Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wenyeji wa Mexico Wasikia Habari Njema

Wenyeji wa Mexico Wasikia Habari Njema

Wenyeji wa Mexico Wasikia Habari Njema

MNAMO Novemba 10, 2002, kikundi cha Mixe, wenyeji wa Mexico, kilikusanyika huko San Miguel, Quetzaltepec. Huo ni mji ulio katika jimbo maridadi la Oaxaca, lililo upande wa kusini. Watu hao walikuwa wamehudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova. Drama ya Biblia ndiyo iliyokuwa jambo kuu katika programu ya asubuhi hiyo.

Watu walishangaa waliposikia maneno ya kwanza ya drama ya Biblia. Waliitikia kwa kupiga makofi, na wengi wao walitokwa na machozi. Drama hiyo iliigizwa katika lugha ya Mixe! Ilipomalizika, wengi walishukuru sana kwa zawadi hiyo isiyotazamiwa. Mwanamke mmoja alisema: “Kwa mara ya kwanza, ningeweza kuelewa drama. Ilinigusa moyo.” Mwanamke mwingine alisema hivi: “Sasa ninaweza kufa nikiwa mwenye furaha kwa sababu Yehova ameniwezesha kusikia drama katika lugha yangu mwenyewe.”

Drama iliyoigizwa asubuhi hiyo katika lugha ya Mixe ilikuwa sehemu ya juhudi nyingi zilizofanywa hivi karibuni na Mashahidi wa Yehova huko Mexico ili kuwahubiria wenyeji habari njema ya Ufalme.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Yehova Alisikia Sala

Kuna wenyeji zaidi ya 6,000,000 huko Mexico, idadi hiyo inatosha kuunda taifa lenye utamaduni mbalimbali na lugha 62. Lugha 15 kati ya hizo zinazungumzwa na zaidi ya watu 100,000 kila moja. Zaidi ya wenyeji 1,000,000 hawazungumzi lugha ya Kihispania, ambayo ndiyo lugha rasmi ya Mexico. Na kwa wale wanaozungumza Kihispania, wengi wanaweza kujifunza kwa urahisi zaidi kweli za Biblia katika lugha zao za asili. (Matendo 2:6; 22:2) Wengine wamejifunza Biblia na kuhudhuria kwa uaminifu mikutano ya Kikristo kwa miaka mingi, hata hivyo, uelewaji wao umekuwa na mipaka. Hivyo, kwa muda fulani wamekuwa wakisali ili wapate kweli katika lugha yao ya asili.

Ili kushughulikia tatizo hilo, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico ilianzisha mipango mnamo 1999 ili kufanya mikutano ya kutaniko katika lugha za wenyeji. Vikundi vya kutafsiri pia viliundwa. Kufikia mwaka wa 2000, drama ya kusanyiko la wilaya iliigizwa katika lugha ya Maya na baadaye katika lugha nyingine kadhaa.

Hatua iliyofuata ilikuwa kuanza kutafsiri vichapo vya kujifunzia Biblia vya Mashahidi wa Yehova. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! ndiyo iliyokuwa ya kwanza kutafsiriwa katika Huave, Maya, Mazatec, Totonac, Tzeltal, na Tzotzil. Kisha vichapo zaidi vikafuata, kutia ndani chapa ya kawaida ya Huduma Yetu ya Ufalme katika lugha ya Maya. Vichapo kadhaa vimerekodiwa pia kwenye kaseti. Ili kufundisha wenyeji kusoma na kuandika katika lugha yao wenyewe, broshua yenye kichwa Jitahidi Kusoma na Kuandika inarekebishwa kwa ajili ya matumizi ya wenyeji. Kwa sasa vichapo vya Biblia vinatolewa katika lugha 15 za wenyeji, na vichapo zaidi vitatolewa.

