Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtukuzeni Mungu “Kwa Kinywa Kimoja”

Mtukuzeni Mungu “Kwa Kinywa Kimoja”

Mtukuzeni Mungu “Kwa Kinywa Kimoja”

‘Kwa kinywa kimoja mtukuzeni Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.’—WAROMA 15:6.

1. Paulo aliwaeleza waamini wenzake jambo gani kuhusu kushughulikia maoni yanayotofautiana?

SI WAKRISTO wote wanaofanya uchaguzi uleule au walio na mapendezi yaleyale. Hata hivyo, Wakristo wote wanapaswa kutembea bega kwa bega kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima. Je, hilo linawezekana? Ndiyo, ikiwa haturuhusu tofauti ndogo-ndogo ziwe matatizo makubwa. Hilo ni jambo ambalo mtume Paulo aliwaeleza waamini wenzake katika karne ya kwanza. Alielezaje jambo hilo muhimu? Nasi leo tunawezaje kutumia shauri lake lililoongozwa na roho ya Mungu?

Umuhimu wa Umoja wa Kikristo

2. Paulo alikaziaje uhitaji wa kuwa na umoja?

2 Paulo alijua kwamba umoja wa Kikristo ni muhimu, naye alitoa shauri zuri ili kuwasaidia Wakristo wavumiliane kwa upendo. (Waefeso 4:1-3; Wakolosai 3:12-14) Hata hivyo, baada ya kuanzisha makutaniko mengi na kutembelea mengine katika muda wa miaka zaidi ya 20, Paulo alijua kwamba linaweza kuwa jambo gumu kudumisha umoja. (1 Wakorintho 1:11-13; Wagalatia 2:11-14) Hivyo, aliwahimiza hivi waamini wenzake waliokuwa wakiishi Roma: “Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awawezeshe . . . ili kwa umoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (Waroma 15:5, 6) Leo pia tunapaswa kumtukuza Yehova Mungu “kwa kinywa kimoja” tukiwa kikundi cha watu wake wenye umoja. Sisi hufanya hivyo kwa kadiri gani?

3, 4. (a) Wakristo huko Roma walikuwa na malezi gani tofauti-tofauti? (b) Wakristo huko Roma wangewezaje kumtumikia Yehova “kwa kinywa kimoja”?

3 Wakristo wengi huko Roma walikuwa marafiki wa kibinafsi wa Paulo. (Waroma 16:3-16) Ingawa malezi yao yalikuwa tofauti, Paulo aliwakubali ndugu zake wote kama “wapendwa wa Mungu.” Aliandika: “Namshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuhusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa kotekote ulimwenguni.” Ni wazi kwamba Waroma walikuwa kielelezo kizuri katika njia nyingi. (Waroma 1:7, 8; 15:14) Wakati huohuo, baadhi ya washiriki wa kutaniko walikuwa na maoni tofauti kuhusu mambo fulani. Kwa kuwa leo Wakristo wametoka katika malezi na tamaduni mbalimbali, kuchunguza shauri la Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu kuhusu jinsi ya kushughulikia tofauti kati yao, kunaweza kuwasaidia wazungumze “kwa kinywa kimoja.”

4 Huko Roma kulikuwa na waamini Wayahudi na wasio Wayahudi. (Waroma 4:1; 11:13) Yaonekana Wakristo fulani Wayahudi hawakuacha desturi fulani ambazo walikuwa wamezishika chini ya Sheria ya Musa, hata ingawa walipaswa kuwa wametambua kwamba desturi hizo hazikuwa muhimu kwa wokovu. Kwa upande mwingine, Wakristo kadhaa Wayahudi walikubali kwamba dhabihu ya Kristo iliwaweka huru kutokana na vizuizi fulani walivyofuata kabla ya kuwa Wakristo. Kwa sababu hiyo, walibadili baadhi ya tabia na desturi zao. (Wagalatia 4:8-11) Hata hivyo, kama Paulo alivyosema, wote walikuwa “wapendwa wa Mungu.” Wote wangeweza kumtukuza Mungu “kwa kinywa kimoja” ikiwa tu wangedumisha mtazamo wa akili unaofaa kuelekea mmoja na mwenzake. Leo, huenda sisi pia tukawa na maoni tofauti-tofauti kuhusu mambo fulani, hivyo tunapaswa kuchunguza kwa makini jinsi Paulo anavyoeleza kanuni hiyo muhimu.—Waroma 15:4.

