Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulitegemea Nguvu za Yehova

Tulitegemea Nguvu za Yehova

Simulizi la Maisha

Tulitegemea Nguvu za Yehova

LIMESIMULIWA NA ERZSÉBET HAFFNER

“Sitawaruhusu wakuhamishe,” akasema Tibor Haffner aliposikia kwamba nilikuwa nimeamriwa niondoke Chekoslovakia. Kisha akaongeza kusema: “Ukikubali nitakuoa, kisha utabaki nami milele.”

JANUARI 29, 1938, majuma machache tu baada ya kuniomba bila kutarajia niwe mke wake, niliolewa na Tibor, ndugu Mkristo ambaye ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza kuihubiria familia yetu. Huo haukuwa uamuzi rahisi. Nilikuwa tu nimefikisha umri wa miaka 18, na nikiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, nilitaka kutumia miaka yangu ya ujana katika kumtumikia Mungu tu. Nililia na kusali. Baada ya kutulia nilitambua kwamba ombi la Tibor la kunioa lilihusisha mengi zaidi ya tendo la fadhili, nami nilihisi kwamba nilitaka kuishi na mwanamume huyo aliyenipenda kikweli.

Lakini kwa nini nilikabili hatari ya kuhamishwa na hali niliishi katika nchi ambayo ilijivunia mfumo wake wa kidemokrasia na uhuru wa kidini? Nafikiri sasa, napaswa kuwaeleza mengi zaidi kuhusu malezi yangu.

Nilizaliwa Desemba 26, 1919, katika kijiji cha Sajószentpéter, Hungaria, kilometa 160 hivi mashariki ya Budapest. Wazazi wangu walikuwa Wagiriki nao walikuwa Wakatoliki. Kwa kusikitisha, baba yangu alikufa kabla sijazaliwa. Punde si punde, mama yangu aliolewa na mjane wa kiume aliyekuwa na watoto wanne, kisha tukahamia Lučenec, jiji maridadi katika nchi ambayo ilikuwa Chekoslovakia. Siku hizo, haikuwa rahisi kuishi katika familia ya kambo. Mimi ndiye niliyekuwa mdogo kati ya watoto watano, nami sikuhisi nikiwa sehemu ya familia hiyo. Hali ya kiuchumi ilikuwa ngumu, nami nilikosa vitu vya kimwili na pia upendo na utunzaji wa kawaida kutoka kwa wazazi.

Je, Kuna Yeyote Anayejua Jibu?

Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilisumbuliwa na maswali mazito. Nilifurahia sana kusoma historia ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na nilishangaa kuona mauaji yaliyofanywa na mataifa yenye ustaarabu ambayo yalidai kuwa ya Kikristo. Isitoshe, niliona utukuzo wa matumizi ya nguvu za kijeshi uliokuwa ukiongezeka kila mahali. Mambo hayo hayakupatana na yale niliyojifunza kanisani kuhusu kumpenda jirani.

Hivyo, nilienda kwa kasisi Mkatoliki na kumuuliza: “Ni amri gani inayopaswa kutuunganisha tukiwa Wakristo—kwenda vitani na kuua jirani zetu au kuwapenda?” Akiwa amekasirishwa na swali langu, alijibu kwamba yeye hufundisha mambo aliyoambiwa na wakubwa wake. Nilikumbana na hali hiyohiyo nilipomtembelea mhudumu wa wafuasi wa Calvin, kisha rabi Myahudi. Sikupata jibu lolote, ila tu walishangazwa na swali langu lisilo la kawaida. Mwishowe, nilienda kumwona mhudumu wa Kanisa la Lutheri. Aliudhika, lakini kabla sijaondoka, alisema: “Ikiwa kweli ungependa kupata jibu, waulize Mashahidi wa Yehova.”

