Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?

Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?

Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?

“Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu.”—UFUNUO 4:11.

1, 2. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba wanadamu hubuni vitu kwa kuiga uumbaji? (b) Ni swali gani ambalo hutokea, na jibu ni nini?

SIKU moja katika miaka ya 1940 injinia mmoja Mswisi, George de Mestral alienda kumtembeza mbwa wake. Aliporudi nyumbani, aliona kwamba nguo zake na pia manyoya ya mbwa wake yalikuwa yamejaa mbegu fulani zenye miiba-miiba. Kwa kuwa alitaka kujua mengi kuhusu mbegu hizo, alizichunguza kwa darubini naye alishangazwa na kulabu ndogo zilizokwamilia kitu chochote chenye manyoya. Mwishowe, alivumbua kishikizo cha nguo kinachofanya kazi sawasawa na mbegu hizo. Si De Mestral peke yake aliyeiga vitu vya asili. Huko Marekani, ndugu wawili Wilbur na Orville Wright walibuni eropleni baada ya kuchunguza jinsi ndege wakubwa wanavyoruka. Injinia Mfaransa Alexandre-Gustave Eiffel alibuni mnara ulio Paris uliopewa jina lake, akitumia kanuni za msingi ambazo huwezesha mfupa wa paja la binadamu kutegemeza uzito wa mwili.

2 Mifano hiyo inaonyesha vizuri jinsi ambavyo mara nyingi wanadamu hubuni vitu kwa kuiga uumbaji. Hata hivyo, ni jambo la busara kuuliza: Ni mara nyingi kadiri gani wabuni humpa sifa Yule aliyebuni zile mbegu ndogo zenye miiba-miiba, ndege wakubwa, mfupa wa paja la binadamu, na ubuni mwingine wote ulio mkamilifu ambao wanadamu wengi huiga? Inasikitisha, lakini ukweli ni kwamba katika ulimwengu wa leo, ni mara chache sana Mungu hupewa sifa au utukufu anaostahili.

3, 4. Ni nini maana ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa “utukufu,” nalo linapaswa kurejelea nini linapotumiwa kumhusu Yehova?

3 Huenda wengine wakajiuliza, ‘Kwa nini Mungu anapaswa kutukuzwa? Si tayari Mungu ametukuka?’ Ni kweli kwamba Yehova ndiye aliyetukuka zaidi katika ulimwengu wote, lakini hilo halimaanishi kwamba wanadamu wote humwona hivyo. Katika Biblia, maana ya msingi ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa “utukufu” ni “uzito.” Linarejelea kitu chochote ambacho humfanya mtu aonekane na wengine kuwa mwenye kutokeza au mashuhuri. Linapotumiwa kumhusu Mungu, neno hilo hurejelea kile ambacho humfanya Mungu awe mwenye kutokeza kwa wanadamu.

4 Watu wengi leo hawaelewi ni nini hufanya Mungu awe mwenye kutokeza. (Zaburi 10:4; 14:1) Kwa kweli, mara nyingi watu mashuhuri katika jamii, ambao hawamwamini Mungu, wamefanya watu wasimheshimu Muumba mtukufu wa ulimwengu wote. Wamefanya hivyo katika njia zipi?

“Hawana Sababu ya Kujitetea”

5. Wanasayansi wengi hutoa maelezo gani yanayopuuza maajabu ya uumbaji?

5 Wanasayansi wengi husisitiza kwamba hakuna Mungu. Hivyo basi, wao huelezaje maajabu ya uumbaji, kutia ndani wanadamu? Wao husema kwamba uumbaji ulitokana na mageuzi, nguvu fulani ambazo zilitokeza vitu kiaksidenti tu. Kwa mfano, mwana-mageuzi, Stephen Jay Gould, aliandika: “Tumekuwapo kwa sababu kikundi fulani cha samaki wasio wa kawaida walikuwa na mapezi ya kipekee, ambayo yangeweza kubadilika na kuwa miguu ya viumbe wa nchi kavu . . . Huenda tukatamani kupata jibu kutoka kwa ‘chanzo kilicho juu,’ lakini hatuwezi kupata.” Vivyo hivyo, Richard E. Leakey na Roger Lewin waliandika: “Labda wanadamu walitokana na aksidenti kubwa ya kibiolojia.” Hata wanasayansi fulani ambao husifu umaridadi na ubuni katika uumbaji hawampi Mungu sifa.

