Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Urithi Gani Unaopaswa Kuwaachia Watoto Wako?

Ni Urithi Gani Unaopaswa Kuwaachia Watoto Wako?

Ni Urithi Gani Unaopaswa Kuwaachia Watoto Wako?

PAVLOS, mwanamume mwenye familia kutoka kusini mwa Ulaya, hupatikana nyumbani mara chache sana ili kuwa pamoja na mke na watoto wake—binti wawili, wenye umri wa miaka 13 na 11, na mwana mwenye umri wa miaka 7. Pavlos hufanya kazi siku saba katika juma, naye hutumia saa nyingi kwa siku akijaribu kuchuma pesa za kutosha ili kutimiza ndoto yake. Anataka amnunulie kila mmoja wa binti zake nyumba, na kumwanzishia mwanaye biashara ndogo. Mke wake, Sofia, hufanya kazi kwa bidii ili kununua vitambaa na shuka, vyombo vya kutayarishia chakula, vyombo vya kauri, na vya fedha kwa ajili ya nyumba hizo. Wanapoulizwa kwa nini wao hufanya kazi kwa bidii hivyo, wanajibu kwa umoja hivi: “Kwa ajili ya watoto wetu!”

Kama vile Pavlos na Sofia, wazazi wengi ulimwenguni pote hufanya yote wawezayo ili kuwapa watoto wao mwanzo mzuri maishani. Baadhi ya wazazi huweka akiba ya pesa ili watoto wao wazitumie wakati ujao. Wengine huhakikisha kwamba watoto wao wanapata elimu inayofaa na kujifunza ustadi mbalimbali ambao utawasaidia baadaye maishani. Ingawa wazazi wengi huona urithi huo kuwa wonyesho wa upendo kwa watoto wao, mara nyingi kufanya matayarisho hayo huwaletea wazazi mkazo mkubwa wa kutimiza matarajio ya watu wa jamaa, marafiki, na jamii wanamoishi. Hivyo, wazazi wanaojali hujiuliza kwa kufaa, ‘Ni kiasi gani cha urithi tunachopaswa kuwaachia watoto wetu?’

Kuweka Akiba kwa Ajili ya Wakati Ujao

Ni jambo la kawaida na pia la Kimaandiko kwa wazazi Wakristo kuwawekea watoto wao akiba. Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wa siku zake: “Ni kawaida wazazi kuwawekea watoto wao akiba, na si watoto kuwawekea wazazi wao.” (2 Wakorintho 12:14, Biblia Habari Njema) Paulo aliongeza kwamba kuwatunza wazazi ni wajibu mzito. Aliandika: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Masimulizi mengi ya Biblia yanaonyesha kwamba mambo yanayohusu urithi yalikuwa muhimu miongoni mwa watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia.—Ruthu 2:19, 20; 3:9-13; 4:1-22; Ayubu 42:15.

Hata hivyo, nyakati nyingine, wazazi wanahangaika sana kuhusu kuwawekea watoto wao urithi mwingi. Kwa nini? Manolis ambaye ni baba aliyehamia Marekani kutoka kusini mwa Ulaya, anaonyesha sababu moja: “Wazazi walioteseka kutokana na uharibifu wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, njaa na umaskini, wameazimia kuboresha hali ya maisha ya watoto wao.” Anaongeza: “Nyakati nyingine wazazi hujidhuru kwa sababu ya kuhangaikia wajibu wao kupita kiasi na tamaa ya kuwapa watoto wao mwanzo mzuri maishani.” Kwa kweli, wazazi wengine hujinyima mambo ya lazima ili kukusanya vitu vya kimwili kwa ajili ya watoto wao. Lakini je, ni jambo la hekima kwa wazazi kufuatia mambo hayo?

“Ubatili na Msiba Mkubwa”

Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alitoa onyo kuhusu urithi. Aliandika: “Nami, naam mimi, nikachukia kazi yangu yote iliyo ngumu ambayo niliifanya kwa bidii chini ya jua, ambayo ningemwachia mtu ambaye angekuja baada yangu. Na ni nani anayejua kama atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo, atachukua usimamizi wa kazi yangu yote iliyo ngumu niliyoifanya kwa bidii ambayo ndani yake nilitumia hekima chini ya jua. Hilo pia ni ubatili. . . . Kwa maana kuna mwanadamu ambaye amefanya kazi yake ngumu kwa hekima na kwa ujuzi na kwa ustadi, lakini mwanadamu ambaye hakufanyia kazi ngumu kitu hicho atapewa fungu lake huyo. Hilo pia ni ubatili na msiba mkubwa.”—Mhubiri 2:18-21.

Kama Sulemani anavyoeleza, wale wanaopokea urithi huenda wasitambue thamani yake kamili kwa sababu wao wenyewe hawakufanya kazi ngumu ili kuupata. Kwa sababu hiyo, huenda warithi wakatumia bila hekima urithi ambao wazazi wao walijitahidi kuwakusanyia. Huenda hata wakatapanya mali hizo ambazo zilipatikana kwa kazi ngumu. (Luka 15:11-16) Huo ungekuwa “ubatili na msiba mkubwa” kama nini!

