Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Serikali ya Ufalme wa Mungu Ni Halisi Leo

Serikali ya Ufalme wa Mungu Ni Halisi Leo

Serikali ya Ufalme wa Mungu Ni Halisi Leo

“Inawezekanaje nchi nyingi sana zenye tamaduni mbalimbali ambazo hazijasitawi kwa kiwango kilekile, zikubaliane? Imesemekana kwamba jamii ya wanadamu itaungana tu ikishambuliwa kutoka sayari nyingine.” —The Age, gazeti la Australia.

SHAMBULIZI kutoka sayari nyingine? Ingawa hatujui kama shambulizi hilo litaunganisha mataifa yote ya dunia, unabii wa Biblia unataja msiba unaokaribia ambao utafanya mataifa ya ulimwengu yaungane. Na kwa kweli, msiba huo utasababishwa na nguvu kutoka nje ya sayari yetu.

Mfalme Daudi wa Israeli la kale alitoa unabii kuhusu hali hiyo ya ulimwengu. Aliandika hivi kwa kuongozwa na roho ya Mungu: “Wafalme wa dunia wanachukua msimamo wao nao maofisa wakuu wamejikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake, wakisema: ‘Na tuzikate pingu zao na kuzitupa kamba zao mbali nasi!’” (Zaburi 2:2, 3; Matendo 4:25, 26) Ona kwamba watawala wa ulimwengu wangejikusanya pamoja dhidi ya Yehova, Muumba wa ulimwengu wote, na dhidi ya mtiwa-mafuta wake, au Mfalme wake aliyeteuliwa, Yesu Kristo. Hilo lingetukiaje?

Kulingana na kronolojia ya Biblia na unabii uliotimizwa, mnamo 1914, Ufalme wa Mungu ulisimamishwa mbinguni, Yesu Kristo akiwa Mfalme. * Wakati huo mataifa ya ulimwengu yalikuwa na wazo moja. Badala ya kujinyenyekeza chini ya enzi kuu ya Ufalme wa Mungu uliokuwa umezaliwa, yalijihusisha na pambano la kupata mamlaka—vile Vita Vikuu, au Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

Yehova Mungu anaonaje hatua hiyo ya watawala wa kibinadamu? “Yule anayeketi mbinguni atacheka; Yehova mwenyewe atawadharau. Wakati huo atasema nao katika hasira yake na katika ghadhabu yake atawafadhaisha.” Kisha Yehova atamwambia hivi Mwana wake, ambaye ni Mfalme aliyetiwa mafuta wa Ufalme huo: “Niombe, ili nikupe mataifa yawe urithi wako na miisho ya dunia iwe miliki yako mwenyewe. Utawavunja kwa fimbo ya chuma ya enzi, utawavunja vipande-vipande, kama chombo cha mfinyanzi.”—Zaburi 2:4, 5, 8, 9.

Mataifa yanayoleta upinzani yatavunjwa kabisa kwa fimbo ya chuma wakati wa Har–Magedoni. Kitabu cha mwisho cha Biblia cha Ufunuo kinafafanua tukio hilo kuwa upeo wa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” ambapo “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wanakusanywa pamoja. (Ufunuo 16:14, 16) Chini ya uvutano wa roho waovu, mwishowe mataifa ya dunia yataungana yakiwa na lengo moja: kupigana na Mungu Mweza-Yote.

Wakati ambapo wanadamu watajikusanya pamoja ili kupigana na enzi kuu ya Mungu unakaribia upesi. Hata hivyo, “umoja” wao hautawafaidi. Badala yake, tendo lao litakuwa mwanzo wa amani ambayo wanadamu wamengojea kwa muda mrefu. Jinsi gani? Kwenye vita hivyo vya mwisho, Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za ulimwengu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Ufalme wa Mungu, wala si tengenezo lolote la kibinadamu ndio utakaotosheleza tamaa ya wanadamu ya kuwa na amani ulimwenguni.

