Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’

‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’

‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’

“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—MATHAYO 28:19, 20.

1. Ni mazungumzo gani yaliyotokea kati ya mwanafunzi Filipo na mtu fulani kutoka Ethiopia?

MTU fulani kutoka Ethiopia alikuwa amesafiri hadi Yerusalemu. Huko alimwabudu Yehova, Mungu aliyempenda. Yaonekana pia alipenda Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Alipokuwa akirudi nyumbani katika gari lake la kukokotwa, alikuwa akisoma nakala ya maandishi ya nabii Isaya, wakati alipokutana na Filipo, mwanafunzi wa Kristo. Filipo alimuuliza Mwethiopia huyo hivi: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Mtu huyo akajibu: “Ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Filipo alimsaidia mwanafunzi huyo mnyoofu wa Biblia kuwa mwanafunzi wa Kristo.—Matendo 8:26-39.

2. (a) Ni katika njia gani jibu lililotolewa na Mwethiopia lilikuwa muhimu sana? (b) Tutazungumzia maswali gani kuhusu mgawo ambao Kristo alitoa wa kufanya wanafunzi?

2 Jibu la Mwethiopia huyo ni muhimu sana. Alisema: ‘Ninawezaje, mtu fulani asiponiongoza.’ Naam, alihitaji mtu wa kumwongoza. Maneno hayo yanaonyesha umuhimu wa maagizo hususa ambayo Yesu alitia ndani katika mgawo aliotoa wa kufanya wanafunzi. Ni maagizo gani? Ili kupata jibu, na tuendelee na mazungumzo yetu kuhusu maneno ya Yesu katika Mathayo sura ya 28. Makala iliyotangulia ilikazia maswali—kwa nini? na wapi? Sasa tutazungumzia maswali mengine mawili kuhusu amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi—nini? na lini?

“Kuwafundisha Kushika Mambo Yote”

3. (a) Mtu anakuwaje mwanafunzi wa Yesu Kristo? (b) Kufanya wanafunzi hutia ndani kufundisha nini?

3 Tunapaswa kufundisha nini ili kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Kristo? Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo ni lazima tufundishe mambo ambayo Kristo aliamuru. * Lakini ni nini kinachoweza kufanywa ili kuhakikisha kwamba mtu anayefundishwa amri za Yesu hatakuwa tu mwanafunzi bali ataendelea kuwa mwanafunzi? Jambo moja muhimu tunaloona ni kwamba Yesu alichagua maneno yake kwa makini. Ona kwamba hakusema tu: ‘Wafundisheni kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ Bali alisema: ‘Wafundisheni kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ (Mathayo 19:17) Hiyo inamaanisha nini?

4. (a) Inamaanisha nini kutii amri fulani? (b) Onyesha jinsi ambavyo sisi humfundisha mtu kushika amri za Kristo?

4 Kushika amri humaanisha “kutenda kupatana” na amri iliyotolewa, yaani, kuitii, au kuifuata. Basi, tunawezaje kumfundisha mtu kushika, au kutii, mambo ambayo Kristo aliamuru? Fikiria jinsi mtu anayewafundisha watu kuendesha gari anavyowaonyesha wanafunzi wake kushika sheria za barabarani. Mwalimu huyo anaweza kuwafundisha wanafunzi wake sheria za barabarani wanapokuwa darasani. Hata hivyo, ili kuwafundisha wanafunzi hao jinsi ya kutii sheria hizo, anapaswa kuwaongoza wanapoendesha gari katika barabara yenye magari na wanapojitahidi kutumia mambo ambayo wamejifunza. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia pamoja na watu, sisi huwafundisha amri za Kristo. Hata hivyo, tunahitaji pia kuwaongoza wanafunzi wanapojitahidi kufuata maagizo ya Kristo maishani na katika huduma. (Yohana 14:15; 1 Yohana 2:3) Hivyo, ili kufuata kikamili amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi tunahitaji kuwafundisha na kuwaongoza watu. Kwa njia hiyo, tunaiga kielelezo kilichowekwa na Yesu na Yehova mwenyewe.—Zaburi 48:14; Ufunuo 7:17.

