Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Msafiri Jasiri wa Kueneza Injili’

‘Msafiri Jasiri wa Kueneza Injili’

‘Msafiri Jasiri wa Kueneza Injili’

INASEMEKANA kwamba kufikia umri wa miaka 18, George Borrow alikuwa amejua lugha 12. Miaka miwili baadaye angeweza “kutafsiri vizuri na kwa urahisi” lugha 20.

Mnamo 1833, mtu huyo aliyekuwa na kipawa cha pekee alialikwa ili ahojiwe na Chama cha Biblia cha Uingereza na Nchi za Kigeni, huko London, Uingereza. Kwa kuwa alitaka kutumia nafasi hiyo nzuri na hakuwa na pesa za kugharimia safari hiyo, Borrow aliyekuwa na umri wa miaka 30 alitembea kilometa 180 kutoka nyumbani kwake huko Norwich, kwa muda wa saa 28 tu.

Chama hicho cha Biblia kilimpa kazi ngumu. Kilimpa miezi sita tu kujifunza lugha ya Manchu iliyotumiwa sehemu fulani nchini China. Aliomba kitabu cha sarufi, lakini wakampa nakala ya Injili ya Mathayo katika Kimanchu na kamusi ya Kimanchu na Kifaransa. Hata hivyo, baada ya majuma 19 aliandikia chama hicho barua na kusema, “Nimekijua Kimanchu vizuri” kwa “msaada wa Mungu.” Hilo lilikuwa jambo la pekee hasa kwa sababu wakati huohuo yasemekana Borrow alikuwa akisahihisha Injili ya Luka katika lugha ya Nahuatl, mojawapo ya lugha za wenyeji wa Mexico.

Biblia Katika Kimanchu

Serikali ya China ilianza kutumia Kimanchu katika miaka ya 1600, wakati lugha hiyo ilipoanza kuandikwa kwa kutumia hati iliyokuwa na alfabeti za lugha ya Uighur ya Mongolia. Ingawa mwishowe lugha hiyo iliacha kutumiwa sana, washiriki wa Chama cha Biblia cha Uingereza na Nchi za Kigeni walikuwa na hamu ya kuchapa na kugawanya Biblia katika Kimanchu. Kufikia mwaka wa 1822, walikuwa wamegharimia uchapishaji wa nakala 550 za Injili ya Mathayo, iliyotafsiriwa na Stepan Lipoftsoff wa Tano. Alikuwa mshiriki wa Ofisi ya Mambo ya Nje ya Urusi, aliyekuwa ameishi China kwa miaka 20. Injili hiyo ya Mathayo ilichapishwa huko St. Petersburg, lakini baada ya nakala chache tu kugawanywa, mafuriko yakaharibu zile zilizosalia.

Baada ya muda mfupi, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalitafsiriwa. Mnamo 1834, Biblia ilianza kuvutia zaidi baada ya kupatikana kwa hati ya zamani yenye Maandiko mengi ya Kiebrania. Ni nani angeweza kusimamia kusahihishwa kwa Biblia ya Kimanchu iliyokuwapo na kumaliza kuitafsiri? Washiriki wa Chama cha Biblia cha Uingereza na Nchi za Kigeni walimtuma George Borrow akawafanyie kazi hiyo.

Aenda Urusi

Alipofika St. Petersburg, Borrow alianza kujifunza Kimanchu kwa undani zaidi ili aweze kusahihisha na kuhariri maandishi ya Biblia kwa usahihi zaidi. Hata hivyo, hiyo ilikuwa kazi ngumu sana, naye aliifanya kwa saa 13 kwa siku, akisaidia kupanga herufi za kuchapa tafsiri ya Agano Jipya, ambayo baadaye ilitajwa kuwa “chapa nzuri ya nchi za mashariki.” Nakala elfu moja zilichapwa mwaka wa 1835. Lakini mpango wa Borrow wa kupeleka nakala hizo huko China na kuzigawanya ulizuiwa. Serikali ya Urusi ilimkataza Borrow kwenda kwenye mpaka wa China iwapo angebeba “hata Biblia moja ya Kimanchu,” kwa kuhofia kwamba kugawanywa kwa Biblia hizo kungeonekana kuwa kazi ya umishonari ambayo ingehatarisha uhusiano mzuri kati ya Urusi na China.

Nakala chache ziligawanywa miaka kumi hivi baadaye, nazo tafsiri za Injili ya Mathayo na Marko, zilizokuwa na safu za Kimanchu na Kichina, zikatolewa mwaka wa 1859. Hata hivyo, kufikia wakati huo, watu wengi ambao wangeweza kusoma Kimanchu walipendelea kusoma Kichina, na matarajio ya kuwa na Biblia nzima katika Kimanchu yakaanza kudidimia. Lugha ya Manchu ilikuwa inatoweka, na muda si muda Kichina kingechukua mahali pake. Badiliko hilo lilikamilika kufikia mwaka wa 1912, wakati China ilipokuwa jamhuri.

Peninsula ya Iberia

Kwa kuchochewa na mambo aliyojionea, George Borrow alirudi London. Alipewa mgawo mwingine wa kwenda Ureno na Hispania mwaka wa 1835, “ili akachunguze ni kwa kadiri gani watu walikuwa tayari kupokea kweli za Kikristo,” kama alivyosema baadaye. Wakati huo, Chama cha Biblia cha Uingereza na Nchi za Kigeni hakikuwa kimeshughulika sana na nchi hizo mbili. Borrow alifurahia kuzungumzia Biblia pamoja na Wareno wa mashambani, lakini baada ya muda mfupi, ubaridi na chuki ya kidini aliyokabili huko ikamfanya aondoke Ureno na kwenda Hispania.

