Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Mashahidi wa Yehova husema kwamba ile hesabu 144,000 inayotajwa katika kitabu cha Ufunuo ni halisi wala si ya mfano?

Mtume Yohana aliandika hivi: “Nikaisikia hesabu ya wale waliotiwa muhuri, 144,000.” (Ufunuo 7:4) Katika Biblia, usemi “wale waliotiwa muhuri” unarejelea kikundi cha watu ambao wamechaguliwa kati ya wanadamu wakatawale pamoja na Kristo mbinguni juu ya dunia Paradiso inayokuja. (2 Wakorintho 1:21, 22; Ufunuo 5:9, 10; 20:6) Hesabu yao, 144,000 hueleweka kuwa halisi kwa sababu kadhaa. Sababu moja inapatikana katika muktadha wa Ufunuo 7:4.

Baada ya mtume Yohana kuelezwa katika maono kuhusu kikundi hicho cha watu 144,000, alionyeshwa kikundi kingine. Yohana anakifafanua kikundi hiki cha pili kuwa “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Umati huo mkubwa unarejelea wale watakaookoka “dhiki kubwa” inayokuja ambayo itaharibu ulimwengu mwovu wa sasa.—Ufunuo 7:9, 14.

Hata hivyo, ona tofauti ambayo Yohana anaonyesha kati ya mstari wa 4 na wa 9 katika Ufunuo sura ya 7. Anasema kwamba hesabu ya kikundi cha kwanza, cha “wale waliotiwa muhuri,” ni hususa. Hata hivyo, hesabu ya kikundi cha pili, “umati mkubwa,” si hususa. Kwa kufikiria hilo, ni jambo linalopatana na akili kuiona ile hesabu 144,000 kuwa halisi. Kama hesabu hiyo 144,000 ingekuwa ya mfano, na iwe inarejelea kikundi kisichoweza kuhesabiwa, basi hakungekuwa na tofauti yoyote kati ya mistari hiyo miwili. Kwa hiyo, muktadha unathibitisha kwamba ile hesabu 144,000 lazima iwe halisi.

Wasomi kadhaa wa Biblia wa zamani na wa sasa walikata kauli ileile, yaani, hesabu hiyo ni halisi. Kwa mfano, akielezea andiko la Ufunuo 7:4, 9, mtunga-kamusi Mwingereza Dakt. Ethelbert W. Bullinger alisema hivi miaka ipatayo 100 iliyopita: “Hiyo ni taarifa iliyo rahisi na wazi: hesabu hususa inalinganishwa na hesabu isiyo hususa katika sura hiihii.” (The Apocalypse or “The Day of the Lord,” ukurasa wa 282) Hivi karibuni, Robert L. Thomas, Jr., profesa wa Agano Jipya kwenye chuo cha theolojia kiitwacho The Master’s Seminary huko Marekani, aliandika hivi: “Hakuna msingi wowote wa kuiona hesabu hiyo kuwa ya mfano.” Aliongeza kusema: “Hiyo ni hesabu hususa [kwenye 7:4] tofauti na hesabu isiyo hususa kwenye 7:9. Hesabu hiyo ikionwa kuwa ya mfano, hakuna hesabu yoyote katika kitabu hicho inayoweza kuchukuliwa kuwa halisi.”—Revelation: An Exegetical Commentary, Buku la 1, ukurasa wa 474.

Wengine hudai kwamba kwa kuwa kitabu cha Ufunuo kinatumia sana lugha ya mfano, hesabu zote zinazopatikana katika kitabu hiki, kutia ndani ile hesabu 144,000 lazima ziwe za mfano. (Ufunuo 1:1, 4; 2:10) Hata hivyo, ni wazi kwamba kauli hiyo si sahihi. Ni kweli kwamba kitabu cha Ufunuo kina hesabu nyingi za mfano, lakini pia kina hesabu halisi. Kwa mfano, Yohana anazungumza kuhusu yale “majina kumi na mawili ya mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 21:14) Bila shaka, hesabu 12 inayotajwa katika mstari huu ni halisi, si ya mfano. Isitoshe, mtume Yohana anaandika kuhusu “ile miaka elfu” ya utawala wa Kristo. Hesabu hiyo pia inapaswa kuonwa kuwa halisi kama tunavyoona tunapoichunguza Biblia kwa makini. * (Ufunuo 20:3, 5-7) Hivyo, kama hesabu fulani katika kitabu cha Ufunuo itaonwa kuwa halisi au ya mfano, itategemea muktadha wake.

Wazo la kwamba ile hesabu 144,000 ni halisi na kwamba inarejelea idadi ndogo ya watu, ambao ni wachache wanapolinganishwa na “umati mkubwa,” pia linapatana na mistari mingine ya Biblia. Kwa mfano, baadaye katika maono ambayo Yohana anapokea, wale 144,000 wanatajwa kuwa ‘walionunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza.’ (Ufunuo 14:1, 4) Usemi “matunda ya kwanza” unarejelea wawakilishi wachache. Pia, Yesu alipokuwa duniani, alizungumza kuhusu wale ambao wangetawala pamoja naye katika Ufalme wake wa mbinguni na kuwaita “kundi dogo.” (Luka 12:32; 22:29) Kwa kweli, wale kati ya wanadamu watakaokuwa watawala mbinguni ni wachache wanapolinganishwa na wale wanadamu watakaoishi katika dunia Paradiso inayokuja.

Kwa hiyo, muktadha wa Ufunuo 7:4 na habari nyingine inayohusiana na hiyo ambayo imetajwa katika sehemu nyingine ya Biblia inathibitisha kwamba ile hesabu 144,000 inapaswa kuonwa kuwa halisi. Inarejelea wale watakaotawala mbinguni pamoja na Kristo juu ya dunia paradiso, ambayo itajaa watu wengi wenye furaha na wasio na hesabu wanaomwabudu Yehova Mungu.—Zaburi 37:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kwa habari zaidi kuhusu Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! ukurasa wa 289-290, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 31]

Hesabu ya warithi wa kimbingu haizidi 144,000

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ule “umati mkubwa” hauwezi kuhesabiwa

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

Stars: Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin