Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nufaika kwa Kufuatia Kanuni za Kiroho

Nufaika kwa Kufuatia Kanuni za Kiroho

Nufaika kwa Kufuatia Kanuni za Kiroho

“Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.

KUFANYA kazi mno kunaweza kutokeza mkazo, nao mkazo unaweza kusababisha matatizo ya afya ambayo yanaweza kutokeza kifo. Katika nchi nyingi, familia zinatenganishwa na talaka. Mara nyingi, misiba hiyo husababishwa na kuhangaikia mno vitu vya kimwili. Badala ya kufurahia vitu alivyo navyo, mtu anayejishughulisha sana kupata mali, anaweza kujikuta akitaka kuzidisha mali zake, bila kujali madhara yanayoweza kumpata. Kitabu fulani cha kujisaidia mwenyewe kinasema: “Katika nchi fulani, mtazamo wa kushindana na majirani ni jambo la kawaida hata kama majirani hao wanahatarisha afya yao kwa kufanya kazi kupita kiasi.”

Kutamani kuwa na vitu vingi zaidi kunaweza kumfanya mtu asitosheke, na akose furaha. Mara nyingi udhaifu wetu kuhusiana na jambo hilo hutumiwa vibaya na watangazaji wa bidhaa wenye uvutano mkubwa sana! Matangazo ya redio na televisheni yanakutia moyo sikuzote ununue vitu ambavyo labda huhitaji au ambavyo huna pesa za kuvinunua. Yote hayo yanaweza kukuletea madhara makubwa.

Kujiingiza kabisa katika anasa kunaweza kutudhuru kimwili na kiadili. Kwa mfano, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Methali 14:30) Kinyume na hilo, kujikaza kupita kiasi, mahangaiko, na mikazo inayotokana na kukusanya mali za kimwili inaweza kuharibu afya na furaha yetu. Pia mahusiano huathiriwa miradi ya kimwili inapodhibiti maisha yetu. Wakati familia ya mtu na maisha ya kijamii yanapoharibika, kwa ujumla ubora wa maisha yake huathiriwa vibaya.

Ubora wa Kanuni za Kiroho

“Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo,” akaonya mtume Paulo karne nyingi zilizopita. (Waroma 12:2) Ulimwengu unawapenda wale wanaojiambatanisha na viwango vyake. (Yohana 15:19) Nao unajaribu kuvutia hisi yako ya kuona, kugusa, kuonja, kunusa, na kusikia. Naam, ulimwengu hujaribu kukusadikisha ufuatie vitu vya kimwili. Mkazo unawekwa juu ya “tamaa ya macho” ili kwamba wewe na wengine mfuatie vitu vya kimwili.—1 Yohana 2:15-17.

Lakini kuna mambo yaliyo muhimu kuliko pesa, umashuhuri, na utajiri wa kimwili. Karne nyingi mapema, Mfalme Sulemani alijikusanyia vitu vingi sana vya kimwili. Alijenga nyumba, naye akawa na mabustani, mashamba ya matunda, watumishi, mifugo, waimbaji wa kiume na wa kike, pamoja na dhahabu na fedha nyingi. Sulemani aliongeza mali zake kuliko wote waliomtangulia. Alikuwa tajiri sana. Sulemani alikuwa na karibu kila kitu ambacho kingeweza kutamanika. Lakini, alipoangalia yale aliyotimiza, alisema: “Kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:1-11.

Akiwa na hekima ya kipekee ambayo Yehova alimpa, Sulemani alitambua kwamba uradhi mkuu zaidi hutokana na kufuatia kanuni za kiroho. Aliandika: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.

Yale yaliyoandikwa katika Neno la Mungu, Biblia, ni hazina yenye thamani zaidi kuliko dhahabu au fedha. (Methali 16:16) Kweli muhimu ni kama mawe ya thamani na zimewekwa katika Biblia ili uweze kuzipata. Je, utachimba na kuzitafuta? (Methali 2:1-6) Muumba wetu, aliye Chanzo cha kanuni za kweli, anakuhimiza ufanye hivyo, naye atakusaidia. Jinsi gani?

Yehova anaandaa kweli zenye thamani kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake. (Zaburi 1:1-3; Isaya 48:17, 18; Mathayo 24:45-47; 1 Wakorintho 2:10) Kuchunguza kweli hizo zenye thamani kubwa, kunakutolea nafasi ya kuchagua kwa akili njia bora zaidi inayothawabisha maishani. Na si vigumu kufanya uchaguzi huo kwa kuwa Yehova, Muumba wetu, anajua kile tunachohitaji ili kuwa wenye furaha kwelikweli.

Biblia Hututia Moyo Tufuatie Kanuni Bora Zaidi

Mashauri bora yanayopatikana katika Biblia, ni yenye kutumika na hayana kifani. Kanuni za maadili ambazo Biblia inaunga mkono ni za hali ya juu. Mashauri inayotoa huwa yenye manufaa sikuzote. Yamethibitika kuwa ya kweli nayo yametumika kwa muda mrefu. Biblia hutoa mashauri mazuri kuhusu kufanya kazi kwa bidii, kuwa mnyoofu, kutumia pesa kwa hekima, na kuepuka uvivu.—Methali 6:6-8; 20:23; 31:16.