Nilijaribu kuwatafuta Mashahidi bila mafanikio. Siku chache baadaye nilipokuwa nikirudi nyumbani kutoka kazini, niliona mlango umefunguliwa kidogo. Mwanamume kijana mwenye sura nzuri alikuwa akimsomea mama Biblia. Kwa ghafula, nikawaza, ‘Lazima huyo awe ni Shahidi wa Yehova!’ Tulimkaribisha mtu huyo, Tibor Haffner, nami nikamuuliza maswali yaleyale. Badala ya kujibu kwa maneno yake, alinionyesha yale ambayo Biblia husema kuhusu alama ya kuwatambulisha Wakristo wa kweli, na vilevile kuhusu nyakati tunamoishi.—Yohana 13:34, 35; 2 Timotheo 3:1-5.

Baada ya miezi michache, kabla sijafikisha umri wa miaka 17, nikabatizwa. Nilihisi kwamba lazima kila mtu asikie kweli hizi zenye thamani ambazo nilipata kwa njia ngumu sana. Nilianza utumishi wa wakati wote, jambo ambalo halikuwa rahisi nchini Chekoslovakia mwishoni mwa miaka ya 1930. Ingawa kazi yetu ilikuwa imeandikishwa rasmi, tulikabili upinzani mkali sana uliochochewa na makasisi.

Twateswa

Siku moja mwishoni mwa mwaka wa 1937, nilikuwa nikihubiri pamoja na dada mwingine Mkristo katika kijiji kimoja kilicho karibu na Lučenec. Baada ya muda mfupi, tulikamatwa na kupelekwa gerezani. “Mtafia hapa,” akasema mlinzi, huku akiufunga mlango wa seli kwa nguvu.

Kufikia jioni, wanawake wengine wanne walikuwa wameletwa katika seli hiyo. Tulianza kuwafariji na kuwahubiria. Walitulia, nasi tukazungumza nao kweli ya Biblia usiku kucha.

Saa kumi na mbili asubuhi, mlinzi aliniita nitoke kwenye seli. Nami nikamwambia mwenzangu: “Tutaonana tena katika Ufalme wa Mungu.” Nilimwambia kwamba ikiwa ataokoka aieleze familia yangu kilichotukia. Nilitoa sala fupi na kuandamana na mlinzi huyo. Alinipeleka nyumbani kwake katika eneo la gereza. “Msichana, ningependa kukuuliza maswali kadhaa,” akasema. “Jana usiku ulisema kwamba jina la Mungu ni Yehova. Je, unaweza kunionyesha jina hilo katika Biblia?” Nilishangaa na kuhisi nimetulia sana. Alileta Biblia yake, kisha nikamwonyesha yeye pamoja na mke wake jina Yehova. Alikuwa na maswali mengi kuhusu habari tuliyokuwa tumezungumzia pamoja na wale wanawake wanne usiku. Kwa kuridhishwa na majibu hayo, alimwomba mke wake atayarishe kiamsha-kinywa kwa ajili yangu na mwenzangu.

Siku chache baadaye, tulifunguliwa, lakini hakimu mmoja akaamua kwamba kwa kuwa nilikuwa raia wa Hungaria, nilipaswa kuondoka Chekoslovakia. Baada ya tukio hilo ndipo Tibor Haffner aliponiomba niwe mke wake. Tulioana kisha tukahamia nyumbani kwa wazazi wake.

Mateso Yazidi

Tuliendelea na kazi ya kuhubiri tukiwa mume na mke, ingawa Tibor pia alikuwa na mambo mengine ya kufanya. Siku chache kabla ya askari wa Hungaria kuingia katika jiji letu mnamo Novemba 1938, mwana wetu Tibor, Jr., akazaliwa. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vinakaribia kuanza huko Ulaya. Sehemu kubwa ya Chekoslovakia ilitwaliwa na Hungaria, na hivyo kutokeza mateso makali kwa Mashahidi wa Yehova walioishi katika maeneo yaliyotwaliwa.

Tibor aliondoka Debrecen Oktoba 10, 1942, ili akakutane na ndugu kadhaa. Lakini wakati huu hakurudi. Baadaye alinieleza kilichotukia. Badala ya kukutana na ndugu hao, alikutana na polisi waliovaa mavazi ya wafanyakazi kwenye daraja ambapo wangekutania. Walikuwa wakimsubiri mume wangu pamoja na Pál Nagypál, ambao walikuwa wa mwisho kufika. Polisi hao waliwapeleka kwenye kituo cha polisi na kupiga nyayo zao kwa rungu hadi wakazimia kwa sababu ya uchungu.

