Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu’

Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu’

Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu’

“Wokovu wa watu waadilifu ni kutoka kwa Yehova; yeye ni ngome yao wakati wa taabu.”—ZABURI 37:39.

1, 2. (a) Yesu alisali kuhusu nini kwa ajili ya wanafunzi wake? (b) Mapenzi ya Mungu ni nini kuelekea watu wake?

YEHOVA ni mweza-yote. Ana uwezo wa kuwalinda waabudu wake waaminifu kwa njia yoyote anayotaka. Hata anaweza kuwatenga watu wake na ulimwengu na kuwaweka mahali salama na penye amani. Hata hivyo, Yesu alimwomba Baba yake wa mbinguni hivi kuwahusu wanafunzi wake: “Ninakuomba, si kwamba uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.”—Yohana 17:15.

2 Yehova ameamua kutotutoa “ulimwenguni.” Badala yake, anataka tuishi kati ya watu wa ulimwengu ili tuwatangazie ujumbe wake wa tumaini na faraja. (Waroma 10:13-15) Lakini, kama Yesu alivyodokeza katika sala yake, kwa kuishi katika ulimwengu huu, inatubidi kukabiliana na “yule mwovu.” Wanadamu wasiotii na roho waovu husababisha mateso na taabu, nao Wakristo pia hupatwa na mambo hayo.—1 Petro 5:9.

3. Ni lazima hata waabudu waaminifu wa Yehova wakabili hali gani, lakini tunapata faraja gani katika Neno lake?

3 Chini ya majaribu hayo, ni jambo la kawaida kuvunjika moyo pindi kwa pindi. (Methali 24:10) Biblia husimulia visa vya watu wengi waaminifu waliopatwa na taabu. Mtunga-zaburi anasema, “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.” (Zaburi 34:19) Naam, hata “mwadilifu” hupatwa na mambo mabaya. Kama mtunga-zaburi Daudi, huenda nyakati nyingine ‘tukafa ganzi na kupondwa kupita kiasi.’ (Zaburi 38:8) Hata hivyo, inafariji kujua kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18; 94:19.

4, 5. (a) Kupatana na Methali 18:10, tunapaswa kufanya nini ili kupata ulinzi wa Mungu? (b) Tunaweza kuchukua hatua zipi muhimu ili kupata ulinzi wa Mungu?

4 Kupatana na sala ya Yesu, kwa kweli Yehova anatulinda. Yeye ni ‘ngome yetu wakati wa taabu.’ (Zaburi 37:39) Kitabu cha Methali kinatumia maneno hayohayo kisemapo: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” (Methali 18:10) Andiko hilo hufunua ukweli wa msingi kuhusu jinsi ambavyo Yehova hujali sana viumbe vyake. Mungu huwalinda hasa waadilifu ambao humtafuta kwa bidii, kana kwamba tunakimbilia mnara wenye nguvu ili kupata ulinzi.

5 Tunapokabili taabu, tunawezaje kumkimbilia Yehova ili kupata ulinzi? Na tuchunguze hatua tatu muhimu tunazoweza kuchukua ili kupata msaada wa Yehova. Kwanza, tunapaswa kusali kwa Baba yetu wa mbinguni. Pili, tunapaswa kufuata mwongozo wa roho yake takatifu. Na tatu, lazima tujitiishe chini ya mpango wa Yehova kwa kushirikiana na Wakristo wenzetu ambao wanaweza kututuliza tunapopatwa na taabu.

Nguvu ya Sala

6. Wakristo wa kweli huionaje sala?

6 Wataalamu fulani wa afya hupendekeza sala ili kutibu hali ya kushuka moyo na mkazo. Huenda pindi tulivu kama wakati tunaposali zikapunguza mkazo, na ndivyo ilivyo na kusikiliza sauti fulani za viumbe au hata kukandwa mgongo. Wakristo wa kweli hawapuuzi sala kwa kuiona tu kuwa tiba ya kihisia-moyo. Tunaona sala kuwa mawasiliano ya heshima pamoja na Muumba. Sala inatia ndani ujitoaji wetu na tumaini letu katika Mungu. Naam, sala ni sehemu ya ibada yetu.

