Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endeleeni Kujipatia Nguvu Katika Bwana”

“Endeleeni Kujipatia Nguvu Katika Bwana”

“Endeleeni Kujipatia Nguvu Katika Bwana”

“Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake.”—WAEFESO 6:10.

1. (a) Ni pigano gani lisilo la kawaida ambalo lilitokea miaka 3,000 hivi iliyopita? (b) Kwa nini Daudi alishinda?

MIAKA 3,000 hivi iliyopita, wapiganaji wawili kutoka vikosi viwili tofauti walikabiliana kwenye uwanja wa vita. Mpiganaji aliyekuwa na umri mdogo alikuwa mvulana mchungaji aitwaye Daudi. Alikabili Goliathi, mtu mwenye kimo na urefu usio wa kawaida. Uzito wa vazi lake la chuma ulikuwa kilogramu 57, naye alibeba upanga mkubwa na mkuki mkubwa na mzito. Daudi hakuvaa silaha yoyote, isipokuwa kombeo. Goliathi, jitu la Wafilisti, alihisi kwamba amedharauliwa kwa kuwa Mwisraeli aliyekuja kupigana naye alikuwa kivulana tu. (1 Samweli 17:42-44) Kwa watazamaji wa pande zote mbili, matokeo yalikuwa ni kana kwamba yamekwisha amuliwa. Lakini si sikuzote wenye nguvu hushinda vitani. (Mhubiri 9:11) Daudi alishinda kwa sababu alipigana kwa nguvu za Yehova. Alisema, “Vita ni vya Yehova.” Masimulizi ya Biblia yanasema kwamba “Daudi, akiwa na kombeo na jiwe, akawa mwenye nguvu zaidi kuliko yule Mfilisti.”—1 Samweli 17:47, 50.

2. Wakristo hupigana vita vya aina gani?

2 Wakristo hawapigani vita halisi. Ingawa wao hufanya amani na watu wote, wanapigana vita vya kiroho dhidi ya maadui wenye nguvu sana. (Waroma 12:18) Katika sura ya mwisho ya barua ya Paulo kwa Waefeso, alieleza vita ambavyo vinahusisha kila Mkristo. Aliandika: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:12.

3. Kulingana na Waefeso 6:10, tunahitaji nini ili tuwe na hakika kwamba tutafanikiwa?

3 ‘Majeshi hayo ya roho waovu’ ni Shetani na mashetani ambao hutamani kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Kwa kuwa wana nguvu zaidi kutushinda, tunajikuta katika hali kama ile ya Daudi, nasi hatuwezi kufanikiwa tusipotegemea nguvu za Mungu. Naam, Paulo anatuhimiza ‘tuendelee kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake.’ (Waefeso 6:10) Baada ya kututolea shauri hilo, mtume huyo anaonyesha maandalizi ya kiroho na sifa za Kikristo ambazo hutuwezesha kushinda pigano hilo.— Waefeso 6:11-17.

4. Tutachunguza mambo gani mawili katika makala hii?

4 Sasa na tuchunguze mambo ambayo Maandiko husema kuhusu nguvu na mbinu za adui yetu. Kisha tutachunguza mbinu za kujikinga ambazo lazima tutumie ili kujilinda. Tukifuata maagizo ya Yehova, tunaweza kuwa na hakika kwamba maadui wetu hawatatushinda.

Kushindana Mweleka na Roho Waovu

5. Matumizi ya maneno “kupigana mweleka” kwenye Waefeso 6:12 yanatusaidiaje kuelewa mbinu ya Shetani?

5 Paulo anaeleza kwamba “tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Bila shaka, Shetani Ibilisi, “mtawala wa roho waovu,” ndiye roho mwovu mkuu zaidi. (Mathayo 12:24-26) Biblia huonyesha kwamba vita vyetu ni vya “kushindana mweleka.” Katika mashindano ya mweleka ya Ugiriki la kale, kila mshindanaji alijaribu kumyumbisha mpinzani wake ili amwangushe. Vivyo hivyo, Ibilisi anataka tuyumbe-yumbe kiroho. Anawezaje kufanya tuyumbe-yumbe?

