Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Elimu Ambayo Imeendelea Katika Maisha Yangu Yote

Elimu Ambayo Imeendelea Katika Maisha Yangu Yote

Simulizi la Maisha

Elimu Ambayo Imeendelea Katika Maisha Yangu Yote

LIMESIMULIWA NA HAROLD GLUYAS

Mandhari fulani niliyoona nikiwa mtoto imedumu katika kumbukumbu langu kwa miaka zaidi ya 70. Nilikuwa nimeketi katika chumba cha kupikia cha Mama, nikitazama kibandiko kilichokuwa na maneno “Chai ya Ceylon.” Pia kilikuwa na picha ya wanawake fulani wakichuma majani chai katika mashamba ya kijani-kibichi ya Ceylon (ambayo sasa ni Sri Lanka). Mandhari hiyo ya eneo lililo mbali sana na sehemu kavu tulikoishi huko Australia Kusini, ilichochea fikira zangu. Nchi hii ya Ceylon ni yenye kuvutia na kusisimua kama nini! Sikujua kabisa kwamba ningeishi katika kisiwa hicho chenye kuvutia kwa miaka 45 nikiwa mmishonari.

NILIZALIWA mnamo Aprili 1922. Wakati huo, ulimwengu ulikuwa tofauti sana na jinsi ulivyo leo. Familia yetu ilifanya kazi katika shamba la ngano lililokuwa karibu na mji wa Kimba, ambao uko katikati ya bara kuu la Australia na mpaka wa kusini wa jangwa kuu la Australia. Maisha yalikuwa yenye hatari nyingi zilizotia ndani ukame wa mara kwa mara, maradhi yanayosababishwa na wadudu, na joto kali. Mama alifanya kazi kwa bidii ili kumtunza Baba na sisi watoto sita katika nyumba ya mashambani, ambayo ilikuwa kibanda kidogo tu kilichojengwa kwa mabati.

Hata hivyo, kwa upande wangu, bara la Australia lilikuwa mahali penye uhuru na penye kusisimua. Ninakumbuka nilipokuwa mtoto jinsi nilivyoshangaa kuona ng’ombe-dume wenye nguvu wakilima pori lenye magugu au dhoruba zenye vumbi zikifunika kabisa eneo hilo. Hivyo, kwa kweli elimu yangu maishani ilianza kabla sijaanza kwenda shule ndogo iliyokuwa na mwalimu mmoja tu aliyefunza madarasa yote, nayo ilikuwa umbali wa kilometa tano kutoka nyumbani.

Wazazi wangu walipenda dini, ingawa hawakuwahi kwenda kanisani, hasa kwa sababu shamba letu lilikuwa mbali na mji. Hata hivyo, katika miaka ya mapema ya 1930, Mama alianza kusikiliza hotuba za Biblia zilizotolewa na Hakimu Rutherford, ambazo zilitangazwa kila juma kwenye kituo cha redio huko Adelaide. Nilifikiri kwamba Hakimu Rutherford alikuwa mhubiri fulani tu huko Adelaide, nami sikupendezwa sana na hotuba hizo. Lakini kila juma Mama alingojea kwa hamu hotuba zake na kusikiliza kwa makini sauti yake ambayo haikusikika vizuri katika redio yetu ya zamani iliyotumia mawe.

Alasiri moja yenye joto na vumbi, gari moja la zamani lilisimama mbele ya nyumba yetu, na wanaume wawili waliovalia vizuri wakatoka nje. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Mama alisikiliza ujumbe wao naye akatoa mchango kwa ajili ya vitabu kadhaa alivyochukua, na ambavyo alianza kuvisoma mara moja. Vitabu hivyo vilimvutia sana hivi kwamba alimwomba Baba ampeleke kwa majirani ili akazungumze nao kuhusu yale aliyokuwa akijifunza.

Manufaa ya Uvutano Mzuri

Muda mfupi baadaye, ilitubidi kuhamia jiji la Adelaide lililoko umbali wa kilometa 500 kwa sababu ya hali ngumu ya mazingira. Familia yetu ilianza kushirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Adelaide nayo ikafanya maendeleo ya kiroho. Pia, tulipohama elimu yangu ilikatizwa. Nilimaliza shule nikiwa na umri wa miaka 13, baada ya kumaliza darasa la saba. Kwa kuwa sikujali sana mambo, jambo hilo lingeweza kunifanya niache kwa urahisi kufuatia mambo ya kiroho ikiwa singepata msaada kutoka kwa ndugu kadhaa wazuri—mapainia, au wahudumu wa wakati wote—ambao walipendezwa kibinafsi nami.

