusiano wa karibu naye, naye sikuzote huwategemeza wale walio na uhusiano huo pamoja naye, hata wanapokuwa katika hali ngumu sana.

Tunamkaribiaje Mungu? Mfalme Daudi aliuliza swali hilo miaka elfu tatu hivi iliyopita, akisema: “Ee Yehova, . . . ni nani atakayekaa katika mlima wako mtakatifu?” (Zaburi 15:1) Daudi alijibu swali lake mwenyewe alipoongeza kusema: “Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake. Yeye hakuchongea kwa ulimi wake. Hakumfanyia mwenzake jambo lolote baya.” (Zaburi 15:2, 3) Yaani, Yehova huwakaribisha wale wanaofuata mwenendo ambao Adamu na Hawa walikataa. Yeye huwakaribia wale wanaofanya mapenzi yake.—Kumbukumbu la Torati 6:24, 25; 1 Yohana 5:3.

Tunawezaje kufanya mapenzi ya Mungu? Lazima tujue lile ambalo ni “zuri nalo linakubalika machoni pa Mwokozi wetu, Mungu,” kisha tuamue kutenda kupatana nalo. (1 Timotheo 2:3) Hiyo hutia ndani kuendelea kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. (Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:16, 17) Tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kusoma Biblia kijuujuu tu. Tunahitaji kuwaiga Wayahudi wa karne ya kwanza huko Beroya waliosikia mahubiri ya Paulo. Tunasoma hivi kuwahusu: “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:11.

Vilevile leo, kujifunza Biblia kwa makini huimarisha imani yetu katika Mungu na hutusaidia kusitawisha uhusiano wa karibu naye. (Waebrania 11:6) Pia hutusaidia kuelewa vizuri kabisa jinsi ambavyo Yehova hushughulika na wanadamu—si kwa faida za muda mfupi tu, bali kwa faida za kudumu, hasa kwa wote walio na mwelekeo unaofaa.

Ona yale Wakristo kadhaa walio na uhusiano wa karibu na Mungu wanayosema. “Ninampenda Yehova sana, na ninamshukuru kwa mambo mengi sana,” asema Danielle, mwenye umri wa miaka 16. “Alinipa wazazi wenye upendo wanaompenda kikweli na ambao wamenifundisha Neno lake.” Mkristo mmoja nchini Uruguay aliandika: “Ninachochewa kumshukuru Yehova sana sana kwa fadhili zake zisizostahiliwa na kwa urafiki wake.” Mungu pia huwakaribisha hata watoto wadogo. Gabriela aliye na umri wa miaka saba anasema: “Ninampenda Mungu zaidi ya kitu kingine chochote duniani! Nina Biblia yangu mwenyewe. Ninapenda kujifunza kumhusu Mungu na Mwanaye.”

Leo, mamilioni ya watu duniani kote hukubaliana kabisa na mtunga-zaburi aliyesema: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zaburi 73:28) Wamesaidiwa kuvumilia matatizo wanayokabili leo, nao wana tumaini hakika la kuishi milele katika dunia Paradiso. (1 Timotheo 4:8) Kwa nini usijitahidi “kumkaribia Mungu”? Naam, tunahakikishiwa hivi: “Hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Ndiyo, Mungu anakujali kwelikweli!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yehova huonyesha kwa njia nyingi kwamba anatujali

[Picha katika ukurasa wa 7]

Hata watoto wadogo wanaweza kumkaribia Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Leo, Yehova hutusaidia kuvumilia. Katika wakati unaofaa, ataondoa magonjwa na kifo