Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wenye Upole Watairithi Nchi”—Jinsi Gani?

“Wenye Upole Watairithi Nchi”—Jinsi Gani?

“Wenye Upole Watairithi Nchi”—Jinsi Gani?

“LABDA unajua maneno ya Yesu yenye kuchangamsha kwamba ‘wapole watairithi nchi.’ Lakini ukifikiria yale ambayo watu wanatendeana na kuifanyia dunia, wewe unaona wapole watarithi nini?”—Mathayo 5:5; Zaburi 37:11, Union Version.

Myriam, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitumia swali hilo kuanzisha mazungumzo ya Biblia. Mwanamume aliyezungumza naye alisema kwamba ikiwa Yesu ndiye aliyetoa ahadi hiyo, basi dunia haiwezi kuwa magofu, bali kitu kinachofaa kurithiwa.

Hakika hilo lilikuwa jibu linalotoa matumaini mazuri. Lakini je, tuna sababu ya kuwa na matumaini kama hayo? Ndiyo, kwa kuwa Biblia hutupa sababu nzuri za kuamini kwamba ahadi hiyo itatimizwa. Kwa kweli, kutimizwa kwa ahadi hiyo kunahusiana sana na kusudi la Mungu kwa wanadamu na kuelekea dunia. Nasi tunahakikishiwa kwamba Mungu atatimiza makusudi yake. (Isaya 55:11) Hivyo basi, mwanzoni Mungu alikuwa na kusudi gani kwa wanadamu, nalo litatimizwaje?

Kusudi la Mungu la Milele Kuelekea Dunia

Yehova Mungu aliiumba dunia akiwa na kusudi hususa. “Yehova, Muumba wa mbingu, yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’” (Isaya 45:18) Kwa hiyo, dunia iliumbwa hasa ikaliwe na wanadamu. Isitoshe, Mungu anakusudia dunia iwe makao ya kudumu ya wanadamu. “Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”—Zaburi 104:5; 119:90.

Kusudi la Mungu kuhusu dunia pia linaonekana wazi katika agizo alilowapa wanadamu wawili wa kwanza. Yehova aliwaambia hivi Adamu na Hawa: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” (Mwanzo 1:28) Dunia ambayo Mungu aliwapa Adamu na Hawa, ingekuwa makao ya milele kwao na kwa uzao wao. Karne nyingi baadaye, mtunga-zaburi alisema: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”—Zaburi 115:16.

Ili tarajio hilo zuri litimizwe, Adamu na Hawa, na pia uzao wao, walipaswa kumkubali Yehova Mungu, aliye Muumba na Mpaji-Uhai, kuwa Mtawala wao Mwenye Enzi Kuu na wawe tayari kumtii. Yehova alitaja mambo waziwazi alipomwamuru mwanadamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Ili Adamu na Hawa waendelee kuishi katika bustani ya Edeni, walipaswa kutii amri hiyo rahisi iliyotolewa waziwazi. Kwa kufanya hivyo, wangeonyesha kwamba walikuwa wenye shukrani kwa mambo yote ambayo Baba yao wa mbinguni alikuwa amewafanyia.

Kwa kuvunja amri waliyokuwa wamepewa, Adamu na Hawa walikataa kumtii Mungu kimakusudi, na hivyo kumkataa yule ambaye aliwaandalia kila kitu walichokuwa nacho. (Mwanzo 3:6) Kwa kufanya hivyo, walipoteza makao yao maridadi ya Paradiso na pia wakawapotezea watoto wao makao hayo. (Waroma 5:12) Je, kutotii kwa wanadamu wa kwanza wawili kulizuia Mungu asitimize kusudi lake la kuumba dunia?

Mungu Ambaye Hakubadilika

Kupitia nabii wake Malaki, Mungu alitangaza: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Malaki 3:6) Kuhusu mstari huo, msomi wa Biblia Mfaransa L. Fillion alisema kwamba maneno hayo yanahusiana sana na kutimizwa kwa ahadi za Mungu. “Yehova angeweza kuwaangamiza watu wake waasi,” akaandika Fillion, “lakini kwa kuwa habadiliki kuhusiana na ahadi zake, hata iweje, yeye atatimiza ahadi zake za wakati uliopita.” Ahadi za Mungu, ziwe kwa mtu binafsi, taifa, au kwa wanadamu wote, hazitasahaulika bali zitatimizwa katika wakati wake unaofaa. “Amelikumbuka agano lake mpaka wakati usio na kipimo, neno ambalo aliamuru, mpaka vizazi elfu.”—Zaburi 105:8.

