Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanachukiwa Bila Sababu

Wanachukiwa Bila Sababu

Wanachukiwa Bila Sababu

“Walinichukia bila sababu.”—YOHANA 15:25.

1, 2. (a) Kwa nini wengine hushangaa Wakristo wanaposemwa vibaya, lakini kwa nini hatupaswi kushangazwa na jambo hilo? (b) Tutachunguza maana gani ya neno “chuki” katika makala hii? (Ona maelezo ya chini.)

MASHAHIDI WA YEHOVA hujitahidi kuishi kupatana na kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu. Kwa sababu hiyo, wana sifa nzuri katika nchi nyingi. Hata hivyo, nyakati nyingine, wameeleweka vibaya. Kwa mfano, ofisa mmoja wa serikali katika jiji la St. Petersburg, Urusi, alikumbuka: “Tulielezwa kwamba Mashahidi wa Yehova ni madhehebu fulani ambayo wafuasi wake huketi kwa siri na kuua watoto wao na kujiua wenyewe.” Lakini baada ya kufanya kazi pamoja na Mashahidi wa Yehova kuhusiana na kusanyiko fulani la kimataifa, ofisa huyohuyo alisema: “Sasa ninawaona kuwa watu wa kawaida wenye kutabasamu . . . Ni wenye amani na watulivu, nao wanapendana sana.” Aliongeza: “Kwa kweli sielewi kwa nini watu husema uwongo kama huo kuwahusu.”—1 Petro 3:16.

2 Watumishi wa Mungu hawafurahi wanaposingiziwa kuwa watenda-maovu, lakini hawashangai watu wanaposema vibaya juu yao. Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Ikiwa ulimwengu unawachukia ninyi, mnajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. . . . Ni ili neno lililoandikwa katika Sheria yao lipate kutimizwa, ‘Walinichukia bila sababu.’” * (Yohana 15:18-20, 25; Zaburi 35:19; 69:4) Mapema zaidi aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ikiwa watu wamemwita mwenye nyumba Beelzebuli, je, hawatawaita hivyo wale watu wa nyumbani mwake hata zaidi?” (Mathayo 10:25) Wakristo wanaelewa kwamba kuvumilia shutuma hiyo ni sehemu ya ule ‘mti wa mateso’ walioukubali walipopata kuwa wafuasi wa Kristo.—Mathayo 16:24.

3. Waabudu wa kweli wameteswa kwa kadiri gani?

3 Waabudu wa kweli wamekuwa wakiteswa tangu zamani, kuanzia wakati wa “Abeli mwadilifu.” (Mathayo 23:34, 35) Kumekuwa na visa vingi sana kuhusu kuteswa kwa waabudu wa kweli. Yesu alisema kwamba wafuasi wake ‘wangechukiwa na watu wote’ kwa sababu ya jina lake. (Mathayo 10:22) Isitoshe, mtume Paulo aliandika kwamba watumishi wote wa Mungu—kutia ndani sisi sote—tunapaswa kutarajia mateso. (2 Timotheo 3:12) Kwa sababu gani?

Chanzo cha Chuki Isiyo na Msingi

4. Biblia hufunuaje chanzo cha chuki yote isiyo na msingi?

4 Neno la Mungu linafunua kwamba tangu mwanzo, mtu fulani asiyeonekana amekuwa akichochea chuki hiyo. Fikiria jinsi Abeli, mtu wa kwanza mwenye imani alivyouawa kikatili. Biblia inasema kwamba Kaini, muuaji aliyekuwa ndugu yake Abeli, ‘alitokana na yule mwovu,’ Shetani Ibilisi. (1 Yohana 3:12) Kaini alionyesha mtazamo wa Shetani, naye Ibilisi akamtumia kutimiza mipango yake miovu. Pia, Biblia hufunua daraka la Shetani kuhusiana na mashambulizi makali yaliyofanywa dhidi ya Ayubu na Yesu Kristo. (Ayubu 1:12; 2:6, 7; Yohana 8:37, 44; 13:27) Kitabu cha Ufunuo kinataja waziwazi chanzo cha mateso yanayowapata wafuasi wa Yesu, kikisema: “Ibilisi ataendelea kuwatupa gerezani baadhi yenu ili mjaribiwe kwa ukamili.” (Ufunuo 2:10) Naam, Shetani ndiye chanzo cha chuki yote isiyo na msingi dhidi ya watu wa Mungu.

5. Kwa nini Shetani anawachukia waabudu wa kweli?

5 Kwa nini Shetani anawachukia waabudu wa kweli? Katika njama inayoonyesha majivuno makuu, Shetani anampinga “Mfalme wa umilele,” Yehova Mungu. (1 Timotheo 1:17; 3:6) Anadai kwamba Mungu hutawala viumbe wake kwa kuwawekea vizuizi vingi sana, na kwamba hakuna anayemtumikia Yehova kwa nia safi, kwamba watu humtumikia tu ili kujifaidi. Shetani anadai kwamba akiruhusiwa awajaribu wanadamu, anaweza kugeuza kila mmoja wao asimtumikie Mungu. (Mwanzo 3:1-6; Ayubu 1:6-12; 2:1-7) Kwa kumchongea Yehova kwamba alishindwa, na kwamba yeye ni mkandamizaji na mwongo, Shetani hujaribu kujifanya kuwa ana haki kama ya Yehova ya kuutawala ulimwengu wote. Kwa hiyo, hasira yake dhidi ya watumishi wa Mungu huchochewa na tamaa yake ya kuabudiwa.—Mathayo 4:8, 9.

6. (a) Tunahusikaje kibinafsi katika suala la enzi kuu ya Yehova? (b) Kuelewa suala hilo hutusaidiaje tudumishe utimilifu? (Ona sanduku, ukurasa wa 16.)

6 Je, unaona jinsi suala hilo linavyohusu maisha yako? Ukiwa mtumishi wa Yehova, yaelekea umeona kwamba ingawa kufanya mapenzi ya Mungu kunahitaji jitihada, kuna manufaa nyingi sana ya kufanya hivyo. Hata hivyo, namna gani ikiwa hali zako za maisha zinafanya iwe vigumu, au hata liwe jambo lenye kuumiza kuendelea kujipatanisha na sheria na kanuni za Yehova? Namna gani ikiwa inaonekana kwamba hupati manufaa yoyote kwa kumtumikia? Je, ungekata kauli kwamba hakuna haja ya kumtumikia Yehova? Au je, upendo wako kwa Yehova na kuthamini sana sifa zake zenye kutokeza kutakuchochea uendelee kutembea katika njia zake? (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Kwa kumruhusu Shetani atuletee magumu fulani, Yehova amempa kila mmoja wetu nafasi ya kutoa jibu kwa dai la Shetani.—Methali 27:11.

“Watu Wanapowashutumu”

7. Ibilisi hutumia mbinu gani ili kujaribu kutugeuza tusimtumikie Yehova?

7 Sasa na tuchunguze kwa makini zaidi mojawapo ya matendo ya hila ambayo Shetani hutumia katika jitihada ya kuthibitisha madai yake dhidi ya Yehova na watumishi wake, yaani, shutuma za uwongo. Yesu alimwita Shetani “baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Jina Ibilisi, linalofafanuliwa kuwa “Mchongezi,” humtambulisha kuwa mchongezi mkuu zaidi wa Mungu, neno lake zuri, na jina lake takatifu. Ibilisi hutumia masingizio, mashtaka ya uwongo, na uwongo wa moja kwa moja ili kupinga enzi kuu ya Yehova, naye hutumia mbinu hizohizo kuchongea watumishi washikamanifu wa Mungu. Kwa kuwashutumu Mashahidi hao, anaweza kufanya iwe vigumu zaidi kwao kuvumilia jaribu kali.

