Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aliwaeleza Wanadarasa Wenzake Imani Yake

Aliwaeleza Wanadarasa Wenzake Imani Yake

Aliwaeleza Wanadarasa Wenzake Imani Yake

JE, UNGEPENDA kuwasaidia wanadarasa wenzako wafahamu vizuri zaidi imani yako inayotegemea Biblia? Magdalena aliye mwanafunzi wa shule ya sekondari mwenye umri wa miaka 18 huko Poland, huzungumza mara nyingi na wanadarasa wenzake kuhusu imani yake akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, mara nyingi yeye huulizwa maswali kama vile, ‘Inamaanisha nini kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?’ na ‘Je, ninyi hamwamini Yesu Kristo?’ Angewezaje kuwasaidia wanadarasa wenzake? Magdalena alimwomba Yehova mwongozo, naye akatenda kulingana na sala zake.—Yakobo 1:5.

Siku moja Magdalena alimwuliza mwalimu anayeheshimu imani yake ikiwa angeweza kuwaonyesha wanadarasa wenzake ile video Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name. * Mwalimu alikubali. Kisha Magdalena akawaambia wanadarasa wenzake: “Ninapanga rafiki fulani atolee darasa letu programu ya dakika 90. Itatia ndani kuona video na mazungumzo kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Je mngependa kuja?” Wote walisema ndiyo. Magdalena na Wojciech, mweneza-injili mwenye uzoefu, wakaanza kujitayarisha kwa ajili ya mradi huo.

Walipanga kuanza utoaji huo kwa hotuba ya dakika 20 ikitegemea broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? * kisha ifuatiwe na mazungumzo ya maswali na majibu. Halafu video ionyeshwe katika maktaba ya shule. Kila mwanafunzi katika darasa angepewa zawadi—bahasha kubwa yenye broshua kadhaa, kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo kazi, * na trakti chache pamoja na magazeti.

Siku ya utoaji ilipofika, wanadarasa 14, mwalimu, na wanafunzi wengine wanne waliokuwa katika maktaba walihudhuria. Kwanza, Wojciech alieleza kwamba washairi na waandishi fulani Wapoland walilitumia jina la Mungu, Yehova, katika maandishi yao. Pia alitaja kwamba katekisimu fulani za zamani za Katoliki zilikuwa na jina hilo la Mungu. Akieleza kuhusu kazi ya siku hizi ya Mashahidi wa Yehova, alionyesha broshua za ofisi mbalimbali za tawi na picha za Majumba ya Kusanyiko kadhaa.

Mazungumzo yenye kupendeza yalifuata. Magdalena na Wojciech walitumia Biblia kujibu maswali. Jambo hilo liliwapendeza waliohudhuria na kuwasadikisha kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuwa wakihubiri maoni yao wenyewe. Ni yapi baadhi ya maswali yaliyoulizwa, nayo yalijibiwaje?

Swali: Biblia ina semi na mifano mingi isiyoeleweka kwa urahisi ambayo inaweza kufasiriwa kwa njia nyingi. Inawezekanaje kuishi kupatana na Biblia?

Jibu: Wengine husema kwamba Biblia ni kama chombo cha muziki unachoweza kutumia kupiga muziki wowote unaopenda. Lakini, ebu fikiri: Ikiwa ungependa kujua mwandishi anamaanisha nini kwa taarifa zake, je, haingefaa kumwuliza? Tofauti na waandishi wa vitabu vya kibinadamu waliokufa, Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, yuko hai. (Waroma 1:20; 1 Wakorintho 8:5, 6) Muktadha wa andiko unaweza kuonyesha fasiri iliyo sahihi. Isitoshe, mara nyingi Maandiko huzungumzia jambo lilelile katika sehemu kadhaa, kwa hiyo kuyalinganisha kunaweza kutusaidia. Hivyo, tunaweza kumwacha Mungu aongoze maoni yetu, kana kwamba yeye mwenyewe ndiye anayetuelezea andiko hilo. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kujua na kuishi kulingana na mapenzi yake kama yalivyofunuliwa katika Biblia, au sivyo?

Swali: Kuna tofauti gani kati ya Wakristo na Mashahidi wa Yehova?

Jibu: Sisi ni Wakristo! Lakini badala ya kudai tu kuwa Wakristo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuishi kulingana na wanayoamini na kulingana na yale ambayo Mungu anawafundisha kwa faida yao. (Isaya 48:17, 18) Wao wanajua kwamba wana ukweli, kwa kuwa mafundisho yao yote yanategemea Biblia.—Mathayo 7:13, 14, 21-23.

Swali: Kwa nini ninyi huwaendea watu msiowajua kabisa na kusema nao? Je, huko si kuwalazimishia wengine imani yenu?

Jibu: Je, unafikiri ni kosa mtu anaposema nawe barabarani kwa upole na kukuuliza maoni yako kuhusu jambo fulani? (Yeremia 5:1; Sefania 2:2, 3) (Kisha Wojciech na Magdalena wakaonyesha jinsi walivyowauliza wapita-njia ikiwa Mungu anajali wale waliopatwa na mafuriko yaliyotokea hivi majuzi huko Poland.) Baada ya kusikiliza maoni yake, tunamwelekeza katika Biblia. Iwapo mtu hataki kusema nasi, tunamuaga na kusonga mbele. (Mathayo 10:11-14) Je, huku ni kumlazimisha mtu aseme nasi? Au siku hizi watu hawapaswi kuzungumza?

Swali: Kwa nini hamsherehekei sikukuu?

Jibu: Sisi hukumbuka tukio moja tu ambalo Biblia hutuamuru tuadhimishe—Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo. (1 Wakorintho 11:23-26) Kuhusu sikukuu, unaweza kuchunguza kuhusu mwanzo wazo katika ensaiklopedia na vyanzo vingine vinavyotegemeka. Ikiwa utafanya hivyo, utaona kwa urahisi kwa nini sisi hatusherehekei sikukuu hizo.—2 Wakorintho 6:14-18.

Maswali mengi zaidi yaliulizwa na yakajibiwa. Mazungumzo hayo yalichukua muda mrefu sana hivi kwamba ilitulazimu kuahirisha kuonyesha video.

Wanafunzi waliitikiaje? Acheni Magdalena atueleze: “Nilishangaa kwamba baadhi ya wanafunzi ambao kwa kawaida hutenda kipumbavu na kuwadhihaki wengine, waliuliza maswali yenye maana. Ingawa walidai kuwa hawaamini kuna Mungu, wakati wa mazungumzo walionyesha imani katika Mungu!” Wale waliokuwepo walipokea zawadi kwa shukrani tulizowapa, yaani, jumla ya vitabu 35, broshua 63, na magazeti 34.

Hayo yalikuwa matokeo mazuri kama nini ya mradi uliofanywa shuleni! Zaidi ya kuwasaidia wanadarasa wa Magdalena kuwajua na kuwaelewa Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi, kuliwachochea vijana wengi wafikirie kusudi la maisha. Kwa nini usijitahidi kuwasaidia wanadarasa wenzako wajifunze mengi zaidi kuhusu yale unayoamini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Imetolewa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 4 Imetolewa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 4 Imetolewa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Magdalena na Wojciech wakijitayarisha kwa ajili ya mazungumzo