Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Una Mtazamo wa Kungojea wa Aina Gani?

Una Mtazamo wa Kungojea wa Aina Gani?

Una Mtazamo wa Kungojea wa Aina Gani?

WATU wengi leo hukosa subira wanapolazimika kumngojea mtu au kitu fulani. Hata hivyo, Maandiko huwatia moyo watu wa Mungu wasitawishe ‘mtazamo wa kungojea.’ Tofauti na watu waliomzunguka, nabii Mika alisema hivi: “Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7; Maombolezo 3:26.

Hata hivyo, inamaanisha nini kumngojea Yehova? Mkristo anapaswa kumngojea Mungu jinsi gani? Je, kuna njia inayofaa na isiyofaa ya kufanya hivyo? Yale yaliyompata nabii Yona katika karne ya tisa K.W.K. hutufunza jambo fulani kuhusu hilo.

Kungojea Tukiwa na Sababu Isiyofaa

Yehova Mungu alimwamuru Yona aende akawahubirie watu wa Ninawi, mji mkuu wa Milki ya Ashuru. Kwa sababu ya ukatili na ujeuri uliokuwa dhahiri, Ninawi lilijulikana kuwa “jiji la umwagaji wa damu” kama inavyothibitishwa vizuri na wanahistoria na wanaakiolojia. (Nahumu 3:1) Mwanzoni, Yona alijaribu kuepuka mgawo wake, lakini Yehova alihakikisha kwamba mwishowe nabii huyo alienda Ninawi.—Yona 1:3–3:2.

“Yona akaanza kuingia jijini mwendo wa kutembea wa siku moja, naye aliendelea kutangaza na kusema: ‘Bado siku 40 tu, na Ninawi litaangamizwa.’” (Yona 3:4) Jitihada za Yona zilikuwa na matokeo mazuri sana: “Watu wa Ninawi wakaanza kumwamini Mungu, ndipo wakatangaza kufunga na kuvaa nguo za magunia, kutoka aliye mkubwa zaidi kati yao mpaka aliye mdogo zaidi.” (Yona 3:5) Hivyo, Yehova, Mungu ambaye “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba,” hakuliangamiza jiji hilo.—2 Petro 3:9.

Yona aliitikiaje? Masimulizi yanasema: “Hata hivyo, jambo hilo halikumpendeza Yona hata kidogo, naye akawaka hasira.” (Yona 4:1) Kwa nini? Labda Yona alihisi kwamba tangazo lake la uharibifu ambalo halikutimia katika tarehe hususa lilifanya asiheshimiwe kama nabii. Ni wazi kwamba alifikiria sana sifa yake badala ya kuwahurumia watu wengine na kufikiria wokovu wao.

Bila shaka, Yona hakufikia hatua ya kuacha kuwa nabii. Hata hivyo, alingojea ili ‘kuona jambo ambalo lingepata jiji hilo.’ Naam, alisitawisha mtazamo wenye uchungu ambao ulimfanya aache kwa muda kazi yake na kungojea aone jambo ambalo lingetukia. Alipotambua kwamba mambo hayakutukia kama alivyotarajia, alijitengenezea kibanda, akaketi chini ya kivuli, na kungojea kwa hasira aone jambo ambalo lingetukia. Lakini, Yehova hakukubaliana na mtazamo wa Yona, hivyo, kwa upendo, alisahihisha maoni yenye makosa ya nabii wake.—Yona 4:5, 9-11.

Kwa Nini Yehova Ana Subira?

Ingawa watu wa Ninawi walitubu nao hawakuangamizwa, baadaye walirudia njia zao mbaya. Yehova alitabiri uharibifu wa jiji hilo kupitia manabii Nahumu na Sefania. Akisema kuhusu “jiji la umwagaji wa damu,” Yehova alitangaza kwamba angeharibu Ashuru na kufanya Ninawi liwe mahame yenye ukiwa. (Nahumu 3:1; Sefania 2:13) Mnamo 632 K.W.K., Ninawi liliharibiwa, nalo halikujengwa tena kamwe.

Vivyo hivyo, leo ulimwengu una hatia kubwa zaidi ya umwagaji-damu kuliko Ninawi la kale. Kwa sababu hiyo na nyingine, Yehova ameamuru kwamba mfumo huu mwovu wa mambo utakwisha kwenye “dhiki kuu” isiyo na kifani.—Mathayo 24:21, 22.

Hata hivyo, Yehova amezuia uharibifu ulioahidiwa ili watu wanyoofu leo, kama watu wa Ninawi waliotubu, waweze kutubu na kuokoka. Mtume Petro anarejelea subira ya Mungu kwa maneno haya: “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyoona kukawia, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Petro 3:9, 10, 13.

Kungojea kwa Njia Inayofaa

Petro anaendelea kusema hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Petro 3:11, 12) Ona kwamba tunapokuwa tukingojea siku ya Yehova, tunapaswa kuonyesha “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu,” yaani, inafaa tuwe wenye kutenda wala si wasiotenda.

Naam, kuwa na mtazamo wa kungojea unaofaa kunaonyesha kwamba tuna uhakika kabisa kwamba siku ya Yehova itakuja wakati ambao Yehova amekusudia. Imani kama hiyo hutokeza matendo matakatifu na vitendo vya ujitoaji-kimungu, na tendo lililo muhimu zaidi ni kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Yesu aliweka kielelezo kizuri cha kuhubiri, naye aliwaagiza wanafunzi wake watiwa-mafuta hivi: “Viuno vyenu na vifungwe mishipi na taa zenu ziwe zikiwaka, nanyi mtakuwa kama watu wanaomngoja bwana wao wakati anaporudi kutoka kwenye karamu ya ndoa, ili atakapofika na kupiga hodi wapate kumfungulia mara moja. Wenye furaha ni watumwa ambao bwana anapofika anawakuta wakikesha!”—Luka 12:35-37.

