Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Tafuteni Ni Nani Anayestahili’

‘Tafuteni Ni Nani Anayestahili’

‘Tafuteni Ni Nani Anayestahili’

DAMASKO lilikuwa jiji lenye ufanisi la karne ya kwanza katika Wakati wetu wa Kawaida. Jiji hilo lililozungukwa na mashamba ya matunda, lilikuwa mahali pa kupumzikia pa misafara ambayo ilitoka nchi za mashariki ya Damasko. Muda mfupi baada ya Yesu Kristo kufa, kulikuwa na kutaniko la Kikristo jijini Damasko. Miongoni mwa washiriki wake mlikuwemo Wayahudi ambao huenda walipata kuwa wafuasi wa Yesu kwenye Sherehe ya Pentekoste huko Yerusalemu mwaka wa 33 W.K. (Matendo 2:5, 41) Huenda wanafunzi fulani kutoka Yudea walihamia Damasko mateso yalipoanza baada ya Stefano kupigwa mawe.—Matendo 8:1.

Yaelekea katika mwaka wa 34 W.K., Mkristo fulani kutoka Damasko aitwaye Anania alipata mgawo usio wa kawaida. Bwana alimwambia: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na kwenye nyumba ya Yuda tafuta mtu anayeitwa jina Sauli, kutoka Tarso. Kwa maana, tazama! anasali.”—Matendo 9:11.

Barabara iliyoitwa Nyoofu ilikuwa na urefu wa kilometa moja na nusu, nayo ilipita katikati ya Damasko. Kwa kutazama mchoro wa karne ya 19 kwenye ukurasa huu, tunaweza kuwazia jinsi barabara hiyo ilivyokuwa nyakati za kale. Kutokana na jinsi barabara hiyo ilivyokuwa, huenda Anania alilazimika kutafuta kwa muda fulani ili kuipata nyumba ya Yuda. Hata hivyo, Anania aliipata na kutokana na ziara yake, Sauli akawa mtume Paulo, mtangazaji mwenye bidii wa habari njema.—Matendo 9:12-19.

Yesu alikuwa amewatuma wanafunzi wake na kuwaambia ‘watafute ni nani wanaostahili’ habari njema. (Mathayo 10:11) Yaonekana kwamba Anania alimtafuta Sauli kihalisi. Kama Anania, Mashahidi wa Yehova hutafuta kwa furaha watu wanaostahili, nao hufurahi watu wanapokubali habari njema za Ufalme. Kuwapata hufanya jitihada zao ziwe na maana.—1 Wakorintho 15:58.

[Picha katika ukurasa wa 32]

From the book La Tierra Santa, Volume II, 1830

[Picha katika ukurasa wa 32]

“Barabara inayoitwa Nyoofu” leo