Kulikuwa na jambo jingine gumu nchini Hispania, hasa kuhusiana na jamii ya Wahamaji ambao, baada ya muda mfupi, Borrow alianzisha uhusiano wa karibu nao kwa kuwa angeweza kuzungumza lugha yao iitwayo Gitano. Punde baada ya kuwasili, Borrow alianza kutafsiri “Agano Jipya” katika lugha ya jamii hiyo ya Gitano ya Hispania. Aliwaalika wanawake wawili wa jamii hiyo wamsaidie katika sehemu fulani ya kazi hiyo. Angewasomea tafsiri ya Kihispania kisha kuwaomba wamtafsirie. Kwa njia hiyo aliweza kujifunza matumizi sahihi ya semi za lugha ya jamii hiyo. Kwa sababu ya jitihada hiyo, Injili ya Luka ilichapishwa mwaka wa 1838, jambo lililomchochea askofu mmoja kusema: “Atageuza imani ya Wahispania wote kupitia lugha ya Gitano.”

George Borrow aliidhinishwa kutafuta “mtu mwenye uwezo wa kutafsiri Biblia katika lugha ya Basque.” Kazi hiyo ilipewa Oteiza, daktari “anayejua lugha hiyo vizuri, na ambayo hata mimi ninaijua kwa kadiri fulani,” akaandika Borrow. Mnamo 1838, Injili ya Luka ikawa kitabu cha kwanza cha Biblia kutafsiriwa katika lugha ya Basque ya Hispania.

Akichochewa na tamaa yake ya kuwaelimisha watu wa kawaida, Borrow alifunga safari ndefu, ambazo mara nyingi zilikuwa hatari, ili kugawanya vitabu vya Biblia kati ya watu maskini wa mashambani. Alitaka kuwaweka huru kutoka katika ushirikina na ujinga wa kidini. Kwa mfano, ili kuonyesha kwamba vyeti vya msamaha walivyokuwa wakinunua havikuwa na maana yoyote, angesema hivi: “Je, inawezekana kwamba Mungu, ambaye ni mzuri, akubali kununuliwa kwa msamaha wa dhambi?” Lakini washiriki wa Chama cha Biblia walihofia kwamba shambulio hilo juu ya mafundisho ya kidini lingefanya kazi yao ipigwe marufuku, hivyo wakamwagiza ashughulike tu na ugawanyaji wa Biblia.

Borrow alipewa ruhusa kwa mdomo achape El Nuevo Testamento, Agano Jipya katika Kihispania, bila maandishi yanayoeleza kuhusu dini ya Katoliki. Alipewa ruhusa hiyo licha ya kupingwa mwanzoni na waziri mkuu, aliyesema kwamba tafsiri hiyo ni “kitabu kisichofaa” na hatari. Wakati huo Borrow alianzisha kituo cha kuweka Biblia huko Madrid ili kuuza Agano Jipya katika Kihispania. Hatua hiyo ilifanya akosane na viongozi wa kidini na wa serikali na kufungwa gerezani kwa siku 12. Alipopinga kifungo hicho, Borrow aliombwa aondoke kimya-kimya. Kwa kuwa alijua vizuri kwamba alikuwa amefungwa kinyume cha sheria, alitaja mfano wa mtume Paulo, naye akaamua kubaki gerezani hadi ionyeshwe wazi kwamba hakuwa na hatia, na kwamba jina lake lilistahili kuheshimiwa.—Matendo 16:37.

Kufikia wakati mjumbe wao mwenye bidii alipoondoka Hispania mwaka wa 1840, Chama cha Biblia kingeweza kusema hivi: “Karibu nakala 14,000 za Biblia zimegawanywa nchini Hispania katika miaka mitano iliyopita.” Akiwa ametimiza sehemu kuu kuhusiana na hilo, Borrow alisema kwa ufupi kwamba kipindi alichokuwa nchini Hispania ndicho ‘kilichokuwa chenye furaha zaidi katika maisha yake.’

Katika kitabu The Bible in Spain, kilichochapishwa mara ya kwanza mwaka wa 1842—na bado kinachapishwa—Borrow anasimulia kinaganaga safari zake na mambo yaliyompata. Katika kitabu hicho, ambacho kilifanikiwa sana, Borrow alijiita “msafiri wa kueneza Injili.” Aliandika: “Nilinuia kutembelea maeneo yaliyojificha na yaliyo mbali kwenye vilima na milima yenye mawemawe, ili kuzungumza na watu kama vile Kristo alivyofanya.”

Kwa kugawanya na kutafsiri Biblia kwa bidii, George Borrow aliwawekea wengine msingi wa kuigawanya na kuitafsiri Biblia. Hiyo lilikuwa heshima kubwa kama nini!

[Ramani katika ukurasa wa 29]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Katika jitihada zake za kutafsiri na kuigawanya Biblia, George Borrow alisafiri kutoka (1) Uingereza hadi  (2) Urusi, (3) Ureno, na (4) Hispania

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Maneno ya utangulizi ya Injili ya Yohana katika Kimanchu, iliyochapishwa 1835, ambayo yanaanzia juu kwenda chini, nayo husomwa kutoka kushoto kwenda kulia

[Hisani]

From the book The Bible of Every Land, 1860

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 27]

From the book The Life of George Borrow by Clement K. Shorter, 1919