Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Hufanya Maisha Yawe na Kusudi Halisi?

Ni Nini Hufanya Maisha Yawe na Kusudi Halisi?

Ni Nini Hufanya Maisha Yawe na Kusudi Halisi?

WAKATI Jesse, mwanafunzi wa sekondari mwenye umri wa miaka 17, alipoulizwa kuhusu kusudi la maisha, alijibu, “Maadamu uko hai, jifurahishe kadiri uwezavyo.” Suzie alikuwa na maoni tofauti. Alisema: “Ninaamini kwa moyo mweupe kwamba kusudi la maisha ni kile unachofanya yawe.”

Je, umewahi kujiuliza kuhusu kusudi la maisha? Je, kuna kusudi fulani kwa ajili ya wanadamu wote? Au je, Suzie anasema kweli kwamba maisha ni kile ambacho hasa kila mmoja wetu huyafanya yawe? Hata jamii yetu iwe imeendelea kiteknolojia kadiri gani, kuna kitu fulani ndani yetu ambacho yaonekana hutamani kujua kusudi la maisha. Wakati fulani maishani, wengi wetu hujiuliza, ‘Kwa nini tupo hapa?’

Sayansi ya kisasa imejitahidi kujibu swali hilo. Imetoa jibu gani? “Kulingana na hatua mbalimbali katika mageuzi, kuwa hai hakuna kusudi lolote,” asema David P. Barash, profesa wa saikolojia na zuolojia. Wanabiolojia wa mageuzi wanaamini kwamba viumbe-hai vina kusudi moja tu: kuishi na kuzaana. Hivyo, Profesa Barash anadokeza: “Katika ulimwengu mkubwa usio na kusudi na usiowajali watu, wanadamu wana daraka la kufanya maisha yetu yawe na kusudi kwa maamuzi wanayofanya kwa hiari na kwa kujua.”

Chanzo cha Maana na Kusudi la Maisha

Je, hilo tu ndilo kusudi la maisha—kila mmoja wetu afanye atakalo? Badala ya kutuacha tutange-tange bila kusudi lolote katika ulimwengu usio na kusudi, kwa muda mrefu Biblia imeonyesha kwamba tupo hapa kwa kusudi fulani. Kuwepo kwetu hakutokani na aksidenti tu. Tunaambiwa kwamba Muumba alitumia miaka mingi sana kutayarisha dunia kwa ajili ya mwanadamu. Hakuna jambo lililotokea kwa aksidenti. Alihakikisha kwamba kila kitu kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31; Isaya 45:18) Kwa nini? Kwa sababu Mungu alikuwa na kusudi fulani kuelekea mwanadamu.

Hata hivyo, jambo la kupendeza ni kwamba Mungu hakupanga kimbele wakati ujao wa kila mtu, ama kwa kuingilia maisha yetu moja kwa moja au kwa jinsi alivyotuumba. Ingawa tunaathiriwa na mambo fulani tuliyorithi, tunaweza kudhibiti matendo yetu kwa kiwango kikubwa. Sote tuna uhuru wa kuchagua jinsi tutakavyojiendesha maishani.

Ingawa kila mmoja wetu anaweza kuchagua jinsi atakavyotumia maisha yake, litakuwa kosa kumpuuza Muumba katika mipango yetu. Kwa kweli, wengi wametambua kwamba ili maisha yawe na maana na kusudi halisi, ni lazima tuwe na uhusiano na Mungu. Uhusiano muhimu uliopo kati ya Mungu na kusudi letu maishani unakaziwa na jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, ambalo kihalisi linamaanisha, “Yeye Husababisha Kuwa.” (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18) Yaani, yeye hutimiza hatua kwa hatua mambo yote anayoahidi, na sikuzote yeye hutimiza yale ambayo amekusudia kufanya. (Kutoka 3:14; Isaya 55:10, 11) Fikiria maana ya jina hilo. Jina Yehova hutuhakikishia sote kwamba yeye ndiye Chanzo cha kusudi lenye maana na la kudumu.

Kukubali tu kwamba kuna Muumba huathiri sana maoni ya mtu kuelekea maisha. Linet, mwenye umri wa miaka 19 anasema: “Ninapoona vitu vyote vizuri ambavyo Yehova ameumba na kusudi la vitu hivyo, mimi hujua pia kwamba niliumbwa kwa sababu fulani.” Amber aongeza kusema: “Watu wasemapo kwamba hawajui kama Mungu yuko, mimi hushukuru kwamba ninajua yuko. Vitu ambavyo Yehova aliumba huthibitisha kwamba yeye yuko.” (Waroma 1:20) Bila shaka, kuna tofauti kati ya kutambua kwamba kuna Muumba na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye.

Urafiki Pamoja na Mungu

Hapa tena, Biblia inaweza kutusaidia. Sura zake za kwanza zinathibitisha wazi kwamba Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo. Kwa mfano, hakuwaumba Adamu na Hawa na kukosa kuwaambia yeye ni nani. Badala yake, aliwasiliana nao kwa ukawaida. Hakuwaacha Edeni wajiongoze wenyewe huku akijishughulisha na mambo mengine. Badala yake, aliwapa mwongozo hususa kuhusu njia bora ya maisha. Aliwapa kazi yenye kuridhisha, naye akapanga waendelee kupata elimu. (Mwanzo 1:26-30; 2:7-9) Je, hungetazamia mzazi mwenye uwezo na upendo afanye hivyo? Sasa fikiria maana ya jambo hilo. “Kujua kwamba Yehova aliiumba dunia na kutuumba tukiwa na uwezo wa kufurahia uumbaji wake,” asema Denielle, “hunionyesha kwamba anataka tuwe na furaha.”

