Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Iweni na Upendo Mwororo kwa Mtu na Mwenzake”

“Iweni na Upendo Mwororo kwa Mtu na Mwenzake”

“Iweni na Upendo Mwororo kwa Mtu na Mwenzake”

“Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.”—WAROMA 12:10.

1, 2. Mmishonari mmoja wa kisasa na mtume Paulo walikuwa na uhusiano gani pamoja na ndugu zao?

KATIKA miaka 43 ya utumishi wa umishonari huko Mashariki ya Mbali, Don alijulikana kwa shauku aliyokuwa nayo kuelekea wale aliowatumikia. Alipokuwa anapambana na ugonjwa ambao hatimaye ulimuua, baadhi ya wanafunzi wake wa Biblia wa zamani walisafiri maelfu ya kilometa ili kumwona na kumwambia, “Kamsahamnida, kamsahamnida!”—“Asante sana, sana!” katika Kikorea. Upendo mwororo wa Don ulikuwa umegusa mioyo yao.

2 Si Don tu aliyegusa mioyo ya watu. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alionyesha upendo mwingi mwororo kwa wale aliowatumikia. Paulo alikuwa mwenye kujidhabihu. Ingawa alikuwa mtu mwenye usadikisho imara, pia alikuwa mpole na mwenye kujali, “kama mama mwenye kunyonyesha anavyowatunza kwa upendo watoto wake mwenyewe.” Aliandikia kutaniko la Thesalonike hivi: “Tukiwa na upendo mwororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa ninyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu ninyi mlikuwa wapendwa kwetu.” (1 Wathesalonike 2:7, 8) Baadaye, wakati Paulo alipowaambia ndugu zake wa Efeso kwamba hawangemwona tena, ‘wote walilia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo.’ (Matendo 20:25, 37) Ni wazi kwamba uhusiano kati ya Paulo na ndugu zake ulizidi ule uhusiano wa kuwa na imani moja. Walikuwa na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.

Upendo Mwororo na Upendo

3. Maneno ya Biblia upendo mwororo na upendo yanahusianaje?

3 Katika Biblia, upendo mwororo, hisia-mwenzi, na huruma ni sifa zinazohusiana sana na upendo ambao ndio sifa bora zaidi kati ya sifa za Kikristo. (1 Wathesalonike 2:8; 2 Petro 1:7) Kama pande za almasi maridadi, sifa hizo zote za kimungu zilizo bora hufanya kazi pamoja na kuwa na matokeo mazuri sana. Sifa hizo hufanya Wakristo wawe na ukaribu si kati ya mtu na mwenzake tu bali pia kati yao na Baba yao wa mbinguni. Kwa hiyo, mtume Paulo aliwahimiza hivi waamini wenzake: “Upendo wenu na uwe bila unafiki. . . . Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.”—Waroma 12:9, 10.

4. Maneno “upendo mwororo” yanamaanisha nini?

4 Neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia kumaanisha “upendo mwororo” lina sehemu mbili, sehemu moja inamaanisha urafiki, na ile nyingine upendo wa asili. Kama msomi mmoja wa Biblia anavyoeleza, hiyo inamaanisha kwamba Wakristo “wanapaswa kutambuliwa kwa ujitoaji ambao unapatikana katika familia yenye upendo, yenye uhusiano wa karibu, na yenye kutegemezana.” Je, hivyo ndivyo unavyohisi kuhusu ndugu na dada zako Wakristo? Hali yenye shauku, yaani, kuhisi kuwa wa jamaa moja, inapaswa kuenea katika kutaniko la Kikristo. (Wagalatia 6:10) Hivyo, The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips, hutafsiri Waroma 12:10 hivi: “Na tuwe na upendo wenye shauku kwelikweli kwa mtu na mwenzake kama kati ya ndugu.” Nayo tafsiri ya The Jerusalem Bible inasema: “Pendaneni kama vile ndugu wanavyopaswa kupendana.” Naam, Wakristo hupendana si kwa sababu tu ni jambo linalofaa au kwa sababu wana wajibu wa kufanya hivyo. ‘Tukiwa na upendo wa kindugu usio na unafiki,’ tunapaswa ‘kupendana sana kutoka moyoni.’—1 Petro 1:22.

