Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuchoka Lakini Si Kuchoka Kabisa

Kuchoka Lakini Si Kuchoka Kabisa

Kuchoka Lakini Si Kuchoka Kabisa

“Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, . . . anampa nguvu mtu aliyechoka; naye huzijaza nguvu kamili kwa mtu asiye na nguvu zenye msukumo.”—ISAYA 40:28, 29.

1, 2. (a) Ni mwaliko gani wenye kuvutia unaotolewa kwa wote wanaotaka kufuata ibada safi? (b) Ni nini kinachoweza kuhatarisha sana hali yetu ya kiroho?

TUKIWA wanafunzi wa Yesu tunaufahamu vizuri mwaliko wake wenye kuvutia: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. . . . Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30) Pia Wakristo wanapewa “majira ya kuburudisha . . . kutoka kwa uso wa Yehova.” (Matendo 3:19) Bila shaka, umejionea mwenyewe matokeo yenye kuburudisha ya kujifunza kweli za Biblia, kuwa na tumaini zuri la wakati ujao, na kutumia kanuni za Yehova katika maisha yako.

2 Hata hivyo, waabudu fulani wa Yehova hupatwa na uchovu wa kihisia-moyo pindi kwa pindi. Nyakati nyingine, vipindi hivyo vya kuvunjika moyo huwa vifupi. Wakati mwingine vinaweza kudumu kwa muda mrefu. Baada ya muda, huenda wengine wakahisi kwamba madaraka yao ya Kikristo yamekuwa mzigo mzito badala ya mzigo wenye kuburudisha kama alivyoahidi Yesu. Maoni hayo yasiyofaa yanaweza kuhatarisha sana uhusiano wa Mkristo pamoja na Yehova.

3. Kwa nini Yesu alitoa shauri linalopatikana katika Yohana 14:1?

3 Muda mfupi kabla Yesu hajakamatwa na kuuawa, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mioyo yenu isitaabike. Iweni na imani katika Mungu, iweni na imani pia katika mimi.” (Yohana 14:1) Yesu alisema maneno hayo mitume walipokuwa karibu kukabili matukio yenye msiba. Hayo yangefuatwa na mateso. Yesu alijua kwamba mitume wake wangeweza kukwazwa kwa sababu tu ya kuvunjika moyo. (Yohana 16:1) Iwapo huzuni hiyo haingezuiliwa, ingeweza kudhoofisha hali yao ya kiroho na kuwafanya waache kumtumaini Yehova. Ndivyo ilivyo pia kwa Wakristo leo. Kuvunjika moyo kwa muda mrefu kunaweza kusababisha maumivu makali, na mioyo yetu inaweza kulemewa. (Yeremia 8:18) Mtu tuliye kwa ndani anaweza kudhoofika. Chini ya mkazo huo, huenda tukadhoofika kihisia-moyo na kiroho, na hata kupoteza tamaa yetu ya kumwabudu Yehova.

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia kulinda mioyo yetu ya mfano isichoke kabisa?

4 Kwa kweli, shauri hili la Biblia linafaa: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Biblia hutoa shauri linalofaa ambalo hutusaidia kulinda moyo wetu wa mfano kutokana na kuvunjika moyo na uchovu wa kiroho. Hata hivyo, kwanza tunahitaji kutambua waziwazi kisababishi cha uchovu wetu.

Ukristo Haukandamizi

5. Ni jambo gani kuhusu kuwa mwanafunzi Mkristo linaloonekana kuwa lenye kupingana?

5 Ni kweli kwamba kuwa Mkristo hutaka mtu ajitahidi sana. (Luka 13:24) Hata Yesu alisema: “Yeyote yule asiyeuchukua mti wake wa mateso na kunifuata hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:27) Yakichukuliwa kijuujuu tu, huenda maneno hayo yakaonekana kuwa yanapingana na taarifa ya Yesu kuhusu mzigo wake mwepesi na wenye kuburudisha, lakini sivyo.

6, 7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba namna yetu ya ibada haichoshi?

6 Ingawa kazi ngumu na inayohitaji jitihada huuchosha mwili, inaweza kuwa yenye kuridhisha na kuburudisha inapofanywa kwa kusudi zuri. (Mhubiri 3:13, 22) Na kusudi lililo bora zaidi ni kuwaeleza majirani wetu kweli nzuri za Biblia. Pia jitihada yetu ya kuishi kupatana na viwango vya juu vya maadili vya Mungu huwa si kitu inapolinganishwa na manufaa tunayopata. (Methali 2:10-20) Hata tunaponyanyaswa, tunaona hilo kuwa pendeleo kuteseka kwa ajili ya Ufalme wa Mungu.—1 Petro 4:14.