Urithi na Pupa

Kuna jambo lingine ambalo wazazi wanapaswa kulifikiria. Katika tamaduni ambazo huhangaikia sana mali zinazotokana na urithi na zawadi za ndoa, huenda watoto wakawa wenye pupa, wakidai mali, au mahari nyingi ambayo wazazi hawawezi kutoa. “Ole wake baba mwenye mabinti wawili au watatu,” asema kwa utani Loukas, baba kutoka Ugiriki. Anasema: “Mabinti wanaweza kulinganisha kile ambacho baba yao anaweza kutoa na kile ambacho wazazi wengine hurundikia watoto wao ‘kwa ukarimu.’ Huenda wakasema kwamba matarajio yao ya kuolewa yatadidimia ikiwa hawana mahari ya kutosha.” *

Manolis, aliyetangulia kutajwa, anasema: “Huenda mwanamume kijana akarefusha muda wa uchumba hadi baba ya msichana anayetazamia kumwoa amwahidi kumpa kitu fulani kwa ajili ya msichana huyo, ambacho kwa kawaida ni mali isiyohamishika au kiasi kikubwa cha pesa. Hiyo inaweza kuwa njia fulani ya kumlazimisha baba ya msichana atoe mali.”

Biblia huonya dhidi ya kila namna ya pupa. Sulemani aliandika: “Urithi hupatikana kwa pupa mwanzoni, lakini wakati wake ujao hautabarikiwa.” (Methali 20:21) Mtume Paulo alikazia: “Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.”—1 Timotheo 6:10; Waefeso 5:5.

“Hekima Pamoja na Urithi”

Kwa kweli, urithi una thamani fulani, lakini hekima ina thamani kuu kuliko vitu vya kimwili. Mfalme Sulemani aliandika: “Hekima pamoja na urithi ni nzuri na ni yenye faida . . . Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi; lakini faida ya ujuzi ni kwamba hekima huwahifadhi hai waliyo nayo.” (Mhubiri 7:11, 12; Methali 2:7; 3:21) Ingawa pesa huandaa ulinzi wa kiasi fulani kwa kumwezesha yule aliye nazo kupata kile anachohitaji, bado zinaweza kutoweka. Kwa upande mwingine, hekima, yaani, uwezo wa kutumia ujuzi katika kutatua matatizo au kufikia miradi fulani, inaweza kumlinda mtu aepuke kuhatarisha maisha yake kwa upumbavu. Hekima inayotegemea woga wa Mungu unaofaa, inaweza kumsaidia mtu huyo apate uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokaribia, ambao kwa kweli ni urithi wenye thamani!—2 Petro 3:13.

Wazazi Wakristo wanaonyesha hekima kama hiyo kwa kujua ni mambo gani ambayo wao na watoto wao wanastahili kutanguliza maishani. (Wafilipi 1:10) Vitu vya kimwili vilivyokusanywa ili vitumiwe na watoto havipaswi kuonwa kuwa muhimu kuliko mambo ya kiroho. Yesu aliwatia wafuasi wake moyo hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme [wa Mungu] na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:33) Wazazi ambao huwekea familia zao za Kikristo miradi ya kiroho wanaweza kutarajia kuthawabishwa sana. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika: “Baba ya mtu mwadilifu hakika atakuwa na shangwe; na mtu anayekuwa baba ya mwenye hekima atamshangilia pia. Baba yako na mama yako watashangilia, naye mama aliyekuzaa atakuwa na shangwe.”—Methali 23:24, 25.

Urithi Wenye Kudumu

Masuala ya urithi wa mali yalikuwa muhimu sana kwa Waisraeli wa kale. (1 Wafalme 21:2-6) Hata hivyo, Yehova aliwahimiza: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Vivyo hivyo, wazazi Wakristo wanaambiwa: “Endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Wazazi ambao wana mtazamo wa kiroho wanatambua kwamba kuwatimizia watu wa jamaa zao mahitaji hutia ndani kuwapa maagizo kutoka katika Biblia. Andreas, baba aliye na watoto watatu anaeleza: “Ikiwa watoto wanajifunza kutumia kanuni za kimungu katika maisha yao, watakuwa tayari zaidi kwa ajili ya wakati ujao.” Urithi kama huo huwasaidia pia kuanzisha na kusitawisha uhusiano wa kibinafsi na Muumba wao.—1 Timotheo 6:19.

Je, umefikiria kufanya matayarisho kwa ajili ya wakati ujao wa kiroho wa mtoto wako? Kwa mfano, wazazi wanaweza kufanya nini ikiwa mtoto wao yuko katika utumishi wa wakati wote? Ingawa mhudumu wa wakati wote hapaswi kudai wala kutarajia msaada wa kifedha, huenda wazazi wenye upendo wakaamua ‘kushiriki naye kulingana na mahitaji yake’ ili kumsaidia aendelee na utumishi wa wakati wote. (Waroma 12:13; 1 Samweli 2:18, 19; Wafilipi 4:14-18) Bila shaka, mtazamo kama huo wa kusaidia utamfurahisha Yehova.

Hivyo basi, wazazi wanapaswa kuwaachia watoto wao nini? Zaidi ya kuwatimizia mahitaji yao ya kimwili, wazazi Wakristo watahakikisha kwamba watoto wao wanapokea urithi mzuri wa kiroho ambao utawanufaisha milele. Katika njia hiyo, maneno yanayopatikana katika Zaburi 37:18 yatatimia: “Yehova anazijua siku za watu wasio na kosa, nao urithi wao wenyewe utaendelea mpaka wakati usio na kipimo.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Manukuu katika fungu hili na lile lifuatalo yanaonyesha desturi katika nchi fulani ambako familia ya bibi-arusi inatarajiwa kulipa mahari au kutoa zawadi kwa familia ya bwana-arusi. Katika tamaduni nyingi za Afrika mwanamume au familia yake ndio hutarajiwa kulipa mahari na kutoa zawadi kwa familia ya bibi-arusi. Hata hivyo, kanuni zinazotajwa zinaweza kutumika pande zote mbili.

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Ungependa watoto wako wawe na wakati ujao wa aina gani?