Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapendezwa na “Sheria ya Yehova”?

Je, Unapendezwa na “Sheria ya Yehova”?

Je, Unapendezwa na “Sheria ya Yehova”?

‘Mwenye furaha ni mtu ambaye mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova.’—ZABURI 1:1, 2.

1. Kwa nini sisi ni wenye furaha tukiwa watumishi wa Yehova?

YEHOVA hutusaidia na kutubariki tukiwa watumishi wake washikamanifu. Ni kweli kwamba tunakabili majaribu mengi. Hata hivyo, sisi tuna furaha ya kweli. Hiyo haishangazi kwa kuwa tunamtumikia “Mungu mwenye furaha,” nayo roho yake takatifu hutokeza shangwe mioyoni mwetu. (1 Timotheo 1:11; Wagalatia 5:22) Shangwe ni hali ya kuwa na furaha ya kweli inayotokana na kutarajia au kupata kitu fulani kizuri. Na bila shaka, Baba yetu wa mbinguni hutupa zawadi njema. (Yakobo 1:17) Si ajabu kwamba sisi ni wenye furaha!

2. Tutazungumzia zaburi zipi?

2 Sifa ya furaha inakaziwa sana katika kitabu cha Zaburi. Kwa mfano, inakaziwa katika Zaburi ya 1 na ya 2. Wafuasi wa mapema wa Yesu Kristo walisema kwamba zaburi ya pili iliandikwa na Mfalme Daudi wa Israeli. (Matendo 4:25, 26) Mtungaji wa zaburi ya kwanza asiyetajwa jina anaanza wimbo wake ulioongozwa na roho ya Mungu kwa maneno haya: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu.” (Zaburi 1:1) Katika makala hii na ile inayofuata, na tuone jinsi Zaburi ya 1 na ya 2 zinavyotupa sababu ya kushangilia.

Siri ya Kupata Furaha

3. Kulingana na Zaburi 1:1, ni sababu zipi ambazo hufanya mtu anayeshika sheria za Mungu awe mwenye furaha?

3 Zaburi ya 1 inaonyesha ni kwa sababu gani mtu anayeshika sheria za Mungu ni mwenye furaha. Akitaja sababu za kuwa na furaha hiyo, mtunga-zaburi anaimba: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, na katika njia ya watenda-dhambi hakusimama, na katika kiti cha wenye dhihaka hakuketi.”—Zaburi 1:1.

4. Zekaria na Elisabeti walifuatia njia gani bora ya maisha?

4 Ili tuwe wenye furaha kikweli, lazima tutimize matakwa ya uadilifu ya Yehova. Zekaria na Elisabeti, waliokuwa na pendeleo lenye shangwe la kumzaa Yohana Mbatizaji, “walikuwa waadilifu mbele za Mungu kwa sababu ya kutembea bila lawama kulingana na amri zote na matakwa ya kisheria ya Yehova.” (Luka 1:5, 6) Tunaweza kuwa wenye furaha tukitenda vivyo hivyo na kukataa katakata ‘kutembea katika shauri la waovu’ au kuongozwa na shauri lao ovu.

5. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka “njia ya watenda-dhambi”?

5 Tukikataa mawazo ya waovu, ‘hatutasimama katika njia ya watenda-dhambi.’ Kwa kweli, hatutaenda mahali ambapo mara nyingi wao huwa, yaani, kwenye sehemu za vitumbuizo visivyo vya adili au zenye sifa mbaya. Namna gani tukishawishiwa kujiunga na watenda-dhambi katika mwenendo wao usiopatana na Maandiko? Basi na tumwombe Mungu msaada ili tutende kupatana na maneno haya ya mtume Paulo: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza?” (2 Wakorintho 6:14) Tukimtegemea Mungu na tukiwa “safi moyoni,” tutakataa mtazamo na mtindo wa maisha wa watenda-dhambi na tutakuwa na nia na tamaa safi, pamoja na “imani bila unafiki.” —Mathayo 5:8; 1 Timotheo 1:5.

6. Kwa nini tunapaswa kujihadhari na wenye dhihaka?

6 Bila shaka, ili kumfurahisha Yehova hatupaswi ‘kuketi katika kiti cha wenye dhihaka.’ Wengine hudhihaki wale wanaoshika sheria za Mungu, lakini katika ‘siku hizi za mwisho,’ mara nyingi watu waliokuwa Wakristo ambao sasa ni waasi-imani huwadhihaki kwa dharau nyingi sana. Mtume Petro aliwaonya waamini wenzake hivi: “Wapendwa, . . . mnajua hili kwanza, kwamba katika siku za mwisho watakuja wadhihaki na dhihaka zao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Petro 3:1-4) Ikiwa ‘hatutaketi kamwe katika kiti cha wenye dhihaka,’ tutaepuka msiba ambao hakika utawapata.—Methali 1:22-27.

