Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?

Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?

Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?

“Namjua mtu mmoja katika muungano na Kristo ambaye . . . alinyakuliwa kuingia katika paradiso.”—2 WAKORINTHO 12:2-4.

1. Ni ahadi gani za Biblia ambazo huwavutia watu wengi?

PARADISO. Je, unaweza kukumbuka jinsi ulivyohisi uliposikia mara ya kwanza kuhusu paradiso ya kidunia ambayo Mungu ameahidi? Huenda ukakumbuka wakati ulipojifunza kwamba ‘macho ya vipofu yatafunguliwa, masikio ya viziwi yatazibuliwa, nayo nyika itabubujika’ kwa uzuri mwingi. Au namna gani ule unabii kuhusu mbwa-mwitu pamoja na mwana-kondoo na mbuzi pamoja na chui? Yaelekea ulifurahi sana kusoma kuhusu kufufuliwa kwa wapendwa waliokufa wakiwa na tarajio la kuishi katika Paradiso.—Isaya 11:6; 35:5, 6; Yohana 5:28, 29.

2, 3. (a) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba una sababu ya kuwa na tumaini linalotegemea Biblia? (b) Tuna sababu gani nyingine ya kuwa na tumaini?

2 Una sababu ya kuamini ahadi za Biblia kuhusu Paradiso hiyo. Kwa mfano, una hakika katika maneno haya ambayo Yesu alimwambia mtenda-maovu aliyekuwa ametundikwa mtini: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Unatumaini ahadi hii: “Lakini kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” Pia unatumaini ahadi kwamba Mungu atafuta machozi yetu; kifo hakitakuwapo tena; nayo huzuni, kilio, na maumivu yatakoma. Hiyo inamaanisha kwamba paradiso ya kidunia itakuwapo tena!—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:4.

3 Sababu nyingine ya kuwa na tumaini hilo la Paradiso inahusiana na jambo fulani ambalo Wakristo ulimwenguni pote ni sehemu yake leo. Ni jambo gani hilo? Mungu ametokeza paradiso ya kiroho na kuwaingiza watu wake. Huenda usemi “paradiso ya kiroho” ukaonekana kuwa usio halisi na mgumu kueleweka, lakini paradiso hiyo ilitabiriwa, nayo ipo hakika.

Maono ya Paradiso

4. Andiko la 2 Wakorintho 12:2-4 linataja maono gani, na yaelekea ni nani aliyeyaona?

4 Kuhusu Paradiso hiyo, ona yale mtume Paulo aliyoandika: “Namjua mtu mmoja katika muungano na Kristo ambaye . . . alinyakuliwa akiwa hivyo mpaka kwenye mbingu ya tatu. Ndiyo, namjua mtu wa namna hiyo—kama ni katika mwili au bila mwili, mimi sijui, Mungu anajua—kwamba alinyakuliwa kuingia katika paradiso na kusikia maneno yasiyoweza kutamkwa ambayo si halali mtu kuyasema.” (2 Wakorintho 12:2-4) Fungu hilo la maneno linafuata mistari ambayo Paulo alitetea utume wake. Isitoshe, Biblia haitaji mtu mwingine yeyote aliyeona maono hayo, na Paulo ndiye anayetueleza kuyahusu. Basi yaelekea Paulo ndiye aliyeona maono hayo. Paulo aliingia katika “paradiso” gani Yehova alipomwonyesha maono hayo?—2 Wakorintho 11:5, 23-31.

5. Ni nini ambacho Paulo hakuona, na je, “paradiso” hiyo ilikuwa halisi au ya kiroho?

5 Muktadha haudokezi kwamba “mbingu ya tatu” inarejelea angahewa inayozunguka dunia yetu, au anga la juu. Mara nyingi Biblia hutumia namba tatu kuonyesha mkazo au nguvu. (Mhubiri 4:12; Isaya 6:3; Mathayo 26:34, 75; Ufunuo 4:8) Hivyo, paradiso ambayo Paulo aliona katika maono ilikuwa imekwezwa au kutukuzwa.