Muda si muda, uvutano wa ndugu hao wenye bidii ulichochea upendezi wangu kuelekea mambo ya kiroho. Nilipenda sana kuwa pamoja nao na nilivutiwa na bidii yao. Hivyo, tangazo lililowatia watu moyo kufanya utumishi wa wakati wote lilipotolewa kwenye kusanyiko la wilaya huko Adelaide mnamo 1940, bila kutarajia, mara moja nilitoa jina langu. Wakati huo, hata sikuwa nimebatizwa na sikuwa na uzoefu mwingi katika kuhubiri. Hata hivyo, siku chache baadaye, nilialikwa kujiunga na kikundi kidogo cha mapainia huko Warrnambool, mji ulio umbali wa kilometa mia kadhaa kutoka Adelaide, kwenye jimbo jirani la Victoria.

Licha ya mwanzo huo usio imara, punde si punde nilianza kupenda huduma ya shambani, na ninafurahi kusema kwamba nimedumisha upendo huo kwa miaka mingi. Kwa kweli, hilo lilikuwa badiliko muhimu kwangu, nami nikaanza kufanya maendeleo halisi ya kiroho. Nilijifunza umuhimu wa kuwakaribia wale waliopenda mambo ya kiroho. Niligundua jinsi uvutano mzuri unavyoweza kutokeza sifa zetu nzuri licha ya elimu yetu ndogo na jinsi mambo tunayojifunza yanavyoweza kutufaidi katika maisha yetu yote.

Kutiwa Nguvu na Majaribu

Nilikuwa nimefanya upainia kwa muda mfupi tu wakati kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipopigwa marufuku huko Australia. Kwa kuwa sikuwa na hakika kuhusu jambo la kufanya, nilitafuta mwongozo kutoka kwa akina ndugu, ambao waliniambia kwamba hakuna marufuku kuhusu kusema na watu juu ya Biblia. Hivyo, nikiwa pamoja na mapainia wengine, nilianza kwenda nyumba kwa nyumba nikiwa na ujumbe rahisi kutoka katika Biblia. Hilo lilinitia nguvu kwa ajili ya majaribu yaliyokuwa mbele.

Miezi minne baadaye, nilifikisha umri wa miaka 18 na niliamuriwa kuingia kwenye utumishi wa jeshi. Hilo lilinipa nafasi ya kutetea imani yangu mbele ya hakimu na maofisa kadhaa wa jeshi. Wakati huo, yapata ndugu 20 hivi walikuwa katika jela huko Adelaide kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo, na baada ya muda nikaungana nao. Tulipewa kazi ngumu ya kuchimba mawe na kutengeneza barabara. Hilo lilinisaidia kusitawisha sifa kama vile uvumilivu na azimio. Mwishowe, mwenendo wetu mzuri na msimamo thabiti ulifanya tuheshimiwe na walinzi wengi wa gereza.

Baada ya kuachwa huru miezi mingi baadaye, nilifurahia chakula kizuri na papo hapo nikaanza tena utumishi wa painia. Hata hivyo, haikuwa rahisi kupata mapainia wa kuandamana nao. Kwa hiyo, niliulizwa ikiwa ningetumika peke yangu katika eneo la mbali la mashambani huko Kusini mwa Australia. Nilikubali nami nikasafiri kwa mashua kwenda Rasi ya Yorke, nikiwa tu na vifaa vya kuhubiri na baiskeli. Nilipofika, familia moja yenye kupendezwa ilinielekeza kwenye nyumba ndogo ya wageni ambapo mwanamke mmoja mwenye fadhili alinitunza kama mtoto wake. Mchana niliendesha baiskeli kwenye barabara zenye vumbi huku nikihubiri katika miji midogo iliyotapakaa kwenye rasi hiyo. Ili kuhubiri katika maeneo ya mbali, mara kwa mara nililala kwenye hoteli ndogo au kwenye nyumba za wageni. Kwa kufanya hivyo, nilizunguka mamia ya kilometa na kufurahia mambo mengi mazuri yaliyoonwa. Sikusumbuliwa kamwe na wazo la kwamba nilikuwa peke yangu katika utumishi, na kwa kuwa niliona utunzaji wa Yehova, niliweza kumkaribia zaidi.

Kupambana na Hali ya Kuhisi Kwamba Sifai

Mnamo 1946, nilipokea barua ya kunialika kuanza kazi ya kusafiri nikiwa mtumishi wa akina ndugu (ambaye sasa ni mwangalizi wa mzunguko). Hilo lilitia ndani kutembelea makutaniko kadhaa katika mzunguko hususa. Lazima nikiri kwamba niliona madaraka ya mgawo huo kuwa kazi ngumu kwelikweli. Siku moja, nilisikia ndugu fulani akisema, “Harold si msemaji mzuri, lakini anafanya vema katika kazi ya kuhubiri.” Maneno hayo yalinitia moyo sana. Nilijua vizuri kwamba sikuwa msemaji mzuri na kwamba sikujua sana kupanga mambo, lakini niliamini kwamba kazi ya kuhubiri ndiyo iliyokuwa utendaji muhimu zaidi kwa Wakristo.