Kisha wakaamriwa wavae viatu vyao na kusimama. Licha ya maumivu, walilazimishwa kwenda kwenye kituo cha gari-moshi. Polisi walileta mtu mwingine aliyekuwa na bendeji nyingi sana kichwani hivi kwamba hangeweza kuona vizuri. Huyo alikuwa Ndugu András Pilling, ambaye pia alikuwa amekuja kwenye mkutano huo. Mume wangu alipelekwa kizuizini kwa gari-moshi huko Alag, karibu na Budapest. Mmoja wa walinzi aliyeona jinsi Tibor alivyojeruhiwa miguuni alisema hivi kimzaha: “Watu wanaweza kuwa wakatili kweli! Usijali, tutakuponya.” Walinzi wengine wawili walianza kumpiga Tibor miguuni, na damu ikatapakaa kila mahali. Alizimia baada ya dakika chache.

Mwezi uliofuata, Tibor pamoja na ndugu na dada wengine zaidi ya 60 walipelekwa mahakamani. Ndugu András Bartha, Dénes Faluvégi, na János Konrád walihukumiwa kunyongwa. Ndugu András Pilling alihukumiwa kifungo cha maisha, naye mume wangu akahukumiwa kifungo cha miaka 12 gerezani. Walifanya uhalifu gani? Mwendesha-mashtaka aliwashtaki kwa uhaini mkubwa, kukataa utumishi wa kijeshi, ujasusi, na kuchongea kanisa takatifu zaidi. Baadaye hukumu hizo zilibadilishwa kuwa kifungo cha maisha.

Kumfuata Mume Wangu

Siku mbili baada ya Tibor kuondoka kwenda mkutanoni huko Debrecen, niliamka kabla ya saa 12 ili kupiga nguo zetu pasi. Kwa ghafula, mlango ulibishwa kwa nguvu. Niliwaza, ‘Wamekuja.’ Polisi sita waliingia na kuniambia kwamba wana idhini ya kusaka nyumba yetu. Wote waliokuwa nyumbani walikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi, kutia ndani mwana wetu wa miaka mitatu. Siku hiyohiyo tulihamishwa hadi gereza la Pétervására, huko Hungaria.

Baada ya kufika huko, nilishikwa na homa hivyo nikatenganishwa na wafungwa wengine. Nilipopona, askari wawili waliingia ndani ya seli yangu na kuanza kubishana juu yangu. “Lazima tumpige risasi! Nitampiga risasi!” akasema askari mmoja. Lakini yule mwingine alitaka kujua hali yangu ya afya kabla hawajanipiga risasi. Niliwasihi wasiniue. Mwishowe waliondoka katika seli hiyo, nami nikamshukuru Yehova kwa kunisaidia.

Walinzi walikuwa na njia ya kipekee ya kuhoji watu. Waliniamuru nilale kifudifudi sakafuni, wakaweka soksi kinywani mwangu, wakanifunga mikono na miguu, na kunichapa hadi nikaanza kuvuja damu. Waliacha kunipiga wakati tu askari mmoja aliposema kwamba amechoka. Waliniuliza mume wangu alikuwa akutane na nani siku ambayo alikamatwa. Sikuwaambia, hivyo waliendelea kunipiga kwa siku tatu. Siku ya nne niliruhusiwa kumpeleka mwana wangu kwa mama yangu. Katika hali ya hewa ya baridi kali, nilimbeba mtoto wangu kwenye mgongo uliokuwa umejeruhiwa na kutembea umbali wa kilometa 13 hivi hadi kwenye kituo cha reli. Kutoka hapo, nilisafiri kwenda nyumbani kwa gari-moshi, lakini nilipaswa kurudi kambini siku hiyohiyo.