5. Kwa nini huenda mtu tunayejifunza Biblia naye akasita kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi?

5 Kuwafundisha wengine kushika amri za Yesu hutia ndani kuwasaidia watii amri ya kufanya wanafunzi. Huenda hilo likawa jambo gumu kwa baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia. Hata kama hapo awali walikuwa washiriki wenye bidii wa kanisa fulani la dini zinazojiita za Kikristo, haielekei kwamba wale waliokuwa walimu wao wa kidini waliwafundisha kwenda na kufanya wanafunzi. Viongozi fulani wa dini wanakiri waziwazi kwamba dini zinazojiita za Kikristo zimeshindwa kabisa kuwafundisha waumini wao kueneza injili. John R. W. Stott, msomi wa Biblia alisema hivi kuhusu amri ya Yesu ya kwenda ulimwenguni na kuwasaidia watu wa namna zote wawe wanafunzi: “Leo udhaifu ulio mkubwa zaidi wa Wakristo waeneza-injili ni kule kushindwa kwetu kutii kile kinachomaanishwa na amri hiyo.” Aliongeza kusema: “Tuna mwelekeo wa kutangaza ujumbe wetu kutoka mbali. Wakati mwingine sisi huonekana kama watu ambao wanawashauri watu wanaozama maji huku tukiwa mahali salama ufuoni. Hatuingii majini kuwaokoa. Tunaogopa kulowa maji.”

6. (a) Tunawezaje kuiga kielelezo cha Filipo tunapomsaidia mwanafunzi wa Biblia? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba tunajali wakati mwanafunzi wa Biblia anapoanza kuhubiri?

6 Ikiwa mtu tunayejifunza Biblia naye alikuwa mshiriki wa dini ambayo waumini wake ‘huogopa kulowa maji,’ huenda ikawa vigumu kwake kuacha kuogopa maji ya mfano, na kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Atahitaji msaada. Hivyo, tunahitaji kuwa wenye subira tunapotoa maagizo na mwongozo ambao humsaidia kuwa na uelewaji wenye kina na kumchochea kutenda, kama vile mafundisho ya Filipo yalivyomsaidia yule Mwethiopia kuelewa mambo na kumchochea kubatizwa. (Yohana 16:13; Matendo 8:35-38) Pia, tamaa yetu ya kuwafundisha wanafunzi wa Biblia kushika amri ya kufanya wanafunzi hutuchochea kuwasaidia na kuwaongoza wanapochukua hatua za kwanza katika kuhubiri Ufalme.—Mhubiri 4:9, 10; Luka 6:40.

“Mambo Yote”

7. Kuwafundisha wengine ‘washike mambo yote’ hutia ndani kuwafundisha amri zipi?

7 Hatuwafundishi tu wanafunzi wetu wapya kufanya wanafunzi. Yesu alituagiza tuwafundishe wengine ‘washike mambo yote’ aliyoamuru. Bila shaka, hilo linatia ndani amri mbili zilizo kuu—kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:37-39) Mwanafunzi mpya anawezaje kufundishwa ashike amri hizo?

8. Onyesha jinsi mwanafunzi mpya anavyoweza kufundishwa amri ya kuonyesha upendo.

8 Fikiria tena mfano wa mtu anayefundishwa kuendesha gari. Mwanafunzi huyo anapoendesha gari katika barabara yenye magari akiwa pamoja na mwalimu wake, yeye hujifunza kwa kumsikiliza mwalimu wake na pia kwa kuwatazama madereva wengine. Kwa mfano, huenda mwalimu huyo akamwonyesha dereva ambaye kwa fadhili anamruhusu mwingine apite mbele yake; au dereva ambaye kwa heshima anapunguza mwangaza wa taa zake za mbele ili asifanye madereva kutoka upande ule mwingine wasione vizuri; au dereva anayejitolea kumsaidia rafiki ambaye gari lake limeharibika. Mifano hiyo humfundisha mwanafunzi mambo muhimu anayoweza kutumia anapoendesha gari. Vivyo hivyo, mwanafunzi mpya anayesafiri kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima hujifunza kutoka kwa mwalimu wake na pia kutokana na vielelezo vizuri anavyoona kwenye kutaniko.—Mathayo 7:13, 14.

