Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninyi Msali Hivi”

“Ninyi Msali Hivi”

“Ninyi Msali Hivi”

JE, UNAJUA maneno ya Sala ya Bwana? Ilikuwa sala ya kielelezo iliyofundishwa na Yesu Kristo. Katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, Yesu alisema: “Basi, ninyi msali hivi.” (Mathayo 6:9) Kwa kuwa ilianzishwa na Yesu, mara nyingi inaitwa Sala ya Bwana au Baba Yetu.—Kilatini, Paternoster.

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wameitia akilini Sala ya Bwana, nao huirudia mara nyingi, pengine kila siku. Katika miaka ya karibuni, wengi wameikariri sala hiyo shuleni na katika matukio ya umma. Kwa nini Sala ya Bwana inathaminiwa sana?

Cyprian, mwanatheolojia wa karne ya tatu aliandika: “Je, kuna sala ambayo ni ya kiroho zaidi kuliko ile tuliyopewa na Kristo . . . ? Ni sala ya aina gani kwa Baba ambayo inaweza kuwa ya kweli zaidi kuliko ile tuliyopewa na Mwana ambaye ndiye Kweli?”—Yohana 14:6.

Katika katekisimu yake, Kanisa Katoliki huiona Sala ya Bwana kuwa “sala ya msingi ya Kikristo.” Kichapo The World Book Encyclopedia kinakiri jinsi sala hii ilivyo muhimu katika dini zote zinazojiita za Kikristo, na kuitaja kuwa mojawapo ya “taarifa za msingi za imani ya Kikristo.”

Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba wengi ambao hukariri Sala ya Bwana hawaielewi kabisa. “Ikiwa umelelewa katika dini fulani ya Kikristo huenda unaweza kuisema Sala ya Bwana mbiombio bila kutulia ili kupumua,” lasema gazeti la Kanada Ottawa Citizen, “lakini huenda ukaona ni vigumu kuisema polepole na kwa kuielewa.”

Je, kweli ni muhimu kuelewa sala tunazomtolea Mungu? Kwa nini Yesu alitupa Sala ya Bwana? Inamaanisha nini kwako? Acheni sasa tuzungumzie maswali hayo.