7. Kwa nini tunapaswa kutii maneno ya Zaburi 1:1?

7 Tusipotii maneno ya utangulizi ya Zaburi ya 1, hali ya kiroho ambayo tumesitawisha kwa kujifunza Biblia inaweza kuharibika. Kwa kweli, maisha yetu yanaweza kuwa mabaya hata zaidi. Hali yetu ya kiroho inaweza kuanza kuharibika tukifuata shauri la waovu. Kisha tunaweza kuanza kushirikiana nao kwa ukawaida. Baada ya muda, huenda hata tukawa waasi-imani wenye dhihaka. Bila shaka, kuwa na urafiki na waovu kunaweza kukuza ndani yetu roho ya kutomwogopa Yehova Mungu na pia kunaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja naye. (1 Wakorintho 15:33; Yakobo 4:4) Tusikubali kamwe kupatwa na hali kama hiyo!

8. Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kukazia fikira mambo ya kiroho?

8 Sala itatusaidia kukazia fikira mambo ya kiroho na kuepuka kushirikiana na waovu. “Msihangaike juu ya kitu chochote” akaandika Paulo, “bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Mtume huyo alitutia moyo tufikirie mambo yaliyo ya kweli, ya hangaiko zito, ya uadilifu, safi kiadili, ya kupendeka, yanayosemwa vema, yenye wema wa adili, na yanayostahili sifa. (Wafilipi 4:6-8) Na tufuate shauri la Paulo nasi tusiwe kama waovu.

9. Ingawa tunajiepusha na mazoea maovu, sisi hujitahidije kuwasaidia watu wa aina zote?

9 Ingawa tunakataa mazoea maovu, sisi hutumia busara kuwahubiria wengine, kama vile mtume Paulo alivyozungumza na Gavana Mroma Feliksi “juu ya uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja.” (Matendo 24:24, 25; Wakolosai 4:6) Tunahubiri habari njema za Ufalme kwa watu wa aina zote, nasi huwatendea kwa fadhili. Tuna hakika kwamba wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ watakuwa waamini, nao watapendezwa na sheria ya Mungu.—Matendo 13:48.

Hupendezwa na Sheria ya Yehova

10. Ni nini kitakachotusaidia kushika kabisa katika akili na moyo mambo tunayojifunza katika funzo letu la kibinafsi?

10 Mtunga-zaburi anaendelea kusema hivi kuhusu mtu mwenye furaha: “Bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zaburi 1:2) Tukiwa watumishi wa Yehova ‘tunapendezwa na sheria yake.’ Ikiwezekana, tunapofanya funzo la kibinafsi na kutafakari, huenda tukasoma “kwa sauti ya chini,” kwa kutamka maneno yasikike. Kufanya hivyo tunaposoma sehemu yoyote ya Maandiko kutatusaidia kushika kabisa mambo hayo katika akili na moyo.

11. Kwa nini tuisome Biblia “mchana na usiku”?

11 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametutia moyo kuisoma Biblia kila siku. (Mathayo 24:45) Kwa sababu tuna tamaa kubwa ya kuufahamu vizuri zaidi ujumbe wa Yehova kwa wanadamu, inafaa tusome Biblia “mchana na usiku”—naam, hata wakati ambapo kwa sababu fulani hatuwezi kulala. Petro alituhimiza hivi: “Kama watoto wachanga waliozaliwa hivi karibuni, kuzeni tamaa kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia hayo mkue kufikia wokovu.” (1 Petro 2:1, 2) Je, wewe hupendezwa kusoma Biblia kila siku na kutafakari Neno la Mungu na makusudi yake usiku? Mtunga-zaburi alifanya hivyo.—Zaburi 63:6.

12. Tutafanya nini ikiwa tunapendezwa na sheria ya Yehova?

12 Furaha yetu ya milele inategemea kupendezwa na sheria ya Mungu. Hiyo ni kamilifu na yenye uadilifu, na tunapata thawabu kubwa kwa kuishika. (Zaburi 19:7-11) Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.” (Yakobo 1:25) Ikiwa tunapendezwa kikweli na sheria ya Yehova, hakuna siku itakayopita bila kujifunza mambo ya kiroho. Naam, tutachochewa ‘kuchunguza ndani ya mambo mazito ya Mungu’ na kutanguliza Ufalme maishani.—1 Wakorintho 2:10-13; Mathayo 6:33.