9. Mwanafunzi mpya hujifunzaje maana ya kushika amri ya kuonyesha upendo?

9 Kwa mfano, huenda mwanafunzi wa Biblia akamwona mzazi asiye na mwenzi wa ndoa ambaye hujitahidi sana kuja kwenye Jumba la Ufalme akiandamana na watoto wake wadogo. Huenda akamwona mtu aliyeshuka moyo ambaye huhudhuria mikutano kwa uaminifu ingawa anapambana na mshuko-moyo, mjane mzee anayewapeleka wazee wengine kwenye kila mkutano wa kutaniko kwa gari lake, au kijana anayesaidia kusafisha Jumba la Ufalme. Huenda mwanafunzi huyo wa Biblia akamwona mzee wa kutaniko ambaye kwa uaminifu huwa mstari wa mbele katika utumishi wa shambani licha ya kuwa na madaraka mengi kutanikoni. Huenda akakutana na Shahidi ambaye ni mlemavu na asiyeweza kutoka nyumbani lakini ambaye huwatia moyo wote kiroho wanaomtembelea. Huenda mwanafunzi huyo akaona mume na mke ambao wanajitahidi sana kufanya marekebisho maishani mwao ili kuwatunza wazazi wao waliozeeka. Kwa kuwatazama Wakristo hao wenye fadhili, wenye kusaidia, na wanaotegemeka, mwanafunzi huyo mpya hujifunza kupitia kielelezo chao maana ya kutii amri ya Kristo ya kumpenda Mungu na jirani, na hasa waamini wenzetu. (Methali 24:32; Yohana 13:35; Wagalatia 6:10; 1 Timotheo 5:4, 8; 1 Petro 5:2, 3) Kwa njia hiyo, kila mshiriki wa kutaniko la Kikristo anaweza—na anapaswa—kufundisha na kuongoza.—Mathayo 5:16.

“Mpaka Umalizio wa Mfumo wa Mambo”

10. (a) Tutaendelea kufanya wanafunzi mpaka lini? (b) Yesu aliweka kielelezo gani kuhusu kutimiza migawo?

10 Tunapaswa kuendelea kufanya wanafunzi mpaka lini? Mpaka umalizio wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 28:20) Je, tutaweza kutimiza sehemu hii ya mgawo wa Yesu? Tunaazimia kufanya hivyo tukiwa kutaniko la duniani pote. Katika miaka iliyopita tumefurahia kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kuwatafuta wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Matendo 13:48) Leo, Mashahidi wa Yehova hutumia wastani wa saa zaidi ya milioni tatu kila siku katika mwaka kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ulimwenguni pote. Sisi hufanya hivyo kwa kuwa tunafuata kielelezo cha Yesu. Alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Hiyo pia ndiyo tamaa yetu ya kutoka moyoni. (Yohana 20:21) Hatutaki tu kuanza kazi tuliyokabidhiwa, bali tunataka kuimaliza.—Mathayo 24:13; Yohana 17:4.

11. Ni nini kimewapata baadhi ya ndugu na dada zetu Wakristo, nasi tunapaswa kujiuliza nini?

11 Hata hivyo, tunasikitika kuona kwamba baadhi ya waamini wenzetu wamekuwa dhaifu kiroho, na hivyo wamepunguza mwendo au wameacha kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Je, kuna njia ya kuwasaidia waanze kushirikiana tena na kutaniko na kurudia kazi yao ya kufanya wanafunzi? (Waroma 15:1; Waebrania 12:12) Jinsi ambavyo Yesu aliwasaidia mitume wake walipopatwa na udhaifu wa muda huonyesha jinsi tunavyoweza kufanya leo.

Onyesha Kwamba Unajali

12. (a) Punde kabla ya Yesu kufa, mitume wake walifanya nini? (b) Yesu alishughulikaje na mitume wake licha ya wao kuonyesha udhaifu mkubwa?

