Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Vaeni Mavazi Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”

“Vaeni Mavazi Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”

“Vaeni Mavazi Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”

“Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.”—WAEFESO 6:11.

1, 2. Kwa maneno yako mwenyewe, eleza kuhusu silaha ya kiroho ambayo Wakristo wanahitaji kuvaa.

ROMA ilikuwa imefikia kilele cha utawala wake katika karne ya kwanza W.K. Nguvu za vikosi vya Waroma ziliwezesha jiji la Roma kudhibiti sehemu kubwa ya ulimwengu uliojulikana wakati huo. Mwanahistoria mmoja alitaja jeshi hilo kuwa “lenye kufanikiwa zaidi katika historia.” Jeshi stadi la Roma lilikuwa na askari waliopewa nidhamu na waliopata mazoezi makali, lakini pia walifanikiwa kuwa jeshi lenye kupigana vizuri kwa sababu ya silaha zao. Mtume Paulo alitumia mfano wa silaha za askari Mroma kueleza kuhusu silaha za kiroho ambazo Wakristo wanahitaji ili kupigana kwa mafanikio dhidi ya Ibilisi.

2 Tunapata maelezo kuhusu mavazi hayo ya kiroho kwenye Waefeso 6:14-17. Paulo aliandika: “Simameni imara, viuno vyenu vikiwa vimefungwa kwa ile kweli, na mkiwa mmevaa bamba la kifuani la uadilifu, na mkiwa mmevaa miguuni mwenu viatu vya habari njema ya amani. Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu. Pia, ipokeeni kofia ya chuma ya wokovu, na upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” Kwa maoni ya kibinadamu, mavazi kamili ya silaha ambayo Paulo alieleza yalimkinga kabisa askari Mroma. Askari huyo pia alibeba upanga, ambao ni silaha yake kuu aliyotumia kupigana na mtu mwingine.

3. Kwa nini tunapaswa kutii maagizo ya Yesu Kristo na kufuata kielelezo chake?

3 Mafanikio ya jeshi la Roma hayakutegemea tu silaha na mazoezi, bali pia utii wa askari kwa kamanda wao. Vivyo hivyo, Wakristo wanapaswa kumtii Yesu Kristo, ambaye Biblia humtaja kuwa “kamanda kwa vikundi vya mataifa.” (Isaya 55:4) Yeye pia ni “kichwa cha kutaniko.” (Waefeso 5:23) Yesu hututolea maagizo ili tuwe na hali nzuri ya kiroho, naye huweka kielelezo kikamilifu kuhusu jinsi ya kuvaa mavazi hayo ya kiroho. (1 Petro 2:21) Kwa kuwa utu kama wa Kristo unafanana sana na mavazi yetu ya silaha za kiroho, Maandiko hutushauri ‘tujivike silaha’ ya mwelekeo wa akili wa Kristo. (1 Petro 4:1) Tunapochanganua kila sehemu ya silaha zetu za kiroho, basi tutatumia kielelezo cha Yesu ili kuonyesha umuhimu wa silaha hizo, na matokeo yake.

Kulinda Kiuno, Kifua, na Miguu

4. Kuhusiana na silaha za askari, mshipi ulikuwa muhimu kwa njia gani, nao unafananisha nini?

4 Viuno vikiwa vimefungwa kwa ile kweli. Katika nyakati za Biblia, askari walivaa mshipi wa ngozi uliokuwa na upana wa sentimeta 5 hadi 15. Watafsiri fulani hudokeza kwamba mstari huo unapaswa kutafsiriwa hivi, “kweli ikiwa mshipi uliofungwa kiunoni mwako.” Mshipi wa askari ulimsaidia kulinda kiuno chake, na ulikuwa na mahali pazuri pa kuning’iniza upanga. Askari alipofunga kiuno chake, alikuwa tayari kupigana. Paulo alitumia mfano wa mshipi wa askari ili kuonyesha kadiri ambayo kweli ya Kimaandiko inapaswa kuwa na uvutano maishani mwetu. Tunapaswa kuukaza mshipi huo kwa njia ya mfano, ili tuishi kupatana na ile kweli na kuweza kuitetea wakati wowote ule. (Zaburi 43:3; 1 Petro 3:15) Kwa kufikiria lengo hilo, tunahitaji kujifunza Biblia kwa bidii na kutafakari habari zake. Yesu alikuwa na ‘sheria ya Mungu ndani yake.’ (Zaburi 40:8) Kwa hiyo, alipoulizwa maswali na wapinzani, angeweza kujibu kwa kunukuu Maandiko kutoka akilini.—Mathayo 19:3-6; 22:23-32.