“Kufanya Kila Jitihada”

Kazi ya kutafsiri haijawa rahisi. Sababu moja ni kwamba, kuna vichapo vichache sana vya kilimwengu ambavyo vimechapishwa katika lugha za wenyeji wa Mexico. Katika visa vingi, imekuwa vigumu kupata kamusi. Pia lugha fulani zina lahaja nyingi. Kwa mfano, lugha ya Zapotec peke yake ina lahaja tano tofauti. Lugha hizo ndogo-ndogo zimekuwa tofauti sana hivi kwamba Wazapotec kutoka maeneo mbalimbali hawaelewani.

Isitoshe, ikiwa hakuna viwango vilivyowekwa kwa ajili ya lugha fulani, inawabidi watafsiri waanzishe viwango vyao wenyewe. Kufanya hivyo kunahitaji utafiti na mazungumzo mengi. Haishangazi kwamba mwanzoni, watafsiri wengi walihisi kama Élida wa kikundi cha watafsiri wa lugha ya Huave! Anakumbuka: “Nilipoalikwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico ili kufanya kazi ya kutafsiri, nilikuwa na hisia mbili—shangwe na woga.”

Watafsiri wanapaswa pia kujifunza jinsi ya kutumia kompyuta, kupanga ratiba, na mbinu mbalimbali za kutafsiri. Kwa kweli, kazi hiyo imekuwa ngumu sana kwao. Wanahisije kuihusu? Gloria, mshiriki wa kikundi cha watafsiri wa lugha ya Maya, anajibu: “Hatuwezi kueleza shangwe tuliyo nayo ya kushiriki katika kutafsiri vichapo vya Biblia katika lugha ya Maya, lugha yetu ya asili.” Naye msimamizi mmoja wa Idara ya Tafsiri anasema hivi kuhusu watafsiri: “Tamaa ya kuwa na vichapo vya Biblia katika lugha zao ni kubwa sana hivi kwamba, wanafanya kila jitihada ili kukabiliana na tatizo hilo.” Je, jitihada hiyo imekuwa yenye manufaa?

“Asante, Yehova!”

Tumejionea jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi katika eneo la wenyeji. Hudhurio la mikutano ya Kikristo na makusanyiko limeongezeka. Kwa mfano, mwaka wa 2001, Mashahidi 223 wanaozungumza lugha ya Mixe walikusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Hata hivyo, jumla ya hudhurio lilikuwa 1,674, yaani, mara saba na nusu ya hesabu ya Mashahidi hao!

Baadhi ya watu ambao wanakubali kweli sasa wanaweza kuielewa vizuri zaidi tangu mwanzo. Mirna anakumbuka kile kilichompata kabla ya mikutano kuanza kufanywa katika lugha ya Maya. “Nilibatizwa baada ya kujifunza Biblia kwa miezi mitatu,” anasema. “Nilijua kwamba ningebatizwa, lakini ni lazima nikiri kwamba kwa kweli sikuelewa kweli za Biblia kwa kadiri nilivyopaswa kuzielewa. Ninafikiri sababu ni kwamba lugha yangu ya asili ni Maya, nami sikukielewa Kihispania vizuri sana. Ilinichukua wakati kuielewa kweli vizuri.” Leo, yeye na mume wake wanafurahi kuwa washiriki wa kikundi cha watafsiri wa lugha ya Maya.

Wote makutanikoni wana shangwe kubwa kupokea vichapo katika lugha zao wenyewe. Wakati broshua Furahia Milele Maisha Duniani! iliyotafsiriwa hivi karibuni ilipotolewa katika lugha ya Tzotzil, mwanamke mmoja aliyeanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo aliikumbatia na kusema: “Asante, Yehova!” Ripoti zinaonyesha kwamba wanafunzi wengi wa Biblia wamefanya maendeleo haraka na kufikia ubatizo, wahubiri wasiotenda wamechochewa kuanza kuhubiri tena, nao ndugu wengi Wakristo sasa wanahisi kwamba wana sifa zinazowastahilisha kukubali madaraka kutanikoni. Baadhi ya wenye nyumba wanakuwa tayari sana kukubali na kujifunza vichapo vya Biblia katika lugha zao wenyewe.