Msimamizi Mkuu wa Serikali Hiyo ya Ufalme

Huo ndio Ufalme ambao watu wengi wanyoofu wameomba kuuhusu, wakisema: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu si hali ya kuwaziwa ya moyoni, bali ni serikali halisi ambayo imetimiza mambo mazuri tangu isimamishwe mbinguni mwaka wa 1914. Basi na tuchunguze mambo fulani muhimu yanayoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na unafanya kazi leo.

Kwanza kabisa, una kikundi cha wasimamizi chenye uwezo na nguvu ambacho kinasimamiwa na Mfalme aliyetawazwa, Yesu Kristo. Yehova Mungu alimweka Yesu Kristo kuwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo mwaka wa 33 W.K. (Waefeso 1:22) Tangu wakati huo, Yesu amekuwa akitumia ukichwa wake, na hivyo kuonyesha uwezo wake wa kuwa msimamizi. Kwa mfano, njaa kuu ilipotokea Yudea katika karne ya kwanza, kutaniko la Kikristo lilichukua hatua mara moja kuwasaidia washiriki wake. Kazi ya kutoa msaada ilipangwa, nao Barnaba na Sauli wakatumwa toka Antiokia kupeleka misaada.—Matendo 11:27-30.

Wakati huu ambapo serikali ya Ufalme inatenda kazi, tunaweza kutarajia mengi zaidi kutoka kwa Yesu Kristo. Misiba inapotokea—matetemeko ya nchi, njaa, mafuriko, vimbunga, dhoruba, au milipuko ya volkeno—kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova huchukua hatua mara moja ili kusaidia waamini wenzao na watu wengine katika maeneo yaliyoathiriwa. Kwa mfano, wakati matetemeko ya nchi yenye kusababisha uharibifu yalipotukia huko El Salvador mnamo Januari na Februari 2001, kazi za kutoa misaada zilipangwa katika sehemu zote za nchi, na vikundi vya Mashahidi wa Yehova kutoka Kanada, Guatemala, na Marekani vilisaidia. Majengo yao matatu ya ibada pamoja na nyumba zaidi ya 500 zilijengwa upya baada ya muda mfupi.

Raia za Serikali ya Ufalme wa Mungu

Tangu usimamishwe mwaka wa 1914, Ufalme wa kimbingu wa Mungu umekuwa ukikusanya na kupanga raia zake kutoka kwa watu wote ulimwenguni. Hilo linapatana na kutimizwa kwa unabii huu wenye kutokeza ulioandikwa na Isaya: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, . . . na mataifa yote yatamiminika huko.” Unabii huo unaonyesha kwamba “vikundi vingi vya watu” wangeenda juu kwenye mlima na kukubali mafundisho na sheria za Yehova.—Isaya 2:2, 3.

Kazi hiyo imetokeza tengenezo muhimu zaidi katika nyakati za sasa—undugu wa kimataifa wa Wakristo zaidi ya 6,000,000 katika nchi zaidi ya 230 duniani. Kwenye makusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova, mara nyingi watazamaji hushangaa kuona umati mkubwa wa watu wenye upendo, amani, na umoja, ambao huchangamana bila kujali taifa, utamaduni, au lugha. (Matendo 10:34, 35) Je, hukubali kwamba ni lazima serikali iwe yenye nguvu, thabiti, na halisi ili iweze kuleta pamoja makabila mengi ya watu waishi kwa amani na upatano?

Ufalme wa Mungu na Elimu

Kila serikali ina viwango ambavyo lazima raia zake wavitimize, na yeyote anayetaka kuishi chini ya serikali hiyo anapaswa kuvitimiza. Vivyo hivyo, Ufalme wa Mungu una viwango ambavyo wote wanaotaka kuwa raia zake wanapaswa kuvitimiza. Hata hivyo, kazi kubwa sana inahitajiwa ili kuwawezesha watu wengi wenye malezi tofauti-tofauti wakubali na kufuata viwango vilevile. Hivyo basi, hili ni jambo lingine linalothibitisha kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi, yaani, programu yake ya elimu yenye matokeo ambayo hufikia na kubadili akili na moyo.

