Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kila Mtu Aliye Mwerevu Atatenda kwa Ujuzi”

“Kila Mtu Aliye Mwerevu Atatenda kwa Ujuzi”

“Kila Mtu Aliye Mwerevu Atatenda kwa Ujuzi”

MWONGOZO wa Neno la Mungu, Biblia, ‘ni wa kutamaniwa kuliko dhahabu, naam, kuliko dhahabu safi sana.’ (Zaburi 19:7-10) Kwa nini? Kwa sababu “Sheria ya mwenye hekima [Yehova] ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya kifo.” (Methali 13:14) Linapotumiwa, shauri la Biblia huboresha maisha yetu na pia hutusaidia kuepuka mitego ambayo huyahatarisha. Hivyo, ni muhimu kama nini kutafuta ujuzi wa Biblia na kutenda kupatana nao!

Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alitoa shauri kwenye Methali 13:15-25, ambalo hutusaidia kutenda kwa ujuzi ili tuweze kufurahia maisha bora na marefu zaidi. * Akitumia methali fupi-fupi, anaonyesha jinsi Neno la Mungu linavyoweza kutusaidia kupata kibali cha wengine, kuendelea kuwa waaminifu katika huduma yetu, kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea nidhamu, na kuchagua marafiki wetu kwa hekima. Pia anazungumzia hekima ya kuwaachia watoto wetu urithi na pia kuwatia nidhamu kwa upendo.

Ufahamu Mzuri Huleta Kibali

“Ufahamu mzuri huleta kibali,” asema Sulemani, “lakini njia ya wale wanaotenda kwa hila ni ngumu.” (Methali 13:15) Neno la awali ambalo limetafsiriwa “ufahamu mzuri,” au uelewaji mzuri, “linafafanua uwezo wa kutumia busara, kufanya maamuzi mazuri, na kuwa na maoni ya hekima,” chasema kitabu kimoja cha marejeo. Si vigumu kwa mtu aliye na sifa hizo kupata kibali cha wengine.

Fikiria jinsi mtume Paulo alivyoshughulika kwa ufahamu na Mkristo mwenzake Filemoni alimpomrudisha Onesimo, mtumwa wa Filemoni aliyekuwa ametoroka, lakini baadaye akawa Mkristo. Paulo alimhimiza Filemoni amkaribishe Onesimo kwa fadhili, kama vile tu ambavyo angemkaribisha mtume mwenyewe. Hata Paulo alijitolea kumlipa Filemoni ikiwa alimdai Onesimo kitu chochote. Naam, Paulo angeweza kutumia mamlaka yake na kumwagiza Filemoni amkaribishe Onesimo kwa fadhili. Lakini mtume huyo aliamua kushughulikia jambo hilo kwa busara na kwa upendo. Kwa kufanya hivyo, Paulo alikuwa na hakika kwamba Filemoni angekubaliana naye, na hata kuchochewa kufanya mengi zaidi ya alivyoombwa kufanya. Tunapaswa kushughulika na waamini wenzetu vivyo hivyo.—Filemoni 8-21.

Kwa upande mwingine, njia ya mwenye hila ni ngumu. Katika maana gani? Kulingana na msomi mmoja, neno linalotumiwa hapa linamaanisha “kitu chenye nguvu au thabiti, likirejelea tabia yenye ukatili ya waovu. . . . Mtu ambaye ameazimia kufuata njia zake mbovu, na kuwa mgumu au kupuuza maagizo yenye hekima ya wengine, ataangamia.”

Sulemani anaendelea: “Kila mtu aliye mwerevu atatenda kwa ujuzi, lakini mjinga ataeneza upumbavu kila mahali.” (Methali 13:16) Mtu huyu mwerevu hana hila. Hapa werevu unahusianishwa na ujuzi, nao hupatikana kwa mtu mwenye hekima, ambaye hufikiri kabla ya kutenda. Anapochambuliwa isivyofaa au hata kutukanwa, mtu mwerevu hudhibiti ulimi wake. Kupitia sala, yeye hujitahidi kuonyesha matunda ya roho takatifu ili asiudhike kupita kiasi. (Wagalatia 5:22, 23) Mtu mwenye hekima hamruhusu yule mtu mwingine au hali imdhibiti, bali hujidhibiti na kuepuka mabishano ambayo mara nyingi hutokea wakati mtu ambaye hukasirika haraka anapoudhiwa.

Mtu mwerevu hutenda kwa ujuzi anapofanya maamuzi. Yeye anajua kwamba ili atende kwa hekima ataepuka kukisia mambo, kutenda kwa kusukumwa na hisia, au kufuata tu umati. Hivyo, yeye huchukua wakati kuchunguza hali yake. Huchunguza mambo yote na kuamua ni yapi anayopaswa kufanya. Kisha huchunguza Biblia na kuamua ni sheria gani au kanuni zipi anazoweza kutumia. Njia ya mtu huyo hudumu ikiwa imenyooka.—Methali 3:5, 6.