7 Kwa kweli mzigo wa Yesu ni wenye kuburudisha, hasa unapolinganishwa na giza la kiroho la wale walio chini ya nira ya dini ya uwongo. Mungu ana upendo mwororo kutuelekea naye hadai mambo tusiyoweza kutimiza. ‘Amri za Yehova si mzigo mzito.’ (1 Yohana 5:3) Ukristo wa kweli, kama unavyoonyeshwa katika Maandiko, si wenye kukandamiza. Ni wazi kwamba, namna yetu ya ibada haisababishi uchovu na kuvunjika moyo.

‘Ondoa Kila Uzito’

8. Mara nyingi uchovu wa kiroho husababishwa na nini?

8 Mara nyingi uchovu wowote wa kiroho tunaopata hutokana na mzigo wa ziada tunaobebeshwa na mfumo huu mwovu wa mambo. Kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” tunazungukwa na uvutano mbaya ambao unaweza kutuchosha na kufanya tupoteze usawaziko wetu wa Kikristo. (1 Yohana 5:19) Kufuatia mambo yasiyo ya lazima kunaweza kutuvuruga na kufanya iwe vigumu kushikamana kwa ukawaida na utendaji wetu wa Kikristo. Mizigo hiyo ya ziada inaweza kutulemea na hata kutukandamiza. Kwa kufaa, Biblia hutuhimiza ‘tuondoe kila uzito.’—Waebrania 12:1-3.

9. Tunawezaje kulemewa na ufuatiaji wa vitu vya kimwili?

9 Kwa mfano, fikira zetu zinaweza kuathiriwa na maoni ya ulimwengu ya kuhangaikia sana umashuhuri, pesa, vitumbuizo, safari za anasa, na kufuatia vitu vingine vya kimwili. (1 Yohana 2:15-17) Wakristo fulani wa karne ya kwanza waliofuatia utajiri walifanya maisha yao yawe magumu. Mtume Paulo alisema: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

10. Tunaweza kujifunza nini kuhusu utajiri katika mfano wa Yesu wa mpandaji?

10 Tunapohisi uchovu na kuvunjika moyo katika utumishi wetu kwa Mungu, je, inaweza kuwa ni kwa sababu vitu vya kimwili vinaingilia hali yetu ya kiroho? Uwezekano huo ni halisi sana, kama inavyoonyeshwa na mfano wa Yesu wa mpandaji. Yesu alilinganisha “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri na tamaa za mambo yale mengine,” na miiba ambayo ‘hupenya na kuisonga’ mbegu ya neno la Mungu katika mioyo yetu. (Marko 4:18, 19) Kwa hiyo, Biblia inatushauri hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”—Waebrania 13:5.

11. Tunawezaje kuondoa vitu vinavyoweza kutulemea?

11 Nyakati nyingine, maisha yetu hayawi magumu kwa sababu ya kufuatia vitu zaidi vya kimwili, bali kwa sababu ya vitu ambavyo tayari tuko navyo. Wengine wanaweza kuhisi uchovu wa kihisia-moyo kwa sababu ya matatizo mabaya ya afya, kufiwa na wapendwa wao, au matatizo mengine yenye kusikitisha. Mara kwa mara wameona uhitaji wa kufanya marekebisho. Mume fulani na mke wake waliamua kuacha kufuatia baadhi ya mambo waliyopenda na miradi fulani ya kibinafsi isiyo ya lazima. Walichunguza vitu vyao na kupakia vyote ambayo vilihusiana na miradi hiyo kisha wakaviondoa. Pindi kwa pindi, sote tunaweza kunufaika kwa kuchunguza mazoea na mali zetu, huku tukiondoa uzito wote usio wa lazima ili tusichoke na kuzimia katika nafsi zetu.

Ni Muhimu Kuwa na Kiasi na Usawaziko

12. Tunapaswa kutambua nini kuhusu makosa yetu?

12 Makosa yetu, hata katika mambo madogo, yanaweza kufanya maisha yetu yawe magumu hatua kwa hatua. Jinsi maneno haya ya Daudi yalivyo ya kweli: “Makosa yangu yamepita juu ya kichwa changu; kama mzigo mzito, ni mazito sana kwangu.” (Zaburi 38:4) Mara nyingi marekebisho machache yanayofaa yatafanya mizigo yetu isiwe mizito sana.