6. Ni nini huwavunja watu wengi moyo wasimpe Mungu sifa anayostahili akiwa Muumba?

6 Watu waliosoma sana wanapodai kwamba nadharia ya mageuzi ni ya kweli, wanadokeza kwamba wajinga tu ndio hukataa kuiamini. Wengi huitikiaje dai hilo? Miaka kadhaa iliyopita, mtu fulani aliyejua mengi sana kuhusu nadharia ya mageuzi aliwahoji watu waliokubali nadharia hiyo. Alisema: “Niligundua kwamba watu wengi wanaamini nadharia ya mageuzi kwa sababu wameambiwa kwamba watu wote wenye akili wanaamini nadharia hiyo.” Naam, watu wenye elimu wanapotoa maoni yao kuhusu kutokuwapo kwa Mungu, wao huwavunja wengine moyo wasimpe Mungu sifa anayostahili akiwa Muumba.—Methali 14:15, 18.

7. Kulingana na Waroma 1:20, ni nini kinachoweza kuonekana waziwazi kupitia uumbaji unaoonekana, na kwa nini?

7 Je, wanasayansi wamefikia kauli yao kwa sababu kuna uthibitisho unaounga mkono mageuzi? La! Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba kuna Muumba. Mtume Paulo aliandika hivi kumhusu: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu [wa wanadamu] na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba [wasioamini] hawana sababu ya kujitetea.” (Waroma 1:20) Tunaona waziwazi uthibitisho wa kuwapo kwa Muumba katika uumbaji wake. Hivyo, Paulo anasema kwamba tangu kuumbwa kwa mwanadamu, imewezekana kwa wanadamu ‘kuelewa’ uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu kupitia uumbaji unaoonekana. Uthibitisho huo unapatikana wapi?

8. (a) Mbingu halisi hushuhudiaje kwamba Mungu ana nguvu na hekima? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ulimwengu ulitokezwa?

8 Tunaona uthibitisho kwamba kuna Mungu kupitia mbingu zenye nyota. Zaburi 19:1 inasema, “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu.” “Mbingu,” yaani, jua, mwezi, na nyota, hushuhudia kwamba Mungu ana nguvu na hekima. Hesabu kubwa ya nyota hutuogopesha. Nazo nyota hizo zote za mbinguni husafiri angani kulingana na sheria hususa za asili, bali si kiholela. * (Isaya 40:26) Si jambo la busara hata kidogo kusema kwamba utaratibu huo ulitokea kiaksidenti tu. Jambo muhimu ni kwamba, wanasayansi wengi husema ulimwengu wote ulitukia kwa ghafula. Profesa mmoja aliandika hivi kueleza umuhimu wa imani hiyo: “Wazo la kwamba ulimwengu umekuweko sikuzote linakubalika na wakana-Mungu na wale wanaoamini kwamba habari za Mungu haziwezi kujulikana. Vivyo hivyo, ikiwa ulimwengu una mwanzo, lazima uwe ulitokezwa; kwani ni nani anayeweza kuwazia kwamba kunaweza kuwa na matokeo bila kisababishi?”

9. Hekima ya Yehova inaonekanaje katika wanyama?

9 Pia duniani tunaona uthibitisho kwamba kuna Mungu. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyotokeza.” (Zaburi 104:24) ‘Vitu vilivyotokezwa’ na Yehova kutia ndani wanyama, huthibitisha kwamba ana hekima. Kama tulivyotangulia kuona, vitu vilivyo hai vimebuniwa kwa njia bora sana hivi kwamba mara nyingi wanasayansi hujaribu kuviiga. Fikiria mifano mingine michache. Watafiti wanachunguza pembe za paa wakiwa na nia ya kutengeneza kofia za chuma zenye nguvu zaidi; wanachunguza aina fulani ya nzi ambaye ana uwezo mzuri sana wa kusikia wakitaka kuboresha vifaa vya kusaidia watu kusikia; na wanachunguza manyoya ya bawa la bundi wakiwa na wazo la kuboresha ndege ambazo ni vigumu kugunduliwa na rada. Hata mwanadamu ajaribu kadiri gani, hataweza kuiga kikamili ubuni ulio mkamilifu. Kitabu Biomimicry—Innovation Inspired by Nature kinasema: “Viumbe-hai vimefanya kila kitu ambacho sisi wanadamu tunataka kufanya bila kutumia nishati kupita kiasi, kuchafua dunia, au kuhatarisha wakati wao ujao.” Hiyo ni hekima iliyoje!