Mwaka wa 1947 kulikuwa na msisimko mkubwa kuhusu ziara ya Ndugu Nathan Knorr na Milton Henschel kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn. Hiyo ilikuwa ziara ya kwanza tangu Ndugu Rutherford alipokuja mnamo 1938. Kusanyiko kubwa lilifanywa huko Sydney wakati wa ziara hiyo. Kama vile vijana wengine wengi mapainia, nilipendezwa na mazoezi ya umishonari yaliyokuwa yakitolewa kwenye Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) iliyokuwa imeanzishwa tu huko South Lansing, New York, U.S.A. Wengi wetu kati ya wahudhuriaji tulijiuliza ikiwa tungetakiwa kuwa na elimu ya juu ili kukubaliwa kuhudhuria shule hiyo. Hata hivyo, Ndugu Knorr alieleza kwamba ikiwa tungeweza kusoma makala katika gazeti Mnara wa Mlinzi na kukumbuka mambo makuu, huenda tungeweza kufanya vema Gileadi.

Nilihisi kwamba sikustahili kwa sababu sikuwa na elimu. Nilishangaa kwamba miezi kadhaa baadaye nilitiwa moyo nijaze ombi la kujiunga na shule ya Gileadi. Baadaye, nilikubaliwa kuwa mwanafunzi, na nilihudhuria darasa la 16, lililofanywa mnamo 1950. Kuhudhuria shule kuliimarisha sana uhakika wangu. Nilitambua kwamba si lazima mtu awe na elimu ya juu ili afanikiwe. Badala yake, bidii na utii ndiyo yaliyokuwa matakwa muhimu. Walimu wetu walitutia moyo tufanye yote tuwezayo. Nilipotii shauri lao, nilifanya maendeleo makubwa na kuelewa vizuri mambo yaliyofundishwa.

Kutoka Australia Hadi Ceylon (Sri Lanka)

Baada ya kuhitimu, mimi na ndugu wawili kutoka Australia tulipewa mgawo kwenda Ceylon (sasa Sri Lanka). Tulifika katika mji mkuu, Kolombo, mnamo Septemba 1951. Kulikuwa na joto na unyevunyevu, na pia mchanganyiko wa mandhari, harufu nzuri, na sauti nyingi geni. Tuliposhuka kwenye meli, mmoja wa wamishonari aliyekuwa akitumika katika nchi hiyo alinikaribisha na kunipa kikaratasi cha mwaliko kilichokuwa na tangazo la hotuba ya watu wote ambayo ingetolewa jijini Jumapili iliyofuata. Nilishanga kuona jina langu kwenye kikaratasi hicho, kama msemaji. Unaweza kuwazia wasiwasi niliokuwa nao. Lakini miaka ambayo nilifanya upainia huko Australia ilinifunza kukubali mgawo wowote ambao nilipewa. Hivyo, kwa msaada wa Yehova, nilitoa hotuba hiyo vizuri. Sisi pamoja na ndugu wanne waseja ambao wakati huo walikuwa kwenye nyumba ya wamishonari ya Kolombo, tulianza kushiriki katika huduma ya shambani. Wakati huohuo, sisi watatu tulianza kujifunza lugha ngumu ya Sinhala. Mara nyingi, tulihubiri tukiwa peke yetu, na tulifurahia kuona kwamba wenyeji walikuwa wenye heshima na wakaribishaji. Punde si punde, hudhurio la mikutano lilianza kuongezeka.

Kadiri wakati ulivyopita, nilianza kumfikiria sana dada mmoja painia mwenye kuvutia, Sybil, ambaye tulikutana nilipokuwa nikisafiri kwa meli kwenda kuhudhuria Shule ya Gileadi. Alikuwa akisafiri kwenda kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa huko New York. Baadaye, alihudhuria darasa la 21 la Gileadi na kutumwa Hong Kong mnamo 1953. Niliamua kumwandikia, nasi tuliendelea kuandikiana hadi 1955 wakati Sybil alipokuja kujiunga nami huko Ceylon, ambako tulifunga ndoa.

Mgawo wetu wa kwanza tukiwa pamoja kama mume na mke wamishonari ulikuwa Jaffna, jiji lililo mbali kaskazini ya Sri Lanka. Katikati ya miaka ya 1950, tofauti za kisiasa zilianza kugawanya jamii za Wasinhala na Watamil, na hivyo kuanzisha hali iliyosababisha mapambano ya kutumia silaha ambayo yalitokea miaka ya baadaye. Lilikuwa jambo lenye kugusa moyo kama nini kuona Mashahidi Wasinhala na Watamil wakilindana kwa muda wa miezi kadhaa wakati wa miaka hiyo yenye magumu! Majaribu hayo yaliboresha na kuimarisha imani ya ndugu hao.