8. Shetani alimshutumu Ayubu jinsi gani, na matokeo yakawaje?

8 Fikiria mambo yaliyompata Ayubu, ambaye jina lake humaanisha “Kitu cha Kuchukiwa.” Mbali na kumpotezea Ayubu riziki, watoto wake, na afya yake, Shetani alifanya Ayubu aonekana kuwa mtenda-dhambi aliyekuwa akiadhibiwa na Mungu. Ingawa alikuwa anaheshimiwa sana hapo awali, Ayubu alichukiwa hata na jamaa zake na marafiki wa karibu. (Ayubu 19:13-19; 29:1, 2, 7-11) Isitoshe, kwa kutumia wafariji wa uwongo, Shetani alijaribu ‘kumponda Ayubu kwa maneno,’ kwanza kwa kusingizia kwamba lazima awe alitenda dhambi fulani nzito kisha kumshutumu moja kwa moja kuwa mkosaji. (Ayubu 4:6-9; 19:2; 22:5-10) Hilo lingekuwa jambo lenye kumvunja moyo Ayubu kama nini!

9. Yesu alifanywaje aonekane kuwa mtenda-dhambi?

9 Akiwa mteteaji mkuu zaidi wa enzi kuu ya Yehova, Mwana wa Mungu alipata kuwa mtu aliyechukiwa zaidi na Shetani. Yesu alipokuja duniani, Shetani alijaribu kumharibia sifa zake za kiroho kama alivyojaribu kufanya kuelekea Ayubu, na kumfanya Yesu aonekane kuwa mtenda-dhambi. (Isaya 53:2-4; Yohana 9:24) Watu walimwita Yesu mlevi na mlafi na kusema kwamba ‘alikuwa na roho mwovu.’ (Mathayo 11:18, 19; Yohana 7:20; 8:48; 10:20) Alishtakiwa kwa uwongo kwamba alikufuru. (Mathayo 9:2, 3; 26:63-66; Yohana 10:33-36) Yesu alisononeshwa na jambo hilo kwa kuwa alijua kwamba lilimletea Baba yake suto isivyo haki. (Luka 22:41-44) Mwishowe, Yesu alitundikwa mtini kama mhalifu aliyelaaniwa. (Mathayo 27:38-44) Kwa kudumisha utimilifu kikamili, Yesu alivumilia ‘maneno mengi yaliyo kinyume yaliyotolewa na watenda-dhambi.’—Waebrania 12:2, 3.

10. Mabaki ya watiwa-mafuta wamekuwaje shabaha ya Shetani katika nyakati hizi?

10 Vivyo hivyo, nyakati hizi, mabaki ya wafuasi watiwa-mafuta Wakristo wanachukiwa na Ibilisi. Shetani anatajwa kuwa ‘mshtaki wa ndugu za Kristo, anayewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu.’ (Ufunuo 12:9, 10) Tangu alipofukuzwa kutoka mbinguni na kutupwa kwenye ujirani wa dunia, Shetani amezidisha jitihada zake za kufanya ndugu za Kristo waonekane kuwa watu waliotengwa na kudharauliwa. (1 Wakorintho 4:13) Katika nchi fulani, wamechongewa kwa kuitwa madhehebu hatari, kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza. (Matendo 24:5, 14; 28:22) Kama ilivyotajwa mwanzoni, wamesingiziwa kwa kutumia propaganda za uwongo. Hata hivyo, “kupitia utukufu na aibu, kupitia habari ambazo ni mbaya na habari ambazo ni njema,” ndugu watiwa-mafuta wa Kristo, wakiungwa mkono na “kondoo wengine” wamejitahidi kwa unyenyekevu ‘kushika amri za Mungu na kufanya kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.’—2 Wakorintho 6:8; Yohana 10:16; Ufunuo 12:17.

11, 12. (a) Huenda shutuma inayowapata Wakristo inasababishwa na nini? (b) Mkristo anaweza kuteseka isivyo haki kwa ajili ya imani yake katika njia zipi?