“Mjumbe Mwaminifu Huponya”

Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tumepewa daraka la kutangaza ujumbe kutoka kwa Mungu. Maneno ya methali inayofuata hutusaidia kuendelea kuwa waaminifu katika kutimiza kazi hiyo. Inasema: “Mjumbe mwovu ataanguka katika jambo baya, lakini mjumbe mwaminifu huponya.”Methali 13:17.

Andiko hilo linakazia sifa za mjumbe. Namna gani kama kwa ukatili mjumbe ataubadili au kuupotosha ujumbe? Je, hatahukumiwa vikali? Kumbuka Gehazi, mtumishi wa nabii Elisha, ambaye kwa sababu ya pupa alimpelekea ujumbe wa uwongo Naamani, mkuu wa jeshi la Siria. Ukoma ambao Naamani alikuwa ameponywa ulimshika Gehazi. (2 Wafalme 5:20-27) Namna gani kama mjumbe anakosa uaminifu na kuacha kutangaza ujumbe? Biblia inasema ‘Ikiwa kwa kweli wewe hutasema ili kumwonya mwovu aiache njia yake, yeye mwenyewe kwa kuwa ni mwovu atakufa katika kosa lake mwenyewe, lakini damu yake mimi Yehova nitaidai katika mkono wako mwenyewe.’—Ezekieli 33:8.

Kwa upande mwingine, mjumbe mwaminifu atajiponya na kuwaponya wanaomsikiliza. Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Timotheo 4:16) Fikiria jinsi kutangaza kwa uaminifu habari njema ya Ufalme kunavyoponya. Huwachochea watu wenye moyo ufaao, na kuwaongoza kwenye kweli ambayo huwaweka huru. (Yohana 8:32) Hata watu wakikataa kusikiliza ujumbe, mjumbe mshikamanifu ‘hakika ataiokoa nafsi yake.’ (Ezekieli 33:9) Na tusipuuze kamwe kazi yetu ya kuhubiri. (1 Wakorintho 9:16) Acheni sikuzote tuwe waangalifu ‘kuhubiri neno,’ bila kupunguza uzito wake ili livutie watu.—2 Timotheo 4:2.

‘Anayeshika Karipio Hutukuzwa’

Je, mtu mwenye hekima anapaswa kuchukia shauri lenye manufaa analopokea? Methali 13:18 inasema: “Anayepuuza nidhamu hupatwa na umaskini na aibu, lakini anayeshika karipio ndiye anayetukuzwa.” Lingekuwa jambo la hekima kuonyesha uthamini hata kwa karipio ambalo hatukuomba. Shauri zuri linaweza kutusaidia sana wakati ambapo hata hatujui kama tunalihitaji. Kukubali shauri hilo kunaweza kutuepusha na maumivu ya moyoni na kutusaidia kuepuka msiba. Kulipuuza kutatuaibisha.

Pongezi, wakati inapostahili, hutujenga na kututia moyo sana. Lakini tunahitaji pia kutazamia na kukubali karipio. Fikiria barua mbili ambazo mtume Paulo alimwandikia Timotheo. Ingawa anampongeza kwa uaminifu wake, Paulo pia anampa Timotheo mashauri mengi sana katika barua hizo. Paulo anamshauri sana kijana huyo kuhusu kushika imani na dhamiri njema, jinsi ya kushughulika na wengine kutanikoni, kusitawisha ujitoaji-kimungu na ujitoshelevu, kuwafundisha wengine, kukataa uasi-imani, na kutimiza huduma yake. Washiriki wa kutaniko walio wachanga wanapaswa kutafuta na kukubali mashauri kutoka kwa wale walio na uzoefu zaidi.

‘Tembea na Watu Wenye Hekima’

“Tamaa inapotimizwa inafurahisha nafsi,” asema mfalme mwenye hekima, “lakini kuepuka yaliyo mabaya ni chukizo kwa wajinga.” (Methali 13:19) Kuhusu maana ya methali hii, kitabu kimoja cha marejeo kinasema: “Mtu huhisi ameridhika sana anapofikia mradi au anapotimiza tamaa fulani, . . . Kwa kuwa mtu hufurahi sana anapotimiza mradi wake, basi, ni lazima wapumbavu wachukizwe sana kuuacha uovu. Tamaa yao inaweza kutimizwa tu kupitia njia mbovu, na kama wangeacha uovu, wangekosa furaha inayotokana na kutimiza tamaa zao.” Ni muhimu kama nini kusitawisha tamaa zinazofaa!

Watu tunaoshirikiana nao huathiri sana mawazo yetu, mapendezi yetu, na mambo tunayochukizwa nayo! Sulemani anataja ukweli usiobadilika anaposema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Naam, mashirika yetu hata kupitia vitumbuizo, Intaneti, na mambo tunayosoma, huathiri jinsi tulivyo na tutakavyokuwa. Ni muhimu kama nini kuchagua marafiki wetu kwa hekima!

