Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yenye Kuridhisha na Yenye Furaha ya Kujidhabihu kwa Kupenda

Maisha Yenye Kuridhisha na Yenye Furaha ya Kujidhabihu kwa Kupenda

Simulizi la Maisha

Maisha Yenye Kuridhisha na Yenye Furaha ya Kujidhabihu kwa Kupenda

LIMESIMULIWA NA MARIAN NA ROSA SZUMIGA

“Nitakutolea dhabihu kwa kupenda,” yasema Zaburi 54:6. Maneno hayo yamekuwa muhimu sana katika maisha ya Marian Szumiga na mke wake Rosa, wanaoishi Ufaransa. Hivi karibuni, walisimulia baadhi ya mambo makuu katika maisha yao marefu na yenye kuridhisha katika utumishi wa Yehova.

MARIAN: Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki ambao walihama kutoka Poland. Baba alikuwa mtu mnyenyekevu ambaye hakuwahi kwenda shule. Hata hivyo, wakati wa vita vya kwanza vya ulimwengu, alijifunza kusoma na kuandika alipokuwa vitani. Baba alikuwa mtu aliyemwogopa Mungu, lakini mara nyingi kanisa lilimkatisha tamaa.

Kuna tukio moja hasa ambalo hakulisahau kamwe. Siku moja wakati wa vita, kasisi mmoja alitembelea kikosi cha jeshi cha Baba. Kombora lilipolipuka karibu na kikosi hicho, kasisi huyo alitimua mbio kwa woga, huku akimpiga farasi wake kwa msalaba ili akimbie. Baba alishangaa kuona “mwakilishi” wa Mungu akitumia kitu “kitakatifu” ili aponyoke haraka. Licha ya mambo hayo na maafa aliyojionea vitani, imani ya Baba katika Mungu haikudhoofika. Mara nyingi alimshukuru Mungu aliporudi salama kutoka vitani.

“Poland Ndogo”

Mwaka wa 1911, baba yangu alifunga ndoa na msichana mmoja aliyeitwa Anna Cisowski, kutoka kijiji jirani. Punde baada ya vita, mwaka wa 1919, Baba na Mama walihama Poland na kwenda Ufaransa ambako Baba alipata kazi katika migodi ya makaa ya mawe. Nilizaliwa mnamo Machi 1926 huko Cagnac-les-Mines kusini-magharibi mwa Ufaransa. Baadaye, wazazi wangu waliishi katika jamii ya Wapoland huko Loos-en-Gohelle, karibu na Lens, kaskazini mwa Ufaransa. Mwokaji wa mahali hapo alikuwa Mpoland, muuza-nyama alikuwa Mpoland, naye kasisi wa parokia pia alikuwa Mpoland. Si ajabu kwamba eneo hilo liliitwa Poland Ndogo. Wazazi wangu walishiriki katika shughuli za kijamii. Mara nyingi baba alipanga maonyesho, ambayo yalitia ndani kusimulia hadithi, kucheza muziki, na kuimba. Pia, alizungumza kwa ukawaida na kasisi, lakini kila mara kasisi alipojibu, “Mambo mengi ni mafumbo,” yeye hakuridhika.

Siku moja mwaka wa 1930, wanawake wawili walibisha mlango wetu. Walikuwa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Baba alipata Biblia kutoka kwao, kitabu ambacho kwa miaka mingi alitamani kukisoma. Yeye na Mama pia walisoma kwa hamu nyingi vichapo vinavyozungumzia Biblia, ambavyo wanawake hao waliwaachia. Wazazi wangu waliguswa moyo sana na mambo waliyosoma katika vichapo hivyo. Licha ya kuwa na shughuli nyingi maishani, wazazi wangu walianza kuhudhuria mikutano iliyopangwa na Wanafunzi wa Biblia. Mazungumzo pamoja na kasisi yalizidi kuwa makali hadi siku moja akatisha kwamba ikiwa wazazi wangu wataendelea kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia, dada yangu Stéphanie angefukuzwa kutoka katekisimu. “Usijisumbue,” baba akamjibu. “Tangu sasa na kuendelea, binti yangu na pia wale watoto wengine wataenda pamoja nasi kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia.” Baba alijiondoa kanisani, na mapema mwaka wa 1932, wazazi wangu wakabatizwa. Wakati huo, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme wapatao 800 tu nchini Ufaransa.

