Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kile Kinachohitajiwa Hasa ili Kuwa na Furaha

Kile Kinachohitajiwa Hasa ili Kuwa na Furaha

Kile Kinachohitajiwa Hasa ili Kuwa na Furaha

YEHOVA, “Mungu mwenye furaha,” na Yesu Kristo, “yule Mwenye Uwezo Mkubwa aliye wa pekee na mwenye furaha,” wanajua kile kinachohitajiwa ili kuwa na furaha. (1 Timotheo 1:11; 6:15) Kwa hiyo, haishangazi kwamba siri ya kupata furaha inapatikana katika Neno la Mungu, Biblia.—Ufunuo 1:3; 22:7.

Katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, Yesu anafafanua kile kinachohitajiwa ili kuwa na furaha. Anasema: “Wenye furaha” ni wale (1) wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, (2) wanaoomboleza, (3) walio na tabia-pole, (4) walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, (5) walio na rehema, (6) walio safi moyoni, (7) wanaofanya amani, (8) ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, na (9) wanaoshutumiwa na kuteswa kwa ajili yake.—Mathayo 5:3-11. *

Je, Taarifa za Yesu Ni Sahihi?

Unahitaji maelezo kidogo kuhusu taarifa za Yesu ili kuzielewa. Bila shaka, mtu mwenye tabia-pole, huruma, na mwenye kufanya amani ambaye anachochewa na moyo safi atakuwa mwenye furaha zaidi kuliko mtu mwenye hasira, mtaka-vita, na asiye na huruma.

Hata hivyo, huenda tukashangaa jinsi watu walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu au wanaoomboleza wanavyoweza kutajwa kuwa wenye furaha. Watu hao huona hali za ulimwengu jinsi zilivyo kikweli. Wao ‘huugua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa’ siku zetu. (Ezekieli 9:4) Kuugua na kulia hakuwaletei furaha. Hata hivyo, wanapojifunza kuhusu kusudi la Mungu la kuwapa haki waliokandamizwa na kuleta hali za uadilifu duniani, wanafurahi sana.—Isaya 11:4.

Kupenda uadilifu pia hufanya watu waomboleze wanaposhindwa tena na tena kufanya yaliyo sawa. Hivyo wanatambua uhitaji wao wa kiroho. Watu hao wako tayari kutafuta mwongozo wa Mungu kwa sababu wanatambua kwamba yeye peke yake ndiye anayeweza kuwasaidia watu washinde udhaifu wao.—Methali 16:3, 9; 20:24.

Watu wanaoomboleza, walio na njaa na kiu ya uadilifu, na wanaotambua uhitaji wao wa kiroho hufahamu umuhimu wa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Muumba. Kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu huleta furaha, lakini kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu huleta furaha kubwa hata zaidi. Naam, hapana shaka kwamba wale ambao kwa kweli wanapenda yaliyo sawa, na ambao wako tayari kukubali mwongozo wa Mungu, wanaweza kutajwa kuwa wenye furaha ya kweli.

Hata hivyo, huenda ukaona ni vigumu kuamini kwamba mtu anayeteswa na kushutumiwa anaweza kuwa mwenye furaha. Lakini taarifa hiyo lazima iwe ya kweli kwa kuwa Yesu mwenyewe alisema hivyo. Basi, tunapaswa kuyaelewaje maneno yake?

Inawezekanaje Kuwa na Furaha Licha ya Kuteswa?

Ona kwamba Yesu hakusema kuwa shutuma na mateso huleta furaha. Alisema: “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, . . . watu wanapowashutumu na kuwatesa . . . kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:10, 11) Hivyo, mtu hupata furaha tu ikiwa anashutumiwa kwa sababu ya kuwa mfuasi wa Kristo na kwa sababu ya kuishi kupatana na kanuni za uadilifu ambazo Yesu alifundisha.

Hilo linaonyeshwa na mambo yaliyowapata Wakristo wa mapema. Washiriki wa Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi, ‘waliwaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema juu ya msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende zao.’ Mitume walifanyaje? “Kwa hiyo, wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—Matendo 5:40-42; 13:50-52.

Mtume Petro alitoa ufafanuzi zaidi kuhusu uhusiano uliopo kati ya shutuma na furaha. Aliandika: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:14) Naam, unapoteseka ukiwa Mkristo kwa sababu ya kufanya yaliyo sawa, hata ingawa kuteseka huko hakupendezi, utapata furaha kwa kujua kwamba unapokea roho takatifu ya Mungu. Roho ya Mungu inahusianaje na furaha?

Matendo ya Mwili au Matunda ya Roho?

Roho ya Mungu hukaa tu juu ya wale wanaomtii Mungu kuwa mtawala. (Matendo 5:32) Yehova hawapi roho yake wale wanaozoea kufanya “matendo ya mwili.” Matendo hayo ni “uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo.” (Wagalatia 5:19-21) Kweli, “matendo ya mwili” ni ya kawaida katika ulimwengu wa leo. Hata hivyo, wale wanaoyazoea hawapati furaha ya kweli na ya kudumu. Badala yake, kutenda mambo hayo hufanya uhusiano wa mtu pamoja na jamaa zake na marafiki wake uharibike. Isitoshe, Neno la Mungu linasema kwamba wale ‘wanaozoea mambo hayo hawataurithi ufalme wa Mungu.’