12 Kifo cha Yesu kilipokaribia mwishoni mwa huduma yake duniani, mitume ‘walimwacha na kukimbia.’ Kama Yesu alivyokuwa ametabiri, ‘walitawanyika na kwenda kila mmoja kwenye nyumba yake.’ (Marko 14:50; Yohana 16:32) Yesu alishughulikaje na rafiki zake waliokuwa wamedhoofika kiroho? Punde baada ya Yesu kufufuka, aliwaambia hivi baadhi ya wafuasi wake: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu, ili wapate kwenda zao Galilaya; na huko wataniona.” (Mathayo 28:10) Ingawa mitume walionyesha udhaifu mkubwa, bado Yesu aliwaita “ndugu zangu.” (Mathayo 12:49) Hakuwa amekata tamaa kuwaelekea. Kwa njia hiyo, Yesu akawa mwenye rehema na mwenye kusamehe, kama vile Yehova alivyo mwenye rehema na mwenye kusamehe. (2 Wafalme 13:23) Tunawezaje kumwiga Yesu?

13. Tunapaswa kuwaonaje wale ambao wamekuwa dhaifu kiroho?

13 Tunapaswa kuwajali sana wale waliopunguza mwendo au walioacha kushiriki katika huduma. Tungali tunakumbuka kazi za upendo ambazo waamini hao wenzetu walifanya zamani— wengine labda kwa miaka mingi. (Waebrania 6:10) Kwa kweli tunakosa ushirika wao. (Luka 15:4-7; 1 Wathesalonike 2:17) Lakini tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali?

14. Kwa kumwiga Yesu, tunawezaje kumsaidia mtu aliye dhaifu?

14 Yesu aliwaambia mitume waliovunjika moyo kwamba wanapaswa kwenda Galilaya na kwamba wangemwona huko. Kwa kweli, Yesu aliwaalika wahudhurie mkutano fulani wa kipekee. (Mathayo 28:10) Vivyo hivyo leo, tunawatia moyo wale walio dhaifu kiroho wahudhurie mikutano ya kutaniko la Kikristo, na huenda tukahitaji kuwatia moyo mara nyingi ili wafanye hivyo. Kuhusu mitume, mwaliko wa Yesu ulikuwa na matokeo, kwa kuwa ‘wale wanafunzi kumi na mmoja waliingia Galilaya mpaka kwenye mlima ambako Yesu alikuwa amewafanyia mpango.’ (Mathayo 28:16) Tunafurahi kama nini wakati wale walio dhaifu wanapoitikia mwaliko wetu wa uchangamfu, na kuanza tena kuhudhuria mikutano ya Kikristo!—Luka 15:6.

15. Tunawezaje kufuata kielelezo cha Yesu katika kuwakaribisha watu dhaifu wanaokuja mahali petu pa mikutano?

15 Tutafanyaje Mkristo aliye dhaifu anapofika kwenye Jumba la Ufalme? Yesu, alifanya nini alipoona mitume wake ambao imani yao ilikuwa imedhoofika kwa muda, wakiwa mahali walipopanga kukutana? ‘Yesu alikaribia na kuzungumza nao.’ (Mathayo 28:18) Hakuwatazama tu kutoka mbali, bali alienda walipokuwa. Wazia jinsi mitume walivyofurahi wakati Yesu alipochukua hatua hiyo! Sisi pia na tuchukue hatua ya kwanza na kuwakaribisha kwa uchangamfu wale walio dhaifu kiroho ambao wanajitahidi kurudi katika kutaniko la Kikristo.

16. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi ambavyo Yesu alishughulika na wafuasi wake? (b) Tunawezaje kuonyesha maoni kama ya Yesu kuelekea walio dhaifu? (Ona maelezo ya chini.)

