Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.”—MATHAYO 28:18, 19.

1, 2. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo gani? (b) Ni maswali gani kuhusu amri za Yesu tutakayozungumzia?

ILIKUWA siku ya masika huko Israeli mwaka wa 33 W.K., nao wanafunzi wa Yesu walikuwa wamekusanyika kwenye mlima fulani huko Galilaya. Bwana wao aliyefufuliwa alikuwa karibu kupanda mbinguni, lakini kwanza alihitaji kuwaambia jambo fulani muhimu. Yesu alitaka kuwapa mgawo fulani. Mgawo gani huo? Wanafunzi wake waliitikiaje? Na mgawo huo unatuhusuje leo?

2 Yale ambayo Yesu alisema yameandikwa kwenye Mathayo 28:18-20: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alitaja “mamlaka yote,” “mataifa yote,” “mambo yote,” na “siku zote.” Amri zake kuhusu taarifa hizo nne hutokeza maswali manne mafupi ambayo ni muhimu. Maswali hayo ni, kwa nini? wapi? nini? na lini? Na tuzungumzie maswali hayo moja baada ya lingine. *

“Nimepewa Mamlaka Yote”

3. Kwa nini tunapaswa kutii amri ya kufanya wanafunzi?

3 Kwanza, kwa nini tunapaswa kutii amri ya kufanya wanafunzi? Yesu alisema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Maneno “kwa hiyo” huonyesha sababu kuu kwa nini tunapaswa kutii amri hiyo. Hiyo ni kwa sababu Yesu, aliyetoa amri hiyo, ana “mamlaka yote.” Mamlaka yake ni kuu kadiri gani?

4. (a) Yesu ana mamlaka kuu kadiri gani? (b) Kufahamu mamlaka ya Yesu kunapaswa kuathirije maoni yetu kuhusu amri ya kufanya wanafunzi?

4 Yesu ana mamlaka juu ya kutaniko lake, na tangu mwaka wa 1914 amekuwa na mamlaka juu ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa hivi karibuni. (Wakolosai 1:13; Ufunuo 11:15) Yeye ni malaika mkuu na hivyo ana mamlaka juu ya jeshi la mbinguni la mamia ya mamilioni ya malaika. (1 Wathesalonike 4:16; 1 Petro 3:22; Ufunuo 19:14-16) Amepewa mamlaka na Babake ili kuangamiza ‘serikali zote na mamlaka yote na nguvu zote’ zinazopinga kanuni za uadilifu. (1 Wakorintho 15:24-26; Waefeso 1:20-23) Mamlaka ya Yesu si juu ya wale walio hai tu. Yeye pia ni “mwamuzi wa walio hai na wafu,” naye ana nguvu alizopewa na Mungu za kuwafufua wale waliolala katika kifo. (Matendo 10:42; Yohana 5:26-28) Bila shaka, amri inayotolewa na Mtu aliyepewa mamlaka kuu kama hiyo inapaswa kuonwa kuwa muhimu sana. Kwa hiyo, sisi hutii kwa heshima na kwa hiari amri ya Kristo ya ‘kwenda na kufanya wanafunzi.’

5. (a) Petro alitiije maneno ya Yesu? (b) Petro alibarikiwaje kwa kutii maagizo ya Yesu?

5 Mapema katika huduma yake duniani, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwa njia yenye kutokeza kwamba kutambua mamlaka yake na kutii amri zake kungewaletea baraka. Pindi moja alimwambia hivi Petro ambaye alikuwa mvuvi: “Vuta mpaka mahali penye kilindi, nanyi mshushe nyavu zenu, mvue.” Petro alikuwa na hakika kwamba hakukuwa na samaki, hivyo akamwambia Yesu: “Mwalimu, tulitaabika usiku wote na hatukupata chochote.” Hata hivyo, Petro aliongeza kusema hivi kwa unyenyekevu: “Lakini nitazishusha nyavu kwa amri yako.” Baada ya kutii amri ya Kristo, Petro alivua “samaki wengi sana.” Akiwa amelemewa na hisia, Petro ‘alianguka magotini pa Yesu, akisema: “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana.”’ Lakini Yesu akamjibu: “Acha kuogopa. Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:1-10; Mathayo 4:18) Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo?