7. Inamaanisha nini kusali tukiwa na tumaini, na sala ya namna hiyo hutusaidiaje kukabiliana na taabu?

7 Tunapaswa kusali tukiwa na tumaini katika Yehova. Mtume Yohana aliandika: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Kwa kweli, Yehova, ambaye ni Mkuu Kuliko Wote, Mungu wa pekee wa kweli na Mweza-Yote, husikiliza kwa makini sala zenye bidii za waabudu wake. Inafariji kujua tu kwamba Mungu wetu mwenye upendo hutusikia tunapomweleza mahangaiko na matatizo yetu.—Wafilipi 4:6.

8. Kwa nini Wakristo waaminifu hawapaswi kuona haya au wahisi kwamba hawafai wanaposali kwa Yehova?

8 Wakristo waaminifu hawapaswi kamwe kuona haya, kuhisi kwamba hawafai, au kukosa tumaini wanaposali kwa Yehova. Ni kweli kwamba tunapokata tamaa au kulemewa na matatizo, huenda sikuzote tusiwe na mwelekeo wa kusali kwa Yehova. Katika pindi hizo tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova ‘huwaonyesha huruma watu wake walioteseka’ na kwamba “huwafariji wale walioshushwa chini.” (Isaya 49:13; 2 Wakorintho 7:6) Nyakati za taabu hasa, tunapaswa kumwendea Baba yetu wa mbinguni tukiwa na tumaini kwa kuwa yeye ni ngome yetu.

9. Imani hutimiza fungu gani tunaposali kwa Mungu?

9 Ili kunufaika kikamili kutokana na pendeleo la sala, ni lazima tuwe na imani ya kweli. Biblia inasema kwamba “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Imani inahusisha mengi zaidi ya kukubali tu kwamba Mungu “yuko.” Imani ya kweli inatia ndani kuamini kwa dhati kwamba Mungu anaweza na anataka kututhawabisha kwa utii wetu. “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.” (1 Petro 3:12) Kutambua daima kwamba Yehova anapendezwa nasi hufanya sala zetu ziwe na maana ya pekee.

10. Sala zetu zapaswa kuwaje ili Yehova atutegemeze kiroho?

10 Yehova husikiliza sala zetu tunaposali kwa moyo kamili. Mtunga-zaburi aliandika: “Nimeita kwa moyo wangu wote. Unijibu, Ee Yehova.” (Zaburi 119:145) Tofauti na sala za kidesturi za dini nyingi, sala zetu si za kidesturi, bali hutoka moyoni. Tunaposali kwa Yehova kwa ‘moyo wetu wote,’ maneno yetu hujaa maana na kusudi. Baada ya kutoa sala hizo kwa bidii, tunaanza kuhisi kitulizo kinachotokana na kumtupia ‘Yehova mzigo wetu.’ Kama Biblia inavyoahidi, ‘yeye mwenyewe atatutegemeza.’—Zaburi 55:22; 1 Petro 5:6, 7.

Roho ya Mungu Ni Msaidizi Wetu

11. Ni njia gani moja ambayo Yehova hutumia ili kutujibu ‘tunapoendelea kuomba’ msaada wake?

11 Yehova si Msikiaji wa sala tu bali yeye pia hujibu sala. (Zaburi 65:2) Daudi aliandika: “Katika siku ya taabu yangu nitakuitia wewe, kwa maana utanijibu.” (Zaburi 86:7) Kwa hiyo, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake ‘waendelee kuomba’ msaada wa Yehova kwa sababu ‘Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:9-13) Naam, nguvu za utendaji za Mungu hutenda kama msaidizi, au mfariji kwa watu wake.—Yohana 14:16.