“Mkaribishane”

5, 6. Kwa nini kulikuwa na maoni tofauti katika kutaniko la Roma?

5 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo anataja kisa fulani ambapo maoni yalitofautiana. Anaandika: “Mtu mmoja ana imani ya kula kila kitu, lakini mtu aliye dhaifu hula mboga za majani.” Kwa nini ilikuwa hivyo? Sheria ya Musa ilikataza kula nyama ya nguruwe. (Waroma 14:2; Mambo ya Walawi 11:7) Hata hivyo, haikuwa lazima kufuata Sheria hiyo baada ya Yesu kufa. (Waefeso 2:15) Kisha, miaka mitatu na nusu baada ya Yesu kufa, malaika alimwambia mtume Petro kwamba kulingana na maoni ya Mungu hakuna chakula kinachopaswa kuonwa kuwa najisi. (Matendo 11:7-12) Kwa kufikiria mambo hayo, huenda Wakristo fulani Wayahudi walihisi kwamba wangeweza kula nyama ya nguruwe—au kula vyakula vingine vilivyokuwa vimekatazwa chini ya Sheria.

6 Hata hivyo, yaonekana Wakristo wengine Wayahudi hata walichukizwa na wazo la kula vyakula ambavyo hapo awali vilionwa kuwa si safi. Huenda watu hao waliokuwa na hisia nyepesi waliudhika kuwaona Wakristo wenzao Wayahudi wakila vyakula hivyo. Isitoshe, Wakristo fulani wasio Wayahudi ambao yaelekea walilelewa katika dini ambazo hazikuwakataza kula vyakula fulani, walishangaa kuona watu wakibishana kuhusu chakula. Bila shaka, halikuwa kosa kwa mtu kujiepusha na vyakula fulani, mradi tu hangesisitiza kwamba ilikuwa lazima kufanya hivyo ili kupata wokovu. Lakini maoni hayo tofauti yangeweza kuchochea mabishano kwa urahisi kutanikoni. Wakristo wa Roma wangehitaji kuwa waangalifu ili tofauti hizo zisiwazuie kumtukuza Mungu “kwa kinywa kimoja.”

7. Kulikuwa na maoni gani tofauti kuhusu kushika siku ya pekee kila juma?

7 Paulo anatoa mfano wa pili: “Mtu mmoja anahukumu siku moja kuwa juu ya nyingine; mtu mwingine anahukumu siku moja kuwa kama nyingine zote.” (Waroma 14:5a) Chini ya Sheria ya Musa, hakuna kazi iliyopaswa kufanywa siku ya Sabato. Hata kulikuwa na vizuizi vikali kuhusu kusafiri siku hiyo. (Kutoka 20:8-10; Mathayo 24:20; Matendo 1:12) Lakini Sheria ilipokomeshwa, vizuizi hivyo havikutumika tena. Lakini huenda Wakristo fulani Wayahudi walihofu kufanya kazi yoyote au kusafiri mbali katika siku ambayo hapo awali waliiona kuwa takatifu. Hata baada ya kuwa Wakristo, huenda waliitenga siku hiyo ya saba kwa ajili ya mambo ya kiroho tu, hata ingawa kulingana na maoni ya Mungu hawakupaswa kuishika tena Sabato. Je, walikosea kufanya hivyo? La, mradi tu hawakusisitiza kwamba bado Mungu aliwataka washike Sabato. Hivyo, kwa kufikiria dhamiri za ndugu zake Wakristo, Paulo aliandika: “Kila mtu na asadikishwe kikamili katika akili yake mwenyewe.”—Waroma 14:5b.