Rosa: Wazazi wangu walitoka Hungaria na, kama vile familia ya Marian, waliishi kaskazini ya Ufaransa ambako walifanya kazi katika migodi ya makaa ya mawe. Nilizaliwa mwaka wa 1925. Mnamo 1937, Shahidi mmoja wa Yehova, Auguste Beugin, au Papa Auguste kama tulivyomwita, alianza kuwaletea wazazi wangu Mnara wa Mlinzi katika Kihungaria. Walipendezwa na magazeti hayo lakini hakuna hata mmoja wao aliyepata kuwa Shahidi wa Yehova.

Ingawa nilikuwa mdogo, moyo wangu uliguswa na yale niliyosoma katika Mnara wa Mlinzi, naye Suzanne Beugin, binti-mkwe wa Papa Auguste, akapendezwa nami kibinafsi. Wazazi wangu walimruhusu kwenda nami mikutanoni. Baadaye, wakati nilipoanza kufanya kazi, baba alikasirika kuona nikihudhuria mikutano Jumapili. Ingawa alikuwa mwema kiasili, alilalamika, “Katikati ya juma hupatikani nyumbani na Jumapili unaenda kwenye mikutano yenu!” Lakini, niliendelea kwenda mikutanoni. Hivyo, siku moja baba akaniambia, “Funga virago vyako na uondoke!” Ilikuwa jioni sana. Nilikuwa na umri wa miaka 17 tu, na sikujua niende wapi. Niliishia nyumbani kwa Suzanne, huku nikilia sana. Nilikaa na Suzanne karibu juma moja hivi kabla ya Baba kumtuma dada yangu anichukue ili nirudi nyumbani. Nilikuwa mwenye haya kiasili, lakini wazo linalotajwa kwenye 1 Yohana 4:18 lilinisaidia kusimama imara. Andiko hilo linaonyesha kwamba “upendo mkamilifu hutupa woga nje.” Nilibatizwa mwaka wa 1942.

Urithi wa Kiroho Wenye Thamani

Marian: Nilibatizwa mwaka wa 1942, pamoja na dada zangu Stéphanie na Mélanie na ndugu yangu Stéphane. Nyumbani, familia yetu ilikazia fikira Neno la Mungu. Sote tulipokuwa tumeketi kuizunguka meza, Baba alitusomea Biblia katika Kipoland. Mara nyingi tulitumia jioni zetu kusikiliza wazazi wetu walipotuelezea mambo yaliyoonwa katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Nyakati hizo zenye kutuimarisha kiroho zilitufunza kumpenda Yehova na kumtegemea zaidi na zaidi. Afya mbaya ilimlazimisha baba aache kazi, lakini aliendelea kututunza kiroho na kimwili.

Kwa kuwa sasa Baba alikuwa na wakati wa ziada, aliongoza funzo la Biblia mara moja kwa juma katika Kipoland pamoja na vijana kutanikoni. Huko nilijifunza kusoma Kipoland. Pia Baba aliwatia moyo vijana kwa njia mbalimbali. Wakati Ndugu Gustave Zopfer, ambaye wakati huo alisimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa, alipotembelea kutaniko letu, Baba alipanga kwaya, na pia drama ya Biblia kuhusu ile karamu ya Mfalme Belshaza na mwandiko ukutani. (Danieli 5:1-31) Sehemu ya Danieli iliigizwa na Louis Piéchota, ambaye baadaye alisimama imara dhidi ya Nazi. * Hayo ndiyo mazingira ambamo sisi watoto tulilelewa. Tuliona kwamba sikuzote wazazi wetu walikuwa wenye shughuli nyingi katika mambo ya kiroho. Leo, ninatambua kwamba wazazi wetu walituachia urithi wenye thamani sana.

