Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hesabu

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hesabu

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hesabu

WAKATI Waisraeli walipotoka Misri, walipangwa kuwa taifa. Muda mfupi baadaye, wangeweza kuwa wameingia katika Nchi ya Ahadi, lakini hawakuingia. Badala yake, walitanga-tanga karibu miaka 40 hivi katika “nyika kubwa na yenye kuogopesha.” (Kumbukumbu la Torati 8:15) Kwa nini? Kitabu cha Biblia cha Hesabu kinasimulia yale yaliyotukia. Masimulizi hayo yanapaswa kutuchochea tuone umuhimu wa kumtii Yehova Mungu na kuwaheshimu wawakilishi wake.

Kitabu cha Hesabu kilichoandikwa na Musa katika nyika na kwenye Nchi Tambarare za Moabu, kinazungumzia kipindi cha miaka 38 na miezi 9 kutoka mwaka wa 1512 K.W.K. hadi mwaka wa 1473 K.W.K. (Hesabu 1:1; Kumbukumbu la Torati 1:3) Jina la kitabu hicho linatokana na kule kuhesabiwa kwa Waisraeli mara mbili. Baada ya kuhesabiwa mara ya kwanza, walihesabiwa mara ya pili miaka 38 hivi baadaye. (Sura ya 1-4, 26) Masimulizi hayo yamegawanywa katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza inasimulia mambo yaliyotukia kwenye Mlima Sinai. Nayo sehemu ya pili inazungumzia yale yaliyotukia wakati Waisraeli walipokuwa wakitanga-tanga nyikani. Nayo sehemu ya mwisho inazungumzia mambo yaliyotukia katika Nchi Tambarare za Moabu. Unaposoma masimulizi haya, huenda ukajiuliza, ‘Matukio haya yananifunza nini? Je, kitabu hiki, kina kanuni zinazoweza kunifaidi leo?’

KWENYE MLIMA SINAI

(Hesabu 1:1–10:10)

Waisraeli wanahesabiwa kwa mara ya kwanza wanapokuwa bado wamepiga kambi chini ya Mlima Sinai. Jumla ya wanaume wenye umri wa miaka 20 na zaidi, bila kuhesabu Walawi, ni 603,550. Yaonekana Waisraeli walihesabiwa kwa sababu za kijeshi. Huenda watu wote waliokuwa kambini, kutia ndani wanawake, watoto, na Walawi, walikuwa zaidi ya milioni tatu.

Baada ya watu kuhesabiwa, Waisraeli wanapokea maagizo kuhusu mpangilio wa kutembea, maelezo kuhusu kazi za Walawi na utumishi wa maskani, amri kuhusu kuwatenga watu waliokuwa na magonjwa, na sheria kuhusiana na visa vya wivu na nadhiri zilizowekwa na Wanadhiri. Sura ya 7 ina habari kuhusu dhabihu zilizotolewa na wakuu wa makabila wakati wa kuzinduliwa kwa madhabahu, nayo sura ya 9 inazungumzia sherehe ya Pasaka. Pia, kusanyiko linapewa maagizo kuhusu jinsi ya kupiga kambi na kuivunja.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:1, 2—Ni nini zilizokuwa “alama” ambazo kando yake migawanyo ya makabila matatu ilipiga kambi nyikani? Biblia haitoi maelezo kuhusu alama hizo. Hata hivyo, hazikuonwa kuwa alama takatifu au kupewa umuhimu wa kidini. Alama hizo zilitumiwa kwa kusudi lifaalo—kumsaidia mtu atambue hasa mahali pake kambini.

5:27—‘Kuanguka kwa paja’ la mwanamke aliyekuwa na hatia ya uzinzi kulimaanisha nini? Neno “paja” linatumiwa hapa kuonyesha viungo vya uzazi. (Mwanzo 46:26) ‘Kuanguka’ kwa paja humaanisha kuharibika kwa viungo hivyo, hivi kwamba haingewezekana kuzaa tena.