6. (a) Masimulizi kuhusu samaki waliovuliwa kimuujiza yanaonyesha nini kuhusiana na utii ambao Yesu hutaka? (b) Tunaweza kumwigaje Yesu?

6 Yesu aliwapa Petro, Andrea, na mitume wengine mgawo wa “kuwa wavuvi wa watu,” si kabla, bali baada ya kuvua samaki wengi sana isivyo kawaida. (Marko 1:16, 17) Ni wazi kwamba Yesu hakutaka wamtii bila kufikiri. Aliwapa sababu yenye kusadikisha ya kumtii. Kama vile kutii amri ya Yesu ya kutupa nyavu kulivyowawezesha kuvua samaki wengi isivyo kawaida, ndivyo kutii amri ya Yesu ya ‘kuvua watu’ kungetokeza baraka nyingi. Mitume walitii wakiwa na imani kamili. Masimulizi hayo yanamalizia: “Wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu, wakamfuata.” (Luka 5:11) Leo, tunapowatia wengine moyo washiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunamwiga Yesu. Hatutaki tu watu wafanye yale tunayowaambia, bali sisi huwapa sababu zenye kusadikisha za kutii amri ya Kristo.

Sababu Zenye Kusadikisha na Nia Ifaayo

7, 8. (a) Tuna sababu gani za Kimaandiko za kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi? (b) Ni andiko gani ambalo hasa hukuchochea kuendelea na kazi ya kuhubiri? (Ona pia maelezo ya chini.)

7 Kwa kuwa tunakubali mamlaka ya Kristo, tunashiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Tuna sababu gani nyingine za Kimaandiko za kufanya kazi hiyo ambazo tunaweza kuwaeleza wale tunaotaka kuwachochea watende mema? Fikiria mambo yafuatayo yaliyosemwa na Mashahidi kadhaa waaminifu kutoka nchi mbalimbali, kisha ona jinsi maandiko yaliyotajwa yanavyounga mkono maelezo yao.

8 Roy, aliyebatizwa mwaka wa 1951: “Nilipojiweka wakfu kwa Yehova, niliahidi kumtumikia sikuzote. Ninataka kutimiza ahadi yangu.” (Zaburi 50:14; Mathayo 5:37) Heather, aliyebatizwa mwaka wa 1962: “Ninapofikiria yote ambayo Yehova amenifanyia, nataka kumshukuru kwa kumtumikia kwa uaminifu.” (Zaburi 9:1, 9-11; Wakolosai 3:15) Hannelore, aliyebatizwa mwaka wa 1954: “Kila mara tunapokuwa katika huduma tunasaidiwa na malaika, hilo ni pendeleo lililoje!” (Matendo 10:30-33; Ufunuo 14:6, 7) Honor, aliyebatizwa mwaka wa 1969: “Wakati wa hukumu ya Yehova ufikapo, singependa yeyote katika ujirani wangu amlaumu Yehova na Mashahidi wake kwamba hawakujali na kusema, ‘Sikuonywa!’” (Ezekieli 2:5; 3:17-19; Waroma 10:16, 18) Claudio, aliyebatizwa mwaka wa 1974: “Tunapohubiri, tunakuwa ‘machoni pa Mungu’ na ‘kushirikiana na Kristo.’ Ebu wazia, tunapokuwa katika huduma, tunashirikiana na Marafiki wetu walio bora zaidi!”—2 Wakorintho 2:17. *

9. (a) Masimulizi kuhusu jinsi Petro na mitume wengine walivyovua samaki huonyesha nini kuhusu nia inayofaa ya kumtii Kristo? (b) Ni nini iliyo nia inayofaa ya kumtii Mungu na Kristo leo, na kwa nini?