6. Tumia Maandiko kuonyesha jinsi Ibilisi anavyoweza kutumia mbinu tofauti-tofauti ili kudhoofisha imani yetu.

6 Ibilisi anaweza kutenda kama nyoka, simba anayenguruma, au hata malaika wa nuru. (2 Wakorintho 11:3, 14; 1 Petro 5:8) Anaweza kutumia wanadamu kututesa au kutuvunja moyo. (Ufunuo 2:10) Kwa kuwa Shetani ana mamlaka juu ya ulimwengu wote, anaweza kutumia tamaa na vivutio vya ulimwengu ili kutunasa. (2 Timotheo 2:26; 1 Yohana 2:16; 5:19) Anaweza kutumia maoni ya ulimwengu na ya waasi-imani ili kutudanganya, kama alivyomdanganya Hawa.—1 Timotheo 2:14.

7. Roho waovu wana mipaka gani, nasi tuna msaada gani?

7 Ingawa huenda silaha na nguvu za Shetani na roho wake waovu zikaonekana kuwa kubwa sana, zina mipaka. Roho hao waovu hawawezi kutulazimisha kufanya mambo maovu yasiyompendeza Baba yetu wa mbinguni. Tumeumbwa tukiwa na uwezo wa kutofautisha mema na mabaya, nasi tunaweza kudhibiti mawazo na matendo yetu. Isitoshe, hatupigani peke yetu. Hali katika siku zetu inafanana na ya siku za Elisha: “Wale walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” (2 Wafalme 6:16) Biblia hutuhakikishia kwamba tukijitiisha kwa Mungu na kumpinga Ibilisi, atatukimbia.—Yakobo 4:7.

Tunajua Mbinu za Shetani

8, 9. Shetani alimletea Ayubu majaribu gani ili kuvunja utimilifu wake, nasi tunakabili hatari gani za kiroho leo?

8 Tunazijua mbinu za Shetani kwa sababu Maandiko yanafunua mbinu zake za msingi. (2 Wakorintho 2:11) Ibilisi alitumia hali ngumu sana za kiuchumi, kifo cha wapendwa, upinzani wa familia, kuteseka, na uchambuzi usio na msingi wa marafiki wa uwongo, dhidi ya Ayubu mwadilifu. Ayubu alivunjika moyo na kuhisi kwamba Mungu alikuwa amemwacha. (Ayubu 10:1, 2) Ingawa huenda leo Shetani asisababishe matatizo hayo moja kwa moja, magumu hayo yanaweza kuwaathiri Wakristo wengi, naye Ibilisi anaweza kuyatumia kutimiza makusudi yake.

9 Hatari za kiroho zimeongezeka upesi wakati huu wa mwisho. Tunaishi katika ulimwengu ambamo watu hufuatia zaidi vitu vya kimwili kuliko miradi ya kiroho. Sikuzote vyombo vya habari huonyesha ngono haramu kuwa jambo linalofurahisha badala ya kuumiza. Nao watu wengi wamekuwa ‘wapenda-raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Timotheo 3:1-5) Kufikiri kwa njia hiyo kunaweza kuhatarisha usawaziko wetu wa kiroho ‘tusipofanya pigano kali kwa ajili ya imani.’—Yuda 3.

10-12. (a) Yesu alitoa onyo gani katika mfano wake wa mpandaji? (b) Onyesha jinsi mambo ya kiroho yanavyoweza kusongwa.

10 Mojawapo ya mbinu ambazo Shetani anatumia kwa mafanikio sana ni ile ya kufanya tuzame kabisa katika ulimwengu huu na ufuatiaji wake wa vitu vya kimwili. Katika mfano wake wa mpandaji, Yesu alionya kwamba katika hali fulani “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri hulisonga neno [la Ufalme].” (Mathayo 13:18, 22) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “kusonga” humaanisha “kunyonga kabisa.”

11 Katika misitu ya kitropiki, mtu anaweza kuona mtini unaonyonga. Mtini huo hukua polepole kuzunguka shina la mti mwingine. Pole kwa pole, mtini huo huufunika mti huo mwingine kwa mizizi yake inayozidi kuwa yenye nguvu. Hatimaye, mizizi ya mtini huo ambayo ni mingi, hufyonza karibu rutuba yote katika udongo ambao mti huo mwingine umemea juu yake, huku matawi yake yakiunyima nuru. Mwishowe, mti huo mwingine hufa.