5. Eleza jinsi shauri la Kimaandiko linavyoweza kutusaidia wakati wa jaribu au kishawishi.

5 Tunaporuhusu kweli ya Biblia ituongoze, inaweza kutulinda na mawazo ya uwongo na kutuwezesha kufanya maamuzi ya hekima. Tunapopatwa na kishawishi au jaribu, miongozo ya Biblia itaimarisha azimio letu la kufanya yanayofaa. Itakuwa kana kwamba tunamwona Mfundishaji wetu Mkuu, Yehova, na tutasikia neno nyuma yetu likisema: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—Isaya 30:20, 21.

6. Kwa nini moyo wetu wa mfano unahitaji kulindwa, nao uadilifu unawezaje kuulinda kwa matokeo?

6 Bamba la kifuani la uadilifu. Bamba la kifuani la askari lililinda moyo ambao ni kiungo muhimu. Moyo wetu wa mfano, yaani, mtu wetu wa ndani, unahitaji ulinzi wa pekee kwa sababu una mwelekeo wa kutenda mabaya. (Mwanzo 8:21) Kwa hiyo, tunapaswa kujifunza na kuvipenda viwango vya uadilifu vya Yehova. (Zaburi 119:97, 105) Tukiupenda uadilifu tutakataa maoni ya ulimwengu ambayo hupuuza miongozo ya Yehova iliyo wazi. Isitoshe, tunapopenda yaliyo sawa na kuchukia mabaya, tunaepuka kufuata mwenendo unaoweza kuharibu maisha yetu. (Zaburi 119:99-101; Amosi 5:15) Yesu anatuwekea kielelezo bora kuhusiana na jambo hilo, kwa kuwa Maandiko yanasema hivi kumhusu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria.”—Waebrania 1:9. *

7. Kwa nini askari Mroma alihitaji viatu vizuri, navyo vinafananisha nini?

7 Miguu iwe imevaa viatu vya habari njema ya amani. Askari Waroma walihitaji viatu au makubadhi ya kudumu, kwa kuwa mara nyingi wakati wa shughuli za kijeshi walitembea kilometa 30 kila siku wakiwa wamevaa au wamebeba silaha zenye uzito wa kilogramu 27. Kwa kufaa, Paulo alitaja viatu ili kuwakilisha utayari wetu wa kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa kila mtu atakayesikiliza. Jambo hilo ni muhimu kwa sababu watu watapataje kumjua Yehova ikiwa hatuko tayari kuhubiri?—Waroma 10:13-15.

8. Tunawezaje kuiga kielelezo cha Yesu akiwa mhubiri wa habari njema?

8 Ni kazi gani iliyokuwa muhimu zaidi katika maisha ya Yesu? Alimwambia Gavana Mroma Pontio Pilato hivi: “Nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Yesu alihubiri mahali popote alipopata mtu aliyekuwa tayari kusikiliza, naye alifurahia sana huduma yake hivi kwamba aliiona kuwa muhimu zaidi kuliko mahitaji yake ya kimwili. (Yohana 4:5-34; 18:37) Ikiwa sisi tuna tamaa kama ya Yesu ya kutangaza habari njema, tutapata nafasi nyingi za kuwaeleza wengine kuihusu. Isitoshe, kujihusisha sana na huduma yetu kutatusaidia tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho.—Matendo 18:5.