9 Masimulizi kuhusu kuvuliwa kwa samaki wengi isivyo kawaida yanaonyesha pia umuhimu wa kuwa na nia inayofaa ya kumtii Kristo, yaani, upendo. Petro aliposema, “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi,” Yesu hakuondoka, wala hakumshutumu Petro kwa dhambi yoyote. (Luka 5:8) Yesu hata hakumkemea Petro kwa kumwomba aondoke, bali alimjibu hivi kwa fadhili: “Acha kuogopa.” Ingekuwa nia mbaya kumtii Kristo kwa sababu ya woga usiofaa. Badala yake, Yesu alimwambia Petro kwamba yeye na wenzake wangetumiwa kuwa wavuvi wa watu. Vivyo hivyo, leo hatuogopeshi watu au kuwafanya waone aibu au wahisi wana hatia, ili kuwalazimisha wamtii Kristo. Utii wa nafsi yote unaotegemea upendo kwa Mungu na Kristo ndio tu hufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Mathayo 22:37.

‘Fanyeni Wanafunzi Kutoka kwa Watu wa Mataifa Yote’

10. (a) Ni jambo gani kuhusu amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi lililotokeza tatizo gumu kwa wanafunzi wake? (b) Wanafunzi waliitikiaje amri ya Yesu?

10 Swali la pili tunaloweza kuuliza kuhusiana na amri ya Kristo ni, kazi hiyo ya kufanya wanafunzi inapaswa kufanywa Wapi? Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Kabla Yesu hajaanza huduma yake, watu wa mataifa walikaribishwa ikiwa walikuja Israeli kumtumikia Yehova. (1 Wafalme 8:41-43) Yesu aliwahubiria hasa Wayahudi wa asili, lakini sasa aliwaambia wafuasi wake waende kwa watu wa mataifa yote. Kwa kweli, eneo la uvuvi, au eneo la kuhubiri, la wanafunzi wake lilikuwa kama “kidimbwi” kidogo, yaani, walivua katika eneo la Wayahudi wa asili, lakini baada ya muda mfupi wangevua katika “bahari” nzima ya wanadamu. Ingawa badiliko hilo lilitokeza tatizo gumu kwa wanafunzi, walitii kwa utayari maagizo ya Yesu. Miaka inayopungua 30 baada ya Yesu kufa, mtume Paulo aliweza kuandika kwamba habari njema zilikuwa zimehubiriwa si kwa Wayahudi tu bali kwa “uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

11. Kumekuwa na mpanuko gani wa ‘maeneo ya uvuvi’ tangu mapema karne ya 20?

11 Vivyo hivyo, hivi karibuni eneo la kuhubiri limepanuka. Mwanzoni mwa karne ya 20, ‘maeneo ya uvuvi’ yalikuwa tu katika nchi chache. Hata hivyo, wafuasi wa Kristo wakati huo waliiga kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza, nao walipanua kwa bidii eneo walilohubiri. (Waroma 15:20) Mapema miaka ya 1930, walikuwa wakifanya wanafunzi katika nchi mia moja hivi. Leo ‘maeneo yetu ya uvuvi’ yanapatikana katika nchi 235.—Marko 13:10.

“Kutoka Katika Lugha Zote”

12. Unabii kwenye Zekaria 8:23 unakazia jambo gani gumu?

12 Kufanya wanafunzi katika mataifa yote ni jambo gumu si kwa sababu tu ya ukubwa wa eneo bali pia kwa sababu ya lugha nyingi zinazotumiwa. Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Zekaria: “Na itakuwa katika siku hizo kwamba watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Katika utimizo mkubwa zaidi wa unabii huo, “mtu aliye Myahudi” huwakilisha mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta, nao “watu kumi” huwakilisha “umati mkubwa.” * (Ufunuo 7:9, 10; Wagalatia 6:16) Umati huo mkubwa wa wanafunzi wa Kristo ungepatikana katika mataifa mengi, na kama vile Zekaria alivyosema, wangezungumza lugha mbalimbali. Je, leo watu wa Mungu wanatoka katika mataifa mengi, nao huzungumza lugha mbalimbali? Ndiyo.

