Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari na “Sauti ya Wageni”

Jihadhari na “Sauti ya Wageni”

Jihadhari na “Sauti ya Wageni”

“Hawatamfuata mgeni kamwe bali watamkimbia, kwa sababu hawaijui sauti ya wageni.”—YOHANA 10:5.

1, 2. (a) Maria anaitikiaje Yesu anapomwita kwa jina lake, na ni mfano gani ambao Yesu alitaja mapema kidogo unaoonyeshwa na tukio hilo? (b) Ni nini hutuwezesha kukaa karibu na Yesu?

YESU aliyefufuliwa anamwona mwanamke amesimama karibu na kaburi lake lililo tupu. Anamjua vizuri. Yeye ni Maria Magdalene. Karibu miaka miwili iliyopita, alikuwa amemponya kwa kuondoa roho mwovu aliyekuwa amemwingia. Tangu wakati huo, mwanamke huyo ameandamana naye na mitume wake na kushughulikia mahitaji yao ya kila siku. (Luka 8:1-3) Hata hivyo, leo Maria analia. Amezidiwa na huzuni kwa sababu alimwona Yesu akifa na sasa hata mwili wake umetoweka! Kwa hiyo, Yesu anamuuliza: “Mwanamke, kwa nini unalia? Unamtafuta nani?” Akifikiri Yesu ni mtunza-bustani, anamjibu: “Bwana, ikiwa umemchukua, niambie umemlaza wapi, nami nitamwondoa.” Yesu anamwita: “Maria!” Mara moja Maria anatambua jinsi ambavyo Yesu huzungumza naye. “Mwalimu!” anaitikia kwa furaha na kumkumbatia.—Yohana 20:11-18.

2 Masimulizi hayo yanatoa mfano wenye kugusa hisia kuhusu maneno ambayo Yesu alikuwa amesema mapema kidogo. Akijilinganisha na mchungaji na kuwalinganisha wanafunzi wake na kondoo, yeye anasema kwamba mchungaji huwaita kondoo zake kwa jina, nao wanajua sauti yake. (Yohana 10:3, 4, 14, 27, 28) Kwa kweli, kama vile ambavyo kondoo humtambua mchungaji wake, vivyo hivyo Maria alimtambua Mchungaji wake, Kristo. Leo pia wafuasi wa Yesu humtambua Mchungaji wao. (Yohana 10:16) Kama vile masikio yenye utambuzi ya kondoo humwezesha kukaa karibu na mchungaji wake, vivyo hivyo utambuzi wetu wa kiroho hutuwezesha kutembea kwa ukaribu katika hatua za Mchungaji wetu Mwema, Yesu Kristo.—Yohana 13:15; 1 Yohana 2:6; 5:20.

3. Mfano wa Yesu kuhusu zizi la kondoo hutokeza maswali gani akilini?

3 Hata hivyo, kulingana na mfano huo, uwezo wa kondoo wa kutambua sauti za kibinadamu humwezesha kujua rafiki na pia adui zake. Hilo ni muhimu sana kwa kuwa tuna wapinzani wenye hila. Ni nani hao? Wao hutendaje? Nasi tunawezaje kujilinda? Ili kujua mambo hayo, acheni tuone mambo mengine ambayo Yesu anataja katika mfano wake wa zizi la kondoo.

‘Yeye Ambaye Haingii Kupitia Mlango’

4. Kulingana na mfano wa mchungaji, kondoo wanamfuata nani, nao hawamfuati nani?

4 Yesu anasema: “Yule anayeingia kupitia mlango ndiye mchungaji wa kondoo. Mtunza-mlango humfungulia huyo, nao kondoo huisikiliza sauti yake, naye huwaita kondoo zake mwenyewe kwa jina na kuwatoa nje. Baada ya kuwatoa nje wote walio wake mwenyewe, yeye huenda mbele yao, nao kondoo humfuata, kwa sababu wanaijua sauti yake. Hawatamfuata mgeni kamwe bali watamkimbia, kwa sababu hawaijui sauti ya wageni.” (Yohana 10:2-5) Ona kwamba Yesu anatumia neno “sauti” mara tatu. Anataja sauti ya mchungaji mara mbili, lakini mara ya tatu, anataja “sauti ya wageni.” Yesu anazungumza kuhusu mgeni wa aina gani?