13. Usawaziko unaweza kutusaidiaje tuwe na maoni yanayofaa kuhusu huduma yetu?

13 Biblia inatutia moyo tusitawishe “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.” (Methali 3:21, 22) Biblia inasema, ‘hekima inayotoka juu ni yenye usawaziko.’ (Yakobo 3:17) Wengine wamehisi mkazo wa kufanya kazi ya huduma ya Kikristo kwa kiwango sawa na cha wenzao. Hata hivyo, Biblia inatushauri: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine. Kwa maana kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:4, 5) Ni kweli kwamba vielelezo vizuri vya Wakristo wenzetu, vinaweza kututia moyo tumtumikie Yehova kwa moyo wote, lakini hekima inayotumika na usawaziko vitatusaidia kuweka miradi tunayoweza kuifikia kulingana na hali zetu.

14, 15. Tunawezaje kuonyesha hekima inayotumika tunaposhughulikia mahitaji yetu ya kimwili na ya kihisia-moyo?

14 Tunaweza kuepuka uchovu kwa kuwa na usawaziko hata katika hali zisizoonekana kuwa muhimu. Kwa mfano, je, tunasitawisha mazoea yaliyosawazika ambayo huchangia afya nzuri? Fikiria kielelezo cha mume fulani na mke wake wanaotumikia katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Wameona manufaa ya hekima inayotumika katika kuzuia uchovu. Mke anasema: “Hata tuwe na kazi nyingi namna gani, sisi hujaribu kulala wakati uleule kila siku. Pia tunafanya mazoezi kwa ukawaida. Hilo limetusaidia kwelikweli. Tumejua sehemu ambazo tumepungukiwa, nasi hufanya mambo kupatana na hali hizo. Sisi huepuka kujilinganisha na wale wanaoonekana kuwa na nguvu daima.” Je, sisi hula vyakula vinavyofaa kwa ukawadia na kupata pumziko la kutosha? Kwa ujumla, kuhangaikia afya yetu kwa kiasi kunaweza kupunguza uchovu wa kihisia-moyo na wa kiroho.

15 Wengine wetu tuna mahitaji ya kipekee. Kwa mfano, dada mmoja Mkristo amefanya migawo migumu kadhaa katika utumishi wa wakati wote. Amekuwa na matatizo mabaya ya afya, kutia ndani kansa. Ni nini humsaidia kukabiliana na mikazo? Anasema: “Mimi huona ni muhimu kutafuta pindi ambazo ninaweza kuwa peke yangu ili kufurahia hali yenye utulivu kabisa. Kadiri ninavyohisi mkazo na uchovu ukiongezeka, ndivyo nionavyo umuhimu wa kuwa na pindi zenye utulivu ambapo ninaweza kusoma na kupumzika.” Hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri hutusaidia kutambua na kutosheleza mahitaji yetu na hivyo kuepuka uchovu wa kiroho.

Yehova Mungu Hututia Nguvu

16, 17. (a) Kwa nini ni muhimu sana kutunza afya yetu ya kiroho? (b) Ratiba yetu ya kila siku inapaswa kutia ndani nini?

16 Bila shaka, ni muhimu sana kutunza afya yetu ya kiroho. Tunapokuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova Mungu, huenda tukachoka kimwili, lakini hatutachoka kamwe kumwabudu. Yehova ndiye ‘humpa nguvu mtu aliyechoka; naye huzijaza nguvu kamili kwa mtu asiye na nguvu zenye msukumo.’ (Isaya 40:28, 29) Mtume Paulo ambaye alijionea ukweli wa maneno hayo, aliandika: “Hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku.”—2 Wakorintho 4:16.

17 Ona maneno “siku baada ya siku.” Hayo yanamaanisha kutumia maandalizi ya Yehova kila siku. Mmishonari mmoja aliyetumikia kwa uaminifu kwa miaka 43, alilazimika kukabili pindi za uchovu wa kimwili na kuvunjika moyo. Lakini hakuchoka kabisa. Anasema: “Nimezoea kuamka asubuhi ili kabla sijaanza kazi yoyote, niweze kutumia wakati kusali kwa Yehova na kusoma Neno lake. Kufanya hivyo kila siku kumenisaidia nivumilie hadi sasa.” Kwa kweli, tunaweza kutegemea nguvu za Yehova zinazotuimarisha ikiwa tunasali kwake kwa ukawaida, naam, “siku baada ya siku,” na kutafakari sifa zake kuu na ahadi zake.