13. (a) Kumekuwa na badiliko gani kuhusu lugha kati ya watu wa Mungu leo? (b) Jamii ya mtumwa mwaminifu imefanya nini kuhusu uhitaji unaoongezeka wa chakula cha kiroho katika lugha mbalimbali? (Tia ndani sanduku “Vichapo kwa Ajili ya Wasioweza Kuona.”)

13 Katika mwaka wa 1950 lugha ya asili ya Mashahidi wa Yehova 3 kati ya 5 ulimwenguni ilikuwa Kiingereza. Kufikia mwaka wa 1980 uwiano huo ulibadilika ukawa Mashahidi 2 kati ya 5, na leo ni Shahidi 1 tu kati ya 5 ambaye lugha yake ya asili ni Kiingereza. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara imefanya nini kuhusiana na badiliko hilo? Jamii hiyo imeandaa chakula cha kiroho katika lugha nyingi zaidi. (Mathayo 24:45) Kwa mfano, mwaka wa 1950 vichapo vyetu vilichapishwa katika lugha 90, lakini leo vichapo vyetu vinachapishwa katika lugha 400 hivi. Je, hatua hiyo ya kuwafikiria watu wanaozungumza lugha mbalimbali imekuwa na matokeo? Ndiyo! Wastani wa watu 5,000 hivi ‘kutoka lugha zote’ huwa wanafunzi wa Kristo kila juma! (Ufunuo 7:9) Na ongezeko hilo linaendelea. Katika nchi fulani “nyavu” zinanasa samaki wengi sana!—Luka 5:6; Yohana 21:6.

Je, Unaweza Kushiriki Katika Huduma Yenye Kuthawabisha?

14. Tunawezaje kuwasaidia watu katika eneo letu wanaozungumza lugha tofauti na yetu? (Tia ndani sanduku “Lugha ya Ishara na Kufanya Wanafunzi.”)

14 Kwa sababu ya kuwepo kwa wahamiaji katika nchi nyingi za Magharibi, imewabidi Mashahidi wafanye wanafunzi kutoka ‘kila lugha’ katika nchi zao. (Ufunuo 14:6) Tunawezaje kuwasaidia wale walio katika eneo letu ambao wanazungumza lugha tofauti na yetu? (1 Timotheo 2:4) Tunaweza kutumia vifaa vifaavyo katika uvuaji wa mfano. Wape watu hao vichapo katika lugha yao. Ikiwezekana, panga Shahidi anayezungumza lugha yao awatembelee. (Matendo 22:2) Sasa ni rahisi zaidi kufanya mipango hiyo, kwa kuwa Mashahidi wengi wamejifunza kuzungumza lugha nyingine mbali na lugha yao ya asili ili kuwasaidia wageni wawe wanafunzi wa Kristo. Ripoti zinaonyesha kwamba inathawabisha kusaidia kwa njia hiyo.

15, 16. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba inathawabisha kuwasaidia wale wanaozungumza lugha ya kigeni? (b) Huenda tukafikiria maswali gani kuhusu utumishi katika eneo la lugha ya kigeni?

15 Fikiria mifano miwili kutoka Uholanzi ambako kazi iliyopangwa ya kuhubiri Ufalme inafanywa katika lugha 34. Mashahidi wawili ambao ni mume na mke walijitolea kwenda kufanya wanafunzi kati ya wahamiaji wanaozungumza Kipolandi. Jitihada zao zilikuwa na matokeo makubwa sana hivi kwamba ilimbidi mume kupunguza wakati anaotumia kazini ili awe na siku moja zaidi kila juma ya kujifunza Biblia pamoja na wale wanaopendezwa. Muda si muda, wenzi hao walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 20 kila juma. Walisema: “Huduma yetu hutufurahisha sana.” Wale wanaofanya wanafunzi hufurahi hasa wakati wale wanaosikia kweli za Biblia katika lugha yao wanapotoa shukrani. Kwa mfano, wakati mkutano fulani ulifanywa katika lugha ya Vietnam, mtu mmoja mzee alisimama na kuomba aruhusiwe kuzungumza. Huku akilengwa-lengwa na machozi, aliwaambia Mashahidi hivi: “Asanteni kwa jitihada zenu za kujifunza lugha yangu ngumu. Ninashukuru sana kujifunza mambo mengi mazuri kutoka katika Biblia nikiwa mzee.”

