Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani “Mungu wa Kweli na Uzima wa Milele”?

Ni Nani “Mungu wa Kweli na Uzima wa Milele”?

Ni Nani “Mungu wa Kweli na Uzima wa Milele”?

YEHOVA, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, ndiye Mungu wa kweli. Yeye ndiye Muumba, anayetoa uzima wa milele kwa wale wanaompenda. Hivyo ndivyo wengi wanaosoma na kuiamini Biblia wangejibu swali lililoulizwa katika kichwa. Kwa kweli, Yesu mwenyewe alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Hata hivyo, wengi wanaoenda kanisani huyaamini maneno hayo katika njia tofauti. Maneno yaliyo katika kichwa yametolewa katika 1 Yohana 5:20, inayosema hivi kwa sehemu: “Sisi tumo katika muungano na yule wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyo ndiye Mungu wa kweli na uzima wa milele.”

Watu wanaoamini fundisho la Utatu hudai kwamba, kiwakilishi-nomino kionyeshi “huyo” (houʹtos) kinarejelea mtu anayetajwa mwisho, yaani Yesu Kristo. Wao husisitiza kwamba Yesu ndiye “Mungu wa kweli na uzima wa milele.” Hata hivyo, ufafanuzi huo unapingana na Maandiko mengine yote. Nao wasomi wengi wenye kuaminika hawakubali maoni hayo ya Utatu. Msomi wa Chuo Kikuu cha Cambridge, B. F. Westcott aliandika: “Ni jambo linalopatana na akili kwamba [kiwakilishi-nomino hicho houʹtos] hakirejelei mtu anayetajwa mwisho bali mtu anayezungumziwa na mtume huyo.” Hivyo, mtume Yohana alikuwa akifikiria Baba ya Yesu. Mwanatheolojia Mjerumani Erich Haupt aliandika: ‘Inapaswa kuthibitishwa kama kile kiwakilishi-nomino [houʹtos] ambacho kimetumiwa katika sentensi inayofuata kinarejelea yule mtu aliyetajwa mwisho au kinarejelea yule mtu aliyetangulia kutajwa, yaani Mungu. Kuelewa andiko hilo kuwa ushuhuda wa kwamba kuna Mungu mmoja wa kweli kunaonekana kupatana zaidi na lile onyo [linalopatikana katika mstari unaofuata] dhidi ya sanamu, lakini si kuonyesha kwamba Kristo ni Mungu.’

Hata kitabu A Grammatical Analysis of the Greek New Testament, kilichochapwa na Taasisi ya Papa ya Biblia ya Roma, kinasema: ‘Hapana shaka kwamba kiwakilishi nomino [houʹtos]: kikiwa kiwakilishi muhimu katika mistari ya kumalizia ya 18-20, kinarejelea Mungu halisi na wa kweli, ambaye ni tofauti na miungu ya kipagani (mst. 21).’

Mara nyingi houʹtos, inayotafsiriwa kuwa “huyu” au “huyo,” hairejelei mtu aliyetoka tu kutajwa katika sentensi inayotangulia. Maandiko mengine yanaonyesha jambo hili. Katika 2 Yohana 7, mtume yuleyule aliyeandika barua ya kwanza ya Yohana aliandika hivi: “Wadanganyifu wengi wametokea katika ulimwengu, watu ambao hawamkiri Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili. Hao [houʹtosʹ] ndio yule mdanganyifu na mpinga-Kristo.” Hapa kiwakilishi-nomino hakiwezi kuwa kinarejelea yule anayetajwa mwisho, yaani, Yesu. Kwa wazi, “hao” inarejelea wale waliomkataa Yesu. Wao kwa ujumla ndio “yule mdanganyifu na mpinga-Kristo.”

Katika Gospeli yake, mtume Yohana aliandika: “Andrea ndugu ya Simoni Petro alikuwa mmoja kati ya wale wawili waliosikia aliyoyasema Yohana nao wakamfuata Yesu. Kwanza huyu [houʹtos] alimpata ndugu yake mwenyewe, Simoni.” (Yohana 1:40, 41) Ni wazi kwamba “huyu” inamwakilisha Andrea, wala si mtu anayetajwa mwisho. Katika 1 Yohana 2:22, mtume Yohana anatumia neno houʹtos katika njia ileile.

Luka anatumia houʹtos pia katika njia inayolingana na hiyo, kama inavyoonekana katika Matendo 4:10, 11: “Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, ambaye mlimtundika mtini lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, kupitia kwake, mtu huyu anasimama hapa akiwa na afya mbele yenu. Hilo [houʹtosʹ] ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba si la maana ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’” Kwa wazi, kiwakilishi-nomino “hilo” hakirejelei yule mtu aliyeponywa, ingawa yeye ndiye anayetajwa kabla tu ya houʹtos. Bila shaka, “hilo” katika mstari wa 11 inarejelea Yesu Kristo Mnazareti, ambaye ndiye “jiwe la pembeni” ambalo juu yalo kutaniko la Kikristo lilianzishwa. —Waefeso 2:20; 1 Petro 2:4-8.

Andiko la Matendo 7:18, 19 pia linaeleza wazo hilo: “Akainuka mfalme tofauti juu ya Misri, ambaye hakujua habari za Yosefu. Huyo [houʹtos] akatumia hila ya serikali juu ya jamii yetu.” “Huyo” aliyewakandamiza Wayahudi, hakuwa Yosefu, bali alikuwa Farao, mfalme wa Misri.

Mistari hiyo inathibitisha maoni ya msomi Mgiriki, Daniel Wallace, anayesema kwamba unapotumia viwalikilishi-nomino vya Kigiriki, “kulingana na muktadha, yule anayetajwa mwisho huenda asiwe yule ambaye mwandishi alikuwa anamfikiria.”

“Yule wa Kweli”

Kama mtume Yohana alivyoandika, “yule wa kweli” ni Yehova, Baba ya Yesu Kristo. Yeye ndiye Mungu pekee wa kweli, Muumba. Mtume Paulo aliandika: “Kwetu sisi kuna Mungu mmoja aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake.” (1 Wakorintho 8:6; Isaya 42:8) Sababu nyingine kwa nini Yehova ndiye “yule wa kweli” anayetajwa katika 1 Yohana 5:20 ni kwamba, yeye ndiye Chanzo cha kweli. Mtunga zaburi alimwita Yehova kuwa “Mungu wa ukweli” kwa sababu Yeye ni mwaminifu na katika yote anayofanya Hawezi kusema uwongo. (Zaburi 31:5; Kutoka 34:6; Tito 1:2) Akimrejelea Baba yake wa kimbingu, Mwana alisema: “Neno lako ni kweli.” Na kuhusu mafundisho yake mwenyewe, Yesu alisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.”—Yohana 7:16; 17:17.

Yehova pia ndiye “uzima wa milele.” Yeye ndiye Chemichemi ya uzima, Yule anayeutoa kama zawadi isiyostahiliwa kupitia Kristo. (Zaburi 36:9; Waroma 6:23) Kwa kufaa, mtume Paulo alisema kwamba Mungu “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Mungu alimthawabisha Mwana wake kwa kumfufua kutoka kwa wafu, naye Baba atawapatia thawabu ya uzima wa milele wale wanaomtumikia kwa moyo wao wote.—Matendo 26:23; 2 Wakorintho 1:9.

Basi tufikie mkataa gani? Kwamba Yehova wala si mtu mwingine yeyote, ndiye “Mungu wa kweli na uzima wa milele.” Yeye peke yake ndiye anastahili kupokea ibada kamili kutoka kwa wale aliowaumba.—Ufunuo 4:11.