12. Roho ya Mungu inaweza kutusaidiaje matatizo yanapoonekana kuwa yenye kulemea?

12 Hata tunapokabili majaribu, roho ya Mungu inaweza kutujaza “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Mtume Paulo ambaye alivumilia hali nyingi zenye mkazo alisema hivi kwa uhakika: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Vivyo hivyo, Wakristo wengi leo wamehisi nguvu mpya ya kiroho na ya kihisia-moyo dua zao zinapojibiwa. Mara nyingi, matatizo hayaonekani kuwa yenye kulemea sana tunapopata msaada wa roho ya Mungu. Kwa sababu ya nguvu hizo kutoka kwa Mungu, tunaweza kusema hivi kama mtume huyo: “Tunakazwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa; tunateswa, lakini hatuachwi kabisa bila msaada; tunaangushwa chini, lakini hatuangamizwi.”—2 Wakorintho 4:8, 9.

13, 14. (a) Yehova amethibitikaje kuwa ngome kupitia Neno lake lililoandikwa? (b) Kutumia kanuni za Biblia kumekusaidiaje kibinafsi?

13 Pia roho takatifu imeongoza na kuhifadhi Neno la Mungu lililoandikwa kwa manufaa yetu. Yehova amethibitikaje kuwa ngome nyakati za taabu kupitia Neno lake? Njia moja ni kwa kutupa hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri. (Methali 3:21-24) Biblia huzoeza akili zetu na kuboresha nguvu zetu za kufikiri. (Waroma 12:1) Kwa kusoma na kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kulitumia, tunaweza kufanya ‘nguvu zetu za ufahamu zizoezwe kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Labda umejionea mwenyewe jinsi kanuni za Biblia zilivyokusaidia kufanya maamuzi ya hekima ulipokabili magumu. Biblia hutupa busara inayoweza kutusaidia kupata suluhisho linalofaa kwa matatizo.—Methali 1:4.

14 Neno la Mungu hutupa chanzo kingine cha nguvu, yaani, tumaini la wokovu. (Waroma 15:4) Biblia inatuambia kwamba mambo mabaya hayataendelea kutukia milele. Dhiki zozote tunazopata ni za muda tu. (2 Wakorintho 4:16-18) Tuna “tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.” (Tito 1:2) Tukishangilia katika tumaini hilo, huku tukifikiria daima wakati ujao ambao Yehova anaahidi, tunaweza kuvumilia dhiki.—Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 1:3.

Kutaniko Ni Wonyesho wa Upendo wa Mungu

15. Wakristo wanaweza kusaidianaje?

15 Uandalizi mwingine kutoka kwa Yehova ambao unaweza kutusaidia nyakati za taabu ni ushirika tunaofurahia katika kutaniko la Kikristo. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Neno la Mungu huwatia moyo wote kutanikoni wapendane na kuheshimiana. (Waroma 12:10) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Kuwa na mtazamo huo wa akili kunaweza kutusaidia kukazia fikira mahitaji ya wengine badala ya majaribu yetu. Tunapojitoa kwa wengine, tunawasaidia na pia tunapata furaha na uradhi wa kadiri fulani ambao hufanya tusilemewe na mizigo yetu.—Matendo 20:35.

16. Kila Mkristo anawezaje kuwa mwenye kutia moyo?

16 Wanaume na wanawake waliokomaa kiroho wanaweza kutimiza fungu muhimu katika kuwaimarisha wengine. Ili kufanya hivyo, wao huwa wenye kufikika na kupatikana. (2 Wakorintho 6:11-13) Kutaniko hunufaika sana wote wanapochukua wakati kuwapongeza vijana, kuwaimarisha waamini wapya, na kuwatia moyo wale walioshuka moyo. (Waroma 15:7) Upendo wa kindugu utatusaidia pia tuepuke mtazamo wa kuwatilia shaka wengine. Hatupaswi kukata kauli haraka kwamba magumu ya kibinafsi ni ishara ya udhaifu wa kiroho. Kwa kufaa, Paulo anawahimiza Wakristo ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Biblia inaonyesha kwamba hata Wakristo waaminifu hupatwa na taabu.—Matendo 14:15.

