Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini wanaume Waisraeli waliruhusiwa kuoa wanawake wageni waliotekwa hata ingawa Sheria ya Musa iliamuru kwamba wasifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja na wageni?—Kumbukumbu la Torati 7:1-3; 21:10, 11.

Jambo hilo liliruhusiwa kwa sababu ya hali fulani za kipekee. Yehova alikuwa amewaamuru Waisraeli wabomoe majiji saba ya mataifa katika nchi ya Kanaani na kuwaua wakaaji wake wote. (Kumbukumbu la Torati 20:15-18) Kuhusu mataifa mengine, yaelekea watu wazima pekee waliookoka ni wanawake mabikira waliotekwa. (Hesabu 31:17, 18; Kumbukumbu la Torati 20:14) Mwanamume Mwisraeli angeweza kumwoa mwanamke kama huyo, iwapo tu mwanamke huyo angechukua hatua fulani.

Biblia inasema hivi kuhusu hatua ambazo mwanamke kama huyo alipaswa kuchukua: “Lazima anyoe kichwa chake, atunze kucha zake, na kuvua nguo ya kujitanda ya utekwa wake, akae katika nyumba yako, amlilie baba yake na mama yake kwa mwezi mzima; na baada ya jambo hilo utalala naye, nawe utamchukua awe bibi-arusi wako, naye atakuwa mke wako.”—Kumbukumbu la Torati 21:12, 13.

Mwanamke bikira aliyetekwa ambaye Mwisraeli alitaka awe mke wake alipaswa kunyoa kichwa chake. Kunyoa nywele kulikuwa ishara ya kuomboleza au huzuni. (Isaya 3:24) Kwa mfano, mzee wa ukoo Ayubu alipopoteza watoto na mali yake yote, alinyoa kichwa chake kama ishara ya kuomboleza. (Ayubu 1:20) Mwanamke mgeni alipaswa pia kutunza kucha zake, labda ‘kuzikata’ ili hata kama zingepakwa rangi, mikono yake isivutie. (Kumbukumbu la Torati 21:12, Union Version) Ni nini iliyokuwa “nguo ya kujitanda ya utekwa wake” ambayo mwanamke mateka angevua? Wanawake wa majiji ya wapagani waliokuwa karibu kushindwa walikuwa na desturi ya kuvalia mavazi maridadi kabisa. Walifanya hivyo wakitumaini kuwavutia watekaji wao. Mwanamke mateka alipaswa kuvua vazi hilo wakati wa kuomboleza.

Mwanamke aliyetekwa ambaye angekuwa mke wa mwanamume Mwisraeli alipaswa kuomboleza kwa muda wa mwezi mmoja kwa ajili ya wapendwa wake waliokufa. Majiji hayo yaliyoshindwa yalipaswa kuharibiwa kabisa hivi kwamba mwanamke huyo hangekuwa na uhusiano wowote na watu wa familia na jamii yake. Kwa kuwa askari Waisraeli wangekuwa wameharibu sanamu za miungu yake, vifaa vyake vya ibada vingekuwa vimetoweka. Mwezi wa kuomboleza pia ulikuwa kipindi cha kutakaswa ambapo mwanamke mateka angeachana kabisa na mazoea yote ya ibada yake ya zamani.

Lakini hali ilikuwa tofauti kuhusiana na wanawake wageni kwa ujumla. Shauri hili liliwahusu: “Nawe usifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. Binti yako usimpe mwana wake, wala binti yake usimchukue kwa ajili ya mwana wako.” (Kumbukumbu la Torati 7:3) Kwa nini walikatazwa kufanya hivyo? Andiko la Kumbukumbu la Torati 7:4 linasema: “Kwa maana atamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine.” Hivyo, katazo hilo lilikusudiwa kuwalinda Waisraeli wasichafuliwe kidini. Lakini mwanamke mgeni katika hali zinazotajwa kwenye Kumbukumbu la Torati 21:10-13 hangefanya hivyo. Watu wake wote wa ukoo walikuwa wamekufa, nazo sanamu za miungu yake zilikuwa zimeharibiwa. Hakuwa na mawasiliano yoyote na waabudu wa dini za uwongo. Mwisraeli aliruhusiwa kuoa mgeni chini ya hali hizo.