Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Serikali Nzuri

Kutafuta Serikali Nzuri

Kutafuta Serikali Nzuri

“Kwa sababu mataifa yanazidi kutegemeana, kumetokea matatizo mengi ulimwenguni ambayo hayawezi tena kutatuliwa na taifa moja-moja pasipo msaada wa mataifa mengine. Ushirikiano wa ulimwenguni pote ndio tu unaoweza kutusaidia kukabiliana na hatari na magumu yanayozidi kuwakumba wanadamu.”—Ghulam Umar, mchanganuzi wa masuala ya kisiasa wa Pakistan.

LEO katika ulimwengu kuna hali nyingi zenye kupingana. Wengi wanapata riziki kwa shida sana ijapokuwa wanazungukwa na utajiri mwingi. Kizazi hiki chenye ujuzi wa kompyuta ndicho kimeelimika zaidi na chenye ujuzi mwingi zaidi katika historia ya wanadamu. Hata hivyo, inazidi kuwa vigumu kwa watu wengi kupata kazi yenye kudumu. Ingawa inaonekana kwamba wanadamu wana uhuru mwingi zaidi kuliko zamani, mamilioni wanaishi katika woga na ukosefu wa usalama. Huenda tukawa tumezungukwa na nafasi za kazi zenye kuvutia, lakini ufisadi na uvunjaji wa sheria katika ngazi zote za jamii hufanya wengi wakose tumaini.

Wanadamu wanakabili matatizo mengi sana hivi kwamba hakuna taifa hata moja au kikundi cha mataifa kinachoweza kuyatatua. Kwa hiyo, wachunguzi wengi wamekata kauli kwamba ili kuwe na amani na usalama ulimwenguni, mataifa yote yanapaswa kuungana chini ya serikali moja. Kwa mfano, Albert Einstein aliunga mkono maoni kama hayo zamani. Mnamo mwaka wa 1946 alisema hivi: “Ninaamini kabisa kwamba watu wengi ulimwenguni wangependa kuishi kwa amani na usalama . . . Tamaa ya wanadamu ya kupata amani inaweza kutoshelezwa tu kwa kuundwa kwa serikali ya ulimwenguni pote.”

Baada ya miaka zaidi ya 50, uhitaji huo muhimu bado haujatimizwa. Akitaja matatizo ya karne ya 21, mfafanuzi mmoja alitoa maoni haya katika gazeti Le Monde la Paris, Ufaransa: “Ni muhimu kubuni mfumo wa sheria, usimamizi, na katiba ya serikali ya kimataifa ambayo inaweza kuingilia kati mara moja visa vya mauaji ya jamii katika sehemu zote ulimwenguni. Pia ni muhimu kukubali wazo la kwamba kuanzia sasa na kuendelea, Dunia ni nchi moja.” Ni nani au ni nini kilicho na nguvu na uwezo wa kufanya hivyo ili kuhakikisha kwamba wanadamu wana wakati ujao wenye amani?

Je, Umoja wa Mataifa Ndio Suluhisho?

Wengi wanatumaini kwamba shirika la Umoja wa Mataifa ndilo litakaloleta amani ulimwenguni. Je, UM ndiyo serikali inayoweza kuleta amani na usalama wa kweli ulimwenguni? Bila shaka, kuna madai mengi sana ya kisiasa yanayoonekana kuwa yenye kusisimua na kutumainika. Kwa mfano, katika “Tangazo la Milenia” la mwaka wa 2000, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitoa azimio hili muhimu: “Tutafanya yote tuwezayo kuwaweka watu wetu huru kutokana na balaa ya vita, iwe ni vita vya wenyewe kwa wenyewe au kati ya nchi, balaa ambayo imesababisha vifo vya watu zaidi ya milioni 5 katika miaka kumi iliyopita.” Matangazo kama hayo yameleta sifa kwa shirika la UM kutoka kwa watu na sekta nyingi, na vilevile limepata Tuzo la Amani la Nobeli la 2001. Hivyo, kwa kulipa tuzo shirika la UM, Halmashauri ya Nobeli ya Norway ilisema kwamba “shirika la Umoja wa Mataifa ndilo tu linaloweza kufanikiwa kuleta amani na ushirikiano ulimwenguni pote.”

Licha ya hayo yote, je, shirika la Umoja wa Mataifa lililoanzishwa mwaka wa 1945, limekuwa serikali ambayo inaweza kuleta amani ya kweli na ya kudumu ulimwenguni? La, kwa kuwa jitihada zake nyingi zimekosa kufaulu kwa sababu ya kujipenda na kujitukuza kwa nchi wanachama. Kwa ujumla, maoni ya watu yanapatana na maneno ya mhariri wa gazeti fulani aliyesema kwamba kwa kiwango fulani UM “huwakilisha maoni ya watu ulimwenguni” na kwamba “ajenda yake imejaa masuala ambayo yamejadiliwa kwa miaka mingi bila mafanikio.” Swali linabaki: Je, kweli siku moja mataifa ya ulimwengu yataungana?

Biblia inaonyesha kwamba hivi karibuni umoja huo utapatikana. Utapatikanaje? Na ni serikali gani itakayoleta umoja huo? Ili kupata majibu, tafadhali soma makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Einstein aliunga mkono umuhimu wa kuwepo kwa serikali ya ulimwenguni pote

[Hisani]

Einstein: U.S. National Archives photo