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza mwaka wa 1939, kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku nchini Ufaransa. Pindi moja, kijiji chetu kilisakwa. Nyumba zote zilizingirwa na askari wa Ujerumani. Baba alikuwa ametengeneza sakafu bandia chini ya kabati moja, nasi tulificha vichapo mbalimbali vya Biblia chini ya sakafu hiyo. Hata hivyo, nakala kadhaa za kijitabu Fascism or Freedom zilikuwa katika kabati moja. Baba alizificha upesi katika mfuko wa koti moja iliyoning’inizwa kwenye ukuta wa njia ndogo ya kuingia vyumbani. Askari wawili na polisi mmoja Mfaransa walipekua nyumba yetu. Tulingoja kwa wasiwasi. Mmoja wa askari hao alianza kupekua-pekua mavazi yaliyoning’inizwa kwenye ukuta huo, na upesi baadaye akaingia jikoni ambapo tulikuwa, akiwa na vijitabu mkononi mwake. Alitukazia macho, akaweka vijitabu hivyo kwenye meza, naye akaendelea kufanya upekuzi mahali kwingine. Nilivichukua haraka na kuviweka ndani ya kabati ambayo tayari askari walikuwa wameipekua. Askari huyo hakuuliza kuhusu vijitabu hivyo—ni kana kwamba alivisahau kabisa!

Kuanza Utumishi wa Wakati Wote

Mwaka wa 1948, niliamua kujitoa kumtumikia Yehova wakati wote nikiwa painia. Siku chache baadaye, nilipokea barua kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa. Katika barua hiyo nilipata mgawo wa kutumika nikiwa painia katika kutaniko la Sedan, karibu na Ubelgiji. Wazazi wangu walifurahi sana kuona nimeanza kumtumikia Yehova wakati wote. Kwa upande mwingine, baba alisema kwamba kazi ya upainia haingekuwa rahisi. Ingekuwa kazi ngumu. Hata hivyo, alisema kwamba sikuzote ningeweza kurudi nyumbani kwake na kwamba ningeweza kumwomba msaada ikiwa ningepatwa na matatizo. Wazazi wangu walininunulia baiskeli ingawa hawakuwa na pesa nyingi. Bado ningali na risiti ya baiskeli hiyo, na ninapoitazama, macho yangu hujaa machozi. Baba na Mama walikufa mwaka wa 1961, lakini bado ninayakumbuka maneno ya Baba yenye hekima; yamenitia moyo na kunifariji katika miaka yangu yote ya utumishi.

Mtu mwingine aliyenitia moyo ni dada mmoja Mkristo katika kutaniko la Sedan aliyeitwa Elise Motte, mwenye umri wa miaka 75. Wakati wa kiangazi, nilisafiri kwa baiskeli kwenda kuhubiri vijiji vya mbali, naye Elise alinifuata kwa gari-moshi. Hata hivyo, siku moja mainjinia wa gari-moshi walifanya mgomo, naye Elise hangeweza kurudi nyumbani. Suluhisho pekee ambalo ningeweza kufikiria ni kumbeba kwa baiskeli yangu na kumpeleka nyumbani—njia ya kusafiri ambayo si yenye kustarehesha. Asubuhi iliyofuata, nilileta mto na kumbeba Elise nyumbani kwake. Aliacha kusafiri kwa gari-moshi, na pesa za nauli alizohifadhi, alitununulia kinywaji chenye moto wakati wa chakula cha mchana. Nani angefikiria kwamba baiskeli yangu ingetumika kama usafiri wa umma?