Kuhubiri na Kufundisha Huko Sri Lanka

Kujiambatanisha na hali za jamii za Kihindu na Kiislamu kulitaka subira na uvumilivu. Hata hivyo, tulianza kuelewa tamaduni zao na kuvutiwa na sifa za jamii hizo mbili. Kwa kuwa halikuwa jambo la kawaida kuona wageni wakisafiri kwenye mabasi, mara nyingi watu walitutazama kwa mshangao. Sybil aliamua kwamba angekuwa akiitikia kwa kutabasamu. Lilikuwa jambo lenye kufurahisha kama nini kuona watu hao wenye nyuso zenye mshangao wakitabasamu pia!

Pindi moja, tulisimamishwa kwenye kizuizi cha barabarani. Baada ya mlinzi aliyekuwa hapo kutuuliza tunatoka wapi na tunaenda wapi, maswali yake yalianza kuingilia mambo ya kibinafsi.

“Huyu mwanamke ni nani?”

Nikajibu, “Ni mke wangu.”

“Mmeoana kwa miaka mingapi sasa?”

“Miaka minane.”

“Je, mna watoto?”

“Hapana.”

“Mungu wangu! Mmemwona daktari?”

Mwanzoni, tabia hiyo ya kutaka kujua mambo ya wengine ilitushangaza, lakini baadaye tuliiona kuwa wonyesho wao wa kweli wa kupendezwa kibinafsi na wengine. Kwa kweli, tabia hiyo ilikuwa mojawapo ya sifa zao zenye kuvutia. Mtu alihitaji tu kusimama mahali pa umma kwa muda mfupi naye angeona mtu fulani akimkaribia na kumuuliza kwa fadhili ikiwa angeweza kumsaidia kwa vyovyote.

Mabadiliko na Kumbukumbu

Kwa miaka mingi, tumefurahia migawo mbalimbali zaidi ya kazi ya umishonari huko Sri Lanka. Nilipewa mgawo wa kutumika kama mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya, na pia nikawa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Kufikia 1996, nilikuwa na miaka 70 na kitu. Nilitumika nikiwa mmishonari huko Sri Lanka kwa zaidi ya miaka 45. Kulikuwa watu 20 hivi katika mkutano wa kwanza niliohudhuria huko Kolombo. Kwa sasa hesabu hiyo imeongezeka kufikia zaidi ya 3,500! Mimi na Sybil tuliwaona wengi wa wapendwa hao kuwa watoto na wajukuu wetu wa kiroho. Hata hivyo, bado kulikuwa na kazi nyingi ya kufanywa nchini kote, kazi inayohitaji nguvu na uwezo wa akili wa walio vijana zaidi kuliko sisi. Tukiwa na hilo akilini, tulikubali mwaliko kutoka kwa Baraza Linaloongoza wa kurudi Australia. Tulipoondoka, wenzi wa ndoa wamishonari wenye kustahili na walio vijana zaidi walipata nafasi ya kuingia Sri Lanka ili kuchukua nafasi yetu.

Kwa sasa nina umri wa miaka 83 na kitu, na mimi na Sybil tunafurahi kwamba bado tuna afya nzuri vya kutosha ili kuendelea na utumishi wetu wa painia wa pekee katika eneo langu la kwanza la Adelaide. Huduma yetu inatusaidia tuendelee kuwa chonjo kiakili na wenye kubadilikana na hali. Pia imetusaidia kujiambatanisha na hali tofauti za maisha katika nchi hii.

Yehova ameendelea kutosheleza mahitaji yetu yote ya kimwili, nao ndugu na dada katika kutaniko letu wanatuonyesha upendo mwingi na kututegemeza. Hivi karibuni, nilipokea mgawo mpya. Nitatumika nikiwa mwandishi katika kutaniko letu. Hivyo, nimeona kwamba kwa kujitahidi kumtumikia Yehova kwa uaminifu, mazoezi yangu bado yanaendelea. Ninapokumbuka miaka ambayo imepita, sikuzote mimi hushangaa kwamba, kijana asiye maarufu kutoka mashambani angeweza kupata elimu kama hiyo yenye kustaajabisha na ambayo imeendelea katika maisha yangu yote.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Siku ya arusi yetu mwaka wa 1955

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikiwa katika utumishi wa shambani pamoja na Rajan Kadirgamar, ndugu mwenyeji, mnamo 1957

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikiwa na Sybil leo