8. Ingawa wangeweza kuonyesha ufikirio kwa dhamiri ya wengine, Wakristo huko Roma hawakupaswa kufanya nini?

8 Hata hivyo, kwa shauku Paulo aliwatia moyo ndugu zake wawavumilie wale waliokuwa wanapambana na mambo yanayohusiana na dhamiri, lakini akawashutumu vikali wale waliojaribu kuwalazimisha waamini wenzao kujitiisha chini ya Sheria ya Musa kama takwa la kupata wokovu. Kwa mfano, yapata mwaka wa 61 W.K., Paulo aliandika kitabu cha Waebrania, ambacho ni barua yenye ujumbe mzito kwa Wakristo Wayahudi, na kueleza waziwazi kabisa kwamba hakukuwa na maana yoyote kujitiisha chini ya Sheria ya Musa, kwa sababu Wakristo walikuwa na tumaini bora linalotegemea dhabihu ya fidia ya Yesu.—Wagalatia 5:1-12; Tito 1:10, 11; Waebrania 10:1-17.

9, 10. Wakristo wanapaswa kuepuka kufanya nini? Eleza.

9 Kama ambavyo tumeona, Paulo anatoa hoja kwamba kufanya uchaguzi tofauti-tofauti hakupaswi kuhatarisha umoja, mradi tu hakuna kanuni hususa za Kikristo zinazovunjwa. Hivyo, Paulo anawauliza hivi Wakristo walio na dhamiri dhaifu: “Kwa nini wewe unamhukumu ndugu yako?” Naye anawauliza walio na nguvu (labda wale ambao dhamiri zao zinawaruhusu kula vyakula fulani vilivyokuwa vimekatazwa chini ya Sheria au kufanya kazi siku ya Sabato): “Kwa nini wewe pia unamdharau ndugu yako?” (Waroma 14:10) Kulingana na Paulo, Wakristo walio na dhamiri dhaifu hawapaswi kuwashutumu ndugu zao wenye maoni yaliyopanuka. Wakati huohuo, nao Wakristo walio na nguvu hawapaswi kuwadharau wale ambao bado dhamiri zao ni dhaifu kuhusiana na mambo fulani. Wote wanapaswa kuheshimu nia nzuri ya wengine na ‘kutojifikiria wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’—Waroma 12:3, 18.

10 Paulo alifafanua maoni hayo yenye usawaziko hivi: “Yeye anayekula asimdharau yeye asiyekula, na yeye asiyekula asimhukumu yeye anayekula, kwa maana Mungu amemkaribisha huyo.” Anazidi kusema: ‘Kristo pia alitukaribisha sisi, kwa kusudi la kumpa Mungu utukufu.’ Kwa kuwa Mungu na Kristo huwakubali walio na nguvu na walio dhaifu pia, tunapaswa kuwa na mtazamo huohuo na ‘kukaribishana.’ (Waroma 14:3; 15:7) Ni nani ambaye kwa kufaa anaweza kupinga jambo hilo?

Upendo wa Kindugu Hutokeza Umoja Leo

11. Ni hali gani ya kipekee iliyokuwako siku za Paulo?

11 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alizungumzia hali ya kipekee. Katika muda mfupi uliokuwa umepita Yehova alikuwa amekomesha agano fulani na kuanzisha jingine jipya. Ilikuwa vigumu kwa wengine kukubali badiliko hilo. Leo, hakuna hali inayofanana na hiyo kabisa, lakini huenda mambo kama hayo yakatokea nyakati fulani.

12, 13. Leo Wakristo wanaweza kuonyesha ufikirio kwa dhamiri za ndugu zao katika hali zipi?

12 Kwa mfano, huenda wakati mmoja mwanamke Mkristo alikuwa mfuasi wa dini fulani ambayo ilikazia kuvaa mavazi ya kawaida na kutojipamba. Anapokubali ile kweli, huenda akaona ni vigumu kukubaliana na wazo la kwamba kwenye pindi zinazofaa, ni sawa kuvaa mavazi ya kiasi na yenye kuvutia au kujipodoa kwa kiasi. Kwa kuwa hakuna kanuni ya Biblia inayohusika, haingefaa kwa yeyote kumshawishi mwanamke huyo Mkristo atende kinyume cha dhamiri yake. Wakati huohuo, yeye anatambua kwamba hapaswi kuwakosoa wanawake Wakristo ambao dhamiri zao huwaruhusu kujipodoa.