6. Ni tukio gani la kihistoria linalotoa ufahamu kuhusu paradiso ambayo Paulo aliona?

6 Unabii wa Biblia wa mapema unatupa ufahamu. Baada ya watu wake wa kale kukosa uaminifu, Mungu aliamua kuwaacha Wababiloni wavamie Yuda na Yerusalemu. Kulingana na kronolojia ya Biblia, uvamizi huo uliongoza kwenye uharibifu wa mwaka wa 607 K.W.K. Unabii ulisema kwamba nchi ingekuwa ukiwa kwa miaka 70; kisha Mungu angewaruhusu Wayahudi waliotubu warudi na kurudisha ibada safi. Jambo hilo lilitukia kuanzia mwaka wa 537 K.W.K. na kuendelea. (Kumbukumbu la Torati 28:15, 62-68; 2 Wafalme 21:10-15; 24:12-16; 25:1-4; Yeremia 29:10-14) Namna gani nchi yenyewe? Katika miaka hiyo 70, nchi ilijaa mimea ya msituni, ikawa na maeneo makavu, na makao ya mbwa-mwitu. (Yeremia 4:26; 10:22) Hata hivyo, kulikuwa na ahadi hii: “Yehova hakika atamfariji Sayuni. Hakika atafariji mahali pake pote palipoharibiwa, naye ataifanya nyika yake kuwa kama Edeni na nchi yake tambarare ya jangwani kama bustani [au Paradiso, Septuagint] ya Yehova.”—Isaya 51:3.

7. Ni nini ambacho kingetukia baada ya ile miaka 70 ya ukiwa?

7 Hilo lilitukia baada ya ile miaka 70. Hali ziliboreka kwa sababu ya baraka za Mungu. Wazia jambo hili: “Nyika na nchi isiyo na maji itafurahi; na nchi tambarare ya jangwani itakuwa na shangwe na kuchanua maua kama zafarani. Itachanua maua bila shaka, nayo itashangilia kwa shangwe na kwa kilio cha furaha. . . . Kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha. Kwa maana maji yatakuwa yamebubujika katika nyika, na mito katika nchi tambarare ya jangwani. Na nchi iliyokaushwa na joto itakuwa kama dimbwi lenye matete, na nchi yenye kiu kama mabubujiko ya maji. Katika makao ya mbwa-mwitu, mahali pao pa kupumzika, patakuwa na majani mabichi na matete na mimea ya mafunjo.”—Isaya 35:1-7.

Watu Waliorudishwa na Kubadilika

8. Tunajuaje kwamba Isaya sura ya 35 iliwahusu watu?

8 Hilo lilikuwa badiliko lililoje! Nchi yabadilika kutoka hali ya ukiwa na kuwa paradiso. Hata hivyo, unabii huo na pia unabii mwingine wenye kutegemeka ulionyesha kwamba watu wangebadilika, kama vile nchi iliyo ukiwa inavyoweza kubadilika na kuwa yenye kuzaa. Kwa nini tuseme hivyo? Isaya alikuwa anakazia fikira wale “hasa waliokombolewa na Yehova,” ambao wangerudi katika nchi yao “kwa vigelegele vya shangwe” na kupata “furaha na kushangilia.” (Isaya 35:10) Unabii huo ulihusu watu, bali si udongo halisi. Isitoshe, katika sehemu nyingine Isaya alitabiri hivi kuhusu watu waliorudishwa Sayuni: ‘Nao wataitwa miti mikubwa ya uadilifu, bustani ya Yehova. Kwa maana kama vile dunia inavyotoa chipukizi lake, ndivyo Yehova atakavyotoa chipukizi la uadilifu na la sifa mbele ya mataifa yote.’ Isaya pia alisema hivi kuhusu watu wa Mungu: “Yehova hatakosa kukuongoza sikuzote . . . , naye ataitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyonyweshwa maji vizuri.” (Isaya 58:11; 61:3, 11; Yeremia 31:10-12) Kwa hiyo, kama vile ambavyo hali za mazingira ya nchi halisi zingeboreka, ndivyo ambavyo Wayahudi waliorudishwa wangebadilika.