‘Tumefundishwa na Mungu Kupendana’

5, 6. (a) Yehova ametumiaje makusanyiko ya kimataifa kuwafundisha watu wake kuhusu upendo wa Kikristo? (b) Uhusiano kati ya akina ndugu huimarikaje baada ya muda fulani?

5 Ingawa katika ulimwengu huu “upendo wa walio wengi zaidi” unapoa, Yehova anawafundisha watu wake leo “kupendana.” (Mathayo 24:12; 1 Wathesalonike 4:9) Makusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova huandaa pindi za pekee kwa ajili ya mafundisho hayo. Kwenye makusanyiko hayo, Mashahidi wenyeji hukutana na ndugu wanaotoka nchi za mbali, na wengi wamewakaribisha wajumbe hao kutoka nchi za kigeni. Katika kusanyiko moja hivi karibuni, baadhi ya wajumbe walitoka katika nchi ambako kwa kawaida watu hawaonyeshi hisia zao waziwazi. “Wajumbe hao walipofika mara ya kwanza, walikuwa na haya na wasiwasi mwingi,” aeleza Mkristo mmoja aliyesaidia katika idara ya mahali pa kulala. “Lakini siku sita tu baadaye, walipokuwa wakiagana, wao na wale waliowakaribisha walikumbatiana na kulia. Walifurahia aina ya upendo wa Kikristo ambao hawatausahau kamwe.” Kuwaonyesha ndugu zetu ukaribishaji-wageni, bila kujali malezi yao, kunaweza kutokeza sifa bora za mkaribishaji na mwenye kukaribishwa.—Waroma 12:13.

6 Ingawa mambo hayo yaliyoonwa kwenye makusanyiko ni yenye kusisimua, Wakristo wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi kwa kumtumikia Yehova pamoja baada ya muda fulani. Tunapowajua ndugu zetu vizuri, tunaweza kuthamini zaidi sifa zao zenye kuvutia kama vile kusema kweli, kutumainika, ushikamanifu, fadhili, ukarimu, ufikirio, huruma, na kutokuwa na ubinafsi. (Zaburi 15:3-5; Methali 19:22) Mark, aliyetumika akiwa mmishonari Afrika Mashariki, alisema, “Kufanya kazi bega kwa bega pamoja na ndugu zetu hutokeza uhusiano usioweza kuvunjwa.”

7. Ni nini kinachohitajiwa ili kufurahia upendo wa Kikristo kutanikoni?

7 Ili kuwa na uhusiano huo na kuudumisha katika kutaniko, washiriki wake wanapaswa kuwa na ukaribu. Kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, tunaimarisha uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu. Kwa kuwepo kwenye mikutano, kuzungumza kabla na baada ya mikutano, na kuishiriki, tunatiana moyo na kuchocheana “katika upendo na matendo mazuri.” (Waebrania 10:24, 25) Mzee mmoja huko Marekani anaeleza, “Mimi hukumbuka kwa upendo kwamba nilipokuwa mtoto, sikuzote familia yetu ndiyo iliyokuwa ya mwisho kuondoka kwenye Jumba la Ufalme. Tulibaki huko kwa muda mrefu iwezekanavyo ili kufurahia mazungumzo yenye kujenga.”

Je, Unahitaji ‘Kupanuka’?

8. (a) Paulo alimaanisha nini alipowahimiza Wakorintho ‘wapanuke’? (b) Tunaweza kufanya nini ili kusaidia kuongeza upendo kutanikoni?

8 Ili kuonyesha upendo huo kikamili, huenda tukahitaji ‘kupanuka’ katika mioyo yetu. Mtume Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Korintho: “Moyo wetu umepanuka. Ninyi hamjasongwa mkakosa nafasi ndani yetu.” Paulo aliwahimiza wao pia ‘wapanuke.’ (2 Wakorintho 6:11-13) Je, wewe pia unaweza ‘kupanuka’ katika upendo wako? Si lazima ungojee wengine wachukue hatua ya kwanza. Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alihusianisha uhitaji wa kuwa na upendo na shauri hili: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10) Ili kuwaonyesha wengine heshima, unaweza kuchukua hatua ya kwanza kuwasalimu kwenye mikutano. Unaweza pia kuwaalika wajiunge nawe katika huduma ya shambani au kutayarisha sehemu fulani ya mkutano. Kufanya hivyo husaidia upendo mwororo uongezeke.