Ngao, Kofia ya Chuma, na Upanga

9. Ngao kubwa ilimlindaje askari Mroma?

9 Ngao kubwa ya imani. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ngao kubwa” hurejelea ngao ambayo ilikuwa kubwa sana hivi kwamba ingefunika sehemu kubwa ya mwili. Ingemlinda mtu dhidi ya ‘mishale inayowaka moto’ inayotajwa kwenye Waefeso 6:16. Katika nyakati za Biblia, askari walitumia vishale vilivyotengenezwa kwa matete yenye chombo kidogo cha chuma ambacho kingeweza kujazwa mafuta mepesi yanayowaka. Msomi mmoja anaeleza kuhusu vishale hivyo kuwa “mojawapo ya silaha hatari zaidi katika vita vya kale.” Ikiwa askari hakuwa na ngao kubwa ya kujilinda dhidi ya mishale hiyo, angeweza kujeruhiwa vibaya au hata kuuawa.

10, 11. (a) Ni ‘mishale gani inayowaka moto’ ya Shetani ambayo inaweza kudhoofisha imani yetu? (b) Kielelezo cha Yesu kinaonyeshaje umuhimu wa kuwa na imani nyakati za jaribu?

10 Shetani hutumia ‘mishale gani inayowaka moto’ ili kudhoofisha imani yetu? Huenda akachochea mateso au upinzani katika familia, kazini, au shuleni. Tamaa ya kupata vitu vingi zaidi vya kimwili, na kishawishi cha kufanya ngono vimewadhuru Wakristo fulani kiroho. ‘Zaidi ya mambo yote, tunapaswa kuichukua ngao kubwa ya imani,’ ili kujilinda dhidi ya hatari hizo. Imani hutokana na kujifunza kumhusu Yehova, kuwasiliana naye kwa ukawaida katika sala, na kutambua jinsi anavyotulinda na kutubariki.—Yoshua 23:14; Luka 17:5; Waroma 10:17.

11 Yesu alipokuwa duniani, alionyesha umuhimu wa kuwa na imani yenye nguvu nyakati za hatari. Alitumaini kabisa maamuzi ya Baba yake, naye alifurahia kufanya mapenzi ya Mungu. (Mathayo 26:42, 53, 54; Yohana 6:38) Hata alipopatwa na maumivu makali katika bustani ya Gethsemane, Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Si kulingana na mapenzi yangu, bali kulingana na mapenzi yako.” (Mathayo 26:39) Yesu hakusahau kamwe umuhimu wa kudumisha utimilifu na kumfurahisha Baba yake. (Methali 27:11) Tukiwa na uhakika kama huo katika Yehova, hatutaruhusu uchambuzi au upinzani udhoofishe imani yetu. Badala yake, imani yetu itaimarishwa ikiwa tutamtegemea Mungu, kumpenda, na kutii amri zake. (Zaburi 19:7-11; 1 Yohana 5:3) Vitu vya kimwili au raha za kimwili za muda haziwezi kulinganishwa na baraka ambazo Yehova atawapa wale wanaompenda.—Methali 10:22.

12. Kofia yetu ya chuma ya mfano hulinda sehemu gani muhimu, na kwa nini ulinzi huo ni muhimu?

12 Kofia ya chuma ya wokovu. Kofia ya chuma ililinda kichwa na ubongo wa askari, yaani, kitovu cha uwezo wa kufikiri. Tumaini letu la Kikristo linalinganishwa na kofia ya chuma kwa sababu linalinda akili zetu. (1 Wathesalonike 5:8) Ingawa tumefanya upya akili zetu kupitia ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, bado sisi ni wanadamu dhaifu na wasio wakamilifu. Akili zetu zinaweza kupotoshwa kwa urahisi. Miradi ya mfumo huu wa mambo inaweza kutukengeusha au hata kuchukua mahali pa tumaini letu tulilopewa na Mungu. (Waroma 7:18; 12:2) Ibilisi alijaribu pasipo mafanikio kumkengeusha Yesu kwa kumtolea “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” (Mathayo 4:8) Lakini Yesu alikataa katakata toleo hilo, naye Paulo akasema hivi kumhusu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele [ya Yesu], yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:2.