10. Kwa nini si jambo la akili kukataa kwamba kuna Muumba Mkuu? Toa mfano.

10 Hata kama utatazama anga au uumbaji ulio hapa duniani, kuna uthibitisho ulio wazi kwamba kuna Muumba. (Yeremia 10:12) Tunapaswa kukubaliana kabisa na viumbe wa mbinguni wanaopaaza sauti: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote.” (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, wanasayansi wengi hukosa kuona kwa ‘macho ya moyo wao,’ uthibitisho kwamba kuna Muumba, hata ingawa huenda wakashangazwa na jinsi ambavyo vitu wanavyoona kwa macho yao vimebuniwa. (Waefeso 1:18) Tunaweza kutoa mfano ufuatao: Ni jambo lisilo la akili kuvutiwa na umaridadi na ubuni wa uumbaji kisha kukataa kwamba kuna Muumba Mkuu, kama vile kuvutiwa na mchoro mzuri na wakati huohuo kukataa kwamba kuna mchoraji aliyechora picha hiyo kwenye turubai. Haishangazi kwamba wale wanaokataa kumwamini Mungu wanasemekana kuwa “hawana sababu ya kujitetea”!

“Viongozi Vipofu” Huwapotosha Wengi

11, 12. Fundisho la kwamba mambo yatakayompata mtu hupangwa mapema hutegemea wazo gani, na ni nini kinachoonyesha kwamba fundisho hilo halimtukuzi Mungu?

11 Watu wengi wa dini huamini kwa moyo mweupe kwamba ibada yao humtukuza Mungu. (Waroma 10:2, 3) Hata hivyo, kwa ujumla dini hufanyiza sehemu nyingine ya jamii ya wanadamu ambayo imewazuia watu wengi kumtukuza Mungu. Jinsi gani? Acheni tuzungumzie njia mbili.

12 Kwanza, dini hufanya watu wasimtukuze Mungu kupitia mafundisho ya uwongo. Kwa mfano, fikiria fundisho la kwamba mambo yatakayompata mtu hupangwa mapema. Fundisho hilo linategemea wazo la kwamba kwa kuwa Mungu ana uwezo wa kujua wakati ujao, lazima awe anajua kimbele matokeo ya kila kitu. Hivyo, fundisho hilo hudokeza kwamba Mungu alipanga mapema mambo yatakayotukia wakati ujao—mema au mabaya—kwa kila mtu. Kulingana na wazo hilo, Mungu ndiye anayepaswa kulaumiwa kwa mateso na uovu wote ulimwenguni leo. Bila shaka, wazo hilo halimtukuzi Mungu kwa kuwa linamshutumu isivyo haki badala ya kumshutumu Adui wake mkuu, Shetani, ambaye Biblia humwita “mtawala wa ulimwengu”!—Yohana 14:30; 1 Yohana 5:19.

13. Kwa nini ni jambo la upumbavu kufikiri kwamba Mungu hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua wakati ujao? Toa mfano.

13 Fundisho la kwamba mambo yatakayompata mtu hupangwa mapema si la Kimaandiko nalo humchongea Mungu. Fundisho hilo hufanya tusielewe mambo anayoweza kufanya na yale ambayo anafanya kikweli. Biblia hutaja waziwazi kwamba Mungu anaweza kujua kimbele matukio. (Isaya 46:9, 10) Hata hivyo, si jambo la akili kufikiri kwamba hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua wakati ujao au yeye ndiye anayepaswa kulaumiwa kwa kila jambo linalotokea. Kwa mfano: Kama ungekuwa na nguvu nyingi, je, ungehisi kwamba unataka kuinua kila kitu kizito unachoona? La! Vivyo hivyo, si lazima Mungu ajue kimbele kila kitu hata ingawa ana uwezo wa kujua wakati ujao. Yeye anachagua mambo anayotaka kujua kimbele. * Ni wazi kwamba mafundisho ya uwongo, kutia ndani fundisho la kwamba mambo yatakayompata mtu hupangwa mapema, hayamtukuzi Mungu.

14. Dini kubwa humvunjia Mungu heshima katika njia gani?

14 Njia ya pili ambayo dini kubwa humvunjia Mungu heshima ni kupitia mwenendo wa wafuasi wao. Wakristo wanapaswa kufuata mafundisho ya Yesu. Yesu aliwafunza wafuasi wake wafuate kanuni kama vile ‘kupendana’ na kubaki wakiwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:12; 17:14-16) Namna gani makasisi wa dini zinazojiita za Kikristo? Je, kweli wamefuata mafundisho hayo?

15. (a) Makasisi wamehusikaje katika vita vya mataifa? (b) Mwenendo wa makasisi umeathirije mamilioni ya watu?

