Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusitawisha Maoni ya Kristo Kuhusu Umashuhuri

Kusitawisha Maoni ya Kristo Kuhusu Umashuhuri

Kusitawisha Maoni ya Kristo Kuhusu Umashuhuri

“Yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu.”—MATHAYO 20:26.

1. Ulimwengu una maoni gani kuhusu umashuhuri?

KARIBU na jiji la kale la Misri la Thebes (Karnak ya sasa), yapata kilometa 500 kusini ya Cairo, kuna sanamu ya Farao Amenhotep wa Tatu yenye urefu wa meta 18. Mtu hujiona kuwa mdogo mno anapojilinganisha na sanamu hiyo kubwa sana. Sanamu hiyo ambayo bila shaka ilikusudiwa kuwafanya watu wamwogope mtawala huyo, huonyesha maoni ya ulimwengu kuhusu umashuhuri, yaani, kujifanya kuwa maarufu sana na kuwafanya wengine wahisi kuwa si kitu.

2. Yesu aliwawekea wafuasi wake kielelezo gani, na tunahitaji kujiuliza maswali gani?

2 Linganisha maoni hayo na maoni ambayo Yesu Kristo alifunza. Ingawa alikuwa “Bwana na Mwalimu” wa wafuasi wake, Yesu aliwafundisha kwamba umashuhuri hutokana na kuwatumikia wengine. Siku ya mwisho ya maisha yake duniani, Yesu alionyesha maana ya mambo aliyofundisha kwa kuwaosha wanafunzi wake miguu. Bila shaka, hilo lilikuwa tendo la unyenyekevu. (Yohana 13:4, 5, 14) Kutumikia au kutumikiwa, ni lipi linalokuvutia zaidi? Je, kielelezo cha Kristo huamsha tamaa ndani yako ya kuwa mnyenyekevu kama alivyokuwa? Basi na tuchunguze maoni ya Kristo kuhusu umashuhuri na kuyatofautisha na maoni yaliyo ya kawaida katika ulimwengu.

Epuka Maoni ya Ulimwengu Kuhusu Umashuhuri

3. Ni vielelezo gani vya Biblia vinavyoonyesha matokeo yenye kuhuzunisha ya wale wanaotamani utukufu wa wanadamu?

3 Kuna vielelezo vingi katika Biblia vinavyoonyesha kwamba maoni ya ulimwengu kuhusu umashuhuri huleta hasara. Fikiria Hamani mwenye uwezo ambaye alikuwa mashuhuri katika nyumba ya mfalme wa Uajemi katika siku za Esta na Mordekai. Tamaa ya Hamani ya kupata utukufu ilimletea aibu na kifo. (Esta 3:5; 6:10-12; 7:9, 10) Namna gani Nebukadneza, aliyepatwa na wazimu wakati utawala wake ulipokuwa umefikia kilele? Maoni yake yaliyopotoka kuhusu umashuhuri yalionyeshwa na maneno haya: “Je, hili si Babiloni Mkubwa, ambalo mimi mwenyewe nimelijenga kwa ajili ya nyumba ya kifalme kwa nguvu za uwezo wangu na kwa ajili ya heshima ya utukufu wa enzi yangu?” (Danieli 4:30) Kisha kulikuwa na Herode Agripa wa Kwanza mwenye kiburi, ambaye alikubali utukufu asiostahili badala ya kumpa Mungu utukufu. ‘Aliliwa na wadudu akakata pumzi.’ (Matendo 12:21-23) Kukosa kufahamu maoni ya Yehova kuhusu umashuhuri kulifanya watu hao wote waanguke kutoka mamlakani kwa njia yenye kuaibisha.

4. Ni nani anayechochea roho ya ulimwengu ya kiburi?

4 Inafaa tuwe na tamaa ya kutumia maisha yetu kwa njia itakayotuletea sifa na heshima. Hata hivyo, Ibilisi hutumia tamaa hiyo kwa kuchochea roho ya kiburi, ambayo huonyesha tamaa yake mwenyewe ya kutaka makuu. (Mathayo 4:8, 9) Usisahau kamwe kwamba yeye ndiye “mungu wa mfumo huu wa mambo,” na ameazimia kuendeleza fikira zake hapa duniani. (2 Wakorintho 4:4; Waefeso 2:2; Ufunuo 12:9) Kwa kuwa wanajua chanzo cha fikira hizo, Wakristo huepuka maoni ya ulimwengu kuhusu umashuhuri.