Mambo Tunayojifunza:

6:1-7. Wanadhiri walipaswa kujiepusha na mvinyo na vileo vyovyote, jambo ambalo lilihitaji kujinyima mambo ya kibinafsi. Walipaswa kuacha nywele zao zikue na kuwa ndefu—alama ya ujitiisho kwa Yehova, kama vile wanawake walivyopaswa kujitiisha kwa waume au baba zao. Wanadhiri walipaswa kubaki safi kwa kujitenga na maiti yoyote, hata ya mtu wa ukoo. Leo watumishi wa wakati wote wanaonyesha roho ya kujidhabihu inapohusu kujinyima mambo ya kibinafsi na ujitiisho kwa Yehova na kwa mpango wake. Huenda migawo fulani ikamaanisha kwenda katika nchi ya mbali, jambo linaloweza kufanya iwe vigumu au hata isiwezekane kurudi nyumbani kwa ajili ya mazishi ya mshiriki wa familia.

8:25, 26. Ili kuhakikisha kwamba wanaume wenye uwezo ndio waliochaguliwa kufanya kazi za Walawi, wanaume wazee waliagizwa wastaafu kutoka katika utumishi wa lazima. Hata hivyo, wangeweza kujitolea kuwasaidia Walawi wengine. Ingawa leo wahubiri wa Ufalme hawastaafu, kanuni ya sheria hiyo hutufunza jambo muhimu. Ikiwa kwa sababu ya umri mkubwa Mkristo hawezi kutimiza wajibu fulani, huenda akafanya aina ya utumishi ambao ana uwezo wa kutimiza.

WATANGA-TANGA NYIKANI

(Hesabu 10:11–21:35)

Mwishowe, wingu juu ya maskani linapoondoka, Waisraeli wanaanza safari ambayo itawafikisha kwenye nyika za nchi tambarare za Moabu baada ya miaka 38 na mwezi moja au miwili. Huenda ukaona inafaa kutazama njia ambayo walifuata katika safari yao kwenye ramani katika ukurasa wa 9 wa broshua “Ona Nchi Nzuri,” iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Kwenye njia ya kwenda Kadeshi, katika Nyika ya Parani, Waisraeli wanalalamika mara tatu. Malalamiko yao ya yanakomeshwa wakati Yehova anapotokeza moto na kuwateketeza baadhi yao. Kisha Waisraeli wanalalamika wapewe nyama, naye Yehova anawapa kware. Malalamiko ya Miriamu na Haruni dhidi ya Musa yanafanya Miriamu apigwe kwa ukoma kwa muda.

Wanapopiga kambi huko Kadeshi, Musa anatuma wanaume 12 kupeleleza Nchi ya Ahadi. Wanarudi baada ya siku 40. Kwa kuiamini ripoti mbaya ya wapelelezi 10 kati ya hao, watu wanataka kuwapiga kwa mawe Musa, Haruni, na wale wapelelezi waaminifu Yoshua na Kalebu. Yehova anakusudia kupiga watu kwa tauni, lakini Musa anamsihi Mungu kwa ajili ya watu, naye Mungu anasema kwamba watatanga-tanga nyikani kwa miaka 40 mpaka wale waliohesabiwa wawe wamekufa.

Yehova anatoa masharti ya ziada. Kora na wengine wanaasi dhidi ya Musa na Haruni, lakini waasi hao wanaharibiwa kwa moto au wanamezwa na dunia. Siku inayofuata kusanyiko lote linanung’unika dhidi ya Musa na Haruni. Kwa sababu hiyo, watu 14,700 wanakufa kwa tauni kutoka kwa Yehova. Ili kuonyesha wazi chaguo lake kuhusu kuhani mkuu, Mungu anafanya fimbo ya Haruni ichanue maua. Kisha, Yehova anatoa sheria zaidi kuhusiana na wajibu wa Walawi na utakaso wa watu. Matumizi ya majivu ya ng’ombe mwekundu yanawakilisha utakaso kupitia dhabihu ya Yesu.—Waebrania 9:13, 14.