13 Fikiria mfano mwingine. Huenda mwanamume fulani Mkristo alilelewa katika mazingira ambako watu walichukia kileo. Baada ya kujua kweli, anafahamu maoni ya Biblia kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu na inaweza kutumiwa kwa kiasi. (Zaburi 104:15) Anakubali maoni hayo. Hata hivyo, kwa sababu ya malezi yake, anaamua kutotumia kileo kabisa, lakini yeye hawakosoi wale wanaokitumia kwa kiasi. Hivyo, anafuata maneno haya ya Paulo: “Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.”—Waroma 14:19.

14. Ni katika hali gani Wakristo wanaweza kutumia shauri la Paulo kwa Waroma katika maana yake halisi?

14 Hali nyingine hutokea ambazo huhitaji tutumie shauri la Paulo kwa Waroma katika maana yake halisi. Kutaniko la Kikristo limefanyizwa na watu wengi wenye mapendezi tofauti-tofauti. Hivyo, huenda wakafanya uchaguzi tofauti-tofauti—kwa mfano, kuhusiana na mavazi na mapambo. Bila shaka, Biblia inataja kanuni zilizo wazi ambazo Wakristo wote wanyoofu hufuata. Yeyote kati yetu hapaswi kuvaa mavazi au kuwa na mtindo wa nywele usio wa kawaida au unaopita kiasi au unaoweza kuonyesha kwamba tunashirikiana na watu fulani wasiofaa katika jamii. (1 Yohana 2:15-17) Wakristo hukumbuka kwamba nyakati zote, hata wanapostarehe, wao ni wahudumu wanaomwakilisha Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. (Isaya 43:10; Yohana 17:16; 1 Timotheo 2:9, 10) Hata hivyo, Wakristo wanaweza kufanya uchaguzi mbalimbali unaokubalika kuhusiana na mambo mengi maishani. *

Epuka Kuwakwaza Wengine

15. Ni chini ya hali zipi huenda Mkristo akaepuka kufanya jambo fulani ambalo ni haki yake kwa manufaa ya ndugu zake?

15 Kuna kanuni nyingine moja muhimu ambayo Paulo anatujulisha katika shauri lake kwa Wakristo huko Roma. Huenda nyakati nyingine Mkristo mwenye dhamiri iliyozoezwa vizuri akaamua kutofanya jambo fulani ambalo si kosa. Kwa nini? Kwa sababu anatambua kwamba kufuata mwenendo fulani kunaweza kuwadhuru wengine. Kwa habari hiyo, tunapaswa kufanya nini? Paulo anasema: “Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo ndugu yako anakwazika juu yake.” (Waroma 14:14, 20, 21) Hivyo, “sisi tulio na nguvu tunapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na tusiwe tukijipendeza wenyewe. Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake.” (Waroma 15:1, 2) Ikiwa dhamiri ya Mkristo mwenzetu itaumizwa na mambo tunayofanya, upendo wa kindugu utatuchochea kuonyesha ufikirio na kuepuka kufanya mambo hayo. Kwa habari hiyo, tunaweza kutoa mfano unaohusu matumizi ya vileo. Mkristo anaruhusiwa kunywa divai kwa kiasi. Lakini ikiwa kwa kunywa divai atamkwaza rafikiye, hatasisitiza kunywa eti kwa sababu ana haki ya kufanya hivyo.

16. Tunawezaje kuwaonyesha ufikirio watu wanaoishi katika eneo letu?

16 Kanuni hiyo inaweza pia kutumiwa katika shughuli zetu nje ya kutaniko la Kikristo. Kwa mfano, huenda tunaishi katika eneo ambako dini iliyo kubwa huwafunza wafuasi wake waione siku fulani ya juma kuwa siku ya kupumzika. Kwa sababu hiyo, ili tusiwakwaze jirani zetu na kuiwekea vizuizi kazi yetu ya kuhubiri, tutajitahidi kadiri tuwezavyo kuepuka kufanya jambo lolote siku hiyo ambalo litawakwaza jirani zetu. Katika hali nyingine, Mkristo tajiri anaweza kuhama akatumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa ambalo ni la watu maskini. Anaweza kuamua kuonyesha ufikirio kwa jirani zake katika eneo hilo kwa kuvaa kwa kiasi au kwa kuishi maisha rahisi hata ingawa anaweza kuishi maisha ya hali ya juu.