13. Tunawezaje kudumisha uhakika wetu katika tumaini lililo mbele yetu?

13 Uhakika ambao Yesu alikuwa nao haukutokea tu wenyewe. Tukijaza akili zetu ndoto na miradi ya mfumo huu wa mambo badala ya kukazia fikira tumaini lililo mbele yetu, imani yetu katika ahadi za Mungu itadhoofika zaidi. Baada ya muda, hata tunaweza kupoteza kabisa tumaini hilo. Kwa upande mwingine, tukitafakari kwa ukawaida ahadi za Mungu, tutaendelea kufurahia tumaini lililowekwa mbele yetu.—Waroma 12:12.

14, 15. (a) Upanga wetu wa mfano ni nini, na unaweza kutumiwaje? (b) Eleza jinsi upanga wa roho unavyoweza kutusaidia kupinga kishawishi.

14 Upanga wa roho. Neno la Mungu, au ujumbe, ulioandikwa katika Biblia ni kama upanga wenye makali kuwili, ambao unaweza kubomoa uwongo wa kidini na kusaidia watu wenye mioyo mizuri wapate uhuru wa kiroho. (Yohana 8:32; Waebrania 4:12) Upanga huo wa kiroho unaweza pia kutulinda tunapokabiliwa na vishawishi au jitihada za waasi-imani za kuharibu imani yetu. (2 Wakorintho 10:4, 5) Tunashukuru kama nini kwamba ‘Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu, nalo hutufanya tuwe na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema’!—2 Timotheo 3:16, 17.

15 Aliposhawishiwa na Shetani akiwa nyikani, Yesu alitumia kwa matokeo upanga wa roho ili kupinga mawazo ya uwongo na vishawishi vyenye hila. Yesu alijibu hivi kwa kila kishawishi cha Shetani: “Imeandikwa.” (Mathayo 4:1-11) Vivyo hivyo, David, ambaye ni Shahidi wa Yehova anayeishi Hispania, aliona kwamba Maandiko yalimsaidia kushinda kishawishi. Mvulana huyo alipokuwa na umri wa miaka 19, mwanamke mmoja kijana mwenye kuvutia ambaye alifanya kazi naye katika kampuni ileile inayoshughulikia usafi, alipendekeza “wawe na wakati wa kujifurahisha pamoja.” David alikataa utongozaji wa mwanamke huyo na akamwomba mkubwa wake ampe kazi mahali pengine ili hali hiyo isitokee tena. “Nilikumbuka mfano wa Yosefu,” akasema David. “Alikataa kujihusisha na ukosefu wa adili na kuondoka mahali hapo mara moja. Nilifanya kama yeye.”—Mwanzo 39:10-12.

16. Eleza kwa nini tunahitaji kufanya mazoezi ili ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’

16 Yesu pia alitumia upanga wa roho ili kuwasaidia wengine waponyoke udhibiti wa Shetani. Yesu alisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Ili kuiga ustadi wa Yesu wa kufundisha, tunahitaji kufanya mazoezi. Mwanahistoria Myahudi Josephus aliandika hivi kuhusu askari wa Roma: “Kila askari alifanyishwa mazoezi kila siku na kwa bidii nyingi kana kwamba alikuwa vitani, na ndiyo sababu angeweza kuvumilia kwa urahisi uchovu unaotokana na mapigano.” Katika vita vyetu vya kiroho, tunahitaji kutumia Biblia. Isitoshe, tunapaswa ‘kufanya kabisa yote tuwezayo ili tujitoe kwa Mungu tukiwa watu waliokubaliwa, wafanyakazi wasio na lolote la kuonea aibu, tukilitumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Nasi hupata furaha iliyoje tunapotumia Maandiko kujibu swali la unyoofu la mtu anayependezwa!