15 Fikiria jinsi ambavyo makasisi wamehusika katika vita. Wameunga mkono, wakavifumbia macho, na hata kuwa mstari wa mbele katika vita vingi vya mataifa. Wamebariki vikosi na kuonyesha kwamba ni halali kuua. Tunalazimika kuuliza, ‘Je, makasisi hao hawajui kwamba wenzao kwenye upande ule mwingine wa vita wanafanya vivyo hivyo?’ (Ona sanduku “Mungu Yuko Upande wa Nani?”) Makasisi hawamtukuzi Mungu wanapodai kwamba anawaunga mkono katika vita vyenye umwagaji wa damu; nao hawamtukuzi Mungu wanaposema kwamba viwango vya Biblia vimepitwa na wakati na kufumbia macho mwenendo wa uasherati wa aina yoyote. Viongozi hao hutukumbusha viongozi wa dini ambao Yesu aliwataja kuwa “wenye matendo ya uasi-sheria” na “viongozi vipofu”! (Mathayo 7:15-23; 15:14) Mwenendo wa makasisi umefanya upendo wa mamilioni ya watu kuelekea Mungu upoe.—Mathayo 24:12.

Ni Nani Ambao kwa Kweli Wanamtukuza Mungu?

16. Ili kujibu swali la ni nani wanaomtukuza Mungu kikweli, kwa nini ni lazima tuichunguze Biblia?

16 Ikiwa kwa ujumla watu walio mashuhuri katika ulimwengu wameshindwa kumtukuza Mungu, basi ni nani ambao wanafanya hivyo kikweli? Ili kujibu swali hilo, ni lazima tuichunguze Biblia. Ni jambo linalopatana na akili kwamba Mungu ana haki ya kusema jinsi anavyopaswa kutukuzwa, naye huweka viwango katika Neno lake Biblia, kuhusiana na hilo. (Isaya 42:8) Na tuchunguze njia tatu za kumtukuza Mungu, na katika kila mojawapo, tutashughulika na lile swali la ni nani leo wanaofanya hivyo kikweli.

17. Yehova mwenyewe alionyeshaje kwamba kutukuzwa kwa jina lake ni sehemu muhimu ya mapenzi yake, na ni nani leo wanaolisifu jina la Mungu duniani kote?

17 Kwanza, tunaweza kumtukuza Mungu kwa kulisifu jina lake. Maneno ambayo Yehova alimwambia Yesu yanaonyesha kwamba kulisifu jina la Mungu ni sehemu muhimu ya mapenzi yake. Siku chache kabla Yesu hajafa, alisali hivi: “Baba, litukuze jina lako.” Kisha sauti ikajibu: “Nimelitukuza na pia nitalitukuza tena.” (Yohana 12:28) Bila shaka, Yehova ndiye aliyesema maneno hayo. Kulingana na jinsi alivyoitikia, ni wazi kwamba kutukuzwa kwa jina lake ni muhimu kwake. Basi ni nani leo wanaomtukuza Yehova kwa kulijulisha jina lake na kulisifu duniani kote? Ni Mashahidi wa Yehova, nao wanafanya hivyo katika nchi 235!—Zaburi 86:11, 12.

18. Tunawezaje kuwatambua wale wanaomwabudu Mungu katika “kweli,” na ni kikundi gani ambacho kimekuwa kikifundisha kweli ya Biblia kwa zaidi ya miaka 100?

18 Pili, tunaweza kumtukuza Mungu kwa kufundisha kweli kumhusu. Yesu alisema kwamba waabudu wa kweli ‘wangemwabudu Mungu katika kweli.’ (Yohana 4:24) Tunawezaje kuwatambua wale wanaomwabudu Mungu katika “kweli”? Lazima wakatae mafundisho yasiyotoka katika Biblia na ambayo humwakilisha Mungu na mapenzi yake isivyofaa. Badala yake, wanapaswa kufundisha kweli safi za Neno la Mungu, kutia ndani kweli hizi: Yehova ndiye Mungu Aliye Juu Zaidi, naye peke yake ndiye anayestahili utukufu wa kuwa juu zaidi sana (Zaburi 83:18); Yesu ni Mwana wa Mungu na Mtawala aliyewekwa rasmi wa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi (1 Wakorintho 15:27, 28); Ufalme wa Mungu utatakasa jina la Yehova na kutimiza kusudi lake kuelekea dunia hii na wanadamu wanaoishi humo (Mathayo 6:9, 10); lazima habari njema kuhusu Ufalme huo ihubiriwe duniani kote. (Mathayo 24:14) Kwa zaidi ya miaka 100, ni kikundi kimoja tu ambacho kimekuwa kikihubiri kweli hizo zenye thamani—Mashahidi wa Yehova!

19, 20. (a) Kwa nini mwenendo mzuri wa Mkristo unaweza kumtukuza Mungu? (b) Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kujua wale ambao wanamtukuza Mungu leo kwa kudumisha mwenendo mzuri?