11 Bila shaka, watumishi wa Mungu hawashutumiwi “kwa ajili wa uadilifu” tu. (Mathayo 5:10) Huenda matatizo mengine yakatokana na hali yetu ya kutokamilika. Hatupati sifa yoyote ya pekee ikiwa ‘tunapofanya dhambi na kupigwa makofi, tunavumilia.’ Hata hivyo, ikiwa Mkristo “kwa sababu ya dhamiri kwa Mungu, anavumilia chini ya mambo yenye kuhuzunisha naye anateseka isivyo haki, jambo hilo ni lenye kukubalika” machoni pa Yehova. (1 Petro 2:19, 20) Hilo linaweza kutokea chini ya hali gani?

12 Wengine wametendewa vibaya kwa sababu ya kukataa kushiriki desturi za mazishi zisizopatana na Maandiko. (Kumbukumbu la Torati 14:1) Vijana Mashahidi wamekuwa wakitukanwa kwa sababu ya kushikamana na viwango vya maadili vya Yehova. (1 Petro 4:4) Wazazi fulani Wakristo wameshtakiwa kimakosa kuwa “wasiojali” au “wanaowatendea vibaya” watoto wao kwa sababu ya kutafuta matibabu yasiyohusisha damu. (Matendo 15:29) Wakristo wametengwa na jamaa zao na majirani kwa sababu tu ya kuwa watumishi wa Yehova. (Mathayo 10:34-37) Watu hao wote wanafuata kielelezo cha manabii na cha Yesu mwenyewe kwa kuteseka isivyo haki.—Mathayo 5:11, 12; Yakobo 5:10; 1 Petro 2:21.

Kuvumilia Shutuma

13. Ni nini kinachoweza kutusaidia tudumishe usawaziko wetu wa kiroho tunapokabili shutuma kali?

13 Tunaposhutumiwa vikali kwa ajili ya imani yetu, huenda tukavunjika moyo kama nabii Yeremia, na kuhisi kwamba hatuwezi kuendelea kumtumikia Mungu. (Yeremia 20:7-9) Ni nini kinachoweza kutusaidia kudumisha usawaziko wetu wa kiroho? Jaribu kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Yeye huwaona wale wanaodumisha ushikamanifu chini ya jaribu kuwa washindi, wala si waathiriwa. (Waroma 8:37) Jaribu kuwazia wale waliotetea enzi kuu ya Yehova licha ya aibu ya kila namna ambayo Ibilisi angeweza kuwasababishia—wanawake na wanaume kama Abeli, Ayubu, Maria, mama ya Yesu, na watumishi wengine waaminifu wa zamani na vilevile watumishi wenzetu wa nyakati hizi. (Waebrania 11:35-37; 12:1) Tafakari jinsi walivyodumisha utimilifu wao. Wingu hilo kubwa la washikamanifu linatualika tujiunge nalo kwenye jukwaa la ushindi ambalo limehifadhiwa kwa ajili ya wale wanaoushinda ulimwengu kwa imani yao.—1 Yohana 5:4.

14. Kusali kwa bidii kunaweza kutuimarishaje tudumishe uaminifu?

14 ‘Fikira zinazotufadhaisha zikiwa nyingi ndani yetu,’ tunaweza kusali kwa Yehova kwa bidii, naye atatufariji na kutuimarisha. (Zaburi 50:15; 94:19) Atatupa hekima tunayohitaji ili kukabiliana na jaribu hilo na kutusaidia tukazie fikira suala kuu—enzi kuu ya Yehova—ambalo ndilo kisababishi cha chuki isiyo na msingi dhidi ya watumishi wake. (Yakobo 1:5) Pia Yehova anaweza kutupa “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani hiyo tunayopewa na Mungu hutusaidia kudumisha utulivu na kubaki imara tunapokabiliana na mikazo mikali sana, bila kushindwa na shaka au woga. Kupitia roho yake, Yehova anaweza kututegemeza tuvumilie hali yoyote anayoruhusu itupate.—1 Wakorintho 10:13.

15. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusiwe na kinyongo tunapoteseka?