5. Je, mafanikio, umashuhuri, na mali huhakikisha kwamba mtu atakuwa na uradhi wa kudumu? Eleza.

5 Wazo moja linaloendelezwa na Ibilisi ni kwamba kuwa mashuhuri katika ulimwengu, kusifiwa na watu, na kuwa na pesa nyingi hufanya maisha yawe yenye furaha. Je, hiyo ni kweli? Je, mafanikio, umashuhuri, na mali hufanya maisha yawe yenye uradhi? Biblia hutuonya tusidanganywe na kufikiri kwa namna hiyo. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Nimeona kazi yote ngumu na ustadi wote katika kazi, ya kwamba maana yake ni mashindano kati ya mtu na mwenzake; hilo pia ni ubatili na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:4) Watu wengi ambao wamejitoa ili kupata mali katika ulimwengu wanaweza kuthibitisha kwamba shauri hilo la Biblia lililoongozwa na roho ya Mungu ni la kweli. Mfano mmoja ni mtu fulani aliyesaidia kubuni, kujenga, na kufanyia majaribio chombo cha angani kilichopeleka mwanadamu kwenye mwezi. Alisema hivi: “Nilifanya kazi kwa bidii na kuwa stadi sana katika yale niliyofanya. Hata hivyo, mambo hayo yalikuwa ubatili na hayakunipa furaha na amani ya akili ya kudumu.” * Maoni ya ulimwengu kuhusu umashuhuri, iwe ni katika biashara, michezo, au vitumbuizo, hayatoi uhakikisho kwamba mtu atakuwa na uradhi wa kudumu.

Umashuhuri Hutokana na Utumishi Unaochochewa na Upendo

6. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yakobo na Yohana walikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu umashuhuri?

6 Tukio fulani katika maisha ya Yesu linaonyesha umashuhuri halisi ni nini. Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakisafiri hadi Yerusalemu kusherehekea sikukuu ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. Wakiwa njiani kuelekea Yerusalemu, binamu wawili wa Yesu, Yakobo na Yohana, walionyesha maoni yasiyofaa kuhusu umashuhuri. Kupitia mama yao, walitoa ombi hili kwa Yesu: ‘Toa agizo ili tuketi upande wako wa kuume na upande wako wa kushoto, katika ufalme wako.’ (Mathayo 20:21) Wayahudi waliona kuketi kwenye mkono wa kulia au wa kushoto kuwa pendeleo kubwa. (1 Wafalme 2:19) Kwa kujitakia makuu, Yakobo na Yohana walijaribu kutwaa vyeo mashuhuri. Walitaka kudai vyeo hivyo vya mamlaka. Yesu alijua walichokuwa wakifikiria naye akatumia nafasi hiyo ili kusahihisha maoni yao yasiyofaa kuhusu umashuhuri.

7. Yesu alielezaje jinsi ya kupata umashuhuri wa kweli wa Kikristo?

7 Yesu alijua kwamba katika ulimwengu huu wenye kiburi, mtu anayeonwa kuwa mashuhuri ni yule ambaye husimamia na kuwaamuru wengine na ambaye akitaka jambo fulani lifanywe, linafanywa mara moja. Lakini kati ya wanafunzi wa Yesu, utumishi wa hali ya chini ndio kiwango cha kukadiria umashuhuri. Yesu alisema: “Yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wenu.”—Mathayo 20:26, 27.

8. Inamaanisha nini kuwa mhudumu, na ni maswali gani tunayoweza kujiuliza?

8 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mhudumu” katika Biblia hurejelea mtu ambaye hujitahidi kuwatumikia wengine bila kuacha. Yesu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake jambo muhimu: Kuwaamuru watu wafanye mambo hakumfanyi mtu awe mashuhuri bali ni kuwatumikia wengine kwa kuchochewa na upendo. Jiulize hivi: ‘Ningehisije kama ningekuwa Yakobo au Yohana? Je, ningeelewa kwamba umashuhuri wa kweli hutokana na kutumikia kwa kuchochewa na upendo?’—1 Wakorintho 13:3.