9. Paulo aliona “paradiso” gani, na maono hayo yalitimizwa lini?

9 Kielelezo hicho cha kihistoria kinatusaidia kuelewa maono ambayo Paulo aliona. Yangetia ndani kutaniko la Kikristo, ambalo aliliita “shamba la Mungu linalolimwa” ambalo lilipaswa kuwa na mazao. (1 Wakorintho 3:9) Maono hayo yangetimizwa lini? Paulo aliyaita maono hayo “ufunuo,” ambao ungetokea wakati ujao. Alijua kwamba baada ya yeye kufa kungetokea uasi-imani mkubwa. (2 Wakorintho 12:1; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3, 7) Wakristo wa kweli hawangeweza kulinganishwa na bustani yenye kusitawi kwa kuwa waasi-imani wangeongezeka na kuonekana kama wanawafunika. Hata hivyo, wakati ungefika ambapo ibada ya kweli ingekwezwa tena. Watu wa Mungu wangerudishwa ili ‘waadilifu waweze kung’aa kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.’ (Mathayo 13:24-30, 36-43) Kwa kweli, jambo hilo lilitimia miaka michache baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mbinguni. Na tangu Ufalme huo usimamishwe, imekuwa wazi kabisa kwamba watu wa Mungu wanafurahia paradiso ya kiroho, ambayo Paulo alitangulia kuona.

10, 11. Ingawa sisi si wakamilifu, kwa nini tunaweza kusema kwamba tuko katika paradiso ya kiroho?

10 Tunatambua kwamba sisi si wakamilifu, kwa hiyo hatushangai kwamba mara kwa mara matatizo hutokea, kama yalivyotokea kati ya Wakristo wa siku za Paulo. (1 Wakorintho 1:10-13; Wafilipi 4:2, 3; 2 Wathesalonike 3:6-14) Hata hivyo, fikiria paradiso ya kiroho tunayofurahia sasa. Tunapoilinganisha na hali mbaya tulimokuwa zamani, tumeponywa kiroho. Linganisha njaa tuliyokuwa nayo zamani na chakula cha kiroho tunachofurahia sasa. Badala ya kupambana kana kwamba wako katika nchi kame ya kiroho, watu wa Mungu wana kibali chake na baraka zisizo na kifani. (Isaya 35:1, 7) Badala ya kupofushwa na giza zito la kiroho, tunaona nuru ya uhuru na ya kibali cha Mungu. Wengi ambao hawakuwa wamewahi kusikia unabii wa Biblia wamepata kusikia na kuelewa vile Maandiko yanavyosema. (Isaya 35:5) Kwa mfano, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamejifunza unabii wa Danieli, mstari kwa mstari. Kisha wakachunguza kwa makini kila sura ya kitabu cha Biblia cha Isaya. Chakula hicho cha kiroho chenye kuburudisha kinathibitisha kwamba tuko katika paradiso ya kiroho.

11 Fikiria pia jinsi ambavyo watu wanyoofu wa malezi mbalimbali wamebadili tabia zao kwa kujitahidi kuelewa na kufuata Neno la Mungu. Kwa kweli, wamejitahidi kuacha tabia za kinyama walizokuwa nazo hapo zamani. Labda umejitahidi kuacha tabia fulani mbaya na umepata matokeo mazuri, na pia ndugu na dada zako wa kiroho wamefanya hivyo. (Wakolosai 3:8-14) Kwa hiyo, unaposhirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova, unakuwa pamoja na watu ambao wamekuwa wenye kufanya amani na wenye kupendeza zaidi. Wao si wakamilifu, lakini hawawezi kutajwa kuwa simba wakali au wanyama-mwitu wenye kunyafua. (Isaya 35:9) Ushirika huo wa kiroho na wenye utulivu unaonyesha nini? Unaonyesha wazi kwamba tunafurahia hali ya kiroho ambayo kwa kufaa tunaiita paradiso ya kiroho. Nayo paradiso yetu ya kiroho inaonyesha kimbele paradiso ya kidunia ambayo tutafurahia tukiendelea kuwa waaminifu kwa Mungu.

12, 13. Tunapaswa kufanya nini ili tubaki katika paradiso yetu ya kiroho?

12 Hata hivyo, kuna jambo fulani tusilopaswa kupuuza. Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Mtashika amri yote ninayowaamuru leo, ili muwe na nguvu na mpate kuingia na kuimiliki nchi ambayo mnavuka ili kuimiliki.” (Kumbukumbu la Torati 11:8) Nchi hiyohiyo inatajwa katika Mambo ya Walawi 20:22, 24: “Nanyi mtazishika sheria zangu zote na maamuzi yangu yote ya hukumu na kuzifanya, ili nchi nitakayowaingiza mkae ndani yake isije ikawatapika ninyi. Ndipo nikawaambia ninyi: ‘Ninyi mtaimiliki nchi yao, nami nitawapa ninyi ili mwimiliki, nchi inayotiririka maziwa na asali.’” Naam, kumiliki Nchi ya Ahadi kulitegemea kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu. Mungu aliwaruhusu Wababiloni wawashinde Waisraeli na kuwatoa katika makao yao kwa sababu walikosa kumtii.