16 Yesu alifanya jambo gani lingine? Kwanza, alitoa tangazo fulani: “Nimepewa mamlaka yote.” Pili, akatoa mgawo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Tatu, akatoa ahadi: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote.” Lakini je, umeona jambo ambalo Yesu hakufanya? Hakuwakemea wanafunzi kwa udhaifu na shaka zao. (Mathayo 28:17) Je, njia yake ilikuwa na matokeo? Ndiyo, kwa kuwa muda si muda mitume walikuwa wameanza tena “kufundisha na kutangaza habari njema.” (Matendo 5:42) Kwa kuiga kielelezo cha Yesu kuhusu jinsi tunavyowaona na tunavyowatendea walio dhaifu, tunaweza kutarajia kupata matokeo kama hayo yenye kuchangamsha moyo katika kutaniko letu. *Matendo 20:35.

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”

17, 18. Maneno ya Yesu “mimi nipo pamoja nanyi siku zote” yana matokeo gani yenye kuimarisha?

17 Maneno haya ya mwisho kuhusu mgawo ambao Yesu alitoa, “Nipo pamoja nanyi siku zote,” yana matokeo yenye kuimarisha kwa wote wanaojitahidi kutimiza amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Hata tukabili upinzani wa aina gani kutoka kwa maadui dhidi ya kazi yetu ya kuhubiri Ufalme, na hata watuchongee kwa njia gani, hatupaswi kuogopa. Kwa nini? Kwa kuwa Yesu, Kiongozi wetu, ambaye ana ‘mamlaka yote mbinguni na duniani,’ yuko pamoja nasi ili kutusaidia!

18 Ahadi ya Yesu “mimi nipo pamoja nanyi siku zote” hutufariji sana pia. Tunapojitahidi kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi, sisi hupata furaha na pia huzuni wakati mwingine. (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Baadhi yetu hupatwa na huzuni tunapoomboleza kifo cha mpendwa. (Mwanzo 23:2; Yohana 11:33-36) Wengine wanapambana na uzee, wakati afya na nguvu zinapoendelea kuzorota. (Mhubiri 12:1-6) Hata wengine hukabili vipindi ambapo wanalemewa na hali ya kuvunjika moyo. (1 Wathesalonike 5:14) Na hesabu inayoongezeka kati yetu hupambana na hali ngumu za kiuchumi. Hata hivyo, licha ya magumu hayo, sisi hufanikiwa katika huduma yetu kwa sababu Yesu yuko pamoja nasi “siku zote,” hata zile siku ngumu zaidi maishani mwetu.—Mathayo 11:28-30.

19. (a) Kuna maagizo gani katika mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi? (b) Ni nini hutusaidia kutimiza mgawo ambao Kristo alitoa?

19 Kama ambavyo tumeona katika makala hii na ile iliyotangulia, mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi unahusu sehemu zote nne. Yesu alituambia ni kwa nini na ni wapi tunapopaswa kutekeleza amri yake. Pia alituambia ni nini tunachopaswa kufundisha na tunapaswa kufanya hivyo mpaka lini. Kweli, ni jambo gumu kutimiza mgawo huo. Lakini kwa kuwa Kristo aliye na mamlaka anatuunga mkono na yupo pamoja nasi, tunaweza kuutimiza! Je, hukubali?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kitabu kimoja cha marejeo kinaonyesha kwamba Yesu alisema, “kuwabatiza   . . . kuwafundisha,” bali si ‘kuwabatiza na kuwafundisha.’ Hivyo, katika amri ya kubatiza na kufundisha ‘si lazima mambo hayo mawili yafuatane.’ Bali, “kufundisha ni tendo linaloendelea, ambalo kwa kadiri fulani hutangulia na kufuata ubatizo.”

^ fu. 16 Habari zaidi kuhusu jinsi unavyopaswa kuwaona na kuwasaidia walio dhaifu inapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 2003, ukurasa wa 15-18.

Ungejibuje?

• Tunawafundishaje wengine kushika yale ambayo Yesu aliamuru?

• Mwanafunzi mpya anaweza kujifunza mambo gani kutoka kwa wengine kutanikoni?

• Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale ambao wamekuwa dhaifu kiroho?

• Tunapata nguvu na faraja gani kutokana na ahadi ya Yesu “mimi nipo pamoja nanyi siku zote”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunahitaji kuwafundisha na kuwaongoza watu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mwanafunzi mpya hujifunza mambo muhimu kutokana na kielelezo cha wengine