16 Kwa hiyo, haishangazi kwamba wale wanaotumika katika makutaniko yanayozungumza lugha za kigeni wanathawabishwa sana. Mume na mke kutoka Uingereza walisema: “Tumefurahia zaidi huduma katika maeneo ya lugha za kigeni katika miaka 40 ambayo tumekuwa tukihubiri juu ya Ufalme.” Je, unaweza kurekebisha hali zako ili ushiriki katika huduma hiyo yenye kufurahisha? Ikiwa bado uko shule, je, unaweza kujifunza lugha ya kigeni ili kujitayarisha kwa ajili ya huduma hiyo? Huenda kwa kufanya hivyo ukawa na maisha yenye kuridhisha, yaliyojaa baraka. (Methali 10:22) Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazazi wako?

Kubadili Njia Zetu za Kuhubiri

17. Tunawezaje kuwafikia watu wengi zaidi katika eneo letu la kutaniko?

17 Inaeleweka kwamba hali haziruhusu wengi wetu kutupa “nyavu” katika maeneo ya lugha za kigeni. Hata hivyo, tunaweza kuwafikia watu wengi zaidi kuliko tunavyofanya sasa katika eneo letu la kutaniko. Jinsi gani? Kwa kubadili njia zetu za kuhubiri, bali si ujumbe wetu. Katika maeneo mengi, watu wanaoishi katika nyumba zenye ulinzi mkali wanazidi kuongezeka. Wengine wengi hawapatikani nyumbani tunapowatembelea katika huduma yetu ya nyumba kwa nyumba. Kwa hiyo, huenda tukahitaji kutupa “nyavu” zetu wakati tofauti na sehemu tofauti. Kwa njia hiyo, tunamwiga Yesu. Alijitahidi sana kuzungumza na watu katika hali mbalimbali.—Mathayo 9:9; Luka 19:1-10; Yohana 4:6-15.

18. Kutoa ushahidi katika hali tofauti-tofauti kumekuwaje na matokeo? (Tia ndani sanduku “Kufanya Wanafunzi Katika Maeneo ya Wafanyabiashara.”)

18 Katika maeneo fulani duniani, kuhubiri popote watu wanapoweza kupatikana ni njia muhimu ya kufanya wanafunzi. Wafanya-wanafunzi wenye uzoefu wamekuwa wakizingatia zaidi kutoa ushahidi katika maeneo tofauti-tofauti. Zaidi ya kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, sasa wahubiri wanatoa ushahidi kwenye viwanja vya ndege, ofisini, madukani, kwenye maegesho ya magari, vituo vya basi, barabarani, bustanini, kwenye fuo, na kwingineko. Wengi wa Mashahidi waliobatizwa majuzi huko Hawaii walihubiriwa mara ya kwanza kwenye sehemu hizo. Kubadili njia zetu za kuhubiri hutusaidia kutimiza kikamili amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi.—1 Wakorintho 9:22, 23.

19. Ni sehemu gani za mgawo ambao Yesu alitupatia ambazo zitazungumziwa katika makala inayofuata?

19 Mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi haukutia ndani tu habari kuhusu kwa nini na ni wapi tunakopaswa kufanya kazi hiyo, bali pia habari kuhusu ni nini tunachopaswa kuhubiri na tunapaswa kuendelea kufanya hivyo hadi lini. Sehemu hizo mbili za mgawo ambao Yesu alitupatia zitazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika makala hii, tutazungumzia maswali mawili ya kwanza. Nayo maswali mawili ya mwisho yatazungumziwa katika makala inayofuata.