13 Huenda kuna mambo mengi yanayotupendeza kuhusu paradiso yetu ya kiroho. Hali yenyewe inapendeza na ni yenye kutuliza. Tuna amani na Wakristo ambao wamejitahidi kubadili tabia za kinyama. Wanajitahidi kuwa wenye fadhili na wenye kusaidia. Hata hivyo, ili tubaki katika paradiso yetu ya kiroho tunahitaji mengi zaidi kuliko tu kuwa na uhusiano mzuri na watu hao. Tunahitaji kuwa na uhusiano mzuri na Yehova na kufanya mapenzi yake. (Mika 6:8) Hatukulazimishwa kuingia katika paradiso hiyo ya kiroho, lakini tunaweza kupeperuka na kutoka nje—au kuondolewa—tusipojitahidi kudumisha uhusiano wetu na Mungu.

14. Ni nini kitakachotusaidia tubaki katika paradiso ya kiroho?

14 Jambo muhimu litakalotusaidia ni kuendelea kuimarishwa na Neno la Mungu. Ona lugha ya mfano inayotumiwa kwenye Zaburi 1:1-3: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, . . . Bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. Naye hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” Isitoshe, vichapo vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambavyo vinategemea Biblia huandaa chakula cha kiroho katika paradiso hiyo ya kiroho.—Mathayo 24:45-47.

Kuimarisha Maoni Yako Kuhusu Paradiso

15. Kwa nini Musa hangeweza kuwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, lakini aliona nini?

15 Fikiria jambo lingine linaloonyesha kimbele jinsi Paradiso itakavyokuwa. Baada ya Waisraeli kutanga-tanga nyikani kwa muda wa miaka 40, Musa aliwaongoza hadi nchi tambarare za Moabu, mashariki ya Mto Yordani. Kwa sababu ya kosa ambalo Musa alikuwa amefanya hapo awali, Yehova aliamua kwamba Musa hatawaongoza Waisraeli kuvuka Yordani. (Hesabu 20:7-12; 27:12, 13) Musa alimsihi Mungu hivi: “Acha nivuke, tafadhali, niione hiyo nchi nzuri iliyo ng’ambo ya Yordani.” Hata ingawa hangeingia katika nchi hiyo, bila shaka Musa alitambua kwamba hiyo ilikuwa “nchi nzuri” baada ya kupanda Mlima Pisga na kuona maeneo yake mbalimbali. Unafikiri nchi hiyo ilikuwaje?—Kumbukumbu la Torati 3:25-27.

16, 17. (a) Nyakati za hivi karibuni, nchi hiyo inatofautianaje na Nchi ya Ahadi ya nyakati za kale? (b) Kwa nini tunaweza kuamini kwamba wakati fulani Nchi ya Ahadi ilikuwa kama paradiso?

16 Ikiwa maoni yako kuhusu nchi hiyo yanategemea jinsi ambavyo eneo hilo limekuwa hivi karibuni, huenda ukadhani kwamba hilo lilikuwa eneo kame na lenye mchanga, lenye majangwa ya mawe-mawe, na joto kali. Hata hivyo, kuna sababu ya kuamini kwamba eneo hilo lote lilikuwa tofauti kabisa nyakati za Biblia. Katika jarida Scientific American, mtaalamu wa kilimo, Dakt. Walter C. Lowdermilk alisema kwamba nchi hiyo “imeharibika kwa sababu ya kutumiwa vibaya kwa miaka mingi.” Mtaalamu huyo aliandika: “Nchi hiyo yenye kupendeza sasa imekuwa ‘jangwa’ kwa sababu ya wanadamu wala si kwa sababu ya hali za kiasili.” Hata uchunguzi wake ulionyesha kwamba “pindi fulani nchi hiyo ilikuwa paradiso ya malisho.” Hivyo ni wazi kwamba wanadamu wametumia vibaya na kuharibu nchi ambayo ilikuwa “paradiso ya malisho.” *

17 Kwa kufikiria mambo ambayo umesoma katika Biblia huenda ukaona ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba nchi hiyo ilikuwa kama paradiso. Kumbuka mambo ambayo Yehova aliwahakikishia Waisraeli kupitia Musa: “Nchi mnayovuka ili kuimiliki ni nchi yenye milima na nchi tambarare za mabonde. Inakunywa maji ya mvua ya mbinguni; nchi ambayo Yehova Mungu wako anaitunza.”—Kumbukumbu la Torati 11:8-12.

