Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Yohana alipoandika kwamba “upendo mkamilifu hutupa woga nje,” alimaanisha nini kwa kusema “upendo mkamilifu,” nao ni “woga” upi unaotupwa nje?

“Hakuna woga katika upendo,” akaandika mtume Yohana, “lakini upendo mkamilifu hutupa woga nje, kwa sababu woga hutokeza kizuizi. Kwa kweli, yeye ambaye yuko chini ya woga hajakamilishwa katika upendo.”—1 Yohana 4:18.

Muktadha unaonyesha kwamba Yohana alikuwa akizungumzia uhuru wa kusema—hasa kuhusu uhusiano uliopo kati ya kumpenda Mungu na uhuru wa kusema naye. Tunaweza kuona jambo hilo katika mstari wa 17: “Hivi ndivyo upendo umekamilishwa ndani yetu, kwamba tuwe na uhuru wa kusema katika siku ya hukumu.” Mkristo anaweza kuwa na uhuru wa kusema au kukosa uhuru huo ikitegemea kadiri ambavyo anampenda Mungu na kuhisi upendo wake.

Usemi “upendo mkamilifu” ni muhimu. Kama linavyotumiwa katika Biblia, nyakati zote neno “kamilifu” halimaanishi ukamilifu katika maana yake kamili, yaani, kitu kisicho na kasoro, bali mara nyingi humaanisha ukamili. Kwa mfano, katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Lazima ninyi basi muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” Yesu alikuwa akiwaambia wafuasi wake kwamba ikiwa wangewapenda tu wale waliowapenda, basi upendo wao haungekuwa kamili, ungekuwa na kasoro. Walipaswa kufanya upendo wao uwe kamili kwa kuwapenda hata maadui wao. Vivyo hivyo, basi, wakati Yohana alipoandika kuhusu “upendo mkamilifu,” alikuwa akizungumza kuhusu upendo kwa Mungu ambao ni wa moyo wote, uliokomaa, na unaohusisha sehemu zote za maisha ya mtu.—Mathayo 5:46-48; 19:20, 21.

Mkristo anaposali kwa Mungu, anafahamu vizuri kabisa kwamba yeye ni mwenye dhambi na si mkamilifu. Hata hivyo, ikiwa upendo wake kwa Mungu na hisia zake kumwelekea zimekomaa kabisa, yeye hazuiwi na woga wa kushutumiwa au kukataliwa. Badala yake, yeye hufurahia uhuru wa kusema anapoeleza yale yaliyo moyoni na anapoomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ambayo Mungu ameandaa kwa upendo kupitia Yesu Kristo. Anakuwa na uhakika kwamba Mungu anasikiliza na kukubali maombi yake.

Mtu anawezaje “kukamilishwa katika upendo” na hivyo ‘autupe nje’ woga wa kuhukumiwa au kukataliwa? “Yeyote anayeshika neno lake, kwa kweli katika mtu huyo upendo kwa Mungu umekamilishwa,” akasema mtume Yohana. (1 Yohana 2:5) Ebu fikiria: Ikiwa Mungu alitupenda tulipokuwa tungali watenda dhambi, je, yeye hatatupenda hata zaidi tukitubu kikweli na ‘kulishika neno lake’ kwa bidii? (Waroma 5:8; 1 Yohana 4:10) Kwa kweli, mradi tu tunaendelea kuwa waaminifu, tunaweza kuwa na uhakika uleule aliokuwa nao mtume Paulo aliposema hivi kumhusu Mungu: “Yeye ambaye hakujizuia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini yeye pia pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?”—Waroma 8:32.