5. Kwa nini hatuonyeshi ukaribishaji-wageni kwa aina ya mgeni anayetajwa katika sura ya 10 ya kitabu cha Yohana?

5 Yesu hazungumzi kuhusu mgeni ambaye tunataka kumwonyesha ukaribishaji-wageni—neno ambalo katika lugha ya awali ya Biblia linamaanisha “kupenda wageni.” (Waebrania 13:2) Katika mfano wa Yesu, mgeni huyo hakualikwa. Yeye “haiingii katika zizi la kondoo kupitia mlango bali hupandia mahali pengine.” Huyo ni “mwizi na mporaji.” (Yohana 10:1) Ni nani mtu wa kwanza kutajwa katika Neno la Mungu ambaye alipata kuwa mwizi na mporaji? Ni Shetani Ibilisi. Tunapata uthibitisho katika kitabu cha Mwanzo.

Sauti ya Mgeni Iliposikiwa kwa Mara ya Kwanza

6, 7. Kwa nini kwa kufaa Shetani anaweza kuitwa mgeni na mwizi?

6 Andiko la Mwanzo 3:1-5 hueleza jinsi sauti ya mgeni ilivyosikiwa duniani kwa mara ya kwanza. Masimulizi hayo yanaeleza kwamba Shetani alimkaribia mwanamke wa kwanza, Hawa, kupitia nyoka na kuzungumza naye kwa njia yenye kupotosha. Ni kweli kwamba katika masimulizi hayo Shetani haitwi “mgeni” waziwazi. Hata hivyo, matendo yake yanaonyesha kwamba katika njia nyingi, yeye alikuwa kama yule mgeni aliyetajwa katika mfano wa Yesu kwenye Yohana sura ya 10. Ona mambo kadhaa yanayofanana.

7 Yesu anasema kwamba mgeni huyo huwakaribia kondoo zizini kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Vivyo hivyo, kwa kutumia nyoka Shetani alimkaribia Hawa kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Njia hiyo ya ujanja ilifunua kabisa jinsi Shetani alivyo, yaani, mtu mwenye hila anayejipenyeza mahali bila kibali. Isitoshe, mgeni katika zizi la kondoo ana nia ya kuiba kondoo kutoka kwa mmiliki halali. Kwa kweli, yeye ni mbaya zaidi kuliko mwizi, kwa kuwa anataka pia “kuua na kuharibu.” (Yohana 10:10) Vivyo hivyo, Shetani alikuwa mwizi. Kwa kumdanganya Hawa, aliiba uaminifu wake kwa Mungu. Isitoshe, Shetani pia aliwaletea wanadamu kifo. Hivyo, yeye ni muuaji.

8. Shetani alipotoshaje maneno na makusudi ya Yehova?

8 Udanganyifu wa Shetani ulionekana wazi kupitia jinsi alivyopotosha maneno na makusudi ya Yehova. “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” akamuuliza Hawa. Shetani alijifanya kuwa ameshangaa, kana kwamba alikuwa akisema: ‘Mungu angewezaje kuwaambia mfanye jambo kama hilo ambalo halipatani na akili hata kidogo?’ Aliongeza kusema: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa.” Ona maneno yake: “Mungu anajua.” Ni kana kwamba Shetani alikuwa akisema: ‘Ninajua yale Mungu anayojua. Ninajua makusudi yake, nayo ni mabaya.’ (Mwanzo 2:16, 17; 3:1, 5) Inasikitisha kwamba Hawa na Adamu hawakuikataa sauti ya mgeni huyo, bali waliisikiliza, na kuleta ole juu yao wenyewe na wazao wao pia.—Waroma 5:12, 14.

9. Kwa nini tutarajie sauti ya wageni isikiwe leo?

9 Shetani hutumia njia kama hizo kuwapotosha watu wa Mungu leo. (Ufunuo 12:9) Yeye ni “baba ya uwongo,” na wale ambao, kama yeye, hujaribu kuwapotosha watumishi wa Mungu ni watoto wake. (Yohana 8:44) Acheni tuone baadhi ya njia ambazo sauti ya wageni hao inasikiwa leo.