Wana wa Israeli wanarudi Kadeshi ambako Miriamu anakufa. Kusanyiko linanung’unika tena dhidi ya Musa na Haruni. Kwa nini? Kwa sababu ya ukosefu wa maji. Kwa kuwa Musa na Haruni wanakosa kulitakasa jina la Yehova wanapowapa watu maji kimuujiza, wanapoteza pendeleo la kuingia katika Nchi ya Ahadi. Waisraeli wanaondoka Kadeshi, naye Haruni anakufa kwenye Mlima Hori. Wanaposafiri kuzunguka Edomu, Waisraeli wanachoka nao wanasema vibaya dhidi ya Mungu na Musa. Yehova anatuma nyoka wenye sumu ili kuwaadhibu. Kwa mara nyingine tena, Musa anamsihi Mungu kwa ajili ya watu, naye Mungu anamwagiza afanye nyoka wa shaba na kumweka kwenye nguzo ili wale wanaoumwa wapate kupona kwa kumtazama. Nyoka huyo anafananisha kutundikwa mtini kwa Yesu Kristo kwa faida yetu ya milele. (Yohana 3:14, 15) Waisraeli wanawashinda Sihoni na Ogu, Wafalme wa Waamori, nao wanamiliki nchi yao.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

12:1—Kwa nini Miriamu na Haruni walimnung’unikia Musa? Yaelekea sababu hasa ya kunung’unika kwao ilikuwa tamaa ya Miriamu ya kuwa na uwezo zaidi. Wakati mke wa Musa, Sipora, alipojiunga naye nyikani, huenda Miriamu aliogopa kwamba hangeonwa tena kuwa kiongozi wa wanawake kambini.—Kutoka 18:1-5.

12:9-11—Kwa nini Miriamu peke yake ndiye aliyepigwa kwa ukoma? Kuna uwezekano mkubwa kwamba, yeye ndiye aliyeanza kulalamika na kumshawishi Haruni ajiunge naye. Haruni alionyesha mwelekeo mzuri kwa kutubu makosa yake.

21:14, 15—Kitabu kilichotajwa hapa kilikuwa nini? Maandiko yanarejelea vitabu mbalimbali ambavyo waandikaji wa Biblia walitumia kupata habari. (Yoshua 10:12, 13; 1 Wafalme 11:41; 14:19, 29) “Kitabu cha Vita vya Yehova” kilikuwa kimoja kati ya vitabu hivyo, nacho kilikuwa na masimulizi ya kihistoria kuhusu vita vya watu wa Yehova.

Mambo Tunayojifunza:

11:27-29. Musa anaweka kielelezo bora kuhusu jinsi tunavyopaswa kutenda wengine wanapopata mapendeleo katika utumishi wa Yehova. Badala ya kutafuta kwa wivu utukufu kwa ajili yake mwenyewe, Musa alifurahi Eldadi na Medadi walipoanza kutenda kama manabii.

12:2, 9, 10; 16:1-3, 12-14, 31-35, 41, 46-50. Yehova anatarajia waabudu wake waonyeshe heshima kwa wale wanaopewa mamlaka na Mungu.

14:24. Njia muhimu ya kupinga mikazo ya ulimwengu kuelekea ubaya ni kusitawisha mtazamo wa akili, au “roho iliyo tofauti.” Inapaswa kuwa roho ambayo ni tofauti na ile ya ulimwengu.

15:37-41. Upindo wa kipekee wa vazi la Waisraeli ulikusudiwa kuwakumbusha kwamba walikuwa watu waliotengwa kwa ajili ya ibada ya Mungu na kutii amri zake. Je, sisi pia hatupaswi kuishi kupatana na viwango vya Mungu na kuwa tofauti kabisa na ulimwengu?

KWENYE NCHI TAMBARARE ZA MOABU

(Hesabu 22:1–36:13)

Wana wa Israeli wanapopiga kambi kwenye nyika ya nchi tambarare za Moabu, Wamoabu wanahofu na kuchukizwa kwa sababu yao. Kwa hiyo, Balaki Mfalme wa Moabu, anamtumia Balaamu ili kuwalaani Waisraeli. Lakini Yehova anamlazimisha Balaamu kuwabariki. Halafu, wanawake wa Moabu na Midiani wanatumiwa ili kuwashawishi wanaume Waisraeli wafanye ngono na kuabudu sanamu. Kwa sababu hiyo, Yehova anaharibu wakosaji 24,000. Mwishowe, tauni inakomeshwa Finehasi anapoonyesha kwamba havumilii ushindani wowote kumwelekea Yehova.