Zaidi ya hayo, kama baba yeyote mwenye upendo, Yehova anataka watoto wake wote wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Kuhusiana na hilo, andiko la Matendo 17:27 linatuhakikishia hivi: “Hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” Jambo hilo ni muhimu kadiri gani? Amber anasema: “Kupata kumjua Yehova kumefanya niwe na uhakika kwamba siko peke yangu kamwe. Hata hali ziweje, sikuzote kuna mtu ninayeweza kumkimbilia.” Isitoshe, unapozidi kumjua Yehova utaona kwamba yeye ni mwenye fadhili, haki, na mwema. Unaweza kumtegemea. “Yehova alipopata kuwa rafiki yangu wa karibu,” asema Jeff, “Nilijua kwamba hakuna yeyote ambaye angeweza kunisaidia zaidi wakati wa uhitaji kuliko yeye.”

Kwa kusikitisha, mambo mengi mabaya yamesemwa kumhusu Yehova. Amelaumiwa kwa sababu ya kuteseka kwa wanadamu na kwa matatizo yanayotokana na mwenendo mbaya wa watu wa dini. Pia amelaumiwa kwa ukatili mbaya zaidi ambao umefanywa katika historia ya wanadamu katika jina lake. Lakini andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4, 5 linasema: “Njia zake zote ni haki. . . . Wametenda kwa uharibifu; wao si watoto wake, kasoro ni yao wenyewe.” Kwa hiyo, tuna daraka la kuchunguza ukweli wa mambo.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

Kusudi la Mungu Latimizwa

Hata hivyo, hata tuamue nini, hakuna chochote kitakachomzuia Mungu asitimize kabisa kusudi lake kuelekea dunia hii na wanadamu. Tunapaswa kukumbuka kwamba yeye ndiye Muumba. Basi, kusudi hilo ni lipi? Yesu Kristo alilitaja katika Mahubiri yake ya Mlimani aliposema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” Baadaye, kupitia mtume wake Yohana, Mungu alionyesha kwamba ameazimia “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Mathayo 5:5; Ufunuo 11:18) Kwa sababu Yesu alikuwa pamoja na Mungu wakati wa uumbaji, anajua kwamba tangu mwanzo Mungu alikusudia kuwe na familia ya wanadamu wakamilifu ambao wangekaa duniani milele katika paradiso. (Mwanzo 1:26, 27; Yohana 1:1-3) Naye Mungu habadiliki. (Malaki 3:6) Mungu anatuahidi hivi: “Hakika kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa, na kama vile nilivyotoa shauri, hivyo ndivyo itakavyotimia.”—Isaya 14:24.

Wakati wetu, tayari Yehova ameanza kuweka misingi ya jamii iliyoungana ambayo inategemea upendo kwa Mungu na kwa jirani wala si pupa na ubinafsi ambao umeenea katika ulimwengu wa leo. (Yohana 13:35; Waefeso 4:15, 16; Wafilipi 2:1-4) Hiyo ni jamii ya watu wanaopenda maendeleo ambao wamejitoa na wanaochochewa na imani yao ili kutimiza kusudi lao, ambalo ni kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu unaokuja kabla ya mfumo huu wa mambo kwisha. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Katika nchi zaidi ya 230, Wakristo zaidi ya milioni sita tayari wanaabudu pamoja wakiwa katika undugu wa kimataifa wenye upendo.

Fanya Maisha Yako Yawe na Kusudi

Ikiwa unataka maisha yako yawe na kusudi zaidi, unapaswa kujua kwamba Yehova Mungu anakualika ushirikiane sasa na watu wake—‘taifa lake la uadilifu.’ (Isaya 26:2) Hata hivyo, huenda ikawa unajiuliza, ‘Maisha yakoje katika jamii hiyo ya Kikristo? Je, kweli ninataka kushirikiana na jamii hiyo?’ Sikiliza yale ambayo vijana fulani wanasema:

Quentin: “Kutaniko ndilo hunilinda na ulimwengu. Kutambua kwamba Yehova anahusika katika maisha yangu hunisaidia kuona kwamba yeye yuko na anataka niwe mwenye furaha.”

Jeff: “Kutaniko ndipo mahali bora zaidi ninapoweza kupata kitia-moyo. Ndugu na dada zangu wako huko, nao hunitegemeza na kunipongeza. Kwa kweli, wao ni sehemu ya familia yangu.”

Linet: “Ile shangwe ya kuona mtu akikubali kweli ya Biblia na kufanya uamuzi wa kumtumikia Yehova haiwezi kulinganishwa na chochote. Jambo hilo hunipa furaha nyingi sana maishani.”

Cody: “Maisha yangu hayangekuwa na kusudi lolote bila Yehova. Ningekuwa nikitanga-tanga bila kusudi lolote kama watu wengine wengi nikijaribu kutafuta furaha, lakini bila mafanikio. Badala yake, Yehova amenipa pendeleo kubwa sana la kuwa na uhusiano pamoja naye, na hilo hufanya maisha yangu yawe na kusudi.”

Kwa nini usichunguze jambo hilo mwenyewe? Utatambua kwamba kwa kumkaribia Muumba, Yehova Mungu, utapata kusudi halisi maishani.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Maisha yetu huwa na kusudi tunapokuwa na uhusiano pamoja na Mungu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]

NASA photo