Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miujiza ya Yesu—Je, Kweli Ilitukia?

Miujiza ya Yesu—Je, Kweli Ilitukia?

Miujiza ya Yesu—Je, Kweli Ilitukia?

“WATU walimletea [Yesu Kristo] watu wengi walioingiwa na roho waovu; naye akawafukuza hao roho kwa neno moja, naye akawaponya wote waliokuwa na hali mbaya.” (Mathayo 8:16) Yesu ‘aliamka, akaukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza, utulie!” Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.’ (Marko 4:39) Unayaonaje maneno hayo? Je, unaamini kwamba yanaeleza matukio halisi ya kihistoria, au unayaona kuwa ni hekaya au ni hadithi tu?

Watu wengi leo wana shaka sana kuhusu ukweli wa miujiza ya Yesu. Inaonekana kwamba habari kuhusu miujiza na maajabu mengine ya kimungu hupuuzwa katika enzi hii ambapo watu wanatumia darubini, hadubini, wanachunguza anga, na kubadili maumbile.

Wengine huyaona masimulizi kuhusu miujiza kuwa mambo ya kubuniwa au hekaya tu. Kitabu kimoja kinachodai kuchunguza yule Yesu wa “kweli” kinasema kwamba hadithi kuhusu miujiza ya Kristo ni “matangazo tu” ya kuueneza Ukristo.

Wengine huona miujiza ya Yesu kuwa udanganyifu mtupu. Wakati mwingine, Yesu mwenyewe ndiye hushutumiwa kuwa mdanganyifu. Justin Martyr wa karne ya pili W.K. anasema kwamba wale waliomchambua Yesu “hata walimwita mchawi na mdanganya-watu.” Wengine hudai kwamba Yesu “hakufanya miujiza yake akiwa nabii wa Wayahudi, bali akiwa mchawi aliyezoezwa katika mahekalu ya wapagani.”

Ni Nini Maana ya Neno “–siowezekana”?

Huenda ukahisi kwamba kuna sababu kuu inayofanya watu wawe na shaka na kutoamini miujiza. Wao huliona kuwa jambo gumu, hata lisilowezekana, kukubali kwamba miujiza hufanyika kwa nguvu zinazozidi zile za kibinadamu. “Miujiza haitokei kwa vyovyote,” akasema kijana mmoja mwagnostiki (mtu aaminiye kwamba ya Mungu hayawezi kujulikana). Kisha akanukuu maneno ya David Hume, mwanafalsafa Mskoti wa karne ya 18, aliyeandika: “Muujiza huvunja sheria za asili.”

Hata hivyo, wengi wangekuwa waangalifu sana kusema kwamba jambo fulani lisilo la kawaida haliwezi kutokea. Kichapo The World Book Encyclopedia husema kwamba muujiza ni “tukio lisiloweza kuelezeka kupitia sheria za asili zinazojulikana.” Kulingana na maelezo hayo, miaka mia moja iliyopita wengi wangeziona safari za angani, mawasiliano ya redio, na mitambo ya setilaiti inayoongoza vyombo vya kusafiria kuwa “miujiza.” Kwa kweli, si jambo la hekima kudai kwamba miujiza haiwezekani eti kwa sababu hatuwezi kuieleza kwa kutegemea ujuzi tulio nao sasa.

Tukichunguza uthibitisho fulani wa Biblia kuhusu miujiza ambayo Yesu Kristo alifanya, tutapata nini? Je, miujiza ya Yesu ilitukia kwa kweli?