Kupatana na hayo, Yesu alisema: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba.”—Mathayo 6:19, 20.

Onyo hilo linalofaa, linatumika leo kama lilivyotumika miaka 2,000 iliyopita. Badala ya kufuatia sana mali za kimwili, tunaweza kufaidika sasa kwa kufuatia njia bora zaidi ya maisha. Siri ni kujiwekea hazina za kiroho mbinguni, ambazo hufanya watu waishi maisha yenye furaha na uradhi wa kweli. Tunawezaje kufanya hivyo? Kwa kusoma Neno la Mungu, Biblia, na kutumia yale inayofundisha.

Kanuni za Kiroho Huthawabisha

Zinapotumiwa vizuri, kanuni za kiroho hutufaidi kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. Kama vile tabaka la ozoni lililo juu ya dunia linavyotulinda dhidi ya miale hatari ya jua, ndivyo na kanuni nzuri za kiadili zinavyotusaidia kwa kutuonya dhidi ya matokeo hatari ya kufuatia vitu vya kimwili. Mtume Mkristo Paulo aliandika: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

Kupenda mali hushawishi watu watafute mali zaidi, cheo, na mamlaka. Mara nyingi, njia zenye udanganyifu na kukosa unyoofu hutumiwa ili kufikia miradi hiyo. Tukifuatia vitu vya kimwili tutapoteza wakati, nguvu, na pia uwezo mbalimbali. Tunaweza hata kupoteza usingizi mtamu usiku. (Mhubiri 5:12) Kwa kweli, kufuatia vitu vya kimwili huzuia maendeleo ya kiroho. Mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, Yesu Kristo, alionyesha waziwazi njia bora zaidi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Alijua kwamba utajiri wa kiroho huleta thawabu zenye kudumu na muhimu zaidi kuliko vitu vya kimwili ambavyo ni vya muda.—Luka 12:13-31.

Je, Kufuatia Mambo ya Kiroho Kunafaidi Kwelikweli?

“Wazazi wangu walijaribu kwa bidii kunisadikisha kwamba kanuni za kiroho hazina manufaa,” anakumbuka Greg. “Lakini, nimefaidika sana na amani ya akili kwa kufuatia miradi ya kiroho kwa sababu sina mikazo inayotokana na mashindano ya kupata mali.”

Kanuni za kiroho pia hufanya tuwe na uhusiano bora na wengine. Marafiki wa kweli huvutiwa nawe kwa sababu ya jinsi ulivyo, si kwa sababu ya vitu ulivyo navyo. Biblia hudokeza: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima.” (Methali 13:20, Union Version) Isitoshe, familia inayofanikiwa hujengwa kwa hekima na upendo wala si kwa mali za kimwili.—Waefeso 5:22–6:4.

Hatuzaliwi tukiwa na maadili. Tunapaswa kujifunza maadili hayo kutoka kwa marika wetu au kutoka chanzo cha juu zaidi. Hiyo ndiyo sababu elimu inayotegemea Biblia inaweza kugeuza mtazamo wetu wote wa akili kuelekea vitu vya kimwili. “Nilisaidiwa kuchunguza upya maadili yangu, nami nikajifunza kuridhika na mambo ya lazima,” anasema Don, aliyekuwa mkurugenzi wa benki.

Fuatia Utajiri wa Kiroho Wenye Kudumu

Tunapofuatia kanuni za kiroho tunapata thawabu za kudumu badala ya kujitosheleza kwa muda mfupi tu. Paulo aliandika: “Vitu vinavyoonekana [vya kimwili] ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana [vya kiroho] ni vya milele.” (2 Wakorintho 4:18) Ni kweli kwamba huenda vitu vya kimwili vikatutosheleza kwa muda mfupi, lakini pupa haitamfaidi mtu kwa muda mrefu. Kanuni za kiroho ni za milele.—Methali 11:4; 1 Wakorintho 6:9, 10.

Biblia inashutumu kukazia fikira ufuatiaji wa vitu vya kimwili ambao umeenea leo. Inatufundisha jinsi ya kuzuia tamaa za ubinafsi kwa kuwa na jicho rahisi na kulifanya likazie mambo muhimu zaidi, yaani, utajiri wa kiroho. (Wafilipi 1:10) Inaonyesha kwamba pupa ni kujiabudu. Tunapotumia yale tunayojifunza kutoka katika Neno la Mungu, tunapata furaha kubwa zaidi. Tunajifunza kutoa badala ya kupokea tu. Ni kitia moyo chenye nguvu kama nini kuachana na tamaa za ubinafsi na badala yake kudumisha kanuni za kiroho!