Madaraka Zaidi

Mwaka wa 1950, niliombwa nitumikie nikiwa mwangalizi wa mzunguko katika eneo lote la kaskazini mwa Ufaransa. Kwanza kabisa nilikuwa na wasiwasi kwa kuwa nilikuwa na umri wa miaka 23 tu. Nilifikiri kwamba ofisi ya tawi ilikosea! Nilifikiria maswali mengi: ‘Je, ninastahili kiroho na kimwili kufanya kazi hii? Ninawezaje kuvumilia kulala sehemu mbalimbali kila juma?’ Zaidi ya hayo, tangu umri wa miaka sita, nimekuwa na shida ya macho inayoitwa makengeza. Hali hiyo hufanya jicho langu moja liangalie upande. Kwa sababu hiyo, sikuzote nimekuwa mwenye haya, nikiwa na wasiwasi kuhusu jinsi wengine watakavyoitikia. Ninashukuru kwamba, wakati huo nilisaidiwa sana na Stefan Behunick, mhitimu wa shule ya umishonari ya Gileadi. Ndugu Behunick alikuwa amefukuzwa kutoka Poland kwa sababu ya kuhubiri, naye alipewa mgawo mpya huko Ufaransa. Uhodari wake ulinichochea sana. Alimheshimu Yehova sana na pia ile kweli. Wengine walifikiri kwamba alikuwa mgumu kwangu, lakini alinifunza mambo mengi. Ujasiri wake ulinisaidia kujiamini zaidi.

Kazi ya mzunguko iliniwezesha kufurahia mambo fulani mazuri yaliyoonwa katika utumishi wa shambani. Mwaka wa 1953, niliombwa kumtembelea mtu mmoja aliyeitwa Bwana Paoli, ambaye aliishi kusini ya Paris na aliyekuwa ameandikisha gazeti Mnara wa Mlinzi. Tulikutana, nami nikapata kujua kwamba alikuwa amestaafu kutoka jeshi na kwamba alivutiwa sana na gazeti Mnara wa Mlinzi. Aliniambia kwamba baada ya kusoma makala fulani kuhusu Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika gazeti la karibuni, aliadhimisha Ukumbusho akiwa peke yake, naye akatumia jioni hiyo kusoma Zaburi. Tulizungumza karibu alasiri yote. Kabla sijaondoka, tulizungumza kwa ufupi kuhusu ubatizo. Baadaye, nilimtumia mwaliko ili ahudhurie kusanyiko letu la mzunguko ambalo lingefanywa mapema mnamo 1954. Ndugu Paoli alikuja, na akawa kati ya watu 26 waliobatizwa kwenye kusanyiko hilo. Mambo kama hayo bado yananiletea shangwe.

Rosa: Mnamo Oktoba 1948, nilianza utumishi wa painia. Baada ya kutumika huko Anor, karibu na Ubelgiji, mimi na painia mwingine, Irène Kolanski (sasa Leroy), tulipewa mgawo wa kwenda Paris. Tuliishi katika chumba kidogo sana huko Saint-Germain-des Près katikati ya jiji. Kwa kuwa nililelewa mashambani, niliwaogopa watu wa Paris. Nilifikiri kwamba wote walikuwa wastaarabu na wenye akili sana. Lakini upesi baada ya kuwahubiria nikajua kwamba walikuwa sawa na watu wengine. Mara nyingi tulifukuzwa na walinzi, na ilikuwa vigumu kuanzisha mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, baadhi ya watu walikubali ujumbe wetu.

Wakati wa kusanyiko moja la mzunguko mwaka wa 1951, mimi na Irène tulihojiwa kuhusu utumishi wetu wa painia. Je, unaweza kuwazia ni nani aliyetuhoji? Kijana mmoja aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko ambaye aliitwa Marian Szumiga. Tulikuwa tumekutana kabla ya hapo, lakini baada ya kusanyiko hilo, tulianza kuandikiana barua. Mimi na Marian tulikuwa na mambo mengi yaliyofanana, tulibatizwa mwaka mmoja na hata tukaanza upainia mwaka mmoja. Jambo muhimu zaidi ni kwamba, sote tulitaka kuendelea na utumishi wa wakati wote. Hivyo, baada ya kufikiria jambo hilo katika sala, tulifunga ndoa Julai  31, 1956. Baada ya kufunga ndoa, maisha yangu yalibadilika kabisa. Ilinibidi kuzoea kuwa mke na pia kuandamana na Marian katika kazi ya mzunguko, jambo ambalo lilimaanisha kukaa katika nyumba tofauti kila juma. Mwanzoni, ilikuwa vigumu sana, lakini shangwe kubwa ilikuwa mbele yetu.