Kuhesabiwa kwa watu mara ya pili kunafunua kwamba wanaume wote waliohesabiwa mara ya kwanza walikuwa wamekufa, isipokuwa Yoshua na Kalebu. Yoshua anaagizwa kuchukua nafasi ya Musa. Waisraeli wanapokea maagizo kuhusu matoleo mbalimbali na maagizo juu ya kuweka nadhiri. Wanalipiza pia kisasi juu ya Wamidiani. Kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase linamiliki eneo lililo mashariki ya Mto Yordani. Waisraeli wanapewa maagizo kuhusu kuvuka Yordani na kuimiliki nchi hiyo. Maelezo mengi kuhusu mipaka ya nchi yanatolewa. Urithi unapaswa kugawanywa kwa kura. Walawi wanapewa majiji 48, na 6 kati ya hayo yatatumiwa kuwa majiji ya makimbilio.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

22:20-22—Kwa nini hasira ya Yehova iliwaka dhidi ya Balaamu? Yehova alikuwa amemwambia nabii Balaamu asiwalaani Waisraeli. (Hesabu 22:12) Hata hivyo, nabii huyo alienda pamoja na watu wa Balaki akiwa amekusudia kabisa kuwalaani Waisraeli. Balaamu alitaka kumpendeza mfalme wa Moabu na kupokea zawadi kutoka kwake. (2 Petro 2:15, 16; Yuda 11) Hata baada ya Balaamu kulazimishwa kuwabariki Waisraeli badala ya kuwalaani, bado alitafuta kibali cha mfalme kwa kupendekeza kwamba waabudu wa kike wa Baali watumiwe ili kuwashawishi wanaume Waisraeli. (Hesabu 31:15, 16) Hivyo, hasira ya Mungu dhidi ya Balaamu iliwaka kwa sababu ya pupa mbaya sana ya nabii huyo.

30:6-8—Je, mwanamume Mkristo anaweza kuvunja nadhiri za mke wake? Kuhusu nadhiri, sasa Yehova anashughulika na watumishi wake wakiwa mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, kujiweka wakfu kwa Yehova ni nadhiri ya kibinafsi. (Wagalatia 6:5) Mume hana mamlaka ya kuvunja nadhiri kama hiyo. Hata hivyo, mke anapaswa kuepuka kuweka nadhiri inayopingana na Neno la Mungu au wajibu wake kwa mume wake.

Mambo Tunayojifunza:

25:11. Finehasi alituwekea kielelezo kizuri kama nini cha bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova! Tamaa ya kulinda usafi wa kutaniko inapaswa kutuchochea kuripoti kwa wazee Wakristo dhambi yoyote ya upotovu wa maadili ambayo tunajua.

35:9-29. Jambo la kwamba muuaji asiyekusudia alipaswa kuacha nyumba yake na kukimbilia jiji la makimbilio kwa kipindi fulani hutufundisha kwamba uhai ni mtakatifu na kwamba tunapaswa kuuheshimu.

35:33. Dunia ambayo imechafuliwa na damu iliyomwagwa ya watu wasio na hatia haiwezi kupatanishwa isipokuwa damu ya wale wanaoimwaga imwagwe. Inafaa kama nini kwamba Yehova atawaharibu waovu kabla ya kuigeuza dunia kuwa paradiso!—Methali 2:21, 22; Danieli 2:44.

Neno la Mungu Lina Nguvu

Tunapaswa kuonyesha heshima kwa Yehova na kwa wale waliowekwa rasmi katika vyeo vya madaraka kati ya watu wake. Kitabu cha Hesabu kinakazia ukweli huo. Hilo ni somo muhimu kama nini katika kudumisha amani na umoja kutanikoni leo!

Matukio yanayoelezwa katika kitabu cha Hesabu yanaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa wale wanaopuuza hali yao ya kiroho kuanguka katika makosa, kama vile kunung’unika, uasherati, na ibada ya sanamu. Baadhi ya vielelezo na mambo tunayojifunza kutoka katika kitabu hiki cha Biblia yanaweza kutumiwa kama chanzo cha habari kwa ajili ya mahitaji ya kwenu katika sehemu ya Mkutano wa Utumishi kwenye makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu” maishani mwetu.—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Kupitia wingu la kimuujiza juu ya maskani, Yehova alitoa mwongozo kuhusu kupiga kambi na kuvunja kambi ya Waisraeli

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yehova anastahili utii wetu naye hutazamia tuwaheshimu wawakilishi wake