Lakini, tunawezaje kuwa na hakika kwamba Yehova hakubadili kusudi lake la awali kuhusiana na dunia? Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hilo kwa sababu kusudi la Mungu la kuwapa wanadamu watiifu dunia limetajwa katika Neno lote la Mungu, Biblia, ambalo liliongozwa na roho yake. (Zaburi 25:13; 37:9, 22, 29, 34) Isitoshe, Maandiko yanasema kwamba wale waliobarikiwa na Yehova wanaishi kwa usalama, kila mmoja akiwa ameketi “chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake,” bila ‘mtu yeyote wa kuwatetemesha.’ (Mika 4:4; Ezekieli 34:28) Wale waliochaguliwa na Yehova “hakika watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” Watakuwa na amani hata pamoja na wanyama wa kondeni.—Isaya 11:6-9; 65:21, 25.

Katika njia nyingine, Biblia inaonyesha kimbele kutimizwa kwa ahadi ya Mungu. Wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, taifa la Israeli lilikuwa na amani na ufanisi. Chini ya utawala wake, ‘Yuda na Israeli waliendelea kukaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.’ (1 Wafalme 4:25) Biblia inasema kwamba Yesu ni “mkuu kuliko Sulemani,” naye mtunga-zaburi alitoa unabii huu alipozungumzia utawala wa Yesu: “Katika siku zake aliye mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.” Wakati huo, “kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”—Luka 11:31; Zaburi 72:7, 16.

Kwa kuwa Yehova Mungu ni mwaminifu kwa neno lake, atahakikisha kwamba urithi huo ulioahidiwa utapatikana na pia utafanywa kuwa mzuri sawa na ulivyokuwa zamani. Katika Ufunuo 21:4, Neno la Mungu linatuambia kwamba katika ulimwengu mpya ulioahidiwa, Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [ya watu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” Kwa kweli, ahadi hiyo inamaanisha kwamba kutakuwa na Paradiso.—Luka 23:43.

Jinsi ya Kupata Urithi Ulioahidiwa

Dunia itabadilishwa kuwa paradiso chini ya serikali ambayo itatawala kutoka mbinguni. Yesu Kristo ndiye Mfalme wa Ufalme huo. (Mathayo 6:9, 10) Kwanza, Ufalme huo ‘utawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18; Danieli 2:44) Kisha, Yesu Kristo akiwa “Mkuu wa Amani,” atatimiza unabii huu: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Chini ya Ufalme huo, mamilioni ya wanadamu, kutia ndani wale watakaofufuliwa, wataweza kuirithi dunia.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Ni nani watakaopata urithi huo mzuri? Fikiria maneno haya ya Yesu: “Heri wenye upole; maana watairithi nchi.” (Mathayo 5:5, UV) Inamaanisha nini kuwa mpole? Kwa kawaida kamusi hulifafanua neno “pole” kuwa –enye utulivu; -enye kukosa machachari. Lakini neno la awali la Kigiriki lililotumiwa linamaanisha mengi zaidi. Kitabu New Testament Wordbook, cha William Barclay kinasema neno hilo linamaanisha “upole, lakini upole huo unaambatana na nguvu kama za chuma.” Linaonyesha mtazamo wa akili unaomwezesha mtu kuvumilia ubaya bila uchungu wala kufikiria kulipiza kisasi. Yote hayo hutokana na uhusiano mzuri na Mungu, uhusiano ambao humtia mtu huyo nguvu.—Isaya 12:2; Wafilipi 4:13.

Mtu mpole hukubali kwa unyenyekevu viwango vya Mungu katika sehemu zote za maisha yake; hasisitizi kutenda kulingana na maoni yake au maoni ya wengine. Pia anaweza kufundishika, na yu tayari kufundishwa na Yehova. Mtunga-zaburi Daudi aliandika: “[Yehova] atawafanya wapole watembee katika uamuzi wake wa hukumu, naye atawafundisha wapole njia yake.”—Zaburi 25:9; Methali 3:5, 6.

Je, utakuwa kati ya “wapole” watakaoirithi dunia? Kwa kujifunza kumhusu Yehova na mapenzi yake kupitia kujifunza Neno lake kwa bidii, na kufuata yale unayojifunza, wewe pia unaweza kutarajia kuirithi dunia paradiso na kuishi humo milele.—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kusudi la Mungu kuelekea dunia linaonekana wazi katika kazi aliyowapa Adamu na Hawa

[Picha katika ukurasa wa 6]

Amani na usalama wa utawala wa Sulemani ulionyesha kimbele ule urithi ulioahidiwa

[Hisani]

Sheep and background hill: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.; Arabian oryx: Hai-Bar, Yotvata, Israel; farmer plowing: Garo Nalbandian

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ulimwengu mpya wenye uadilifu unakaribia—je, wewe utakuwepo?