Ni kweli kwamba, kwa kiasi fulani, pesa zinaweza kuwa ulinzi. (Mhubiri 7:12) Lakini Biblia husema: ‘Pesa huwa kama zimepata mabawa ghafula, zikaruka na kutowekea angani kama tai.’ (Methali 23:5, Biblia Habari Njema) Watu wamedhabihu mambo muhimu, yaani, afya, familia, na hata dhamiri njema ili wapate vitu vingi vya kimwili, nao wamepatwa na matokeo mabaya. Kwa upande mwingine, kuwa na hali nzuri ya kiroho hutosheleza uhitaji wetu muhimu zaidi, yaani, uhitaji wa upendo, uhitaji wa kuwa na kusudi, na wa kumwabudu Mungu mwenye upendo, Yehova. Biblia pia huonyesha njia inayoelekeza kwenye uzima wa milele katika paradiso duniani ambako wanadamu watakuwa wakamilifu. Hilo ndilo tumaini ambalo Mungu ametutolea.

Hivi karibuni tamaa ya wanadamu ya kupata ufanisi itatimizwa kabisa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Zaburi 145:16) Wakati huo dunia yote “itajawa na kumjua Yehova.” (Isaya 11:9) Kanuni za kiroho zitasitawi. Ufuatiaji wa vitu vya kimwili na madhara yake vitaondolewa kabisa. (2 Petro 3:13) Halafu vitu vinavyofanya maisha yetu yawe yenye kuridhisha zaidi, yaani, afya kamilifu, kazi nzuri, starehe zinazofaa, mahusiano ya familia yenye uchangamfu, na urafiki wenye kudumu pamoja na Mungu, yote hayo yatawaletea wanadamu furaha halisi ya milele.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Tumia Pesa Zako kwa Hekima!

Tambua mahitaji yako. Yesu alitufundisha kusali hivi: “Utupe mkate wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo.” (Luka 11:3) Usiruhusu mambo unayotamani leo yawe mahitaji ya kesho. Kumbuka kwamba uzima wako hautokani na vitu ulivyo navyo.—Luka 12:16-21.

Pangia matumizi ya pesa. Epuka kununua vitu bila mpango. Biblia inasema: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Methali 21:5) Yesu aliwashauri wasikilizaji wake wahesabu gharama kabla ya kuanzisha mradi wowote wa kifedha.—Luka 14:28-30.

Epuka madeni yasiyo ya lazima. Inapowezekana, weka akiba ya pesa za kununua vitu badala ya kuvinunua kwa mkopo. Kitabu cha Methali kinaonyesha wazo hilo hivi: “Mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” (Methali 22:7) Ukijizuia kununua vitu bila mpango na kutumia vizuri pesa ulizo nazo, unaweza kufanikiwa kununua vitu vyenye thamani kubwa.

Tunza vitu ulivyo navyo. Tunza vizuri vitu ulivyo navyo ili vidumu muda mrefu zaidi, na hivyo kupunguza hasara. Yesu alionyesha mtazamo unaofaa kwa kutunza vizuri vitu alivyotumia.—Yohana 6:10-13.

Tanguliza mambo muhimu. Mtu mwenye hekima ‘hujinunulia wakati’ ili kufuatia miradi iliyo muhimu zaidi.—Waefeso 5:15, 16.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Kuna Njia Bora ya Kujifunza Kuliko Tu Kupitia Mambo Yanayotupata

Mambo yanayotupata maishani, yawe mazuri au machungu, yanaweza kutufundisha masomo muhimu. Lakini je, ni kweli kwamba njia bora zaidi ya kujifunza ni kupitia mambo yanayotupata? La, kuna mwongozo bora zaidi. Mtunga zaburi alitambua mwongozo huo aliposema hivi katika sala: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—Zaburi 119:105.

Kwa nini kujifunza kutokana na mwongozo wa Mungu ni bora kuliko kujifunza kutokana na mambo yanayotupata? Kwanza, kujifunza kwa kujaribu-jaribu mambo kunaweza kudhuru sana. Pia si lazima tujifunze kwa njia hiyo. Mungu aliwaambia Waisraeli wa kale hivi: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:18.

Sababu moja inayofanya Neno la Mungu liwe mwongozo bora zaidi ni kwamba lina masimulizi ya kale zaidi na yaliyo sahihi zaidi kuhusu mambo yaliyowapata wanadamu. Yaelekea unatambua kwamba ni afadhali kujifunza kutokana na mafanikio na makosa ya wengine kuliko kurudia makosa yao na kupatwa na madhara. (1 Wakorintho 10:6-11) Jambo la maana zaidi ni kwamba katika Biblia, Mungu anatupatia sheria bora na kanuni za kutuongoza zinazotegemeka kabisa. “Sheria ya Yehova ni kamilifu . . . Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zaburi 19:7) Kwa hakika, kujifunza kutokana na hekima ya Muumba wetu mwenye upendo ndiyo njia bora zaidi ya kujifunza.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Ulimwengu unataka ukubali maisha ya kufuatia vitu vya kimwili

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yale yaliyoandikwa katika Biblia ni hazina yenye thamani zaidi kuliko dhahabu au fedha