Jinsi Sauti ya Wageni Inavyosikiwa Leo

10. Sauti ya wageni inasikiwa kupitia njia ipi?

10 Mawazo yenye udanganyifu. Mtume Paulo anasema: “Msichukuliwe mbali na mafundisho mbalimbali na yaliyo mageni.” (Waebrania 13:9) Ni mafundisho gani hayo? Kwa kuwa yanaweza ‘kutuchukulia mbali,’ ni wazi kwamba Paulo anarejelea mafundisho ambayo hudhoofisha usawaziko wetu wa kiroho. Ni nani wanaoeneza mafundisho hayo mageni? Paulo aliwaambia hivi wazee fulani Wakristo: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:30) Kwa kweli, leo kama ilivyokuwa katika siku za Paulo, watu fulani ambao wakati mmoja walikuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo sasa wanajaribu kuwapotosha kondoo kwa kusema “mambo yaliyopotoka,” yaani, ukweli nusu-nusu na uwongo mtupu. Kama mtume Petro anavyosema, wao hutumia “maneno yasiyo ya kweli,” yaani, maneno yanayoonekana kuwa ya kweli lakini ambayo kwa kweli hayafai.—2 Petro 2:3.

11. Maneno yanayopatikana kwenye 2 Petro 2:1, 3 yanafunuaje njia na lengo la waasi-imani?

11 Petro anazidi kufunua njia za waasi-imani kwa kusema kwamba “wataingiza ndani kimya-kimya madhehebu yenye kuharibu.” (2 Petro 2:1, 3) Kama vile mwizi katika mfano wa Yesu wa zizi asivyoingia ‘kupitia mlango bali hupandia mahali pengine,’ vivyo hivyo waasi-imani hutukaribia kupitia njia za hila. (Wagalatia 2:4; Yuda 4) Nia yao ni nini? Petro anaongeza kusema: “Watawatumia ninyi vibaya.” Kwa kweli, hata waasi-imani wajitetee jinsi gani, lengo hasa la watu hao wanaojipenyeza mahali bila kibali ni “kuiba na kuua na kuharibu.” (Yohana 10:10) Jihadhari na wageni hao!

12. (a) Mashirika yetu yanawezaje kufanya tusikie sauti ya wageni? (b) Kuna ufanani gani kati ya mbinu za Shetani na zile za wageni leo?

12 Mashirika yenye kudhuru. Huenda sauti ya wageni ikasikiwa kupitia mashirika yetu. Mashirika yenye kudhuru huhatarisha hasa vijana. (1 Wakorintho 15:33) Kumbuka kwamba Shetani alimlenga Hawa—aliyekuwa na umri na uzoefu mdogo zaidi kati ya wanadamu wa kwanza wawili. Alimsadikisha kwamba Yehova alikuwa amemwekea vizuizi vilivyopita kiasi ili kumnyima uhuru, ingawa hilo lilikuwa kinyume cha ukweli wa mambo. Yehova aliwapenda viumbe wake wa kibinadamu, naye alijali hali yao. (Isaya 48:17) Vivyo hivyo leo, wageni hujaribu kuwashawishi ninyi vijana kwamba wazazi wenu Wakristo huwawekea vizuizi vinavyopita kiasi ili kuwanyima uhuru. Wageni hao wanaweza kuwaathirije? Msichana mmoja Mkristo anakiri: “Kwa muda fulani wanadarasa wenzangu walidhoofisha imani yangu kwa kiwango fulani. Walisema tena na tena kwamba imani yangu ina vizuizi na haipatani na akili.” Hata hivyo, ukweli ni kwamba wazazi wako wanakupenda. Hivyo, wanashule wenzako wanapojaribu kukushawishi usiwatumaini wazazi wako, usipotoshwe kama vile Hawa.

13. Daudi alifuata mwenendo gani wa hekima, nasi tunaweza kumwiga kwa njia gani?

13 Kuhusu mashirika yenye kudhuru, mtunga-zaburi Daudi anasema: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zaburi 26:4) Je, umeona tena ile tabia ambayo ni kawaida ya wageni? Wao huficha jinsi walivyo—kama vile Shetani alivyoficha utambulisho wake kwa kutumia nyoka. Kwa kutumia Intaneti, leo watu fulani wasio waadilifu huficha utambulisho na nia yao halisi. Watu wazima waliopotoka hata hujifanya vijana wanapozungumza kupitia Intaneti ili wawatie katika mtego. Tafadhali vijana, iweni wenye tahadhari sana msije mkapata madhara ya kiroho.—Zaburi 119:101; Methali 22:3.