Serikali ya ufalme hutimizaje kazi hiyo ngumu? Kwa kutumia njia kama ile ya mitume ya kuhubiri “nyumba kwa nyumba” na kuwafundisha watu mmoja-mmoja Neno la Mungu. (Matendo 5:42; 20:20) Elimu hiyo ina matokeo kadiri gani? Katika gazeti la Kanada linalochapishwa kila juma, Jacques Johnson, kasisi Mkatoliki, aliandika hivi kuhusu jitihada zake za kumshawishi mwanamke fulani asijifunze na Mashahidi wa Yehova. “Nilishangaa sana na nikatambua kwamba singeshinda vita hivyo,” akasema. “Nilianza kutambua kwamba kwa miezi kadhaa wanawake hao Mashahidi walikuwa wameanzisha uhusiano mzuri na mama huyo ambaye hangeweza kutoka nje. Walianzisha uhusiano huo pamoja naye kwa kumsaidia, kufanya urafiki naye, na pia kuwa na vifungo vya kihisia-moyo. Baada ya muda mfupi, akawa mfuasi mwenye bidii wa dini yao na singeweza kufanya lolote kuzuia jambo hilo.” Kama vile moyo wa mwanamke huyo aliyekuwa Mkatoliki ulivyoguswa na ujumbe wa Biblia unaofundishwa na Mashahidi wa Yehova na pia mwenendo wao wa Kikristo, ndivyo mioyo ya watu wengi ulimwenguni pote inavyoguswa na ujumbe huo.

Aina hii ya elimu, yaani, elimu ya Ufalme, hutegemea Biblia, na pia hutegemeza kanuni zake na viwango vyake vya maadili. Hiyo huwafundisha watu wapendane na kuheshimiana bila kujali malezi yao. (Yohana 13:34, 35) Pia, elimu hiyo huwasaidia watu watii shauri hili: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kwa kuacha mwenendo wao wa zamani na kufuata kwa furaha sheria na kanuni za serikali hiyo ya Ufalme, watu wengi wamepata amani na furaha sasa na matarajio mazuri ya wakati ujao.—Wakolosai 3:9-11.

Msaada mmoja wenye kutokeza wa kutimiza umoja huo ulimwenguni pote ni gazeti hili Mnara wa Mlinzi. Kwa kutumia mpangilio uleule wa kutafsiri na vifaa vya kuchapisha lugha nyingi, makala kuu katika Mnara wa Mlinzi huchapishwa wakati uleule katika lugha 135, na zaidi ya asilimia 95 ya wasomaji wake ulimwenguni pote wanaweza kujifunza habari hiyo katika lugha yao kwa wakati uleule.

Mwandishi mmoja wa dini ya Mormon aliandika orodha ya mafanikio bora zaidi ambayo mishonari wasio wa kanisa lake wamepata. Aliorodhesha Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, yanayochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kuwa magazeti bora zaidi ya kuhubiri Injili na kusema: “Hakuna anayeweza kushutumu magazeti Mnara wa Mlinzi au Amkeni! kwamba huwatia watu moyo wakae tu bila kujali—tofauti na hilo, magazeti hayo huwasaidia watu wawe macho kwa njia ambayo sijapata kuona katika vichapo vingine vya kidini. Habari zinazopatikana katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinasisimua, ni hakika, zimefanyiwa utafiti vizuri na zinahusu hali halisi za ulimwengu.”

Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na unafanya kazi kabisa. Mashahidi wa Yehova huwaeleza jirani zao “hii habari njema ya ufalme” kwa furaha na kwa bidii wakiwaalika wawe raia za ufalme huo. (Mathayo 24:14) Je, unavutiwa na tumaini hilo? Unaweza kupata baraka zinazotokana na kushirikiana na wale wanaoelimishwa na ambao hujitahidi kuishi kupatana na viwango vya Ufalme huo. Jambo bora hata zaidi ni kwamba unaweza kuja kufurahia tumaini la kuishi chini ya utawala wa Ufalme katika ulimwengu mpya ulioahidiwa ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi, ona sura ya 10, “Ufalme wa Mungu Watawala,” katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 90-97.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Mwaka wa 1914, mataifa yalizozana katika vita vya ulimwengu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kazi ya kujitolea ya kutoa msaada ni uthibitisho wa upendo wa Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hunufaika na programu ileile ya elimu