Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu alipowaagiza wafuasi wake ‘wakopeshe bila faida, bila kutumainia kurudishiwa chochote,’ je, alimaanisha kwamba hawakupaswa kuomba warudishiwe hata mkopo wenyewe?

Maneno ya Yesu yanayopatikana katika Luka 6:35 yanaeleweka vizuri kwa kufikiria Sheria ya Musa. Katika Sheria hiyo, Mungu aliwaamuru Waisraeli wasitoze faida kwa mikopo ambayo wangewapa Waisraeli wenzao waliojikuta katika ufukara na kuhitaji msaada. (Kutoka 22:25; Mambo ya Walawi 25:35-37; Mathayo 5:42) Mikopo hiyo haikuwa ya kujipatia faida. Badala yake, ilikusudiwa kupunguza umaskini. Kwani lingekuwa jambo lisilo la upendo hata kidogo kujipatia faida kutokana na hali ngumu ya kiuchumi ya jirani. Hata hivyo, mkopeshaji alikuwa na haki ya kudai mkopo aliotoa, na nyakati nyingine alikopesha kwa rehani.—Kumbukumbu la Torati 15:7, 8.

Huku akiunga mkono Sheria hiyo, Yesu alifafanua zaidi matumizi yake, akisema kwamba yule anayetoa msaada hapaswi kutumainia “kurudishiwa chochote.” Kama Waisraeli, nyakati nyingine Wakristo hupatwa na hali ngumu za kiuchumi au hali nyingine zinazoweza kuwafanya wawe maskini au hata fukara. Ikiwa ndugu Mkristo anayekabili hali kama hiyo yenye kukatisha tamaa anaomba msaada wa kifedha, je, halingekuwa jambo la fadhili kumsaidia? Naam, upendo wa kweli utamchochea Mkristo atake kumsaidia ndugu yake ambaye anajikuta katika hali ngumu sana ya kiuchumi kwa sababu ya hali zinazozidi uwezo wake. (Methali 3:27) Huenda ikawezekana kutoa msaada wa kifedha kwa ndugu mwenye uhitaji, hata ingawa huenda pesa hizo zikawa kidogo kuliko mkopo ambao angepewa.—Zaburi 37:21.

Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo na Barnaba walipewa mgawo wa kupeleka michango ya Wakristo wa Asia Ndogo hadi kwa ndugu zao huko Yudea kwa sababu kulikuwa na njaa. (Matendo 11:28-30) Vivyo hivyo leo, msiba unapotokea, mara nyingi Wakristo hutuma misaada kwa ndugu zao wenye uhitaji. Kwa kufanya hivyo, pia wanatoa ushahidi mzuri kwa wengine. (Mathayo 5:16) Bila shaka, mtazamo na hali ya yule anayeomba msaada inapaswa kufikiriwa. Kwa nini anahitaji msaada? Maneno haya ya Paulo yanafaa: “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, basi na asile chakula.”—2 Wathesalonike 3:10.

Ikiwa ndugu anayeomba mkopo hana uhitaji mkubwa sana lakini anataka tu msaada kwa muda mfupi ili arudie hali yake nzuri ya kiuchumi, huenda ikafaa apewa mkopo usio na faida. Chini ya hali kama hizo, kumkopesha ukiwa na nia ya kumtaka aurudishe mkopo huo, hakupingani na maneno ya Yesu yanayopatikana katika Luka 6:35. Mkataba unapaswa kuandikwa, na mwenye kukopeshwa anapaswa kufanya kila jitihada ya kulipa mkopo huo kupatana na makubaliano yaliyofanywa. Kwa kweli, upendo wa Kikristo unapaswa kumchochea aliyekopeshwa kuulipa mkopo kama vile tu mkopeshaji alivyochochewa na upendo kutoa mkopo.

Mtu anayefikiria kutoa mkopo (au kutoa msaada) anahitaji pia kufikiria hali ya familia yake. Kwa mfano, iwapo atatoa mkopo au msaada, je, ataweza kutekeleza wajibu wake muhimu wa Kimaandiko wa kutimizia familia yake mahitaji? (2 Wakorintho 8:12; 1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, Wakristo hutafuta nafasi za kuonyeshana upendo, wakionyesha upendo huo kwa matendo yanayopatana na kanuni za Biblia.—Yakobo 1:27; 1 Yohana 3:18; 4:7-11.