Maisha Yenye Kuridhisha

Marian: Kwa miaka mingi, tumepata pendeleo la kusaidia katika kutayarisha makusanyiko mengi ya wilaya. Ninakumbuka hasa kusanyiko lililofanywa huko Bordeaux, mwaka wa 1966. Wakati huo, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku huko Ureno. Hivyo, programu ya kusanyiko ilitolewa pia katika Kireno ili kuwanufaisha Mashahidi waliosafiri kwenda Ufaransa. Mamia ya ndugu na dada zetu Wakristo kutoka Ureno walifika, lakini tatizo lilikuwa kupata mahali pa kulala. Kwa kuwa Mashahidi wa Bordeaux hawakuwa na nafasi za kutosha katika nyumba zao, tulikodi jumba tupu la sinema ili kulitumia kama mahali pa kulala. Tuliondoa viti vyote, nayo pazia ya jukwaani ilitumiwa kuligawanya jumba katika sehemu mbili za kulala, moja kwa ajili ya akina ndugu na nyingine kwa ajili ya akina dada. Tuliweka pia mabomba na vidimbwi vya kuogea, tukatia nyasi kavu kwenye sakafu, na kuifunika kwa shuka nzito. Kila mtu aliridhika na mpango huo.

Baada ya vipindi vya kusanyiko, tuliwatembelea ndugu na dada zetu mahali walipolala. Hali ilikuwa nzuri sana. Tulitiwa moyo sana na mambo yaliyowapata licha ya kuvumilia miaka mingi ya upinzani. Walipoondoka mwishoni mwa kusanyiko, macho yetu sote yalijaa machozi.

Tulipata pendeleo lingine miaka miwili mapema, mwaka wa 1964, wakati nilipoombwa niwe mwangalizi wa wilaya. Kwa mara nyingine tena nilijiuliza kama nilikuwa na sifa za kunistahilisha kuwa mwangalizi wa wilaya. Lakini niliwaza kwamba ikiwa wale walio na madaraka waliniomba nikubali mgawo huo, yaelekea waliona kwamba ninaweza kuutimiza. Lilikuwa jambo zuri kufanya kazi kwa ukaribu na waangalizi wengine wasafirio. Walinifunza mambo mengi. Wengi wao ni vielelezo vizuri vya subira na uvumilivu, sifa ambazo ni muhimu machoni pa Yehova. Nimepata kuelewa kwamba tukijifunza kuwa na subira, Yehova anajua mahali pa kutupata.

Mwaka wa 1982, ofisi ya tawi ilituomba tena kushughulikia kikundi kidogo cha wahubiri 12 wanaozungumza Kipoland huko Boulogne-Billancourt, kwenye vitongoji vya Paris. Hilo lilinishangaza. Nilijua maneno ya kitheokrasi katika Kipoland, lakini nilikuwa na tatizo la kuunda sentensi. Hata hivyo, fadhili na utayari wa ndugu hao wa kushirikiana ulinisaidia sana. Leo, kuna wahubiri 170 hivi katika kutaniko hilo, kutia ndani mapainia karibu 60. Baadaye, mimi na Rosa tulitembelea pia vikundi na makutaniko ya lugha ya Kipoland huko Austria, Denmark, na Ujerumani.

Hali Zenye Kubadilika

Tulikuwa tumezoea kutembelea makutaniko tofauti-tofauti, lakini kwa sababu ya afya yangu mbaya ilitubidi tuache kazi yetu ya kusafiri mwaka wa 2001. Tulipata nyumba katika mji wa Pithiviers, ambapo dada yangu Ruth anaishi. Kwa fadhili, ofisi ya tawi ilituweka kuwa mapainia wa pekee na kuturuhusu tuhubiri kiwango cha saa tunachoweza kulingana na hali zetu.