Katika kisa kimoja, mwanamke fulani Shahidi alienda kuongoza funzo la Biblia, lakini mwanafunzi hakuwa nyumbani. Wakati mume wa mwanafunzi huyo alipotokea mlangoni, Shahidi huyo aliomba amsomee mwanamume huyo jambo fulani katika broshua. “Sitaki chochote,” mwanamume huyo akajibu. Dada huyo akamwambia katika lugha ya Totonac kwamba broshua hiyo ilikuwa katika lugha yao ya asili. Mwanamume huyo aliposikia hivyo, akavuta benchi na kukaa chini. Dada alipokuwa akimsomea, yeye aliendelea kusema, “Hiyo ni kweli. Ndiyo, hiyo ni kweli.” Sasa anahudhuria mikutano ya Kikristo.

Huko Yucatán, mume wa Shahidi mmoja alipinga kweli na nyakati nyingine alimpiga mke wake aliporudi kutoka mikutanoni. Mikutano katika lugha ya Maya ilipoanza kufanywa, dada huyo aliamua kumwalika mume wake. Alienda kwenye mikutano naye akaifurahia sana. Sasa anahudhuria mikutano kwa ukawaida, anajifunza Biblia, naye hampigi mke wake tena.

Mwanamume mmoja anayezungumza lugha ya Totonac aliwaambia Mashahidi wawili kwamba hakuwa akisali kamwe kwa sababu kasisi mmoja Mkatoliki alimwambia kwamba Mungu husikia sala katika Kihispania tu. Hata ilimbidi kumlipa kasisi huyo ili asali kwa ajili ya Watotonac. Mashahidi hao walimweleza kwamba Mungu husikia sala katika lugha zote, nao wakampa broshua katika lugha ya Totonac ambayo aliikubali kwa shangwe kubwa.—2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33; Zaburi 65:2.

“Kualtsin Tajtoua”

Kwa kuchochewa na maendeleo hayo, wahubiri wengi wa Ufalme wanajitahidi kujifunza angalau lugha moja ya wenyeji au kuboresha ile wanayojua. Hivyo ndivyo anavyofanya mwangalizi mmoja wa mzunguko anayetembelea makutaniko matano ya lugha ya Nahuatl huko kaskazini mwa Puebla. Anasema: “Watoto ambao walikuwa na zoea la kulala wakati wa mikutano sasa huwa chonjo sana na husikiliza kwa makini ninapozungumza katika lugha ya Nahuatl. Baada ya mkutano mmoja kwisha, mvulana fulani mwenye umri wa miaka minne alinikaribia na kusema: ‘Kualtsin tajtoua’ (unazungumza vizuri). Hilo lilinifanya nihisi kwamba jitihada nilizofanya hazikuwa za bure.”

Kwa kweli, shamba hilo la lugha ya wenyeji ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa,’ na wote wanaoshiriki katika kazi hiyo wanahisi wametiwa moyo sana. (Yohana 4:35) Roberto, ambaye alifanya kazi ya kupanga vikundi vya watafsiri, anasema hivi kwa ufupi: “Limekuwa jambo lisiloweza kusahaulika kuona ndugu na dada zetu wakitoa machozi ya furaha wanaposikiliza kweli katika lugha yao ya asili na kuielewa. Mimi huguswa hisia sana ninapofikiria jambo hilo.” Bila shaka, kuwasaidia watu hawa wanyoofu wachukue msimamo kwa ajili ya Ufalme humletea Yehova shangwe pia.—Methali 27:11.

[Sanduku katika ukurasa wa 10, 11]

Wajue Baadhi ya Watafsiri

● “Wazazi wangu walinifundisha kweli tangu utotoni. Kwa kusikitisha, nilipokuwa na umri wa miaka 11, baba aliacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Miaka miwili baadaye, mama akatuacha. Kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa mkubwa kati ya ndugu na dada zangu watano, ilinibidi kuchukua daraka la mama, ingawa bado nilikuwa nikienda shuleni.