9. Wengine wamechukua hatua zipi ili kuwa na urafiki wa karibu na Wakristo wenzao? (Taja mifano yoyote ya kwenu.)

9 Familia na watu mmoja-mmoja kutanikoni wanaweza ‘kupanuka’ kwa kutembeleana, labda kwa kula pamoja, na kwa kushiriki katika utendaji unaofaa. (Luka 10:42; 14:12-14) Mara kwa mara, Hakop hupanga matembezi ya vikundi vidogo. Anasema kwamba, “watu wa umri wote wanakuwapo, kutia ndani wazazi wasio na mwenzi. Kila mmoja huenda nyumbani akiwa na kumbukumbu zenye furaha, na kujihisi akiwa na ukaribu na mwenzake.” Tukiwa Wakristo, tunapaswa kujitahidi kuwa marafiki wa kweli si waamini wenzi tu.—3 Yohana 14.

10. Tunaweza kufanya nini tunapokuwa na matatizo na ndugu zetu?

10 Hata hivyo, nyakati nyingine huenda hali ya kutokamilika ikafanya iwe vigumu kusitawisha urafiki na upendo. Tunaweza kufanya nini? Kwanza, tunaweza kusali ili tuwe na uhusiano mzuri na ndugu zetu. Ni mapenzi ya Mungu kwamba watumishi wake wawe marafiki, naye atajibu sala hizo za unyoofu. (1 Yohana 4:20, 21; 5:14, 15) Pia tunapaswa kutenda kupatana na sala zetu. Ric, mhudumu asafiriye katika Afrika Mashariki anakumbuka ndugu mmoja ambaye utu wake mgumu ulifanya isiwe rahisi kupatana naye. “Badala ya kumwepuka ndugu huyo, niliazimia kumjua vizuri zaidi,” asema Ric. “Niligundua kwamba baba ya ndugu huyo alitoa nidhamu kwa ukali sana. Nilipofahamu jinsi ndugu huyo alivyong’ang’ana kushinda hali hiyo na jinsi alivyokuwa amefanya maendeleo, nilivutiwa naye. Hivyo tukawa marafiki wakubwa.”—1 Petro 4:8.

Waeleze Wengine Hisia Zako!

11. (a) Ni nini kinachohitajiwa ili upendo uongezeke kutanikoni? (b) Kwa nini kutowaonyesha wengine hisia zetu kunaweza kuleta madhara kiroho?

11 Leo, watu wengi huishi maisha yao yote bila kuwa na rafiki yeyote wa karibu. Inasikitisha kama nini! Haipaswi kuwa hivyo kamwe katika kutaniko la Kikristo. Upendo wa kweli wa kindugu si kuwa tu na mazungumzo ya heshima au adabu nzuri; wala si kuonyesha hisia kwa njia inayopita kiasi. Badala yake, tunapaswa kuwa tayari kueleza hisia zetu, kama Paulo alivyofanya kwa Wakorintho, na kuwaonyesha waamini wenzetu kwamba tunajali hali yao kikweli. Ingawa si kila mtu anayependa kuongea sana, kuwa mnyamavu sana kunaweza kuleta madhara. Biblia inaonya, “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.”—Methali 18:1.

12. Kwa nini mawasiliano mazuri ni muhimu ili kuwa na mahusiano mazuri kutanikoni?

12 Ni muhimu kuwasiliana kwa unyoofu ili kuwa na urafiki wa kweli. (Yohana 15:15) Sote tunahitaji marafiki ambao tunaweza kuwaeleza mawazo na hisia zetu za ndani kabisa. Isitoshe, kadiri tunavyojuana vizuri zaidi, ndivyo inavyokuwa rahisi kutosheleza mahitaji ya mtu na mwenzake. Tunapoonyesha kwamba tunajali masilahi ya mtu na mwenzake kwa njia hiyo, tunasaidia kutaniko kuongeza upendo mwororo, nasi tutaona ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35; Wafilipi 2:1-4.

13. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba tuna upendo wa kweli kwa ndugu zetu?