14. Nyakati nyingine vyombo vya habari huenezaje sauti ya wageni?

14 Shutuma za uwongo. Ingawa ripoti fulani za habari kuhusu Mashahidi wa Yehova hazina ubaguzi, nyakati nyingine vyombo vya habari hutumiwa kueneza sauti yenye ubaguzi ya wageni. Kwa mfano, katika nchi moja ripoti fulani ya habari ilisema kwa uwongo kwamba Mashahidi waliunga mkono utawala wa Hitler wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Katika nchi nyingine, ripoti fulani iliwashutumu Mashahidi kwamba wao huharibu makanisa kimakusudi. Katika nchi kadhaa, vyombo vya habari viliwashutumu Mashahidi kwamba wao huwanyima watoto wao matibabu na pia hupuuza kimakusudi dhambi nzito zinazotendwa na waamini wenzao. (Mathayo 10:22) Hata hivyo, watu wanyoofu wanaotujua kibinafsi hutambua kwamba shutuma hizo ni za uwongo.

15. Kwa nini si jambo la hekima kuamini kila habari inayotangazwa katika vyombo vya habari?

15 Tunapaswa kufanya nini tukikabili shutuma zinazoenezwa kupitia sauti ya wageni hao? Tunapaswa kutii shauri hili la Methali 14:15: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Si jambo la hekima kuamini kila habari inayotangazwa katika vyombo vya habari kuwa ya kweli. Ingawa kwa kweli hatutilii shaka habari zote za kilimwengu, sisi tunatambua kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

“Yajaribuni Maneno Yaliyoongozwa na Roho”

16. (a) Tabia za kondoo halisi huonyeshaje kwamba maneno ya Yesu kwenye Yohana 10:4 ni ya kweli? (b) Biblia hututia moyo tufanye nini?

16 Hata hivyo, tunawezaje kuwa na uhakika kabisa kama mtu tunayeshughulika naye ni rafiki au ni adui? Yesu anasema kwamba kondoo humfuata mchungaji “kwa sababu wanaijua sauti yake.” (Yohana 10:4) Sauti ndiyo humchochea kondoo kumfuata mchungaji, bali si sura yake ya nje. Kitabu kimoja kinachozungumzia nchi zinazotajwa katika Biblia kinaeleza kwamba wakati mmoja mgeni fulani aliyetembea huko alidai kwamba kondoo humtambua mchungaji wao kwa mavazi yake, bali si kwa sauti yake. Mchungaji mmoja alimjibu kwamba kondoo humtambua kwa sauti. Ili kuthibitisha hilo, alibadilishana mavazi yake na mgeni huyo. Huku akiwa amevalia mavazi ya mchungaji huyo, mgeni huyo aliwaita kondoo, lakini hawakuitikia. Hawakuijua sauti yake. Hata hivyo, mchungaji alipowaita, ingawa hakuwa amevalia nguo za mchungaji, kondoo walikuja mara moja. Hivyo, mtu anaweza kufanana na mchungaji, lakini hilo haliwathibitishii kondoo kwamba mtu huyo ni mchungaji. Kwa kweli, kondoo huijaribu sauti ya mtu anayewaita, wakiilinganisha na ile ya mchungaji. Neno la Mungu hutuambia tufanye vivyo hivyo—“yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1; 2 Timotheo 1:13) Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?

17. (a) Tunafahamianaje na sauti ya Yehova? (b) Kumjua Yehova hutuwezesha kufanya nini?

17 Inaeleweka kwamba kadiri tunavyojua sauti, au ujumbe wa Yehova vizuri zaidi, ndivyo tunavyoweza kutambua vizuri zaidi sauti ya mgeni. Biblia huonyesha jinsi tunavyoongeza ujuzi huo. Inasema: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.’” (Isaya 30:21) “Neno” hilo lililo nyuma yetu hutoka katika Neno la Mungu. Kila wakati tunaposoma Neno la Mungu, ni kama sisi husikia sauti ya Mchungaji wetu Mkuu, Yehova. (Zaburi 23:1) Hivyo, kadiri tunavyozidi kujifunza Biblia, ndivyo tunavyofahamiana zaidi na sauti ya Mungu. Ujuzi huo wa kindani hutuwezesha kutambua mara moja sauti ya wageni.—Wagalatia 1:8.

18. (a) Kuijua sauti ya Yehova kunahusisha nini? (b) Kulingana na Mathayo 17:5, kwa nini tunapaswa kuitii sauti ya Yesu?