9. Yesu aliweka kielelezo gani katika kushughulika na wengine?

9 Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake kwamba kiwango cha ulimwengu kuhusu umashuhuri ni tofauti na kiwango cha umashuhuri cha Kristo. Hakujiona kamwe kuwa bora kuliko wale ambao aliwatumikia au kuwafanya wahisi kuwa duni. Watu wa kila aina—wanaume, wanawake, na watoto, matajiri, maskini, na wenye mamlaka, na vilevile watu waliojulikana kuwa watenda-dhambi—walijihisi huru kuwa pamoja naye. (Marko 10:13-16; Luka 7:37-50) Mara nyingi watu hukosa subira wanaposhughulika na wale ambao wamepungukiwa. Yesu alikuwa tofauti. Hata ingawa nyakati nyingine wanafunzi wake walitenda bila kufikiri na waligombana, aliwafundisha kwa subira huku akiwaonyesha kwamba kwa kweli alikuwa mnyenyekevu na mwenye tabia-pole.—Zekaria 9:9; Mathayo 11:29; Luka 22:24-27.

10. Yesu alionyeshaje katika maisha yake yote kwamba aliwatumikia wengine bila ubinafsi?

10 Kielelezo kisicho na ubinafsi ambacho kiliwekwa na Mwana huyu mkuu wa Mungu kilionyesha umashuhuri wa kweli humaanisha nini hasa. Yesu hakuja duniani kutumikiwa bali kuwatumikia wengine, akiwaponya “magonjwa ya namna mbalimbali” na kuwaweka watu huru kutokana na udhibiti wa roho waovu. Ingawa alichoka na alihitaji wakati wa kupumzika, sikuzote alitanguliza mahitaji ya wengine, akijitahidi kuwafariji. (Marko 1:32-34; 6:30-34; Yohana 11:11, 17, 33) Upendo wake ulimchochea kuwasaidia watu kiroho, akisafiri mamia ya kilometa katika barabara zenye vumbi ili kuhubiri habari njema za Ufalme. (Marko 1:38, 39) Bila shaka, Yesu aliona kuwatumikia wengine kuwa jambo muhimu sana.

Iga Unyenyekevu wa Kristo

11. Ni sifa gani ambazo hutakiwa kwa akina ndugu waliowekwa rasmi kutumikia wakiwa waangalizi katika kutaniko?

11 Mwishoni mwa miaka ya 1800 mtazamo unaofaa ambao waangalizi Wakristo walipaswa kusitawisha ulikaziwa wakati wanaume walipokuwa wakichaguliwa wawe wawakilishi wasafirio ili kuwahudumia watu wa Mungu wenye uhitaji. Kulingana na gazeti Zion’s Watch Tower la Septemba 1, 1894, kulihitajiwa wanaume “wapole—ili wasijivune . . . , wenye unyenyekevu wa akili, wasiojitukuza wenyewe bali Kristo—wasiotangaza ujuzi wao, bali Neno lake kwa njia rahisi na yenye nguvu.” Ni wazi kwamba, Wakristo wa kweli hawapaswi kamwe kutafuta madaraka ili kutosheleza tamaa yao ya makuu au kupata umashuhuri, mamlaka, na kuwadhibiti wengine. Mwangalizi mnyenyekevu hukumbuka kwamba madaraka yake yanatia ndani “kazi njema” wala si cheo cha juu cha kujitukuza. (1 Timotheo 3:1, 2) Wazee na watumishi wa huduma wote wanapaswa kujitahidi kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu na kuongoza katika utumishi mtakatifu, hivyo wakiweka kielelezo kinachofaa kuigwa na wengine.—1 Wakorintho 9:19; Wagalatia 5:13; 2 Timotheo 4:5.

12. Wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko wanapaswa kujiuliza maswali gani?

12 Ndugu yeyote anayejitahidi kufikia mapendeleo anaweza kujiuliza hivi: ‘Je, mimi hutafuta nafasi za kuwatumikia wengine, au nina mwelekeo wa kutaka kutumikiwa? Je, niko tayari kufanya kazi za kuwasaidia watu ambazo hazionwi na wengine kwa urahisi?’ Kwa mfano, huenda mwanamume kijana akawa anapenda kutoa hotuba katika kutaniko la Kikristo lakini hapendi kuwasaidia walio wazee. Huenda akapenda kujipendekeza kwa ndugu wenye madaraka kutanikoni lakini asitake kuhubiri. Kijana kama huyo anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, mimi hukazia fikira utumishi wa Mungu ambao hasa utafanya watu wanitambue na kunisifu? Je, ninajitahidi kuonekana kuwa bora mbele ya wengine?’ Bila shaka, tukijitafutia utukufu, hatutakuwa tukiiga kielelezo cha Kristo.—Yohana 5:41.