Sali Kila Wakati

17, 18. (a) Sala hutimiza fungu gani katika kumpinga Shetani? (b) Toa mfano wa kuonyesha umuhimu wa sala.

17 Baada ya kuzungumzia mavazi kamili ya silaha za kiroho, Paulo anataja shauri lingine muhimu. Ili kumpinga Shetani, Wakristo wanapaswa kutoa “kila namna ya sala na dua.” Mara ngapi? ‘Endelezeni sala kila wakati katika roho,’ akaandika Paulo. (Waefeso 6:18) Tunapokabili vishawishi, majaribu, au kuvunjika moyo, sala inaweza kutuimarisha sana. (Mathayo 26:41) Yesu “alitoa dua na pia maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi, naye akasikiwa vizuri kwa sababu ya kumwogopa Mungu.”—Waebrania 5:7.

18 Milagros, ambaye amemtunza mume wake mwenye ugonjwa wa kudumu kwa zaidi ya miaka 15, anasema: “Ninapohisi kuwa nimevunjika moyo, mimi husali kwa Yehova. Hakuna mtu anayeweza kunisaidia zaidi kuliko Yehova. Ni kweli kwamba kuna nyakati ambazo mimi huhisi kwamba siwezi kuvumilia tena. Lakini mara nyingi baada ya kusali kwa Yehova, nimehisi kuwa nimepata nguvu mpya na kuhisi nafuu.”

19, 20. Tunahitaji nini ili kushinda pigano letu dhidi ya Shetani?

19 Ibilisi anajua kwamba wakati wake ni mfupi, naye anazidisha jitihada zake ili atushinde. (Ufunuo 12:12, 17) Tunapaswa kumpinga adui huyo mwenye nguvu na ‘kupigana pigano zuri la imani.’ (1 Timotheo 6:12) Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuwa na nguvu zinazopita zile za kawaida. (2 Wakorintho 4:7) Pia tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu, hivyo tunapaswa kusali ili tuipate. Yesu alisema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:13.

20 Bila shaka, ni muhimu kwamba tuvae mavazi kamili ya silaha ambazo Yehova hutuandalia. Kuvaa silaha hizo za kiroho hutaka tusitawishe sifa za kimungu, kama vile imani na uadilifu. Hilo hutaka tuipende ile kweli kana kwamba tumejifunga kweli hiyo, kwamba tuwe tayari kueneza habari njema kila wakati, na kwamba tuweke karibu akilini tumaini lililo mbele yetu. Tunapaswa kujifunza jinsi ya kutumia upanga wa roho kwa ustadi. Kwa kuvaa mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, tunaweza kushinda tunapopigana mweleka na roho waovu, nasi hakika tunaweza kuleta sifa kwa jina takatifu la Yehova.—Waroma 8:37-39.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Katika unabii wa Isaya, Yehova mwenyewe anaelezwa kuwa anavaa “uadilifu kama vazi la chuma.” Hivyo, anataka waangalizi wa kutaniko watekeleze haki na kutenda kwa uadilifu.—Isaya 59:14, 15, 17.

Ungejibuje?

• Ni nani anayetuwekea kielelezo bora zaidi cha kuvaa silaha za kiroho, na kwa nini tunapaswa kufikiria kielelezo chake kwa makini?

• Tunawezaje kulinda akili zetu na mioyo yetu ya mfano?

• Tunawezaje kuwa stadi katika kutumia upanga wa roho?

• Kwa nini tunapaswa kuendelea kusali kila wakati?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kujifunza Biblia kwa bidii kunaweza kutuchochea kutangaza habari njema kila wakati

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tumaini letu hakika hutusaidia kukabili majaribu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, wewe hutumia “upanga wa roho” katika huduma?