18 Kuijua sauti ya Yehova kunahusisha nini zaidi? Kunahusisha kuitii, na si kuisikia tu. Ona tena Isaya 30:21. Neno la Mungu linatuambia: “Hii ndiyo njia.” Naam, kupitia funzo la Biblia, sisi husikia miongozo ya Yehova. Kisha anaamuru: “Tembeeni ndani yake.” Yehova hutaka tutende kupatana na yale tunayosikia. Hivyo, kwa kutenda kupatana na yale tunayojifunza, tunaonyesha kwamba hatukuisikia tu sauti ya Yehova, bali tuliitii pia. (Kumbukumbu la Torati 28:1) Kuitii sauti ya Yehova pia humaanisha kuitii sauti ya Yesu, kwa kuwa Yehova mwenyewe alituambia tufanye hivyo. (Mathayo 17:5) Yesu, Mchungaji Mwema anatuambia tufanye nini? Yeye hutufundisha tufanye wanafunzi na tumtumaini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45; 28:18-20) Kuitii sauti yake kunamaanisha uzima wa milele kwetu.—Matendo 3:23.

‘Watamkimbia’

19. Tunapaswa kuitikiaje sauti ya wageni?

19 Hivyo basi, tunapaswa kuitikiaje sauti ya wageni? Kwa njia ileile kondoo wanavyoitikia. Yesu anasema: “Hawatamfuata mgeni kamwe bali watamkimbia.” (Yohana 10:5) Sisi huitikia katika njia mbili. Kwanza, ‘hatutamfuata kamwe’ mgeni. Naam, sisi humkataa katakata mgeni. Kwa kweli, katika Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia, neno “kamwe” limetumiwa kuonyesha njia yenye nguvu zaidi ya kukataa kitu katika lugha hiyo. (Mathayo 24:35; Waebrania 13:5) Pili, ‘tutamkimbia,’ au kugeukia mbali naye. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuwatendea wale ambao mafundisho yao hayapatani na sauti ya Mchungaji Mwema.

20. Tutaitikiaje tunapokabiliwa na (a) waasi-imani wadanganyifu, (b) mashirika yenye kudhuru, (c) ripoti za vyombo vya habari zenye ubaguzi?

20 Kwa hiyo, tunapokabiliwa na wale walio na maoni ya uasi-imani, tunataka kufanya yale ambayo Neno la Mungu linasema: “Waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kusababisha kukwazika kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, nanyi mjiepushe nao.” (Waroma 16:17; Tito 3:10) Vivyo hivyo, vijana Wakristo wanaokabili hatari ya mashirika yenye kudhuru wangependa kufuata shauri ambalo Paulo alimpa kijana Timotheo: “Zikimbie tamaa zinazotukia ujanani.” Na tunapokabili shutuma za uwongo katika vyombo vya habari, tutakumbuka shauri lingine ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Nao [wale wanaosikiliza sauti ya wageni] watageuzwa kando kufuata hadithi za uwongo. Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote.” (2 Timotheo 2:22; 4:3-5) Hata sauti ya wageni iwe inasikika kuwa yenye kupendeza jinsi gani, sisi hukimbia chochote kile kinachoweza kudhoofisha imani yetu.—Zaburi 26:5; Methali 7:5, 21; Ufunuo 18:2, 4.

21. Wale wanaokataa sauti ya wageni watapata thawabu gani?

21 Kwa kukataa sauti ya wageni, Wakristo watiwa-mafuta huitikia maneno ya Mchungaji Mwema yanayopatikana kwenye Luka 12:32. Hapo Yesu anawaambia: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” Vivyo hivyo, “kondoo wengine” wanangojea kwa hamu kusikia maneno haya ya Yesu: “Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 10:16; Mathayo 25:34) Tutapata thawabu yenye kufurahisha kama nini ikiwa tutakataa “sauti ya wageni”!

Je, Unakumbuka?

• Ufafanuzi juu ya mgeni katika mfano wa Yesu kuhusu zizi la kondoo unamfaaje Shetani?

• Sauti ya wageni husikiwaje leo?

• Tunawezaje kuitambua sauti ya wageni?

• Tunapaswa kuiitikiaje sauti ya wageni?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Maria alimtambua Kristo

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mgeni hawakaribii kondoo moja kwa moja

[Picha katika ukurasa wa 18]

Sisi huitikiaje sauti ya wageni?