13. (a) Kielelezo cha unyenyekevu cha mwangalizi kinawezaje kuwa na uvutano mzuri kwa wengine? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mkristo anapaswa kuepuka kuonyesha unyenyekevu, au kuwa na unyenyekevu wa akili?

13 Tunapojitahidi kuiga unyenyekevu wa Kristo, tunachochewa kuwatumikia wengine. Fikiria mfano wa mwangalizi fulani wa eneo la dunia ambaye alikuwa akikagua kazi inayofanywa katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Licha ya kuwa na shughuli nyingi na madaraka mazito, mwangalizi huyo alichukua wakati ili kumsaidia ndugu mmoja kijana aliyekuwa aking’ang’ana kuweka sawa vipimo vya mashini ya kuunganishia vitabu. “Nilishangaa sana!” ndugu huyo akasema. “Aliniambia kwamba alitumia mashini kama hiyo alipokuwa kijana huko Betheli, na alikumbuka jinsi ilivyokuwa vigumu kuweka vipimo hivyo kwa usahihi kabisa. Alinisaidia kuweka sawa vipimo vya mashini hiyo kwa muda hata ingawa alikuwa na mambo mengine mengi ya kufanya, tena muhimu. Nilivutiwa sana na jambo hilo.” Ndugu huyo, ambaye sasa ni mwangalizi kwenye ofisi fulani ya tawi ya Mashahidi wa Yehova angali anakumbuka tendo hilo la unyenyekevu. Tusijione kamwe kuwa bora sana hivi kwamba hatuwezi kufanya kazi za hali ya chini au kujiona kuwa wa maana sana kutoweza kufanya kazi hizo. Badala yake, tunapaswa kujivika “unyenyekevu wa akili.” Tunapaswa kuonyesha unyenyekevu kwa kuwa kufanya hivyo ni sehemu ya “utu mpya” ambao lazima Mkristo ajivike.—Wafilipi 2:3; Wakolosai 3:10, 12; Waroma 12:16.

Jinsi ya Kusitawisha Maoni ya Kristo Kuhusu Umashuhuri

14. Kutafakari juu ya uhusiano wetu pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu kunawezaje kutusaidia tusitawishe maoni yanayofaa kuhusu umashuhuri?

14 Tunawezaje kusitawisha maoni yanayofaa kuhusu umashuhuri? Njia moja ni kwa kutafakari juu ya uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Utukufu, nguvu, na hekima yake hufanya awe juu zaidi ya wanadamu duni. (Isaya 40:22) Kutafakari juu ya uhusiano wetu pamoja na wanadamu wenzetu hutusaidia pia kusitawisha unyenyekevu wa akili. Kwa mfano, huenda tukawa bora kuliko wengine katika mambo fulani, lakini huenda wao wakawa bora katika sehemu za maisha ambazo ni muhimu zaidi. Au huenda ndugu zetu Wakristo wakawa na sifa fulani ambazo sisi hatuna. Ni kweli kwamba, kwa sababu ya kujiendesha kwa upole na kwa unyenyekevu, wengi ambao ni wenye thamani machoni pa Mungu hawaelekei kuwa na umashuhuri.—Methali 3:34; Yakobo 4:6.

15. Utimilifu wa watu wa Mungu unaonyeshaje kwamba hakuna aliye na sababu ya kujiona kuwa bora kuliko wengine?

15 Mambo yaliyowapata Mashahidi wa Yehova chini ya majaribu kwa sababu ya imani yao, yanaonyesha ukweli wa jambo hilo. Mara nyingi, wale ambao huonwa na ulimwengu kuwa watu wa kawaida ndio hudumisha utimilifu wao kwa Mungu chini ya majaribu makali. Kutafakari juu ya mifano hiyo kunaweza kutusaidia tuwe wanyenyekevu na kutufundisha ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’—Waroma 12:3. *