‘Waachie Urithi’

“Watenda-dhambi ndio hufuatwa na msiba,” anasema mfalme wa Israeli, “lakini waadilifu ndio ambao wema huwapa thawabu.” (Methali 13:21) Kufuatia uadilifu huthawabisha, kwa maana Yehova huwatunza waadilifu. (Zaburi 37:25) Hata hivyo, ni lazima tutambue kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11) Je, kuna lolote tunaloweza kufanya ili kujitayarisha kwa matukio ya wakati usiofaa?

Sulemani anasema: “Mtu mwema atawaachia urithi wana wa wanawe.” (Methali 13:22a) Wazazi huwaachia watoto wao urithi wenye thamani kubwa wanapowasaidia kujifunza kumhusu Yehova na kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye! Lakini, je, halingekuwa jambo la busara kufanya mipango inapowezekana, ili kuiacha familia katika hali nzuri kimwili endapo mzazi mmoja atakufa ghafula? Katika maeneo mengi, vichwa vya familia wanaweza kufanya mipango ya kuwa na bima, kuandika wosia halali, na kuweka pesa fulani akiba.

Tunaweza kusema nini kuhusu urithi wa waovu? Sulemani anaendelea kusema: “Mali ya mtenda-dhambi huwekwa akiba kwa ajili ya mwadilifu.” (Methali 13:22b) Mbali na faida zozote tunazoweza kupata sasa, andiko hilo litatimizwa wakati Yehova atakapotimiza ahadi yake ya kuumba “mbingu mpya na dunia mpya” ambapo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Wakati huo waovu watakuwa wameharibiwa, nao “wapole wataimiliki dunia.”—Zaburi 37:11.

Mtu mwenye hekima hutenda kwa ujuzi hata anapokuwa na vitu vichache. Methali 13:23 inasema: “Udongo uliolimwa wa watu maskini hutoa chakula kingi, lakini kuna mtu anayefagiliwa mbali kwa sababu ya ukosefu wa hukumu.” Maskini watapata vingi kutokana na bidii yao na baraka za Mungu. Hata hivyo, kunapokuwa na ukosefu wa haki, uamuzi usiofaa unaweza kufanya upoteze mali nyingi sana.

‘Mwangalie kwa Nidhamu’

Watu wasio wakamilifu huhitaji nidhamu, tangu utotoni na kuendelea. “Anayezuia fimbo yake anamchukia mwana wake,” asema mfalme wa Israeli, “lakini anayempenda ni yule anayemwangalia kwa nidhamu.”Methali 13:24.

Fimbo ni ishara ya mamlaka. Kwenye Methali 13:24, fimbo hiyo inamaanisha mamlaka ya mzazi. Katika muktadha huu, kutumia fimbo ya nidhamu hakumaanishi tu kumchapa mtoto. Bali, humaanisha njia yoyote unayotumia ili kumrekebisha. Wakati mwingine, huenda kemeo linalotolewa kwa fadhili likatosha kurekebisha tabia mbaya. Huenda mtoto mwingine akahitaji karipio kali zaidi. “Kemeo huingia ndani zaidi katika mtu mwenye uelewaji kuliko kumpiga mjinga mara mia moja,” yasema Methali 17:10.

Sikuzote mzazi anapaswa kutoa nidhamu kwa upendo na hekima ili watoto wanufaike. Mzazi mwenye upendo hapuuzi makosa ya mtoto wake. Badala yake, yeye huyatafuta ili yaweze kurekebishwa kabla hayajakolea sana. Bila shaka, mzazi mwenye upendo hutii himizo hili la Paulo: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Namna gani ikiwa mzazi anamwendekeza mtoto na kushindwa kumrekebisha inavyohitajiwa? Je, baadaye mzazi kama huyo atapata shukrani kwa kumwendekeza mtoto? La! (Methali 29:21) Biblia inasema: “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” (Methali 29:15) Kutotumia mamlaka yako ukiwa mzazi huonyesha kwamba hujali au huna upendo. Hata hivyo, kutumia mamlaka kwa fadhili na kwa uthabiti, huonyesha kwamba unampenda na unamjali mtoto.

Mtu mwenye hekima na mnyoofu ambaye hutenda kwa ujuzi wa kweli atabarikiwa. Sulemani anatuhakikishia: “Mwadilifu anakula mpaka nafsi yake inaposhiba, lakini tumbo la waovu litakuwa tupu.” (Methali 13:25) Yehova anajua kinachotufaa katika kila sehemu ya maisha yetu—iwe ni mambo yanayohusu familia, uhusiano wetu na wengine, huduma yetu, au tunapotiwa nidhamu. Bila shaka, tukifuata kwa hekima shauri la Neno lake, maisha yetu yatakuwa bora.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ili kupata habari zaidi kuhusu Methali 13:1-14, ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2003, ukurasa wa 21-25.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Anapochambuliwa isivyofaa, mtu mwerevu hudhibiti ulimi wake

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mtangazaji wa Ufalme mwaminifu hutimiza mambo mengi mazuri

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ingawa pongezi hututia moyo, tunapaswa kukubali rekebisho pia

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mzazi mwenye upendo hapuuzi makosa ya mtoto wake