Anakuwa Kama Mti

13-15. Tunawezaje kuwa kama mti uliopandwa kando ya maji mengi?

13 Akiendelea kueleza kuhusu mtu mnyoofu, mtunga-zaburi anasema: “Hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Sisi tunaomtumikia Yehova hupatwa na magumu maishani kama wanadamu wengine wote wasio wakamilifu. (Ayubu 14:1) Huenda tukapatwa na mateso na majaribu mbalimbali yanayohusiana na imani yetu. (Mathayo 5:10-12) Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu tunaweza kuvumilia majaribu hayo kwa mafanikio, kama vile mti wenye afya unavyostahimili upepo mkali.

14 Mti uliopandwa mahali penye maji haukauki wakati wa kiangazi au wa ukame. Ikiwa tunamwogopa Mungu, nguvu zetu zinatoka kwa Chanzo kinachotegemeka daima—Yehova Mungu. Paulo alimtegemea Mungu amsaidie, naye angeweza kusema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye [Yehova] anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Tunapoongozwa na kutegemezwa kiroho na roho takatifu ya Yehova, hatunyauki na kuacha kuzaa matunda au kufa kiroho. Tunazaa matunda katika utumishi wa Mungu na pia kudhihirisha matunda ya roho yake.—Yeremia 17:7, 8; Wagalatia 5:22, 23.

15 Kwa kutumia neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “kama,” mtunga-zaburi anatumia ufananisho. Anafananisha vitu viwili vilivyo tofauti, ingawa vinafanana kwa njia fulani. Kuna tofauti kati ya wanadamu na miti, lakini yaonekana mti uliositawi sana ambao umepandwa kando ya maji mengi ulimkumbusha mtunga-zaburi ufanisi wa kiroho wa wale ambao ‘mapendezi yao ni katika sheria ya Yehova.’ Tukipendezwa na sheria ya Mungu, siku zetu zinaweza kuwa kama za mti. Kwa kweli, tunaweza kuishi milele.—Yohana 17:3.

16. ‘Kila jambo tunalofanya hufanikiwa’ jinsi gani na kwa nini?

16 Tunapokuwa wanyoofu, Yehova hutusaidia kuvumilia majaribu na magumu. Tunakuwa wenye furaha na wenye kuzaa matunda katika utumishi wa Mungu. (Mathayo 13:23; Luka 8:15) ‘Kila jambo tunalofanya hufanikiwa’ kwa kuwa lengo letu kuu ni kufanya mapenzi ya Yehova. Kwa kuwa sikuzote makusudi yake hufanikiwa nasi hupendezwa na amri zake, sisi husitawi kiroho. (Mwanzo 39:23; Yoshua 1:7, 8; Isaya 55:11) Inakuwa hivyo hata tunapokabili shida.—Zaburi 112:1-3; 3 Yohana 2.

Waovu Huonekana Kuwa Wanasitawi

17, 18. (a) Mtunga-zaburi analinganisha waovu na nini? (b) Hata waovu wakisitawi kimwili, kwa nini hawana usalama wa kudumu?

17 Bila shaka, maisha ya waovu ni tofauti sana na ya waadilifu. Huenda waovu wakaonekana kuwa wanasitawi kimwili kwa muda fulani, lakini hawasitawi kiroho. Tunaona jambo hilo kutokana na maneno ambayo mtunga-zaburi anaendelea kusema: “Waovu hawako hivyo, bali wako kama makapi ambayo upepo hupeperusha. Ndiyo sababu waovu hawatasimama katika hukumu, wala watenda-dhambi katika kusanyiko la waadilifu.” (Zaburi 1:4, 5) Ona kwamba mtunga-zaburi anasema, “waovu hawako hivyo.” Anamaanisha kwamba wao ni tofauti na watu wanaoshika sheria za Mungu, ambao wamelinganishwa na miti inayodumu na inayozaa matunda.

18 Hata waovu wakisitawi kimwili, hawana usalama wa kudumu. (Zaburi 37:16; 73:3, 12) Wanakuwa kama yule tajiri asiyetumia akili ambaye alitajwa na Yesu katika mfano fulani wakati Yesu alipoombwa afanye uamuzi katika jambo lililohusu urithi. Yesu aliwaambia hivi wale waliokuwapo: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” Yesu alifafanua jambo hilo kwa kusema kwamba shamba la mtu fulani tajiri lilizaa vizuri hivi kwamba aliamua kubomoa maghala yake na kujenga yaliyo makubwa zaidi, ili kukusanya vitu vyake vyote vyema. Kisha mtu huyo akaamua kula, kunywa, na kujifurahisha. Lakini Mungu akamwambia: “Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?” Akikazia hoja yake Yesu aliongeza kusema: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—Luka 12:13-21.