Nilihukumiwa kifungo cha miaka sita kwenye gereza moja huko Budapest. Baada ya kuwasili, nilipata habari kwamba Tibor pia alikuwa gerezani humo. Tulifurahi sana tulipopewa ruhusa ya kuzungumza kwa dakika chache tukiwa tumetenganishwa na ua wa chuma. Sote tulihisi upendo wa Yehova na tuliimarishwa na pindi hizo muhimu. Kabla ya kukutana tena, sote tungepatwa na majaribu makali sana, na kuponea kifo chupuchupu mara kadhaa.

Kutoka Gereza Moja Hadi Lingine

Tulikuwa dada 80 hivi waliosongamana katika seli moja. Tulitamani sana chakula cha kiroho, lakini ilionekana kuwa jambo lisilowezekana kuingiza chochote gerezani. Je, tungeweza kupata chochote ndani ya gereza hilo? Acheni niwaambie tulilofanya. Nilijitolea kurekebisha soksi za makarani wa gereza. Ndani ya soksi moja, niliweka karatasi ambayo niliomba namba ya Biblia katika orodha ya vitabu vya maktaba ya gereza. Ili wasinishuku, niliomba namba za vitabu vingine viwili.

Siku iliyofuata, nilipokea rundo lingine la soksi kutoka kwa makarani. Jibu lilikuwa katika mojawapo ya soksi hizo. Kisha nilimpa mlinzi namba hizo na kumwomba aniletee vitabu hivyo. Tulifurahi wee tulipopata vitabu hivyo, kutia ndani Biblia! Tulibadilisha vitabu hivyo vingine kila juma, lakini tukabaki na Biblia. Mlinzi alipouliza kuhusu Biblia, sikuzote tulimwambia: “Ni kitabu kikubwa, na kila mtu anataka kukisoma.” Hivyo, tuliweza kuisoma Biblia.

Siku moja, ofisa mmoja alinialika ofisini mwake. Alionekana kuwa mpole isivyo kawaida.

“Bi. Haffner, nina habari njema,” akasema. “Unaweza kwenda nyumbani, labda kesho. Ikiwa kutakuwa na gari-moshi, unaweza kwenda hata leo.”

“Nitafurahi sana,” nikajibu.

“Bila shaka,” akasema. “Una mtoto, na nadhani ungependa kumlea.” Kisha akaongeza kusema, “Tia sahihi barua hii tu.”

“Inahusu nini?” nikauliza.

“Usijali kuihusu,” akasisitiza. “Itie sahihi tu, kisha utaachiliwa.” Halafu akaniambia: “Mara tu ufikapo nyumbani, fanya utakalo. Lakini sasa lazima utie sahihi kuonyesha kwamba wewe si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena.”

Nilirudi nyuma na kukataa katakata.

“Basi utafia hapa!” akafoka kwa hasira na kunifukuza.

Mnamo Mei 1943, nilihamishwa na kupelekwa katika gereza lingine huko Budapest na mwishowe nikapelekwa kwenye kijiji cha Márianosztra, ambako tuliishi katika makao ya watawa pamoja na watawa wa kike 70 hivi. Licha ya njaa na magumu mengine, tulikuwa na hamu ya kuwaeleza tumaini letu. Mmoja wa watawa hao wa kike alipendezwa kikweli na ujumbe wetu na kusema: “Hayo ni mafundisho mazuri. Sijawahi kusikia mafundisho kama hayo. Tafadhali nielezeni zaidi.” Tulimweleza kuhusu ulimwengu mpya na jinsi maisha yatakavyokuwa mazuri huko. Tulipokuwa tukizungumza, mtawa aliyesimamia makao hayo akawasili. Mtawa huyo wa kike mwenye kupendezwa alichukuliwa mara moja, akavuliwa nguo, na kupigwa vikali kwa mjeledi. Tulipokutana naye tena, alitusihi hivi: “Tafadhali niombeeni kwa Yehova ili aniokoe na kunitoa hapa. Ningependa kuwa mmoja wenu.”