18. Biblia hutoa faraja gani kwa waaminifu walio wazee au walio wagonjwa?

18 Hilo ni muhimu sana hasa kwa wale wanaohisi wamevunjika moyo kwa sababu ya uzee na afya mbaya. Watu hao wanaweza kuvunjika moyo, si kwa sababu ya kujilinganisha na wengine, bali kwa sababu ya kulinganisha yale wanayoweza kufanya sasa na yale waliyoweza kufanya zamani. Kwa kweli, inafariji kujua kwamba Yehova anawaheshimu walio wazee! Biblia inasema: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Methali 16:31) Yehova anajua kupungukiwa kwetu naye anathamini sana ibada tunayomtolea kwa moyo wote licha ya udhaifu wetu. Naye Mungu atakumbuka daima kazi nzuri ambazo tumefanya. Maandiko hutuhakikishia hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.” (Waebrania 6:10) Sote tunafurahi kama nini kuwa pamoja na wale ambao wamekuwa washikamanifu kwa Yehova kwa miaka mingi!

Usife Moyo

19. Tunanufaikaje kwa kuendelea kufanya yaliyo mema?

19 Wengi wanaamini kwamba kufanya mazoezi makali ya kimwili kwa ukawaida kunaweza kupunguza uchovu. Vivyo hivyo, utendaji wa kiroho unaweza kutusaidia kupunguza uchovu wa kihisia-moyo au wa kiroho. Biblia inasema: “Na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa. Kwa kweli, basi, tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:9, 10) Ona maneno “kufanya yaliyo mema” na ‘kutenda mema.’ Maneno hayo yanadokeza kwamba tunapaswa kuchukua hatua. Kwa kweli, kuwafanyia wengine mema kunaweza kuzuia tusichoke kabisa kumtumikia Yehova.

20. Ili kupigana na kuvunjika moyo, tunapaswa kuepuka kushirikiana na watu gani?

20 Tofauti na hilo, kushirikiana na kufanya kazi pamoja na watu wanaopuuza sheria za Mungu kunaweza kuwa mzigo wenye kuchosha. Biblia hutuonya hivi: “Uzito wa jiwe na mzigo wa mchanga—lakini usumbufu wa mpumbavu ni mzito kuliko vyote viwili.” (Methali 27:3) Ili kupigana na hisia za kuvunjika moyo na uchovu, tunapaswa kuepuka kushirikiana na wale walio na maoni yasiyofaa na ambao wana mwelekeo wa kutafuta makosa na kuwachambua wengine.

21. Tunawezaje kuwatia moyo wengine kwenye mikutano ya Kikristo?

21 Mikutano ya Kikristo ni uandalizi kutoka kwa Yehova ambao unaweza kutujaza nguvu za kiroho. Tukiwa huko tuna nafasi bora za kutiana moyo kupitia mafundisho na ushirika wenye kuburudisha. (Waebrania 10:25) Wote kutanikoni wanapaswa kujitahidi kuwa wenye kujenga wanapotoa maelezo kwenye mikutano au wanapokuwa na sehemu katika programu. Wale wanaoongoza wakiwa walimu, hasa wana daraka la kuwatia wengine moyo. (Isaya 32:1, 2) Hata inapokuwa lazima kuhimiza au kukaripia, shauri linapaswa kutolewa kwa njia yenye kuburudisha. (Wagalatia 6:1, 2) Kwa kweli, kuwapenda wengine kutatusaidia tumtumikie Yehova bila kuchoka kabisa.—Zaburi 133:1; Yohana 13:35.

22. Licha ya hali yetu ya kutokamilika, kwa nini tunaweza kuwa hodari?

22 Kumwabudu Yehova wakati huu wa mwisho kunahusisha kazi. Na Wakristo pia hupatwa na matokeo ya uchovu wa kiakili, maumivu ya kihisia-moyo, na hali zenye mikazo. Hali yetu ya kutokamilika ni dhaifu, kama chombo cha udongo. Hata hivyo, Biblia inasema: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Naam, tutachoka, lakini acheni tusichoke kabisa au kukata tamaa kamwe. Badala yake, acheni tuwe “hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu.’”—Waebrania 13:6.

Pitio Fupi

• Ni baadhi ya mizigo gani mizito tunayoweza kuondoa?

• Tunawezaje kushiriki katika ‘kuwatendea mema’ Wakristo wenzetu?

• Yehova hututegemezaje tunapohisi uchovu au kuvunjika moyo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alijua kwamba kuvunjika moyo kwa muda mrefu kungeweza kuwafadhaisha mitume

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wengine wameacha kufuatia mambo wanayopenda na miradi ya kibinafsi isiyo ya lazima

[Picha katika ukurasa wa 26]

Licha ya kupungukiwa kwetu Yehova huthamini sana ibada tunayomtolea kwa moyo wote