19, 20. (a) Eleza jinsi kupura na kupepeta kulivyofanywa zamani. (b) Kwa nini waovu wanalinganishwa na makapi?

19 Waovu si ‘matajiri kwa Mungu.’ Hivyo, hawana usalama wala uimara, nao ni kama makapi, yaani, maganda mepesi ya nafaka. Zamani, nafaka ilipovunwa ilipelekwa kwenye sakafu ya kupuria. Sakafu hiyo ilikuwa eneo tambarare ambalo kwa kawaida lilikuwa juu. Huko vyombo vya kupuria, vilivyokuwa na meno makali ya mawe au ya chuma upande wa chini, vilikokotwa na wanyama juu ya nafaka ili kuvunja-vunja mabua na kutenganisha mbegu na makapi. Kisha, sepetu ya kupepeta ilitumiwa kuuinua na kuurusha mchanganyiko huo juu upepo ulipokuwa ukivuma. (Isaya 30:24) Mbegu zilianguka kwenye sakafu ya kupuria, huku mabua yakianguka kando, nayo makapi yakipeperushiwa mbali na upepo huo. (Ruthu 3:2) Baada ya nafaka kuchujwa ili kuondoa mawe na uchafu mwingine usiohitajiwa, ilikuwa tayari kuhifadhiwa au kusagwa. (Luka 22:31) Lakini makapi yalikuwa yametoweka.

20 Kama vile mbegu za nafaka zilivyoanguka chini na kuhifadhiwa huku makapi yakipeperushiwa mbali, ndivyo waadilifu watakavyobaki wakati waovu watakapoondolewa. Hakika, tunafurahi kwamba hivi karibuni waovu hao watatoweka milele. Baada ya waovu kuondolewa, watu wanaopendezwa na sheria ya Yehova watabarikiwa sana. Naam, mwishowe wanadamu watiifu watapokea zawadi ya Mungu ya uzima wa milele.—Mathayo 25:34-46; Waroma 6:23.

“Njia ya Waadilifu” Iliyobarikiwa

21. Yehova ‘huijuaje njia ya waadilifu?’

21 Zaburi ya kwanza inamalizia kwa maneno haya: “Yehova anaijua njia ya waadilifu, bali njia ya waovu itaangamia.” (Zaburi 1:6) Mungu ‘huijuaje njia ya waadilifu?’ Naam, ikiwa sisi ni wanyoofu, tunaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anatambua jinsi tunavyoshika sheria zake maishani mwetu, naye hutukubali kuwa watumishi wake. Kisha tunaweza na tunapaswa kumtupia mahangaiko yetu yote tukiwa na uhakika kwamba yeye anatujali kikweli.—Ezekieli 34:11; 1 Petro 5:6, 7.

22, 23. Ni nini kitakachowapata waovu na waadilifu?

22 “Njia ya waadilifu” itadumu milele, lakini waovu wasiotaka kamwe kubadilika, wataangamia kwa sababu ya hukumu kali ya Yehova. Nayo “njia” yao, au mwenendo wao utakoma pamoja nao. Tunaweza kuwa na hakika kwamba maneno haya ya Daudi yatatimizwa: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:10, 11, 29.

23 Tutapata furaha iliyoje ikiwa tutapewa pendeleo la kuishi katika dunia paradiso wakati waovu hawatakuwapo tena! Kisha wapole na waadilifu watafurahia amani ya kweli kwa sababu sikuzote watapendezwa na “sheria ya Yehova.” Hata hivyo, kabla ya wakati huo, lazima “agizo la Yehova” litekelezwe. (Zaburi 2:7a) Makala inayofuata itatusaidia kuelewa agizo hilo, na kile litakachomaanisha kwetu na kwa wanadamu wote.

Ungejibuje?

• Kwa nini mtu anayeshika sheria za Mungu ni mwenye furaha?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba tunapendezwa na sheria za Yehova?

• Mtu anawezaje kuwa kama mti unaopata maji ya kutosha?

• Njia ya waadilifu inatofautianaje na ya waovu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Sala itatusaidia kuepuka kushirikiana na waovu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kwa nini mtu mwadilifu analinganishwa na mti?