Kutoka hapo tulipelekwa kwenye gereza moja la zamani huko Komárom, jiji lililo kwenye Mto Danube, karibu kilometa 80 magharibi ya Budapest. Maisha yalikuwa mabaya sana. Sawa na dada wengine wengi, nilikuwa mgonjwa sana kutokana na homa kali inayosababishwa na chawa. Nilitapika damu na kudhoofika sana. Hatukuwa na dawa, na nilifikiri kwamba ningekufa. Lakini maofisa walikuwa wakitafuta mtu wa kufanya kazi ya ofisi. Akina dada walitaja jina langu. Hivyo, nilipewa dawa, na kupata nafuu.

Naungana Tena na Familia Yangu

Jeshi la Sovieti lilipoanza kuingia kutoka mashariki, ilitubidi kuhamia upande wa magharibi. Itachukua muda mrefu kusimulia maafa yote tuliyopata. Nilichungulia kaburi mara kadhaa, lakini niliokoka kwa sababu ya ulinzi wa Yehova. Vita vilipokwisha, tulikuwa katika jiji la Cheki la Tábor, lililo kilometa 80 hivi kutoka Prague. Ilituchukua muda wa zaidi ya majuma matatu kabla mimi na dada-mkwe wangu Magdalena, hatujafika nyumbani huko Lučenec, Mei 30, 1945.

Kutoka mbali ningeweza kumwona mama-mkwe wangu na mwana wangu mpendwa Tibor, kwenye ua. Macho yangu yalijaa machozi, nami nikaita, “Tibike!” Alikimbia na kuruka mikononi mwangu. “Mama, hutaenda tena, sivyo?” Hayo yalikuwa maneno yake ya kwanza aliyoniambia, na sitayasahau kamwe.

Yehova alikuwa mwenye rehema pia kwa mume wangu, Tibor. Alipotoka gerezani Budapest, alipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu huko Bor, pamoja na ndugu wengine wapatao 160. Walichungulia kaburi mara nyingi, lakini waliokoka wakiwa kikundi. Tibor alirudi nyumbani Aprili 8, 1945, karibu mwezi mmoja kabla yangu.

Baada ya vita, bado tulihitaji nguvu za Yehova ili kuvumilia majaribu yote ya miaka 40 chini ya utawala wa Kikomunisti nchini Chekoslovakia. Tibor alihukumiwa tena kifungo kirefu gerezani na ikanibidi kumlea mwana wetu bila yeye. Baada ya kuachiliwa, Tibor alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye. Katika miaka 40 ya Ukomunisti, tulitumia kila nafasi kuwaeleza wengine imani yetu. Tulifanikiwa kuwasaidia wengi kujifunza ukweli. Hivyo wakawa watoto wetu wa kiroho.

Tulifurahi kama nini tulipopata uhuru wa kidini mwaka wa 1989! Mwaka uliofuata tulihudhuria kusanyiko letu la kwanza nchini mwetu baada ya muda mrefu sana. Tulipoona maelfu ya akina ndugu na dada zetu ambao walidumisha utimilifu wao kwa miaka mingi, tulijua kwamba Yehova ndiye aliyewaimarisha ndugu hao wote.

Mume wangu Tibor, alikufa Oktoba 14, 1993, akiwa mwaminifu kwa Mungu, na sasa ninaishi karibu na mwana wangu huko Žilina, Slovakia. Sina nguvu nyingi za kimwili, lakini roho yangu inaimarishwa na nguvu za Yehova. Ninaamini pasipo shaka yoyote kwamba kwa nguvu zake ninaweza kuvumilia jaribu lolote katika mfumo huu wa zamani. Isitoshe, ninatazamia kwa hamu wakati ambapo kwa fadhili zisizostahiliwa za Yehova, nitaweza kuishi milele.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mwana wangu Tibor, Jr., (akiwa na umri wa miaka 4) niliyelazimika kumwacha

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tibor, Sr., pamoja na ndugu wengine huko Bor

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa pamoja na Tibor na Magdalena, dada-mkwe wangu, mwaka wa 1947, huko Brno

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nilichungulia kaburi mara kadhaa, lakini niliokoka kwa sababu ya ulinzi wa Yehova