17. Kwa nini ni jambo la busara kuwafikiria wengine tunapofanya uchaguzi?

17 Je, ni jambo la busara kutarajia ‘wale walio na nguvu’ wafanye marekebisho hayo? Fikiria mfano huu: Tunapoendesha gari kwenye barabara kuu, tunaona mbele yetu watoto wanaotembea kwa njia hatari karibu na barabara. Je, tutaendelea kuendesha gari kwa mwendo wa juu kabisa unaoruhusiwa eti kwa sababu tu tuna haki kisheria kufanya hivyo? La, tunapunguza mwendo ili kuepuka hatari inayoweza kuwapata watoto hao. Vivyo hivyo, mara kwa mara tunahitaji kuwa tayari kupunguza mwendo, au kulegeza msimamo wetu tunaposhughulika na waamini wenzetu au watu wengine. Labda tunafanya jambo fulani linalokubalika kabisa. Hakuna kanuni za Biblia zinazovunjwa. Hata hivyo, ikiwa tunaweza kuwaudhi wengine au kuwadhuru wale walio na dhamiri dhaifu, upendo wa Kikristo utatuchochea tutende kwa tahadhari. (Waroma 14:13, 15) Kudumisha umoja na kuendeleza mambo yanayohusu Ufalme ni muhimu zaidi kuliko kushikilia haki zetu.

18, 19. (a) Kwa kuwaonyesha wengine ufikirio tunafuataje kielelezo cha Yesu? (b) Sisi hutenda kwa umoja kabisa kuhusiana na mambo gani, na ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

18 Tunapotenda kwa njia hiyo tunafuata kielelezo bora kabisa. Paulo anasema: “Hata Kristo hakujipendeza mwenyewe; bali kama ilivyoandikwa: ‘Shutuma za wale waliokuwa wanakushutumu zimeniangukia.’” Yesu alikuwa tayari kudhabihu uhai wake kwa ajili yetu. Bila shaka, sisi tu tayari kudhabihu baadhi ya haki zetu ikiwa kufanya hivyo kutawawezesha “wale wasio na nguvu” kumtukuza Mungu kwa umoja pamoja nasi. Kwa kweli, kuwa na mtazamo wa kuvumilia na wa ukarimu kuelekea Wakristo wenye dhamiri dhaifu—au kujizuia kwa hiari kufanya mambo fulani na kutosisitiza kupewa haki zetu—huonyesha “mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.”—Waroma 15:1-5.

19 Ingawa huenda maoni yetu yakatofautiana kwa kadiri fulani kuhusu mambo ambayo kanuni za Biblia hazihusiki, sisi hutenda kwa umoja kabisa kuhusiana na mambo ya ibada. (1 Wakorintho 1:10) Kwa mfano, umoja huo huonekana wazi kupitia jinsi tunavyotenda kuelekea wale wanaopinga ibada ya kweli. Neno la Mungu huwaita wapinzani hao, wageni, nalo hutuonya tujihadhari na “sauti ya wageni.” (Yohana 10:5) Tunawezaje kuwatambua wageni hao? Tunapaswa kutenda jinsi gani kuwaelekea? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kwa habari ya watoto wadogo, mavazi yao hutegemea mapendezi ya wazazi wao.

Ungejibuje?

• Kwa nini kuwa na maoni tofautitofauti kuhusu mambo ya kibinafsi hakupaswi kuhatarisha umoja?

• Kwa nini sisi tukiwa Wakristo tunapaswa kuonyeshana ufikirio wenye upendo?

• Ni katika njia zipi leo tunaweza kutumia shauri la Paulo kuhusu umoja, na ni nini kitakachotuchochea kufanya hivyo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Shauri la Paulo kuhusu umoja lilikuwa muhimu kwa kutaniko

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo wana umoja licha ya malezi yao yenye kutofautiana

[Picha katika ukurasa wa 12]

Dereva huyu anapaswa kufanya nini sasa?