Rosa: Mwaka wa kwanza baada ya sisi kuacha kazi ya mzunguko ulikuwa mgumu sana kwangu. Badiliko hilo lilikuwa kubwa sana hivi kwamba nilijihisi kuwa sifai. Kisha nikajikumbusha, ‘Bado unaweza kutumia kwa matokeo wakati na nguvu ulizo nazo kutumika ukiwa painia.’ Leo, ninafurahia kutumika pamoja na mapainia wengine katika kutaniko letu.

Yehova Ametutunza Sikuzote

Marian: Ninamshukuru sana Yehova kwamba Rosa amekuwa mwandamani wangu kwa miaka 48 iliyopita. Amenitegemeza sana muda wa miaka hiyo yote katika kazi ya kusafiri. Sijawahi kumsikia akisema, ‘Laiti tungeacha kazi ya kusafiri na kuwa na makao yetu wenyewe.’

Rosa: Nyakati nyingine watu walikuwa wakiniambia, “Maisha yenu si ya kawaida. Sikuzote ninyi huishi pamoja na watu wengine.” Lakini kwa kweli “maisha ya kawaida” ni nini? Wakati mwingine sisi hujirundikia vitu vingi ambavyo huenda vikatuzuia kufuatia shughuli za kiroho. Kwa kweli, tunachohitaji tu ni kitanda kizuri, meza, na mambo mengine madogo ya msingi. Tukiwa mapainia, tulikuwa na vitu vichache sana vya kimwili, hata hivyo tulikuwa na kila kitu tulichohitaji ili kufanya mapenzi ya Yehova. Nyakati nyingine niliulizwa, “Mtafanya nini mtakapozeeka mkiwa bila makao yenu wenyewe wala malipo ya uzeeni?” Halafu ningenukuu maneno ya Zaburi 34:10: “Kwa wale wanaomtafuta Yehova, hawatakosa chochote chema.” Yehova ametutunza sikuzote.

Marian: Hilo ni kweli! Naam, Yehova ametupatia mengi zaidi kuliko ilivyo lazima. Kwa mfano, mwaka wa 1958, nilichaguliwa kuwakilisha mzunguko wetu kwenye Kusanyiko la Kimataifa huko New York. Hata hivyo, hatukuwa na pesa za kumlipia Rosa nauli. Jioni moja ndugu fulani alitupatia bahasha iliyoandikwa “New York.” Zawadi iliyokuwemo ilimwezesha Rosa kusafiri pamoja nami!

Mimi na Rosa hatujuti hata kidogo kuhusu miaka yetu katika utumishi wa Yehova. Hatukupoteza chochote bali tulipata kila kitu, yaani, maisha yenye kuridhisha na yenye furaha katika utumishi wa wakati wote. Yehova ni Mungu mzuri sana. Tumejifunza kumtumaini kabisa, nao upendo wetu kwake umeongezeka. Baadhi ya ndugu zetu Wakristo wameteswa na kuuawa kwa sababu ya uaminifu wao. Hata hivyo, ninaamini kwamba kwa miaka mingi, mtu anaweza pia kudhabihu maisha yake siku baada ya siku. Hilo ndilo mimi na Rosa tumejitahidi kufanya mpaka sasa, nasi tumeazimia kufanya hivyo wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Simulizi la maisha la Louis Piéchota “Niliokoka Msafara wa Kifo,” lilichapishwa katika Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 1980 katika Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 20]

François na Anna Szumiga na watoto wao, Stéphanie, Stéphane, Mélanie, na Marian yapata mwaka wa 1930. Marian anasimama juu ya kiti

[Picha katika ukurasa wa 22]

Juu: Kutoa vichapo vya Biblia sokoni huko Armentières, kaskazini mwa Ufaransa, mwaka wa 1950

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kushoto: Stefan Behunick pamoja na Marian mwaka wa 1950

[Picha katika ukurasa wa 23]

Marian na Rosa siku moja kabla ya arusi yao

[Picha katika ukurasa wa 23]

Rosa (mbali kushoto) pamoja na painia mwenzake Irène (wa nne kutoka kushoto), wakitangaza kusanyiko moja mwaka wa 1951

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakati wa ziara za mzunguko tulisafiri hasa kwa baiskeli