12 Vivyo hivyo, mahangaiko ya mfumo huu na utafutaji wa mali na maisha ya starehe yanaweza pole kwa pole kufanya tutumie wakati na nguvu nyingi zaidi. Huku akili zetu zikiwa zimekengeushwa na vitu vya ulimwengu, huenda tukapuuza kwa urahisi funzo la Biblia la kibinafsi na kuacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na hivyo kutengwa na chakula cha kiroho. Ndipo miradi ya kufuatia vitu vya kimwili huchukua mahali pa utendaji wa kiroho, na hatimaye tunakuwa windo rahisi la Shetani.

Tunahitaji Kusimama Imara

13, 14. Tunapaswa kuchukua msimamo gani tunapopingwa na Shetani?

13 Paulo aliwahimiza waamini wenzake ‘wasimame imara kupinga hila za Ibilisi.’ (Waefeso 6:11) Bila shaka, hatuwezi kuwaharibu Ibilisi na roho wake waovu. Yesu Kristo ndiye amepewa jukumu hilo na Mungu. (Ufunuo 20:1, 2) Lakini kabla Shetani hajaondolewa, tunapaswa “kusimama imara,” ili tusishindwe na mashambulizi yake.

14 Mtume Petro pia alikazia uhitaji wa kusimama imara dhidi ya Shetani. Aliandika: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu. Lakini chukueni msimamo mkampinge yeye, mkiwa imara katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu ulimwenguni.” (1 Petro 5:8, 9) Kwa kweli, msaada wa ndugu na dada zetu wa kiroho ni muhimu ili kusimama imara Ibilisi anapotushambulia kama simba anayenguruma.

15, 16. Toa mfano wa Kimaandiko ili kuonyesha jinsi utegemezo wa waamini wenzetu unavyoweza kutusaidia kusimama imara.

15 Wakati simba aliye karibu anaponguruma katika savana ya Afrika, paa hukimbia kwa kasi sana ili waondoke mahali penye hatari. Hata hivyo, tembo huweka mfano bora wa kusaidiana. Kitabu Elephants—Gentle Giants of Africa and Asia kinasema: “Kwa kawaida, kundi la tembo hujilinda kwa kusimama katika duara, huku tembo waliokomaa wakielekeza vichwa vyao nje ya duara hiyo ili kukabili hatari. Tembo wachanga hupata ulinzi katikati ya duara hiyo.” Wanapokabiliwa na wonyesho kama huo wa nguvu na utegemezo, ni mara chache sana simba hushambulia hata tembo wadogo.

16 Sisi pia tunapokabiliwa na Shetani na roho wake waovu, tunahitaji kukaa pamoja, bega kwa bega, na ndugu zetu ambao ni thabiti katika imani. Paulo alikiri kwamba baadhi ya Wakristo wenzake walikuwa ‘msaada wenye kumtia nguvu’ alipokuwa gerezani huko Roma. (Wakolosai 4:10, 11) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ limetumiwa mara moja tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kulingana na Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine, “kitenzi fulani cha neno hilo humaanisha madawa ambayo hutuliza mwasho.” Kama dawa ya kupaka yenye kutuliza, utegemezo kutoka kwa waabudu wakomavu wa Yehova unaweza kupunguza maumivu yanayosababishwa na mateso ya kihisia-moyo au ya kimwili.

17. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa waaminifu kwa Mungu?

17 Kitia-moyo kutoka kwa Wakristo wenzetu leo kinaweza kuimarisha azimio letu la kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Wazee Wakristo hutamani hasa kutoa msaada wa kiroho. (Yakobo 5:13-15) Mambo yanayotusaidia kuwa waaminifu yanatia ndani funzo la kawaida la Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, makusanyiko ya mzunguko, na ya wilaya. Uhusiano wetu wa karibu pamoja na Mungu hutusaidia tuendelee kuwa waaminifu kwake. Kwa kweli, iwe tunakula, tunakunywa, au tunafanya jambo lingine lolote, tunapaswa kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu. (1 Wakorintho 10:31) Bila shaka, ni muhimu kumtegemea Yehova katika sala ili kuendelea katika njia inayompendeza.—Zaburi 37:5.