13 Ili upendo wetu uwe na manufaa kabisa, tunapaswa kuuonyesha. (Methali 27:5) Upendo wetu unapokuwa wa kweli, yaelekea uso wetu utaonyesha hilo, na huenda ukachochea wengine watupende. “Kung’aa kwa macho hufanya moyo ushangilie,” akaandika mtu mwenye hekima. (Methali 15:30) Pia kutenda kwa ufikirio huongeza upendo mwororo. Ingawa hakuna anayeweza kununua upendo wa kweli, zawadi inayotolewa kutoka moyoni inaweza kuwa yenye maana sana. Kadi, barua, na “neno linalosemwa wakati unaofaa”—hayo yote yanaweza kuonyesha upendo mwingi. (Methali 25:11; 27:9) Baada ya kuanzisha urafiki na wengine, ni lazima tuudumishe kwa kuendelea kuonyesha upendo usio na ubinafsi. Hasa nyakati za uhitaji, tutataka kuwasaidia marafiki wetu. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

14. Tunaweza kufanya nini ikiwa inaonekana kwamba mtu fulani haitikii upendo wetu?

14 Ni kweli kwamba hatuwezi kutarajia kuwa na ukaribu na kila mtu kutanikoni. Kwa kawaida, kuna wale ambao tutajihisi kuwa na ukaribu zaidi nao kuliko wengine. Kwa hiyo, ikiwa mtu fulani haonekani kuwa mwenye urafiki kama ambavyo ungependa, usikate kauli upesi kwamba una shida au mtu huyo ana shida. Na usijaribu kumlazimisha mtu huyo awe rafiki yako wa karibu. Ukijitahidi tu kuwa mwenye urafiki kadiri mtu huyo atakavyoruhusu, huenda ukawa na uhusiano wa karibu zaidi naye wakati ujao.

“Nimekukubali Wewe”

15. Kutoa au kutotoa pongezi kuna matokeo gani kwa wengine?

15 Ni lazima Yesu awe alifurahi kama nini aliposikia maneno haya kutoka mbinguni wakati alipobatizwa: “Nimekukubali wewe”! (Marko 1:11) Lazima maneno hayo ya kuonyesha kibali yalizidisha usadikisho wa Yesu kwamba Baba yake alimpenda. (Yohana 5:20) Inasikitisha kwamba wengine hawapati kamwe pongezi kama hiyo kutoka kwa wale wanaowaheshimu na kuwapenda. “Vijana wengi kama mimi wanatoka katika familia ambazo washiriki wake wana imani ya Kikristo iliyo tofauti na yao,” asema Ann. “Nyumbani, sisi huchambuliwa tu. Hilo hutuhuzunisha sana.” Hata hivyo, wanapokuwa sehemu ya kutaniko, wanahisi shauku ya familia ya kiroho inayowategemeza na kuwajali, ambayo inatia ndani akina baba na mama na ndugu na dada katika imani.—Marko 10:29, 30; Wagalatia 6:10.

16. Kwa nini haifai kuonyesha mtazamo wa kuwachambua wengine?

16 Katika tamaduni fulani, ni mara chache sana ambapo wazazi, watu wenye umri mkubwa, na walimu huwapongeza vijana kwa moyo wote kwa sababu wanafikiri kwamba kuwapongeza kunaweza kufanya wajivune na wawe na kiburi. Maoni hayo yanaweza hata kuathiri familia za Kikristo na kutaniko. Wakitoa pongezi kuhusu hotuba au jitihada nyingine ambayo ndugu amefanya, huenda wenye umri mkubwa wakasema: “Ilikuwa sawa tu, lakini unaweza kufanya vizuri zaidi!” Au kwa njia nyingine, huenda hata wakadokeza kwamba hawapendezwi na kijana fulani. Wengi wanaamini kwamba kwa kufanya hivyo wanawachochea vijana wajitahidi kadiri ya uwezo wao. Lakini mara nyingi njia hiyo ina matokeo yaliyo kinyume, kwa kuwa huenda vijana wakajitenga au wakahisi kwamba hawawezi kufikia viwango wanavyotazamiwa kutimiza.