^ fu. 12 Ili upate habari zaidi kuhusu utimizo mbalimbali wa unabii huo, ona gazeti Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 2001, ukurasa wa 12, na kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Pili, ukurasa wa 408, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Tunashiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi kwa sababu zipi na tukiwa na nia gani?

• Leo watumishi wa Yehova wametimiza kwa kadiri gani mgawo waliopewa na Yesu wa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote?

• Tunawezaje kubadili ‘njia zetu za kuvua,’ na kwa nini tufanye hivyo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Vichapo kwa Ajili ya Wasioweza Kuona

Albert ni mzee Mkristo na mhudumu wa wakati wote anayeishi Marekani. Yeye haoni. Kutumia vichapo vya Biblia katika Braille humsaidia vizuri zaidi kutimiza huduma yake na pia kazi yake akiwa mwangalizi wa utumishi. Yeye hushughulikiaje mgawo wake kutanikoni?

“Albert ni mwangalizi wa utumishi mwenye matokeo sana katika kutaniko letu,” asema James, mwangalizi-msimamizi. Albert ni mmoja kati ya watu wasioweza kuona wapatao 5,000 nchini Marekani ambao, katika miaka iliyopita, wamepokea vichapo vya Biblia katika maandishi ya Braille ya Kiingereza na Kihispania. Kwa kweli, kuanzia mwaka wa 1912 na kuendelea, jamii ya mtumwa mwaminifu imechapisha vichapo mbalimbali zaidi ya mia moja katika Braille. Kwa kutumia tekinolojia ya kisasa, sasa mashine za kuchapa za Mashahidi wa Yehova zinachapisha mamilioni ya vichapo vya Braille kila mwaka katika lugha zaidi ya kumi na kuvigawanya katika nchi zaidi ya 70. Je, unajua mtu anayeweza kunufaika na vichapo vya Biblia vilivyotayarishwa kwa ajili ya wasioweza kuona?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Lugha ya Ishara na Kufanya Wanafunzi

Maelfu ya Mashahidi duniani pote, kutia ndani vijana wengi wenye bidii wamejifunza lugha ya ishara ili kuwasaidia watu wasioweza kusikia wawe wanafunzi wa Kristo. Kwa sababu hiyo, Brazili peke yake, watu 63 wasioweza kusikia walibatizwa hivi karibuni katika kipindi cha mwaka mmoja, nao Mashahidi 35 wasioweza kusikia nchini humo sasa ni waeneza-injili wa wakati wote. Ulimwenguni pote, kuna makutaniko na vikundi zaidi ya 1,200 vya lugha ya ishara. Mzunguko pekee wa lugha ya ishara huko Urusi ndio mkubwa zaidi ulimwenguni, nao unahusisha Urusi yote!

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Kufanya Wanafunzi Katika Maeneo ya Wafanyabiashara

Alipokuwa akiwatembelea wafanyabiashara katika ofisi zao, Shahidi mmoja huko Hawaii alikutana na msimamizi wa kampuni fulani ya usafiri. Ingawa mtu huyo alikuwa na shughuli nyingi, alikubali kujifunza Biblia kwa muda wa dakika 30 kila juma ofisini mwake. Kila Jumatano asubuhi, yeye huwaambia wafanyakazi wake wasipeleke simu ofisini mwake, kisha yeye hukazia fikira kikamili funzo hilo. Shahidi mwingine huko Hawaii hujifunza Biblia mara moja kwa juma pamoja na mwenye duka la kurekebisha viatu. Wao hujifunzia kwenye kaunta ya duka. Mteja anapoingia, Shahidi huyo husimama kando. Mteja anapoondoka wao huendelea na funzo lao.

Watu hao wawili, msimamizi na mwenye duka, walifikiwa kwa sababu Mashahidi walichukua hatua ya kwanza kutupa “nyavu” zao kwenye sehemu tofauti. Je, unaweza kufikiria sehemu fulani katika eneo la kutaniko lenu ambako unaweza kupata watu ambao si rahisi kuwapata nyumbani?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, unaweza kutumikia katika eneo la lugha ya kigeni?