17. Tuna nafasi zipi za kuimarisha kifungo cha undugu wa Kikristo?

17 Mikutano ya Kikristo hutupa nafasi bora ya kufarijiana na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Ushirika huo wenye upendo haupatikani tu kwenye mikutano ya kutaniko. Badala yake, watu wa Mungu pia hutafuta nafasi za kuwa na ushirika wenye kujenga katika vikao visivyo rasmi. Taabu zinapotokea, tutakuwa tayari kusaidiana kwa sababu tayari tumekuwa na uhusiano wa karibu na wa kirafiki. Mtume Paulo aliandika: “Kusiwe na mgawanyiko katika mwili, bali . . . viungo vyake vitunzane kwa njia ileile. Na kiungo kimoja kikiumia, vile viungo vingine vyote huumia pamoja nacho; au kiungo kimoja kikitukuzwa, vile viungo vingine vyote hushangilia pamoja nacho.”—1 Wakorintho 12:25, 26.

18. Tunapaswa kuepuka mwelekeo gani tunapohisi kwamba tumeshuka moyo?

18 Nyakati nyingine, huenda tukahisi tumeshuka moyo sana tusiweze kufurahia ushirika wa Wakristo wenzetu. Tunapaswa kupigana na hisia hizo ili tusikose faraja na msaada tunaoweza kupata kutoka kwa waamini wenzetu. Biblia inatuonya: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Kwa kutupatia ndugu na dada, Mungu anaonyesha kwamba anatujali. Tukitambua uandalizi huo wenye upendo, tutapata kitulizo katika nyakati za taabu.

Dumisha Mtazamo Ufaao

19, 20. Maandiko hutusaidiaje kukataa mawazo yasiyofaa?

19 Tunapovunjika moyo na kuhuzunika, ni rahisi kuendelea kufikiria mambo yasiyofaa. Kwa mfano, wengine wanapopata shida, wao huanza kutilia shaka hali yao ya kiroho, na kukata kauli kwamba wanapatwa na magumu kwa kuwa wamepoteza kibali cha Mungu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova hamjaribu yeyote kwa “mambo maovu.” (Yakobo 1:13) “Si kutoka moyoni mwake mwenyewe kwamba [Mungu] amewatesa au kuwahuzunisha wana wa binadamu,” yasema Biblia. (Maombolezo 3:33) Kinyume cha hilo, Yehova huhuzunika sana watumishi wake wanapoteseka.—Isaya 63:8, 9; Zekaria 2:8.

20 Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Anatujali, naye atatutukuza katika wakati unaofaa. (1 Petro 5:6, 7) Kutambua daima kwamba Mungu anatupenda kutatusaidia kudumisha mtazamo mzuri, na hata kushangilia. Yakobo aliandika: “Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapokutana na majaribu ya namna mbalimbali.” (Yakobo 1:2) Kwa nini? Anajibu: “Kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.”—Yakobo 1:12.

21. Hata tuwe tunakabili magumu gani, Mungu anawapa uhakikisho gani wale wanaothibitika kuwa waaminifu kwake?

21 Kama Yesu alivyotuonya, tutapatwa na dhiki ulimwenguni. (Yohana 16:33) Lakini Biblia inaahidi kwamba hakuna “dhiki au taabu au mateso au njaa au uchi au hatari” itakayotutenga na upendo wa Yehova na ule wa Mwana wake. (Waroma 8:35, 39) Inafariji kama nini kujua kwamba taabu zozote tunazopata ni za muda tu! Wakati huu tunapongojea mwisho wa kuteseka kwa wanadamu, Yehova, Baba yetu mwenye upendo, anatulinda. Tukimwendea ili kupata ulinzi, atathibitika kuwa “kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu.”—Zaburi 9:9.

Tumejifunza Nini?

• Wakristo wanapaswa kutazamia nini wanapoishi katika ulimwengu mwovu?

• Sala zetu za bidii zinawezaje kutuimarisha tunapokabili majaribu?

• Roho ya Mungu ni msaidizi katika njia gani?

• Tunaweza kufanya nini ili kusaidiana?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tunapaswa kumtafuta Yehova kana kwamba tunakimbilia mnara wenye nguvu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wale waliokomaa kiroho hutumia kila nafasi kuwapongeza na kuwatia wengine moyo