“Ndugu na dada zetu wa kiroho walitutegemeza kwa upendo, lakini maisha yalikuwa magumu. Nyakati nyingine nilijiuliza: ‘Kwa nini ninapatwa na mambo haya? Mimi ni mchanga sana!’ Niliweza kukabiliana na hali hiyo kwa msaada wa Yehova tu. Baada ya kumaliza shule ya sekondari, nilianza huduma ya wakati wote, na jambo hilo lilinisaidia sana. Wakati kikundi cha watafsiri wa lugha ya Nahuatl kilipoanzishwa, niliombwa nijiunge nacho.

“Sasa baba yangu ameanza kushirikiana tena na kutaniko, na ndugu na dada zangu wadogo wanamtumikia Yehova. Haikuwa kazi bure kujitahidi kudumisha uaminifu kwa Yehova. Ameibariki sana familia yetu.”—Alicia.

● “Mwanadarasa mwenzangu ambaye ni Shahidi alitoa hotuba kuhusu chanzo cha uhai. Sikwenda shule siku hiyo na nilikuwa na wasiwasi kuhusu mtihani, kwa hiyo nikamwomba anieleze habari hiyo. Sikuzote nilijiuliza ni kwa nini watu hufa. Aliponitolea kitabu Creation * na kujitolea kujifunza Biblia pamoja nami, nilikubali. Nilivutiwa sana na upendo na kusudi la Muumba.

“Nilipomaliza shule, nilipata nafasi ya kufundisha Kihispania na lugha ya Tzotzil. Lakini ingenibidi nihamie mbali sana na kufundisha miisho-juma na hivyo kukosa mikutano ya Kikristo. Badala yake, nilifanya kazi ya kutengeneza matofali. Baba yangu, ambaye hakuwa Shahidi, hakupendezwa hata kidogo na uamuzi wangu. Baadaye, nilipokuwa nikitumika nikiwa painia, kikundi cha watafsiri wa vichapo vya Biblia katika lugha ya Tzotzil kilianzishwa. Nilichochewa kujiunga nacho.

“Ninaweza kuona kwamba akina ndugu na dada wanahisi kuwa wamethaminiwa na kuheshimiwa kwa kupata vichapo katika lugha yao. Hilo linaridhisha sana. Ninahisi kuwa ni pendeleo kubwa kupewa mgawo huo.”—Humberto.

● “Mama alituacha nilipokuwa na umri wa miaka sita. Nilipokuwa tineja, baba alianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Siku moja dada fulani alijitolea kujifunza Biblia pamoja nami, na funzo hilo lilitia ndani shauri kwa vijana. Nikiwa tineja asiye na mama, nilihisi kwamba hilo ndilo shauri nililohitaji kabisa. Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 15.

“Mnamo mwaka wa 1999, baba aliuawa na watu fulani waovu waliotaka shamba lake. Nilifadhaika sana. Nilipatwa na mshuko-moyo mkubwa sana na kuhisi kwamba singeendelea kuwa hai. Lakini niliendelea kusali kwa Yehova ili anipe nguvu. Mwangalizi mmoja asafiriye pamoja na mke wake walinitia moyo sana. Punde si punde nikawa painia wa kawaida.

“Pindi moja niliona watu fulani waliokuwa wametembea kwa muda wa saa sita ili tu kusikia hotuba ya dakika 20 katika lugha ya Totonac, hata ingawa sehemu nyingine za mikutano zilifanywa katika lugha ya Kihispania, ambayo hawakuielewa. Hivyo, nilifurahi nilipoalikwa nikasaidie kutafsiri vichapo vya Biblia katika lugha ya Totonac.

“Nilikuwa nikimwambia baba yangu kwamba nilitamani kutumika kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Aliniambia kwamba halingekuwa jambo rahisi kwa msichana mseja kama mimi kualikwa huko. Atasisimuka kama nini atakapofufuliwa na kuona kwamba niliweza kwenda Betheli, na kutafsiri vichapo vya Biblia katika lugha yetu!”—Edith.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1985.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Washiriki wa kikundi cha watafsiri wa lugha ya Tzotzil wakizungumzia neno ambalo ni gumu kutafsiri