Kinyume cha hilo, Mungu huwapa roho yake wale wanaositawisha “matunda ya roho.” Matunda hayo yanatia ndani sifa ya “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia.” (Wagalatia 5:22, 23) Tunapoonyesha sifa hizo, sisi hufanya iwezekane kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na wengine na pamoja na Mungu, jambo ambalo hutokeza furaha ya kweli. (Ona sanduku.) Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba kwa kuonyesha upendo, fadhili, wema, na sifa nyingine za kimungu, tunampendeza Yehova na kuwa na tumaini lenye kufurahisha la kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.

Unaweza Kuamua Kuwa Mwenye Furaha

Wakati Wolfgang na Brigitte, wenzi wa ndoa wanaoishi Ujerumani, walipoanza kujifunza Biblia kwa bidii, walikuwa na vitu vingi vya kimwili ambavyo watu huhisi vinahitajiwa ili kuwa na furaha. Walikuwa na umri mdogo na afya nzuri. Walivaa nguo za bei kubwa, waliishi katika nyumba iliyopambwa vizuri, na walikuwa na biashara nzuri. Walitumia muda mwingi kufuatia vitu zaidi vya kimwili, lakini hawakupata furaha ya kweli kwa kufanya hivyo. Hata hivyo, baada ya muda, Wolfgang na Brigitte walifanya uamuzi muhimu. Walianza kutumia wakati na jitihada nyingi zaidi kufuatia mambo ya kiroho na kutafuta njia za kumkaribia Yehova zaidi. Muda si muda, uamuzi wao ulifanya wabadili mtazamo wao, na jambo hilo likawachochea kurahisisha maisha yao na kutumika wakiwa mapainia, au waeneza-injili wa Ufalme wa wakati wote. Leo, wanafanya kazi ya kujitolea kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani. Isitoshe, wanajifunza lugha fulani ya Asia ili wawasaidie wageni wajifunze kweli ya Neno la Mungu, Biblia.

Je, wenzi hao wa ndoa walipata furaha ya kweli? Wolfgang anasema: “Tangu tulipoanza kufuatia zaidi mambo ya kiroho, tumekuwa wenye furaha zaidi na kuridhika zaidi. Pia kumtumikia Yehova kwa moyo wote kumeimarisha ndoa yetu. Ndoa yetu ilikuwa yenye furaha hapo awali, lakini tulikuwa na madaraka na mapendezi yaliyofanya tuwe na miradi tofauti. Sasa tumeungana kufuatia mradi mmoja.”

Ni Nini Kinachohitajiwa ili Kuwa na Furaha?

Kwa ufupi: Epuka “matendo ya mwili,” na usitawishe “matunda ya roho ya [Mungu].” Ili kuwa na furaha, mtu anapaswa kutamani kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Mtu anayejitahidi kutimiza jambo hilo atakuwa mwenye furaha kama Yesu alivyosema.

Kwa hiyo, usikate kauli kimakosa kwamba huwezi kuwa na furaha. Ni kweli kwamba afya yako inaweza kuwa si nzuri kwa sasa au labda una matatizo katika ndoa yako. Labda sasa huwezi kupata watoto au unajitahidi kutafuta kazi nzuri. Labda huna pesa nyingi kama zamani. Hata hivyo, jipe moyo; hupaswi kukata tamaa! Ufalme wa Mungu utatatua matatizo hayo na mengine mengi. Kwa kweli, hivi karibuni, Yehova Mungu atatimiza ahadi iliyotajwa na mtunga-zaburi: “Ufalme wako ni ufalme kwa nyakati zote zisizo na kipimo . . . Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:13, 16) Kama vile mamilioni ya watumishi wa Yehova ulimwenguni pote wanavyoweza kushuhudia, kukumbuka ahadi hiyo ya Yehova yenye kufariji kutakusaidia sana kuwa mwenye furaha leo.—Ufunuo 21:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kila moja ya taarifa hizo tisa za Yesu inaanza kwa neno la Kigiriki ma·kaʹri·oi. Badala ya kutafsiri neno hilo kuwa “wabarikiwa,” kama tafsiri nyingine zinavyofanya, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyinginezo, kama vile The Jerusalem Bible na Today’s English Version, hutumia neno lililo sahihi zaidi ambalo ni “furaha.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Mambo Yanayochangia Furaha

Upendo huwachochea wengine wakupende.

Shangwe hukuimarisha kukabiliana na magumu.

Amani hukusaidia kudumisha mahusiano mazuri.

Ustahimilivu hukuwezesha uendelee kuwa mwenye furaha hata unapokuwa chini ya jaribu.

Fadhili huwavuta wengine kwako.

Wema hufanya wengine watake kukusaidia unapohitaji msaada.

Imani itakuhakikishia kwamba Mungu atakuongoza kwa upendo.

Upole utakupa utulivu wa moyo, akili, na mwili.

Kujizuia kunamaanisha kwamba makosa yako yatakuwa machache zaidi.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ili kupata furaha, unahitaji kutosheleza mahitaji yako ya kiroho