15 Ni nini kinachoweza kutusaidia tusiwe na kinyongo kuelekea wale wanaotuchukia bila sababu? Kumbuka kwamba Shetani na roho waovu ndio maadui wetu wakuu. (Waefeso 6:12) Ingawa watu fulani hututesa kimakusudi, wengi wanaowapinga watu wa Mungu hufanya hivyo kwa kutojua au kwa kutumiwa vibaya na wengine. (Danieli 6:4-16; 1 Timotheo 1:12, 13) Yehova anataka “watu wa namna zote” wapate nafasi ya ‘kuokolewa na kupata ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Timotheo 2:4) Kwa kweli, watu fulani waliokuwa wapinzani sasa wamekuwa ndugu zetu Wakristo kwa sababu ya kutazama mwenendo wetu usiolaumika. (1 Petro 2:12) Zaidi ya hayo, tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na kielelezo cha Yosefu mwana wa Yakobo. Ingawa Yosefu aliteseka sana kwa sababu ya ndugu zake wa kambo, hakuwawekea kinyongo. Kwa nini? Kwa sababu alitambua kwamba Yehova alihusika katika jambo hilo na kuelekeza mambo ili kutimiza kusudi Lake. (Mwanzo 45:4-8) Vivyo hivyo, Yehova anaweza kutumia mateso yoyote ambayo huenda tukapata isivyo haki ili kulitukuza jina lake.—1 Petro 4:16.

16, 17. Kwa nini hatupaswi kuhangaika isivyofaa kuhusu jitihada za wapinzani za kuzuia kazi ya kuhubiri?

16 Hatupaswi kuhangaika isivyofaa ikiwa kwa wakati fulani inaonekana kwamba wapinzani wanafaulu kuzuia habari njema zisiendelee kutangazwa. Yehova sasa anayatikisa mataifa kupitia ushahidi unaotolewa duniani pote, navyo vitu vyenye kutamanika vinaingia. (Hagai 2:7) Kristo Yesu, Mchungaji Mwema, alisema: “Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata. Nami ninawapa hao uzima wa milele, . . . wala hakuna atakayewanyakua kutoka mkononi mwangu.” (Yohana 10:27-29) Malaika watakatifu pia wanashiriki katika mavuno hayo makubwa ya kiroho. (Mathayo 13:39, 41; Ufunuo 14:6, 7) Kwa hiyo, hakuna chochote ambacho wapinzani husema au kufanya kinachoweza kuzuia kusudi la Mungu.—Isaya 54:17; Matendo 5:38, 39.

17 Mara nyingi, jitihada za wapinzani huwageukia. Katika jamii moja ya Kiafrika, uwongo mwingi mbaya ulikuwa umeenezwa kuhusu Mashahidi wa Yehova, kutia ndani uwongo kwamba walikuwa waabudu wa Ibilisi. Kwa sababu hiyo, kila mara Mashahidi walipotembelea huko, Grace alikimbia na kujificha nyuma ya nyumba yake hadi walipoondoka. Siku moja kasisi wa kanisa lake aliinua kichapo chetu kimoja na kuwaambia wote waliokuwepo wasikisome kwa sababu kingefanya waache imani yao. Hilo lilifanya Grace atake kujua mengi zaidi. Mashahidi waliporudi, badala ya kujificha alizungumza nao na akapata nakala ya kichapo hicho. Funzo la Biblia lilianzishwa, naye akabatizwa mwaka wa 1996. Sasa Grace hutumia wakati wake kuwatafuta wengine ambao huenda wameelezwa habari zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova.