Katika karne ya kwanza, watumwa walikuwa ‘wakijifunga mishipi kwenye viuno vyao’ kwa kupandisha nguo zao juu na kuzifunga kwa mshipi ili kuwawezesha kufanya kazi ngumu. Hivyo, Mkristo anapaswa kuwa mwenye nguvu na bidii katika kazi njema. Anapaswa kushindana na mwelekeo wowote wa ‘uvivu’ katika shughuli za kiroho, labda kwa kuepuka kutumia nguvu zake katika ufuatiaji wa anasa au vitu vya kimwili. Badala yake, anapaswa kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana” anapongojea siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.—Waroma 12:11; 1 Wakorintho 15:58.

Tuwe Wenye Shughuli Nyingi Tunapongojea

Mashahidi wa Yehova wamekuwa na shughuli nyingi wanapongojea siku ya Yehova. Kwa mfano, katika mwaka wa utumishi wa 2003, walitumia wastani wa saa 3,383,000 kila siku katika kazi ya kuhubiri neno la Yehova. Fikiria hili, mtu mmoja angepaswa kuhubiri mfululizo kwa miaka 386 ili kutimiza kazi iliyofanywa kwa siku moja!

Hata hivyo, tunapaswa kujiuliza, ‘Nina mtazamo wa kungojea wa aina gani?’ Yesu alitoa mfano ambao unaeleza bidii ya kazi ambayo Wakristo watiwa-mafuta waaminifu wanatarajiwa kuonyesha. Alizungumza kuhusu watumwa watatu: “[Bwana huyo] akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja, kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe, naye akaenda ng’ambo. Mara moja yule aliyezipokea talanta tano akaenda zake na kufanya biashara nazo na kupata faida ya tano zaidi. Vivyo hivyo yule aliyepokea mbili akapata faida ya mbili zaidi. Lakini yule aliyepokea moja tu akaenda zake, na kuchimba katika udongo na kuficha zile fedha za bwana wake. Baada ya muda mrefu bwana wa watumwa hao alikuja na kufanya hesabu pamoja nao.”—Mathayo 25:15-19.

Watumwa wote watatu walingojea bwana wao arudi. Wale wawili waliokuwa wenye shughuli nyingi walipokuwa wakingojea bwana wao, waliambiwa hivi wakati alipofika: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu!” Hata hivyo, yule aliyengojea bila kufanya lolote alitendewa tofauti. Bwana alisema: “Mtupeni nje katika giza mtumwa huyo asiyefaa kitu.”—Mathayo 25:20-30.

Ingawa mfano huo unahusu Wakristo watiwa-mafuta, unatufundisha sote jambo fulani, hata tuwe na tumaini gani. Bwana, Yesu Kristo, anatarajia kila mmoja wetu afanye kazi kwa bidii katika utumishi wake huku tukingojea siku kuu ya Yehova. Anathamini kazi ya kila mmoja ‘kulingana na uwezo wake mwenyewe’ na hali zake. Wakati wa kungojea utakapokwisha, itakuwa shangwe kama nini Bwana atakapotuambia “vema”!

Subira ya Bwana Wetu Humaanisha Wokovu

Namna gani ikiwa mfumo huu wa mambo umedumu kwa muda mrefu kuliko tulivyofikiri au kutarajia? Kuna sababu inayofanya mfumo huu wa mambo udumu kwa muda mrefu hivyo. Mtume Petro aliandika: “Ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” (2 Petro 3:15) Ujuzi sahihi wa kusudi la Mungu na kutambua kwa unyenyekevu kwamba sisi si muhimu kuliko utimizo wa kusudi lake, kutatuwezesha tuwe wenye subira kama Yehova alivyo mwenye subira kuelekea mfumo huu wa kale.

Ili kuwatia moyo Wakristo wawe wenye subira, mwandikaji wa Biblia Yakobo alitoa mfano mmoja. Aliandika: “Tazama! Mkulima huendelea kungojea matunda yenye thamani ya nchi, anayasubiri mpaka apate mvua ya mapema na mvua ya baadaye. Ninyi pia onyesheni subira; fanyeni mioyo yenu kuwa imara, kwa sababu kuwapo kwa Bwana kumekaribia.”—Yakobo 5:7, 8.

Yehova Mungu hataki tuchoke kabisa wala kukata tamaa tunapoendelea kungojea. Ametupatia kazi ambayo tunapaswa kufanya, naye hufurahi ikiwa tunatumia wakati huu wa kungojea kwa kuwa wenye bidii katika kazi hiyo. Anataka tuwe kati ya wale ambao mtume Paulo anafafanua katika barua yake kwa Waebrania: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho, ili msiwe goigoi, bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Waebrania 6:11, 12.

Hivyo basi, na tusichoke. Badala yake, uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova Mungu, imani yetu katika dhabihu ya fidia ya Yesu, na tumaini letu lenye furaha katika mfumo mpya wa mambo na liendelee kututia nguvu maishani. Kama vile watumwa ‘wema na waaminifu’ katika mfano wa Yesu, na tujionyeshe kuwa wenye kustahili pongezi na zawadi kwa kuwa wenye shughuli nyingi katika kumtukuza Mungu wetu, kama alivyofanya mtunga-zaburi ambaye alisema: “Mimi, nitangoja daima, nami nitaongezea sifa zako zote.”—Zaburi 71:14.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Akiwa amekata tamaa, Yona alingojea aone jambo ambalo lingepata jiji la Ninawi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Na tuonyeshe ujitoaji-kimungu huku tukingojea siku ya Yehova