18. Ni lazima andiko la Isaya 35:2 liwe liliwapa Waisraeli waliokuwa uhamishoni wazo gani kuhusu jinsi Nchi ya Ahadi ingekuwa?

18 Nchi ya Ahadi ilikuwa yenye rutuba na yenye kuzaa sana hivi kwamba, kutaja tu maeneo fulani kulimkumbusha mtu hali za kiparadiso. Jambo hilo linaonekana wazi katika unabii wa Isaya sura ya 35, ambao ulitimizwa mara ya kwanza wakati Waisraeli waliporudi kutoka Babiloni. Isaya alitabiri hivi: “Itachanua maua bila shaka, nayo itashangilia kwa shangwe na kwa kilio cha furaha. Itapewa utukufu wa Lebanoni, fahari ya Karmeli na ya Sharoni. Kutakuwa na wale watakaouona utukufu wa Yehova, fahari ya Mungu wetu.” (Isaya 35:2) Bila shaka, kutajwa kwa maeneo ya Lebanoni, Karmeli, na Sharoni kulitokeza picha nzuri na yenye kuridhisha katika akili za Waisraeli.

19, 20. (a) Fafanua eneo la Sharoni la kale. (b) Ni katika njia gani tunaweza kuimarisha tumaini letu katika Paradiso?

19 Fikiria Sharoni, nchi tambarare iliyo kwenye ukingo wa bahari kati ya milima ya Samaria na Bahari Kuu, au Mediterania. (Ona picha kwenye ukurasa wa 10.) Nchi hiyo ilikuwa maarufu kwa kuwa ilikuwa nzuri na yenye kuzaa. Ilikuwa yenye maji mengi, na hivyo ilifaa kwa malisho ingawa ilikuwa na misitu ya mialoni pande za kaskazini. (1 Mambo ya Nyakati 27:29; Wimbo wa Sulemani 2:1; Isaya 65:10) Hivyo, andiko la Isaya 35:2 lilitabiri kuhusu kurudishwa na kuhusu nchi inayochanuka kwa fahari, na kuwa kama paradiso. Kupatana na maono ambayo Paulo aliona baadaye, unabii huo pia ulikuwa ukielekeza kwenye paradiso nzuri ya kiroho. Mwishowe, unabii huo pamoja na unabii mwingine mwingi huimarisha tumaini letu katika paradiso ya kidunia kwa ajili ya wanadamu.

20 Tunapoishi katika paradiso yetu ya kiroho, tunaweza kuimarisha uthamini wetu kwa paradiso hiyo na kwa tumaini letu kwamba dunia itakuwa Paradiso. Jinsi gani? Kwa kuongeza uelewaji wetu wa mambo tunayosoma katika Biblia. Mara nyingi maelezo na unabii mbalimbali wa Biblia hutaja maeneo hususa. Je, ungependa kuelewa vizuri maeneo hayo yalikuwa wapi, nayo yalihusianaje na maeneo mengine? Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi unavyoweza kunufaika kwa kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Katika kitabu The Geography of the Bible, Denis Baly anasema: “Lazima aina ya mimea iliyokuwako nyakati za Biblia iwe ilibadilika sana.” Kwa sababu gani? ‘Kwa kuwa wanadamu walihitaji miti kwa ajili ya kuni na ujenzi, walianza kukata miti na hivyo kufanya nchi iathiriwe na uharibifu unaotokana na hali ya hewa. Pole kwa pole, ukataji huo wa miti ulifanya hali ya hewa iwe kisababishi kikuu cha uharibifu huo.’

Je, Unakumbuka?

• Mtume Paulo aliona “paradiso” gani katika maono?

Isaya sura ya 35, ilitimizwa lini mara ya kwanza, nayo inahusianaje na maono ambayo Paulo aliona?

• Tunawezaje kuimarisha uthamini wetu wa paradiso yetu ya kiroho, na tumaini letu katika paradiso ya kidunia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nchi Tambarare ya Sharoni, eneo lenye kuzaa la Nchi ya Ahadi

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Musa alitambua kwamba ilikuwa “nchi nzuri”