19 Tatu, tunamtukuza Mungu kwa kuishi kupatana na viwango vyake. Mtume Petro aliandika: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Mwenendo wa Mkristo huonyesha jinsi imani yake ilivyo. Watazamaji wanapoona hivyo, yaani, wanapoona kwamba mwenendo mzuri wa Mkristo ni matokeo ya moja kwa moja ya imani yake, jambo hilo humtukuza Mungu.

20 Ni nani wanaomtukuza Mungu leo kwa kudumisha mwenendo mzuri? Ni kikundi gani cha kidini ambacho kimesifiwa na serikali nyingi kwa kuwa chenye amani, chenye kutii sheria za nchi, na ambacho hulipa kodi? (Waroma 13:1, 3, 6, 7) Ni watu gani ambao wanajulikana ulimwenguni kote kuwa wenye umoja na waamini wenzao, bila kujali tofauti za kijamii, kitaifa, na za kikabila? (Zaburi 133:1; Matendo 10:34, 35) Ni kikundi gani kinachotambuliwa ulimwenguni kote kwa kazi yao ya kufundisha Biblia ambayo huwatia watu moyo waheshimu sheria, maadili ya familia, na maadili ya Biblia? Kuna kikundi kimoja tu ambacho mwenendo wake mzuri kuhusiana na mambo hayo na mengine huthibitisha hilo—Mashahidi wa Yehova!

Je, Wewe Unamtukuza Mungu?

21. Kwa nini tunapaswa kufikiria kama sisi binafsi tunamtukuza Yehova?

21 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi binafsi ninamtukuza Yehova?’ Kulingana na Zaburi 148, karibu uumbaji wote unamtukuza Mungu. Malaika, mbingu halisi, dunia na wanyama—wote humsifu Yehova. (Mstari wa 1-10) Inasikitisha sana kwamba wanadamu wengi leo hawafanyi hivyo. Kwa kuishi maisha yanayomtukuza Mungu, unaungana na uumbaji mwingine unaomsifu Yehova. (Mstari wa 11-13) Hiyo ndiyo njia bora zaidi ya kutumia maisha yako.

22. Unabarikiwa katika njia zipi kwa kumtukuza Yehova, na unapaswa kuazimia kufanya nini?

22 Kwa kumtukuza Yehova, unabarikiwa katika njia nyingi. Unapodhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, unapatanishwa na Mungu na unafurahia uhusiano wenye amani na wenye kuthawabisha pamoja na Baba yako wa mbinguni. (Waroma 5:10) Unapotafuta sababu za kumtukuza Mungu, unakuwa na mtazamo mzuri, na unakuwa mwenye uthamini zaidi. (Yeremia 31:12) Kisha utaweza kuwasaidia wengine waishi maisha yenye furaha na yenye kusudi, na hivyo upate furaha nyingi zaidi. (Matendo 20:35) Na uwe kati ya wale ambao wameazimia kwa dhati kumtukuza Mungu—sasa na milele!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi mbingu halisi zinavyoonyesha kwamba Mungu ana hekima na nguvu, ona sura ya 5 na ya 17 ya kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Ona Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 853, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba kwa ujumla wanasayansi hawajawasaidia watu wamtukuze Mungu?

• Ni katika njia gani mbili dini kubwa zimewazuia watu wasimtukuze Mungu?

• Tunaweza kumtukuza Mungu katika njia zipi?

• Kwa nini unapaswa kuchunguza kama wewe binafsi unamtukuza Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

“Mungu Yuko Upande wa Nani?”

Mwanamume fulani aliyekuwa katika Jeshi la Anga la Ujerumani kwenye Vita vya Pili vya Ulimwengu, lakini ambaye baadaye alipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anakumbuka:

“Kilichonisumbua wakati wa miaka hiyo ya vita . . . ni kuona makasisi wa karibu dini zote—Katoliki, Lutheri, Anglikana, na kadhalika—wakibariki ndege na wanajeshi wa anga kabla ya kuondoka ili kwenda kuangusha makombora yao. Mara nyingi nilijiuliza, ‘Mungu yuko upande wa nani?’

“Askari-jeshi wa Ujerumani walijifunga mshipi wenye kishikizo kilichokuwa na maneno Gott mit uns (Mungu yuko pamoja nasi). Lakini nilijiuliza, ‘Kwa nini Mungu asiwe pamoja na askari wa upande ule mwingine ambao walikuwa wa dini ileile, na ambao walikuwa wakimwomba Mungu yuleyule?’”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mashahidi wa Yehova duniani kote wanamtukuza Mungu kikweli