Imarisha Imani Yako Sasa

18. Kwa nini tunahitaji kuimarisha imani yetu kabla hatujapatwa na majaribu makali, na tunawezaje kufanya hivyo?

18 Kwa kuwa wakati wowote Shetani anaweza kutushambulia ghafula kwa chuki isiyo na msingi, ni muhimu tuimarishe imani yetu sasa. Tunawezaje kufanya hivyo? Ripoti moja kutoka nchi fulani ambako watu wa Yehova wamekuwa wakiteswa ilisema: “Jambo moja limekuwa wazi kabisa: Wale wenye mazoea mazuri ya kiroho na wanaoithamini sana ile kweli ya Biblia hawana tatizo la kuendelea kuwa imara majaribu yanapotokea. Lakini mara nyingi wale ambao katika ‘majira yanayofaa’ hukosa mikutano, hukosa kuhubiri kwa ukawaida, na kulegeza msimamo wao katika mambo madogo-madogo, huanguka chini ya jaribu ‘kali.’” (2 Timotheo 4:2) Ikiwa unaona sehemu fulani ambazo unahitaji kufanyia maendeleo, jitahidi kufanya hivyo bila kukawia.—Zaburi 119:60.

19. Utimilifu wa watumishi wa Mungu chini ya chuki isiyo na msingi hutimiza nini?

19 Waabudu wa kweli wanapodumisha utimilifu hata wanapochukiwa na Shetani wanathibitisha wazi kwamba enzi kuu ya Yehova ni yenye haki, inafaa, na ni adilifu. Uaminifu wao huufurahisha moyo wa Mungu. Ingawa huenda watu wakawashutumu, yule ambaye utukufu wake u juu ya dunia na mbingu “haoni aibu juu yao, kuitwa akiwa Mungu wao.” Kwa kweli, kuhusiana na washikamanifu hao wote, inaweza kusemwa hivi kwa kufaa: “Ulimwengu haukuwafaa.”—Waebrania 11:16, 38.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika Maandiko, neno “chuki” lina maana mbalimbali. Katika hali fulani, neno hilo humaanisha tu kutopenda sana. (Kumbukumbu la Torati 21:15, 16) Pia, neno “chuki” linaweza kumaanisha kutopenda kitu hata kidogo lakini bila kuwa na nia ya kukidhuru, badala yake kujaribu kukiepuka kwa sababu ya kukichukia. Hata hivyo, neno “chuki” linaweza pia kumaanisha uadui mkubwa, unaoendelea kwa muda mrefu na ambao mara nyingi huhusisha uovu. Katika makala hii, tutazungumzia maana hii ya mwisho.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kinachochea chuki isiyo na msingi dhidi ya waabudu wa kweli?

• Shetani alitumiaje shutuma katika jitihada ya kuvunja utimilifu wa Ayubu na Yesu?

• Yehova hutuimarishaje tuendelee kuwa imara licha ya chuki ya Shetani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

Walitambua Suala Halisi

Shahidi mmoja wa Yehova huko Ukrainia, ambako kazi ya kuhubiri Ufalme ilikuwa imepigwa marufuku kwa miaka zaidi ya 50, alisema: “Hali ambayo Mashahidi wa Yehova walijikuta haipaswi kuonwa tu kupitia jinsi wanadamu wengine wanavyowatendea. . . . Maofisa wengi walikuwa tu wakifanya kazi yao. Serikali mpya ilipokuja, maofisa hao walibadilika na kuanza kuunga mkono serikali hiyo, lakini sisi hatukubadilika. Tulitambua kwamba chanzo halisi cha matatizo yetu kilikuwa kimefunuliwa katika Biblia.

“Hatukujiona kuwa watu wasio na hatia wanaokandamizwa na wanadamu wenye uonevu. Kile kilichotusaidia kuvumilia ni kufahamu waziwazi suala lililotokezwa katika bustani ya Edeni, yaani, suala la haki ya Mungu ya kutawala. . . . Tulitetea suala linalohusu masilahi ya kibinafsi ya wanadamu na pia masilahi ya Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Tulielewa kindani zaidi masuala halisi yaliyohusika. Hilo lilifanya tuwe imara na kutuwezesha kudumisha utimilifu wetu hata chini ya hali ngumu kwelikweli.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ni nani aliyesababisha shutuma dhidi ya Yesu?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ayubu, Maria, na watumishi wa Mungu wa kisasa, kama vile Stanley Jones, wametetea enzi kuu ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 16]

Victor Popovych, alikamatwa mwaka wa 1970