Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu alimaanisha nini alipowaambia wanafunzi wake: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni”?

Yesu alikuwa tu amewachagua wanafunzi 70, na “kuwatuma wawili-wawili, wamtangulie kuingia katika kila jiji na mahali ambako yeye mwenyewe alikuwa aende.” Wanafunzi hao 70 waliporudi, walikuwa wenye shangwe sana kwa sababu ya mafanikio ya mahubiri yao. Walisema: “Bwana, hata roho waovu wanatiishwa kwetu kwa kutumia jina lako.” Ndipo Yesu akawaambia: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni.”—Luka 10:1, 17, 18.

Kwanza, huenda ikaonekana kwamba Yesu alikuwa akirejelea jambo ambalo tayari lilikuwa limetukia. Hata hivyo, miaka 60 baada ya Yesu kusema maneno yanayopatikana hapo juu, mtume mzee Yohana alitumia maneno kama hayo alipoandika: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufunuo 12:9.

Yohana alipoandika maneno hayo, bado Shetani alikuwa akiishi mbinguni. Tunajuaje? Kwa sababu Ufunuo ni kitabu cha unabii, wala si cha historia. (Ufunuo 1:1) Hivyo, Yohana alipokuwa hai, Shetani alikuwa bado hajatupwa duniani. Kwa kweli, mambo ya hakika yanaonyesha kwamba alitupwa baada ya Yesu kutawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914. *Ufunuo 12:1-10.

Kwa nini basi Yesu alitaja kufukuzwa kwa Shetani kutoka mbinguni kana kwamba tayari kulikuwa kumetukia? Baadhi ya wasomi husema kwamba Yesu alikuwa akiwakaripia wanafunzi wake kwa kuonyesha kiburi kisichofaa. Wanaamini kwamba alikuwa akisema: ‘Mliwashinda roho waovu, lakini msijivune. Shetani alipata kuwa mwenye kiburi, na jambo hilo likaifanya aanguke haraka.’

Hatuwezi kuwa na uhakika kabisa kuhusu ukweli wa jambo hilo. Hata hivyo, yaelekea sana kwamba Yesu alikuwa akishangilia pamoja na wanafunzi wake na kurejelea kuanguka kwa Shetani wakati ujao. Yesu alijua vizuri zaidi ya mtu mwingine yeyote kati ya wanafunzi wake kwamba Ibilisi alikuwa mwenye chuki ya kikatili. Fikiria shangwe ambayo Yesu alihisi aliposikia kwamba roho waovu wenye nguvu sana walikuwa wakitiishwa kwa wanafunzi wake ambao ni wanadamu wasio wakamilifu. Kutiishwa huko kwa roho waovu kulionyesha kwa sehemu ndogo tu jinsi wakati ujao Yesu, akiwa Mikaeli, yule malaika mkuu, atakavyopigana na Shetani na kumtupa kutoka mbinguni hadi duniani.

Yesu aliposema kwamba alimwona Shetani akiwa “tayari ameanguka,” yaonekana alikuwa akikazia uhakika wa kuanguka kwa Shetani. Maneno hayo yanafanana na unabii mwingine mbalimbali wa Biblia ambao husema kuhusu matukio ya wakati ujao kana kwamba yamekwisha timia. Kwa mfano, ona mchanganyiko wa matumizi ya njeo ya wakati uliopita na ya wakati ujao katika unabii kuhusu Masihi kwenye Isaya 52:13–53:12. Yaelekea Yesu alikuwa akionyesha uhakika wa kwamba kufukuzwa kwa Shetani kutoka mbinguni kungetukia kulingana na kusudi la Baba yake. Pia, Yesu alikuwa na uhakika kwamba katika wakati uliowekwa na Mungu, Shetani na roho wake waovu wangetupwa katika abiso na baadaye waharibiwe milele.—Waroma 16:20; Waebrania 2:14; Ufunuo 20:1-3, 7-10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona vitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, sura ya 10, na Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! sura ya 27, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.