18. Kwa nini hatupaswi kufa moyo ikiwa nguvu zetu zinadhoofishwa na hali zenye kutaabisha?

18 Nyakati nyingine, Shetani hutushambulia tunapojihisi kuwa dhaifu kiroho. Simba hushambulia mnyama aliye dhaifu. Matatizo ya familia, magumu ya kiuchumi, au magonjwa yanaweza kudhoofisha nguvu zetu za kiroho. Lakini tusife moyo katika kufanya yale yanayompendeza Mungu kwa kuwa Paulo alisema: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:10; Wagalatia 6:9; 2 Wathesalonike 3:13) Alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba nguvu kutoka kwa Mungu zinaweza kujazia udhaifu wetu wa kibinadamu, ikiwa tutamwomba Yehova nguvu hizo. Ushindi wa Daudi dhidi ya Goliathi unaonyesha kwamba Mungu anaweza kuimarisha watu wake, naye hufanya hivyo. Mashahidi wa Yehova wa sasa wanaweza kuthibitisha kwamba wamehisi utegemezo wa Mungu nyakati zenye taabu sana.—Danieli 10:19.

19. Toa mfano ili kuonyesha jinsi Yehova anavyowaimarisha watumishi wake.

19 Wenzi fulani wa ndoa waliandika hivi kuhusu utegemezo ambao Mungu aliwapa: “Kwa miaka mingi tumemtumikia Yehova tukiwa mume na mke na tumebarikiwa sana na kupata kuwajua watu wengi wazuri. Pia, Yehova ametuzoeza na kutuimarisha ili kuvumilia magumu kwa mafanikio. Kama Ayubu, sikuzote hatukuelewa kwa nini mambo fulani yalitukia kama yalivyotukia, lakini tulijua kwamba sikuzote Yehova alikuwa tayari kutusaidia.”

20. Ni uthibitisho gani wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba sikuzote Yehova huwategemeza watu wake?

20 Mkono wa Yehova si mfupi sana hivi kwamba hawezi kutegemeza na kuimarisha watu wake waaminifu. (Isaya 59:1) Mtunga-zaburi Daudi aliimba: “Yehova anawategemeza wote wanaoanguka, naye anawainua wote ambao wameinama chini.” (Zaburi 145:14) Kwa kweli, Baba yetu wa mbinguni “hutubebea mzigo wetu kila siku” naye hutuandalia yale tunayohitaji kikweli.—Zaburi 68:19.

Tunahitaji “Mavazi Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”

21. Paulo alikaziaje uhitaji wa kuwa na silaha za kiroho?

21 Tumechunguza baadhi ya mbinu za Shetani na tumeona uhitaji wa kusimama imara licha ya mashambulizi yake. Sasa tunapaswa kufikiria msaada mwingine muhimu ili kulinda imani yetu kwa mafanikio. Katika barua yake kwa Waefeso, mtume Paulo alitaja mara mbili jambo fulani muhimu linalohitajiwa ili kusimama imara kupinga hila za Shetani na kufanikiwa katika kupigana mweleka na roho waovu. Paulo aliandika: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi. . . . Chukueni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mweze kupinga katika ile siku ya uovu, baada ya ninyi kufanya mambo yote kwa ukamili, mweze kusimama imara.”—Waefeso 6:11, 13.

22, 23. (a) Silaha zetu za kiroho hutia ndani nini? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

22 Naam, tunahitaji kuvaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” Paulo alipowaandikia Waefeso barua, alikuwa akilindwa na askari Mroma, ambaye huenda nyakati nyingine alikuwa amevaa mavazi kamili ya silaha. Hata hivyo, mtume huyo aliongozwa na roho ya Mungu kuzungumzia silaha za kiroho ambazo ni muhimu sana kwa kila mtumishi wa Yehova.

23 Silaha hizo za kiroho kutoka kwa Mungu zinatia ndani sifa ambazo lazima Mkristo awe nazo na vilevile maandalizi ya kiroho kutoka kwa Yehova. Katika makala inayofuata, tutachunguza kila sehemu ya silaha hizo za kiroho. Hilo litatusaidia kujua tuko tayari kadiri gani kwa ajili ya vita vyetu vya kiroho. Wakati huohuo, tutaona jinsi ambavyo kielelezo bora cha Yesu Kristo hutusaidia kufanikiwa kumpinga Shetani Ibilisi.

Ungejibuje?

• Wakristo wote wana pigano gani?

• Fafanua baadhi ya mbinu za Shetani.

• Msaada kutoka kwa waamini wenzetu unaweza kutuimarishaje?

• Tunapaswa kutegemea nguvu za nani, na kwa nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wakristo ‘wanashindana mweleka na roho waovu’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo yanaweza kulisonga neno la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakristo wenzetu wanaweza kuwa “msaada wenye kutia nguvu”

[Picha katika ukurasa wa 14]

Je, wewe husali kwa Mungu ili upate nguvu?