17. Kwa nini tunapaswa kutafuta nafasi za kuwapongeza wengine?

17 Hata hivyo, hatupaswi kutoa pongezi kwa sababu tu tunataka kutoa shauri. Pongezi ya kutoka moyoni huongeza upendo mwororo katika familia na kutanikoni, hivyo kuwatia moyo vijana watafute shauri kutoka kwa ndugu na dada wenye uzoefu. Kwa hiyo, badala ya kuwatendea wengine kulingana na utamaduni wetu, acheni ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’ Wapongeze wengine kama vile Yehova afanyavyo.—Waefeso 4:24.

18. (a) Enyi vijana, mnapaswa kulionaje shauri kutoka kwa watu wenye umri mkubwa? (b) Kwa nini watu wenye umri mkubwa huwa waangalifu kuhusu jinsi wanavyotoa shauri?

18 Kwa upande mwingine, enyi vijana msikate kauli kwamba watu wenye umri mkubwa hawawapendi wanapowasahihisha au kuwashauri. (Mhubiri 7:9) Hiyo si kweli! Yaelekea wanachochewa na hangaiko na upendo mwingi kuwaelekea. La sivyo, kwa nini wajisumbue kuzungumza nanyi kuhusu jambo hilo? Kwa kujua jinsi maneno yanavyoweza kuathiri mtu, wenye umri mkubwa—hasa wazee wa kutaniko mara nyingi—hutumia wakati mwingi kutafakari na kusali kabla ya kutoa shauri, kwa kuwa wanataka tu kufanya yaliyo mema.—1 Petro 5:5.

“Yehova Ni Mwenye Upendo Mwororo Sana”

19. Kwa nini wale ambao wamekatishwa tamaa baada ya kuonyesha upendo mwororo wanaweza kumtegemea Yehova?

19 Huenda watu fulani waliopatwa na hali zisizopendeza wakahisi kwamba kuonyesha upendo mwororo kunaweza tu kuwafanya wakate tamaa zaidi. Wanahitaji ujasiri na imani thabiti ili kuwaeleza wengine hisia zao tena. Lakini hawapaswi kusahau kamwe kwamba Yehova “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” Yeye anatualika tumkaribie. (Matendo 17:27; Yakobo 4:8) Pia anaelewa kwamba tunaogopa kuumizwa, naye anaahidi kwamba atatutegemeza na kutusaidia. Mtunga-zaburi Daudi anatuhakikishia hivi: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

20, 21. (a) Tunajuaje kwamba tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova? (b) Ni nini kinachotakiwa ili kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?

20 Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ndio uhusiano muhimu zaidi tunaoweza kusitawisha. Lakini je, uhusiano kama huo unawezekana kweli? Ndiyo. Biblia hueleza kuhusu wanaume na wanawake ambao walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Maneno yao yenye shauku yamehifadhiwa ili kutuhakikishia kwamba hata sisi tunaweza kumkaribia Yehova.—Zaburi 23, 34, 139; Yohana 16:27; Waroma 15:4.

21 Kila mtu anaweza kufikia matakwa ya Yehova ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. “Ee Yehova, ni nani atakayekuwa mgeni katika hema lako?” akauliza Daudi. “Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake.” (Zaburi 15:1, 2; 25:14) Tunapoona kwamba kumtumikia Mungu hutokeza matunda mazuri na kufanya tupate ulinzi na mwongozo wake, tutapata kutambua kwamba “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana.”—Yakobo 5:11.

22. Yehova anataka watu wake wawe na uhusiano wa aina gani?

22 Tumebarikiwa kama nini kwamba Yehova hutamani kuwa na uhusiano wa karibu na wanadamu wasio wakamilifu! Je, basi hatupaswi kuonyeshana upendo mwororo? Kwa msaada wa Yehova, kila mmoja wetu anaweza kuchangia na kuwa na upendo mwororo ambao ni sifa inayotambulisha undugu wetu wa Kikristo. Chini ya Ufalme wa Mungu, watu wote duniani watapendana milele.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni hali gani inayopaswa kuweko katika kutaniko la Kikristo?

• Kila mmoja wetu anawezaje kuchangia upendo mwororo kutanikoni?

• Pongezi ya kutoka moyoni huongezaje upendo wa Kikristo?

• Upendo mwororo wa Yehova hututegemezaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wakristo hupendana si kwa sababu tu wana wajibu wa kufanya hivyo

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, unaweza ‘kupanuka’ katika upendo wako?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, wewe ni mchambuzi au mwenye kutia moyo?