16. Wote kutanikoni wanawezaje kusitawisha umashuhuri kwa kuiga kielelezo kilichowekwa na Yesu?

16 Wakristo wote, vijana kwa wazee, wanapaswa kujitahidi kusitawisha maoni ya Kristo kuhusu umashuhuri. Katika kutaniko kuna kazi mbalimbali zinazopaswa kufanywa. Usikasirike kamwe unapoombwa ufanye kazi ambazo huenda zikaonekana kuwa za hali ya chini. (1 Samweli 25:41; 2 Wafalme 3:11) Wazazi, je, mnawatia moyo watoto na matineja wenu wafanye kwa furaha kazi yoyote wanayopewa, iwe ni kwenye Jumba la Ufalme, kusanyikoni, au mahali pa kusanyiko? Je, wao huona mkifanya kazi za hali ya chini? Ndugu mmoja, ambaye sasa anatumika katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, anakumbuka waziwazi kielelezo cha wazazi wake. Alisema: “Namna walivyofanya kazi ya kusafisha Jumba la Ufalme au mahali pa kusanyiko ilinionyesha kwamba waliona kazi hiyo kuwa muhimu. Mara nyingi walifanya kazi za kunufaisha kutaniko au akina ndugu, hata iwe kazi hizo zilionekana kuwa za hali ya chini kadiri gani. Mtazamo huo umenisaidia kukubali kwa furaha kazi yoyote hapa Betheli.”

17. Wanawake wanyenyekevu wanawezaje kuwa baraka kwa kutaniko?

17 Esta, aliyekuwa malkia wa Milki ya Uajemi katika karne ya tano K.W.K., anatuwekea kielelezo bora cha kutanguliza masilahi ya wengine. Ingawa aliishi katika jumba la mfalme, alikuwa tayari kuhatarisha maisha yake kwa ajili ya watu wa Mungu, akitenda kupatana na mapenzi Yake. (Esta 1:5, 6; 4:14-16) Bila kujali hali yao ya kiuchumi, leo wanawake Wakristo wanaweza kuonyesha mtazamo kama wa Esta kwa kuwatia moyo walioshuka moyo, kuwatembelea wagonjwa, kuhubiri, na kushirikiana na wazee. Dada hao wanyenyekevu ni baraka iliyoje kwa kutaniko!

Baraka za Umashuhuri wa Kristo

18. Ni manufaa gani hutokana na kuonyesha umashuhuri wa Kristo?

18 Unapata manufaa nyingi unapodumisha umashuhuri wa Kristo. Kuwatumikia wengine bila ubinafsi hukuletea wewe shangwe na pia wengine. (Matendo 20:35) Unapojitahidi kuwatumikia ndugu zako kwa furaha, na kwa hiari watakupenda zaidi. (Matendo 20:37) Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba Yehova huona yale unayofanya ili kuendeleza masilahi ya Wakristo wenzako kuwa dhabihu ya sifa inayompendeza.—Wafilipi 2:17.

19. Tunapaswa kuazimia nini kuhusu kuwa na maoni ya Kristo kuelekea umashuhuri?

19 Kila mmoja wetu anahitaji kuchunguza moyo wake na kujiuliza: ‘Je, nitazungumza tu juu ya kusitawisha maoni ya Kristo kuhusu umashuhuri, au nitajitahidi kusitawisha sifa hiyo?’ Maoni ya Yehova ni wazi kuhusu wenye kiburi. (Methali 16:5; 1 Petro 5:5) Matendo yetu na yaonyeshe kwamba tunapendezwa kudhihirisha maoni ya Kristo kuhusu umashuhuri, iwe ni katika kutaniko la Kikristo, katika familia, au tunaposhughulika na wanadamu wenzetu kila siku—tukifanya mambo yote kwa utukufu na sifa ya Mungu.—1 Wakorintho 10:31.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1982, ukurasa wa 3-6, “In Search of Success” (Kutafuta Mafanikio) la Kiingereza.

^ fu. 15 Ona mifano kwenye Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1994, ukurasa wa 181-182, na Mnara wa Mlinzi, Septemba 1, 1993, ukurasa wa 27-31.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini tuepuke maoni ya ulimwengu kuhusu umashuhuri?

• Yesu alikadiriaje umashuhuri?

• Waangalizi wanawezaje kuiga unyenyekevu wa Kristo?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia tusitawishe umashuhuri wa Kristo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Ni Nani Aliye na Umashuhuri wa Kristo?

Mtu anayetaka kutumikiwa au anayetaka kuwatumikia wengine?

Mtu anayependa kuonekana na watu au anayekubali kazi za hali ya chini?

Mtu anayejitukuza au anayewatukuza wengine?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Sanamu kubwa sana ya Farao Amenhotep wa Tatu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, unajua ni nini kilichofanya Hamani aanguke?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, wewe hutafuta nafasi za kuwatumikia wengine?