Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sala ya Bwana Inachomaanisha Kwako

Sala ya Bwana Inachomaanisha Kwako

Sala ya Bwana Inachomaanisha Kwako

ILE Sala ya Bwana, kama ilivyotolewa na Yesu Kristo katika Mahubiri ya Mlimani, inapatikana katika Biblia kwenye Mathayo sura ya 6, mstari wa 9 hadi 13. Kabla tu ya kutoa sala hiyo, Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.”—Mathayo 6:7.

Basi, ni wazi kwamba Yesu hakukusudia Sala ya Bwana ikaririwe neno kwa neno. Ni kweli kwamba alirudia sala hiyo kwa manufaa ya wengine waliokuwa wakimsikiliza. (Luka 11:2-4) Lakini maneno ya sala hiyo yanatofautiana kidogo katika masimulizi ya Injili ya Mathayo na ya Luka. Isitoshe, Yesu na wanafunzi wake hawakutumia maneno yaleyale ya sala ya kielelezo katika sala walizotoa baadaye.

Kwa nini Sala ya Bwana imeandikwa katika Biblia? Kupitia sala hiyo ya kielelezo, Yesu anatufundisha jinsi sala zetu zinavyoweza kukubaliwa na Mungu. Pia katika sala hiyo, tunapata majibu kwa maswali fulani ya msingi kuhusu maisha. Kwa hiyo, na tuzungumzie kila sehemu ya Sala ya Bwana.

Jina la Mungu Ni Nani?

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Maneno hayo ya utangulizi ya sala ya kielelezo hutusaidia tumkaribie Mungu kwa kumwita “Baba yetu.” Kama mtoto, ambaye kwa kawaida huvutiwa na mzazi mwenye upendo na anayeelewa hali zake, tunaweza kumfikia Baba yetu wa mbinguni tukiwa na hakika kwamba anataka kutusikiliza. Mfalme Daudi aliimba hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—Zaburi 65:2.

Yesu anatufundisha tusali kwamba jina la Mungu litakaswe. Lakini jina la Mungu ni nani? Biblia inajibu kwa kusema hivi: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Je, umewahi kusoma jina Yehova katika Biblia?

Kwa kweli, jina la Mungu, Yehova hupatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya kale ya Biblia. Hata hivyo, baadhi ya watafsiri hata wameliondoa jina hilo katika tafsiri zao za Biblia. Hivyo basi, kwa kufaa tunamwomba Muumba wetu alitakase jina lake. (Ezekieli 36:23) Njia moja ya kutenda kupatana na sala hiyo ni kutumia jina Yehova tunaposali kwake.

Mwanamke fulani anayeitwa Patricia alilelewa katika dini ya Katoliki naye aliifahamu vizuri Sala ya Bwana. Aliitikiaje wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipomwonyesha jina la Mungu katika Biblia? “Sikuamini!” akasema kwa mshangao. “Kwa hiyo, nilitoa tafsiri yangu ya Biblia, nayo pia ilikuwa na jina hilo. Kisha Shahidi huyo akanionyesha Mathayo 6:9, 10 na kunieleza kwamba jina la Mungu linadokezwa katika Sala ya Bwana. Nilisisimuka kwelikweli na kumwomba Shahidi huyo ajifunze Biblia pamoja nami.”

Mapenzi ya Mungu Yatendeke Duniani

“Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Sehemu hii ya sala ya kielelezo ya Yesu itatimizwaje? Watu wengi huona mbinguni kuwa mahali penye amani na utulivu. Maandiko husema kwamba mbingu ndiyo ‘makao ya Yehova yaliyoinuliwa ya utakatifu na uzuri.’ (Isaya 63:15) Ndiyo sababu tunasali kwamba mapenzi ya Mungu yatendeke duniani “kama ilivyo mbinguni”! Lakini je, hilo litapata kutukia?

Danieli, nabii wa Yehova alitabiri: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za kidunia], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Hivi karibuni, Ufalme, au serikali hiyo ya kimbingu itachukua hatua ya kuleta amani duniani pote chini ya utawala wenye uadilifu.—2 Petro 3:13.

Kuomba Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yatendeke duniani ni wonyesho wa imani ambao hautakatisha tamaa. Mtume Mkristo Yohana aliandika hivi: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’” Kisha Yohana akaongeza kusema: “Na Yule aliyeketi juu ya kiti cha ufalme akasema: . . . ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:3-5.

Kusali Kuhusu Mahitaji Yetu ya Kimwili

Kupitia maneno aliyosema katika sala ya kielelezo, Yesu alionyesha kwamba tunaposali tunapaswa kuhangaikia hasa jina na mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, sala ya kielelezo inataja pia mambo ya kibinafsi tunayoweza kumwomba Yehova kwa njia inayofaa.

Ya kwanza kati ya mambo hayo ni: “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” (Mathayo 6:11) Hilo si ombi la kupata utajiri. Yesu alitutia moyo tusali ili kupata “mkate wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo.” (Luka 11:3) Kupatana na Sala ya Bwana, tunaweza kusali kwa imani kwamba Mungu atatutimizia mahitaji yetu ya kila siku ikiwa tunampenda na kumtii.

Kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu matatizo ya kiuchumi kunaweza kufanya tupuuze mahitaji yetu ya kiroho na hivyo kukosa kufanya yale ambayo Mungu anataka tufanye. Lakini tukitanguliza ibada ya Mungu maishani, tunaweza kuwa na hakika kwamba dua za kutimiziwa mahitaji ya kimwili, kama vile chakula, na mavazi, zitajibiwa. Yesu alisema: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:26-33) Si rahisi kuutafuta uadilifu wa Mungu kwa kuwa sisi sote ni wenye dhambi na tunahitaji msamaha. (Waroma 5:12) Jambo hilo linatiwa ndani pia katika Sala ya Bwana.

Kusali Kuhusu Msamaha

“Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mathayo 6:12) Katika masimulizi ya Luka ya Sala ya Bwana, “madeni” hayo yanatajwa kuwa “dhambi.” (Luka 11:4) Je, kweli Yehova Mungu atatusamehe dhambi zetu?

Ingawa Mfalme Daudi wa Israeli la kale alifanya dhambi nzito, alitubu na kusali hivi kwa uhakika: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe; na fadhili zenye upendo ni nyingi kwa wale wote wanaokuitia.” (Zaburi 86:5) Jambo hilo linafariji kama nini! Baba yetu wa mbinguni yuko “tayari kusamehe” dhambi za wale wanaosali kwake wakiwa wametubu. Kama vile deni linavyoweza kufutiliwa mbali kabisa, ndivyo Yehova Mungu anavyoweza kutusamehe dhambi zetu kabisa.

Hata hivyo, Yesu alitaja sharti fulani: Ili Mungu atusamehe, ni lazima tuwasamehe wengine. (Mathayo 6:14, 15) Ingawa Ayubu mwadilifu alitendewa vibaya na rafiki zake watatu, alikuwa mwenye kusamehe, na hata alisali kwa ajili yao. (Ayubu 42:10) Tukiwasamehe wale wanaotutendea dhambi, tutampendeza Mungu na tutanufaika na rehema yake.

Utayari wa Mungu wa kusikiliza maombi yetu unapaswa kutuchochea tutafute kibali chake. Na tunaweza kufanya hivyo, hata kama sisi si wakamilifu. (Mathayo 26:41) Yehova anaweza kutusaidia pia kuhusiana na jambo hilo kama vile Yesu alivyoonyesha kwa kumalizia sala ya kielelezo na ombi muhimu.

Kuomba Msaada wa Kufuatia Mwenendo wa Uadilifu

“Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Yehova hatuachi bila msaada wowote tunapokabili kishawishi wala hafanyi tuanguke katika dhambi. Neno lake linasema: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mungu huruhusu tushawishiwe, lakini anaweza kutukomboa kutokana na yule Mshawishi Mkuu, yaani, “yule mwovu” anayeitwa Shetani Ibilisi.

Mtume Petro aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Kwa kweli, Shetani hata alimjaribu mwanadamu mkamilifu, Yesu Kristo! Lengo la Ibilisi lilikuwa nini? Kufanya Yesu aache ibada safi ya Yehova Mungu. (Mathayo 4:1-11) Ikiwa unajitahidi kumtumikia Mungu, Shetani ana lengo la kukumeza wewe pia!

Kupitia ulimwengu ulio chini ya uwezo wake, huenda Ibilisi akatushawishi tujihusishe na mazoea yasiyompendeza Mungu. (1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, ni muhimu kumwomba Mungu msaada kwa ukawaida, hasa tunapokabili kishawishi kinachoendelea. Na tukimwabudu Yehova kulingana na Neno lake, Biblia, atatukomboa kwa kutusaidia tumpinge Ibilisi. Biblia hutuambia, “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili.”—1 Wakorintho 10:13.

Ni Muhimu Kumwamini Mungu

Ni jambo lenye kugusa moyo kama nini kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni anapendezwa na kila mmoja wetu! Hata alimwagiza Mwana wake, Yesu Kristo, atufundishe jinsi ya kusali. Bila shaka, jambo hilo hufanya tutake kumpendeza Yehova Mungu. Tunawezaje kufanya hivyo?

Biblia inasema: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Imani hiyo inaweza kusitawishwaje? Biblia inasema, “Imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Mashahidi wa Yehova hufurahi kuzungumzia mambo yanayohusu Biblia pamoja na wote wanaotamani kumtumikia Mungu katika imani ya kweli.

Inatumainiwa kwamba mazungumzo haya kuhusu Sala ya Bwana yamezidisha uelewaji wako kuhusu maana ya sala hiyo. Kwa kuendelea kutwaa ujuzi zaidi kumhusu Yehova na thawabu atakayowapa “wale wanaomtafuta kwa bidii,” unaweza kuimarisha imani yako katika Mungu. Na ujifunze mengi zaidi kumhusu yeye na makusudi yake ili uwe na uhusiano wa karibu pamoja na Baba yako wa mbinguni, milele.—Yohana 17:3.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii; na utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu. Na usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.”—Mathayo 6:9-13

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova hutimiza mahitaji ya wale wanaompenda

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mungu pia hutusaidia tumpinge Ibilisi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ikiwa sisi, kama Ayubu, tunawasamehe wale wanaotutendea dhambi, tunaweza kunufaika na rehema ya Mungu